Umuhimu Wa Kujifunza Elimu Ya Dini


Abu Ammaar

Elimu yetu ya dini inazidi kuenea na kusambaa. Maendeleo ya teknolojia yamerahisisha kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa elimu miongoni mwa waislamu.Qur’aan kwa mfano sasa inapatikana katika mp3, ipod, mobile phones, computers na kadhalika. Unaweza sasa ukajifunza Qur’aan uko nyumbani ukitumia computer.Vitabu takriban vingi vya kizamani na vya karibuni vinapatikana kwa urahisi. Televisheni na mitandao nayo haiko nyuma katika jitihada hizi za kuielimisha dini yetu. Tuna mitandao na yenye kutegemewa kwa lugha yetu ya Kiswahili. Wahadhiri wetu nao wanatoa mada mbalimbali zenye manufaa kwetu nayo kuhifadhiwa katika njia za cd, mp3 na kaseti na kuwezesha wengine kufaidika pia.Vitabu katika lugha yetu pia navyo viko vingi na vinazidi kutolewa. Magazeti ya kiislamu pia kwa upande mwengine yanaendeleza kazi hii ya kuelimisha.
Yote haya yanafanyika kwa jitihada kubwa na ndugu zetu kutuwekea elimu hii kwa ajili ya manufaa yetu na tuifahamu dini yetu wakiwa tayari wameshatekeleza wajibu wao na kututaka sisi tutekeleze wajibu wetu katika kujifunza na kuelimika.Wajibu ambao ni fardhi kwa kila muislamu.
Kama siku moja Khalifa ‘Umar ibnul Abdul ‘Aziz ambae anahesabika kama ni khalifa wa tano katika makhalifa raashiduun - walioongoka, aliwahi kumuandikia mmoja wa ma amiri wake Abubakar ibnu Hazm na kumwambia:

    انظر ما كان من حديث رسول الله صلى الله عليه وسلم فاكتبه، فإني خفت دروس العلم وذهاب العلماء، ولا تقبل إلا حديث النبي صلى الله عليه وسلم، ولتفشوا العلم،
ولتجلسوا حتى يعلم من لا يعلم، فإن العلم لا يهلك حتى يكون سرا.

Angalia katika hadithi za Mtume na uziandike. Kwani ninachelea elimu kufichwa na maulamaa kutoweka. Na wala usikubali kitu chengine isipokuwa hadithi ya Mtume na idhihirisheni elimu na mkae kusomesha mpaka ajue na afahamu yule asiejua kwani elimu haipotei mpaka ikiwa imefichwa”.
                          Angalia sahihi Bukhari - vipi elimu itakavyopotea
Licha ya kuwepo utajiri wote huu wa elimu lakini wenye kuitafuta na kunufaika nayo ni wachache sana miongoni mwetu. Ni waislamu wachache walio tayari kujitolea muda na wakati wao kusoma dini yao ambayo hawana maarifa nayo. Ni waislamu wachache wanaothamini michango hii inayotolewa na waislamu na kufanyia kazi kisawasawa katika kuhakikisha wanaijua na kuifahamu vyema dini yao.
Kinachosikitisha na kuhuzunisha ni kwa waislamu kukosa msukumo na muelekeo wa kujipa hima ya kuitafuta elimu hii ya dini.Kwa sababu elimu ipo lakini wenye kuitafuta wameadimika, wanaotaka kusoma hatunao, ila tuna waislamu ambao ndio wengi waliokuwa radhi kutekeleza wajibu wao bila ya  kuja au kuwa na maarifa machache tu.

Bila ya kuwa na elimu hatuwezi kujua mfumo wa matendo ya ibada  kama sala, tohara, Hajj na matendo yake na Zakah na utekelezaji wake na kadhalika. Haya ni mambo ya kimsingi ambayo kila muislamu anapaswa kuyafahamu vilivyo na yanahitaji maarifa na upeo ili kuweza kuyatekeleza jinsi inavyotakikana.
Bila ya kuwa na elimu hatutokuwa na uhakika kwamba amali tunazozitenda tumepata ujira au kutopata chochote, tumetenda thawabu au tumefanya dhambi ikiwa ni za kujificha kama hasada, kiburi,chuki, choyo na kadhalika. Au ni za dhahiri kama kusengenya, kutazama yaliyoharamishwa, zinaa na kadhalika.
Bila ya kuwa na elimu hatuweza kuifahamu itikadi yetu sahihi ambayo ni wajibu kwa kila muislamu kuifahamu vyema aqidah yake na kuweza kumjua Allah Subhaanahu Wata’ala, kumpwekesha (Tauhiyd) na kujua sifa na majina yake na kuyatekeleza ipasavyo.
Bila ya kuwa na elimu hatuwezi kuzitambua tofauti zinazojitokeza katika dini yetu na kuweza kuelewa kwa ushuhuda wa kidalili na pia kuweza kujiepusha na mambo mengi ambayo yamezushwa katika dini yetu nasi tukijikuta kuyafuata tu bila ya kuyajua undani wake.
Ushahidi mdogo kuonesha kwamba kiwango cha elimu ya dini miongoni mwa waislamu ni duni tuangalie masuala na majibu na fatawa na aina ya masuala ambayo ni mambo ya kimsingi “basic” yanayoulizwa ambayo kisheria kila muislamu anapaswa kuyafahamu. Hiki nii kielelezo tosha kwamba bado jitihada haijafanyika kwa upande wa wenye kuitafuta elimu.
Hali hii ni kinyume kabisa na enzi za Mtume, masahaba na mataabiina pamoja na watangu wema. Kipindi chao hawakubahatika na kuwa na nyenzo kama tulizobahatika kuwa nazo lakini hamu yao na jitihada waliyoionesha katika kuitafuta elimu ni ushahidi tosha kuonesha jinsi walivyoitilia maanani elimu ya dini yetu ya kiislamu.
Kwa mfano enzi za uhai wa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam, mmoja wa masahaba Abdullah Ibnu ‘Abbass Allah, awawie radhi yeye na baba yake, hakuwahi kukosa vikao vya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam na kuhifadhi yale yote atakayoyasema na baada ya kufariki kwake. Alijihimu kwenda kwa masahaba wengi kujifunza yale waliyofundishwa na Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Akisikia tu! Kuna mtu anajua hadithi ambayo yeye haijui atakwenda kwake haraka na kuiandika.  Ataihakiki na kuilinganisha na hadithi nyengine na aliwahi kwenda kwa masahaba karibu thelathini kuhakiki jambo moja tu
Pia tunamuona mmoja wa Masahaba alitoka Madina kwenda Damascus Syria kuithibitisha hadithi moja tu ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam aliyoisikia na mtu wa kuthibitisha hayo alikuwa ni  sahaba Abu Dardaai, Allah amuwie radhi, ambae kipindi hicho alikuwepo Syria.
Elimu yetu ya dini imepita katika nyanja mbali mbali tokea kwa Mtume Salla Allahu Alayhi Wasallam hadi kutufikia. Katika mtiririko huu kuna elimu ambayo imehifadhiwa kupitia kizazi baada ya kizazi. Pia kuna elimu ambayo ndani yake imepitia tamaduni tofauti na kuingizwa katika dini kama ni sehemu moja wapo ya elimu yetu. Pia kuna watu ambao kwa maksudi wamejaribu kuupotosha umma wetu kwa kutumia nyanja hii hii ya elimu kwa kuingiza yasiyokuwemo au kuongeza kwa yaliyopo kwa lengo la kupotosha na si kuelimisha. Na pia kutia mashaka kwa yaliyopo kwamba hayana ukweli na kadhalika.
Ndiyo maana kwa ulimwengu wetu wa leo na hali hii tuliyonayo, kuisoma elimu ya dini itahitaji mtazamo mwengine na mfumo tofauti na mifumo iliyokuwepo katika siku za zamani.Kwani si rahisi kuweza kupambanua elimu iliyo sahihi na elimu isiyokuwa sahihi bila ya sisi wenyewe kuanza kujifunza kwa mfumo wa kukabiliana na hali halisi inayotukabili. Mazingira tayari yamebadilika na mfumo wa elimu pia itabidi ubadilike. Ule wakati wa kupokea tu elimu bila ya kuwa na uhakika na unachoelimishwa tayari umepita na tupo katika zama za kuisoma dini yetu kiutaalamu na upeo tukizingatia zaidi vigezo vinavyotumika.
Imepokewa katika hadithi sahihi kwamba miongoni mwa alama za siku ya kiama ni elimu kusomeshwa na watu wasiokuwa na elimu. Na matokeo yake ni kupotoka kwa waliofundisha na kupotoshwa kwa wanaofundishwa kwa mujibu wa hadithi ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam:
: (إن الله لا يقبض العلم انتزاعا ينتزعه من العباد، ولكن يقبض العلم بقبض العلماء، حتى إذا لم يبق عالما، اتخذ الناس رؤوسا جهالا، فسئلوا، فأفتوا بغير علم، فضلوا وأضلوا).    
“Hakika Allah haiondoi elimu kwa kuindosha kutoka(vifuani) kwa watu bali huiondosha kwa kuwaondoa Maulamaa mpaka hapatobaki msomi miongoni mwao na watu kuwachagua majahili kuwa ni viongozi ambao watatoa fatwa bila ya kuwa na elimu na watapotea(wao wenyewe) na kuwapoteza watu.”                                                                                               Bukhari                                           
Haya yalitamkwa na Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kabla ya kufariki kwake lakini hali hii tunaishuhudia wenyewe katika jamii zetu jinsi dini yetu inavyochezewa na watu ambao wanawapoteza wenzi wao.Nao si miongoni mwa makafiri waliodhihirisha kufru yao bali ni miongoni mwa waislamu ambao wamejitolea katika kuwapoteza waislamu wenzi wao.
Elimu ya dini ya kiislamu inazidi kusahauliwa kwa kasi ya kutisha licha ya kuwepo utajiri wote wa elimu tulioutaja hapo juu na hasa kwa sisi ambao tuko nchi ambazo hazina chembe chembe za kiislamu katika mfumo wa maisha tunaathirika sana kwa kukosa hata yale mafundisho ya kivitendo ambayo hutokea katika jamii za kiislamu. Lau kama elimu ya ilipewa umuhimu kama ule aliousia Mtume Muhammad Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kama ilivyoelezwa na Abdullah Ibn Masoud, Allah amuwie radhi.na kupokewa na Hakim katika hadithi inayofuata labda matatizo haya yasingelikuwepo:
تعلموا القرآن و علموه الناس و تعلمو الفرائض و علموه الناس فإني امرؤ مقبوض و أن العلم سيقبض و تظهر الفتن حتى يختلف الإثنان في الفريضة لا يجدان من يقضي بها .
“Jifunzeni Quraan na muwafundishe watu, na jifunzeni elimu ya Mirathi na muwafundishe watu, kwani mimi na mja ambae nitakufa na elimu itapotea na kudhihiri fitna(majaribu) na (kufikia) kuwatia shaka watu wawili na kutofautiana katika mirathi na wala wasipate mtu wa kuwapatia hukumu.”
Uislamu ni dini ya elimu na aya ya kwanza kabisa kuteremshwa katika Qur’aan inagusia kusoma ambao ndio ufunguo wa elimu yoyote.
Wengi wetu tunalichukulia jambo la kusoma elimu ya dini kama si lazima bali ni jambo la ziada lakini elimu nyengine na mambo mengine huwa tunayapa kipaumbele na umuhimu kuliko tunavyoipa umuhimu elimu yetu ya dini. Tumsikilize Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam anavyotukumbushia nini cha muhimu hasa katika elimu kama ilivyosimuliwa na Abdullah ibn Amr bin Al Aas (Allah amuwie radhi) na kupokewa na Dar qutni inavyobainisha:

أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال : العلم ثلاثة وماسوى ذلك فهو فضل : آية محكمة ، أو سنة قائمة أو ريضة عادلة ،
Hakika Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam amesema:
“Elimu ni tatu na zisizokuwa hizo ni ziada, (Elimu ya) aya (za Quraan) zinazobainisha hukumu, au sunna (za Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) zilizosimama, au Mirathi adilifu.” 
Allah Subhaanahu Wataala anawashuhudisha wenye kuitafuta elimu na Maulamaa kwamba ni watu wenye tauhiyd na wenye kumfahamu vyema Allah. Aal Imraan/18
 شَهِدَ اللّهُ أَنَّهُ لاَ إِلَـهَ إِلاَّ هُوَ وَالْمَلاَئِكَةُ وَأُوْلُواْ الْعِلْمِ قَآئِمَاً بِالْقِسْطِ لاَ إِلَـهَ إِلاَّ هُوَ الْعَزِيزُ
الْحَكِيم 
Allah, na Malaika, na wenye ilimu, wameshuhudia kuwa hakika hapana mungu ila Yeye, ndiye Mwenye kusimamisha uadilifu; hapana mungu ila Yeye Mwenye nguvu na Mwenye hikima
Moja katika malengo ya kujifunza elimu ya dini ni kutukurubisha na kuwa karibu na muumba - Allah Subhaanahu Wata’ala na kutaka radhi zake. Hujifunza tuweze kujua na kuelewa jinsi ya kumuabudu inavyotakikana na kuweza kumtakasia ibada zake kwa ikhlasi  
Pia kujifunza elimu ni ibada. Hivyo ni wajibu kwa mwenye kujifunza kuitakasa ibada hii kama zilivyo ibada nyenginezo. Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam amemuweka daraja moja mwenye kutafuta elimu na mwenye kupigana jihadi kwa njia ya Allah Subhaanahu Wata’ala.
من خرج في طلب العلم فهو في سبيل الله حتى يرجع))أخرجه التِّرْمِذِي  وقال : حديث حسن
“Mwenye kutoka kwa ajili ya kutafuta elimu huwa katika njia ya Allah mpaka atakaporudi.”
             Attirmidhiy na amesema ni hadith hasan                                                                                      
Kujifunza elimu yetu ya dini si jambo lililowekewa muda maalum. Ni kazi inayoendelea mpaka kuelekea kaburini bado tuna mengi ya kujifunza katika dini yetu. Umri mkubwa pia si kisingizio wala kigezo cha kukataa kujifunza. Tukiacha na kutojifunza dhimma itabaki kwetu na kuwa na viongozi watakaotupoteza, Maustaadh watakaotoa fatwa pasipokuwa na ujuzi wa kufanya hivyo na hatimaye umma wa kiislamu kuangamia na kula hasara.
Ni ibada muhimu kwa kila mmoja wetu kuipigania kwani hata husuda, ingawa ni haramu kisheria, ni jambo lililoruhusiwa kwa hili kama hadithi ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam inavyobainisha.
: (لا حسد إلا في اثنتين: رجل آتاه الله مالا فسلط على هلكته في الحق، ورجل آتاه الله الحكمة فهو يقضي بها ويعلمها     
“Hakuna husuda isipokuwa katika mambo mawili: Mtu ambae Allah amempa utajiri kisha akautumia katika njia ya haki na mtu ambae Allah amempa hekima (elimu ya dini) na akawa akitoa hukumu(sahihi) na kuifundisha kwa wengine.”
                                                                                  Bukhari
Mwisho na tuzidi kuikumbuka hadithi ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam akituhimiza katika kujifunza elimu ya dini pale aliposema kama ilivyopokewa na Bukhari:
                      يطلب به علما سهل الله له طريقا إلى الجنة ومن سلك طريقا …
“…Na atakaenyoosha njia kutafuta ndani yake elimu basi Allah humuwepesishia njia ya kwenda peponi.”
Tumuombe Allah Subhaanahu Wata’ala aturudishie tena hamu ya kuisoma na kuifahamu dini yetu. Pia atuongoze katika njia iliyonyooka.Tumuombe Allah atupe uwezo na muda wa kuweza kurudi kwake kwa kujifunza yale yatakayokuwa na kheri kwetu katika dini, dunia na akhera yetu. Amin Amin

Wabillahi Ttawfiyq.