Abu Hurayrah-mpokezi wa hadithi



Abu Hurayrah-mpokezi wa hadithi

 “An ‘Abi Hurayrata radhiya llah annhu qaal, Qaala rasulullah salla llahu alayhi wassalam….” 
Mamilioni ya waislam tokea mwanzo mwanzo mwa historia ya kiislam hadi hii leo wanaisoma kauli hii ‘kutoka kwa Bwana Abu Hurayrah radhi za Mwenyezi Mungu zimfikie amesema, mjumbe wa Mwenyezi Mungu amesema…….”
 
Katika khutba, mihadhara, darsa kwenye vitabu vya hadithi, sira na fiqh, Abu Hurayrah hutajwa mara kwa mara.
 
Kwa jitihada yake, hadithi nyingi za Mtume (SAW) zimeweza kuwafika kizazi baada ya kizazi baada yake kufikia hadi hata mtoto mdogo wa miaka mitatu/mine akiwa bado hayuko chekechea anamtaja Abu Hurayrah.
 
Abu Hurayrah alisilimu mikononi mwa At-tufail ibn Amr ambaye alikuwa mkuu wa kabila la Dhaws.  Wadhaws waliishi katika eneo la Tihamah ufukweni mwa bahari nyekundu kusini mwa bara la Arab.
 
At-tufayl aliporudi kijijini kwake baada ya kukutana na Mtume (SAW) na kusilimu mwanzoni mwazo mwa uislam, Abu Hurayrah alikuwa wa mwanzo kuitikia wito.  Alisilimu na kuwa tofauti na wadhaws wengi ambao walikataa kusilimu na kuendelea na imani zao potofu.
 
Pia pale At-tufayl alipofanya tena safari kwenda Makka, Abu Hurayrah akafuatana naye.  Hapo akapata heshima ya kukutana na Mtume (SAW) ambaye alimuuliza:
 “Nani jina lako?” 
Akajibu Abu Hurayrah, “Abdu Shams.”
 
“Kuanzia leo utakuwa Abdulrahman,” akasema Mtume (SAW)
 
“Naam, Abdulrahman ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu.”
 
Mtume (SAW) ilibidi alibadilishe jina lake kwani kwa muislam kuitwa Abdu Shams, mja wa jua ni kinyume na kuwa kama juo ndio mungu wake.  Hivyo, akampa jina la Abdulrahman mja wa mwenye kurehemu.  Hata hivyo, jina lake la utani ‘Abu Hurayrah’ likiwa na maana ya (baba wa paka) lilikuwa ndio maarufu zaidi kwani alipenda sana kufuga paka tokea utotoni kwake.
 
Abu Hurayrah muda wote alikuwa Tihamah mpaka mwanzoni mwa mwaka wa saba hijiriya ndipo alipowasili Madina akiwa pamoja na baadhi ya watu wa kabila lake.  Kipindi hicho Mtume (SAW) alikuwa vitani Khaybar. Aliishi msikitini pamoja na Ahlu Suffa – wasiokuwa na uwezo.  Alikuwa bado kuoa na wala hana mtoto.
 
Hata hivyo, aliambatana na mama yake ambaye wakati huo alikuwa bado kusilimu. Abu Hurayrah alikuwa akiomba na kutamani mama yake asilimu lakini alikuwa mkaidi.  Siku moja alimlingania kuamini mungu mmoja na kumfuata Mtume (SAW) lakini mama yake alitamka maneno kuhusu Mtume (SAW) ambayo yalimsikitisha sana, huku akitokwa na machozi alielewa kwa Bwana Mtume (SAW) .  Mtume Muhammad alipomuona na hali ile akamuuliza:
 “Nini kilichokufanya ulie?” 
“Ninajitahidi kumlingania mama yangu uislam na kila siku ananikatalia, leo nilimlingania tena na nimesikia maneno kutoka kwake na sikuyapenda.  Hivyo, muombee dua kwa Mwenyezi Mungu aulainishe moyo wake na kuingia uislam.”
 
Mtume akamkubalia na kumwombea dua, Abu Hurayrah anasema:-
Nikaenda nyumbani na kukuta mlango umefungwa nikasikia maji yakichuruzika kama mtu anaoga na nilipotaka kuingia mama yangu akasema;
 
“Nisubiri hapo hapo, Abu Hurayrah, alipomaliza na kuvaa nguo zake akaniruhusu niingie.  Nilipoingia tu akaanza kutamka kalima: “Ash-hadu anlaa  ilaha ill allah waa-sh hadu anna Muhammadan abduhu waraasuluhu.”
 
“Nikarudi mbio kwa Mtume (SAW) huku nikitokwa machozi ya furaha ikiwa ni muda mfupi tu kabla yake nilitokwa machozi ya huzuni na kumwambia Mtume (SAW), nina habari njema, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu.  Mwenyezi Mungu (SW) ameitikia dua yako na kumuongoza mama wa Abu Hurayrah kwenye uislam.”
 
Alipofika tu Madina, Abu Hurayrah aliazimia kusoma.  Zayd ibn Thabit (RA) anasema: “Wakati mimi Abu Hurayrah na mmoja wa marafiki zangu tupo msikitini tukiomba na kufanya dhikr Mtume (SAW) alitokezea na akaja kujumuika nasi.  Tukanyamaza Mtume (SAW) akasema,
 
‘endeleeni na mlikuwa mkifanya’.
 
Hivyo mimi na rafiki yangu tukaomba kwa Mwenyezi Mungu kabla ya Abu hurayrah na Mtume (SAW) akawa anaitikia Amin.
Kisha Abu Hurayrah akaomba kwa kusema “Ewe Mola ninakuomba kwa ajili ya yale ambayo masahaba hawa wenzangu wamekuomba na ninakuomba elimu ambayo haitosahauliwa.”
Mtume (SAW) akasema, ‘Amin’.
 
Na sisi tukasoma pia, “Tunakuomba mola wetu elimu isiyosahaulika” Mtume (SAW) akajibu: “Kijana huyu wa kidhaws tayari ameshaliomba hilo kabla yenu”
 
Akiwa na hifadhi madhubuti Abu Hurayrah aliweza kuhifadhi katika kipindi cha miaka mine aliokaa na Mtume (SAW), hazina ya busara iliyokuwa ikitoka midomoni mwake.  Aliweza kugundua kwamba ana kipaji cha kuhifadhi hiyo kipaji hiki alikitumia vyema katika kuuhudumia uislam.
 
Abu Hurayrah hakuwa kama walivyokuwa wengi wa Muhajirin wakijishughulisha na biashara.  Wala hakuwa kama wa ansari kwani hakuwa na shamba la kulima na wala vipando vya kuvishughulikia.  Alikaa sana na Mtume (SAW) na kufuatana naye kwenye misafara yake.
 
Hata masahaba walishangazwa sana na wingi wa hadithi alizozihifadhi na mara kwa mara humuuliza wakati alipozisikia na katika mazingira gani.  Mara moja Marwan Al – Hakam alitaka kumjaribu Abu Hurayrah na kuona uwezo wake wa kuhifadhi.  Alikaa naye kwenye chumba na nyuma ya pazia kulikuwa na mwandishi ambaye aliagizwa aandike kila atakachokisikia kutoka kwa Abu Hurayrah.  Haya yote yanafanyika, Abu Hurayrah hana habari.
 
Mwaka mmoja baadaye, Marwan akamwita Abu Hurayarah na kumuuliza tena hadithi ile ile ambayo yule mwandishi aliinukuu.  Abu Hurayrah akaitamka vile vile bila ya kuongeza wala kupunguza kitu.
 
Licha ya kuwa na kipaji cha kuhifadhi.  Abu Hurayrah alikuwa pia na hima ya kuwafundisha waislam hadithi na dini kwa ujumla.  Inasemekana siku moja alipita soko kuu la Madina na kama kawaida ya sokoni aliwaona watu walivyoshughulika na biashara.  Alikaa na kuwatazama kwa muda kasha akawambia:
 
“Mbona mmelala hivi, watu wa Madina?”
 
Wakamuuliza, “Umeona kitu gani kwetu Abu Hurayrah mpaka kutwambia tumelala?”
 
“Mirathi ya Mtume (SAW) inagawiwa na nyinyi mko hapa.  Hamwendi kuchukua sehemu yenu?” aliwajibu.
 
“Wapi huko Abu Hurayrah?”
 
Akawajibu, “Msikitini”
 
Wakatoka mbio kuelekea msikitini, Abu Hurayrah akawasubiri mpaka waliporudi.
 
“Vipi Abu Hurayrah? Mbona tumekwenda msikitini na kuingia hadi ndani lakini hatukuona kitu chochote kinachogawiwa?”
Akawauliza, “Hamkumuona mtu yoyote msikitini?”
 
“Eee ndio, tuliona baadhi ya watu wanasali, wengine wanasoma Quran na wengine wanajadiliana kipi ni halali na kipi haramu.” Wakamjibu.
 
“Ole wenu, yale ndio mirathi ya Mtume (SAW)”.
 
Kwa kuwa Abu Hurayrah aliamua moja kwa moja kujifunga na kutafuta elimu, hakupata muda wa kujishughulisha na kazi au biashara na hivyo kuyafanya maisha yake kuwa duni na ya hali ya chini kabisa.  Mara nyingi alikuwa hana hata chakula na anaeleza:
 
“Nikiwa na njaa hujidai kwenda kwa sahaba yoyote yule na kumuuliza aya fulani ya Quran na hukaa hapo kujifunza ili  tukimaliza tunakwenda pamoja kula. 
Siku moja nilishikwa na njaa kali sana mpaka nikaweka kijiwe juu ya tumbo langu, nikakaa pembezoni mwa ujia wapitao masahaba.  Akapita Abubakar na kama kawaida yangu nikamuuliza aya ya Quran lakini hakunialika nyumbani kwake kisha alipita Umar naye pia hakunialika.  Akapita Mtume (SAW) ma aliponiona tu alijua kwamba nina njaa akaniita, “Abu Hurayrah”
“Labbayka” nikamjibu na nikamfuata mpaka nyumbani kwake.  Akakuta bakuli la maziwa na akauliza ahli yake:  Mmeyapata haya?
Akajibiwa, “Kuna mtu kaleta hapa kwa ajili yako”
Mtume (SAW) akaniambia, “ewe Abu Hurayrah, nenda kwa Ahlu Suffah kawaalike”
Abu Hurayrah akafanya kama alivyoagizwa na wote wakanywa maziwa yale.
 
Ukaja muda ambao waislam wakabarikiwa na mali na utajiri aina kwa aina.  Abu Hurayrah naye akabahatika kupata sehemu yake.  Akawa na nyumba mke na kujaaliwa mtoto.  Hata hivyo, utajiri haukumbadilisha kiti chochote wala hakusahau siku za umasikini wake muda woke mwingi aliuutuma kwa ajili ya ibada kusimama na kusali sala za usiku kwake ilikuwa ada na pia kwa familia  yake.  Huanza yeye thuluthi ya usiku kisha humuamsha mkewe thuluthi ya pili na thuluthi ya mwisho himalizia binti yao.  Kwa utaratibu huu nyumba ya Abu Hurayrah usiku mzima ni ibada, dhikr na sala.
 
Enzi za ukhalifa wa Umar, Abu Hurayrah alichaguliwa kuwa Amir wa Bahrain.  Umar aliwatahadharisha sana ma-amir wake kutojishughulisha sana na kupata mali hata ikiwa ni kwa njia za halali.  Aliwaasa waishi maisha yasiyokuwa na fahari wale kuwa na anasa kupindukia.
 
Wakati Abu Hurayrah yupo Bahrain akabahatika kuwa tajiri mkubwa, Umar aliposikia haraka akamwita aje Madina.
Alipofika, Umar akataka apewe habari vipi na wapi alipata mali zake.  Abu Hurayrah akajibu,
 
“kutoka katika biashara yangu ya kupandishia farasi na zawadi nilizokuwa nikiletewa”
 
“Zikabidhi zote Baytul Maal,”  akaamrisha Umar.
 
Abu Hurayrah akafanya kama alivyoagizwa na akanyanyua mikono yake na kuomba, “Ewe mola msamaha Amirul Muuminiin.”  Baadaye Umar akamtaka tena Abu Hurayrah awe Amir lakini alikataa na alipoulizwa kwa nini anakataa?.
Abu Hurayrah akajibu, “Ili heshima yangu isiingie doa, utajiri wangu kuchukuliwa na mgongoni kwangu kusemwa.”
 
Akaongeza, “Naogopa kuhukumu bila ya elimu na kuongea bila ya hekima.”
 
Maisha yake yote Abu Hurayrah alikuwa mkarimu sana na mama yake.  Anapotaka kutoka nyumbani huenda hadi mlango wa chumba chake na kusema:
“Assalam Aleykum, Ya Ummatah, warahamatullahi wabarakatuh.”
 
Na mama yake humjibu, “Waalykas salaam, ya Bunayyah, warahmatullah wakarakatu.”
Kisha Abu Hurayrah husema pia, “Mwenyezi Mungu akurehemu kwani ulinilea na kunienzi nilipokuwa mdogo.”
“Mwenyezi Mungu akurehemu kwani umenitoa kwenye makosa nilipokuwa mzee,” mama humjibu.
 
Ilikuwa ni tabia yake Abu Hurayrah kuwahimiza waislam kuwatendea wema wazazi wao.
Siku moja aliwaona watu wawili wakitembea kwa pamoja.  Mmoja alikuwa mkubwa wa umri kuliko mwenzake. Akamuuliza yule aliyeonekana kuwa kijana:
 
“Huyu ni nani wako.”
 
Akajibu, “ni baba yangu.”
 
“Usimwite kwa jina lake, usitembee ukawa uko mbele yake na usikae kabla yake.”Abu Hurayrah alimpa nasaha yule kijana.
 
Waislam wana deni kubwa la heshima kwa Abu Hurayrah hasa kwa kuweza kusaidia kuzihifadhi na kuzitunza hadithi za Mtume Muhammad (SAW) na ambao ni msingi mkuu wa pili katika sheria baada ya Quran.  Alifariki mwa 59 Hijriya akiwa na umri wa miaka  sabini na nane.