‘Uthmaan Bin ‘Affaan (Radhiya Allaahu ‘Anhu) Ambaye Alibashiriwa Pepo
Kubashiriwa Pepo na Ushahidi
Abu Muusa alisimulia.
Siku
moja, nilikuwa nimekaa katika bustani na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi
wa aalihi wa sallam) Al-Madiynah, alipokuja mtu na kuomba ruhusa ya
kuingia.
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema:
“Mfungulie
lango, na umbashirie Pepo.” Kwa hiyo nilimfungulia, alikuwa Abu Bakr,
nilimbashiria Pepo. Mtu mwingine alikuja na kuomba ruhusa ya kuingia.
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema: “Mfungulie
lango, na umbashirie Pepo.”Alikuwa ‘Umar. Nilimfungulia, na nikampa
habari njema za Peponi. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa
sallam) alikuwa ameegemea kisha akasimama wima na kusema:
“Mfungulie lango, na mbashirie Pepo na utukufu utakaomshukia.” Alikuwa ‘Uthmaan. Nilimfungulia
lango na nikampa habari njema za Peponi, na nikamwambia aliyodhukuru
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).
’Uthmaan alisema; “Allaah pekee Ndiye Anayestahili kuombwa msaada.”[Al-Bukhariy na Muslim]
Katika mapokezi mengine Anas alisema:
“Mjumbe
wa Allaah, Abu Bakr, ‘Umar na ‘Uthmaan walipanda Mlima Uhud. Mlima
ulipotetema, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema:
“Nyamaza
(tulia) Ewe Uhud kwa sababu kuna Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam), mkweli na Mashahidi wawili juu yako.”
Hadiyth ya tatu iliyosimuliwa na Sa’iyd bin Zayd inaeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema:-
“Abu
Bakr yumo Peponi. ‘Umar yumo Peponi. ‘Uthmaan yumo Peponi. ‘Aliy yumo
Peponi. Twalhah yumo Peponi. Az-Zubayr yumo Peponi. ‘Abdur-Rahmaan bin
‘Awf yumo Peponi, na Sa’d yumo Peponi.”
Sa’iyd aliongezea kusema:
Mwandishi wa Wahyi
Zaidi ya sifa bainifu njema za ‘Uthmaan alikuwa mmoja wa waandishi wa wahyi. Alisimulia ‘Aaishah:
“Nilimwona Mjumbe wa Allaah akiegemeza
paja lake kwa ‘Uthmaan, nilipokuwa nikimfuta jasho usoni mwake wahyi
ulipokuwa ukimteremkia alimwambia ‘Uthmaan: “Ewe ‘Uthmaan andika,
WaLlaahi, mja huyo ana hadhi mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam) wa Allaah, na Allaah Aliridhia kutukuzwa kwake!
Alisimulia Ja’far bin Muhammad kwa mamlaka ya baba yake”
“Kila
Mjumbe wa Allaah alipokaa, Abu Bakr alikuwa kuliani kwake, ‘Umar alikaa
kushotoni kwake na ‘Uthmaan alikaa mbele yake, kwa sababu alikuwa
katibu myeka wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).”
Aliyekusanya Qur-aan Tukufu
Wakati
wa kupeleka jeshi Armenia, kulikuwa na majeshi mawili ya Waislamu. Moja
lilitoka Syria na jengine kutoka Iraaq. Hudhayfah bin Al-Yamaani
alishiriki katika jeshi hilo na aligundua tofauti katika matamshi ya
baadhi ya maneno katika Qur-aan.
Watu
wa Kuufah walisoma Qur-aan kwa mujibu wa mapokezi ya ‘Abdullaah bin
Mas’uud ambapo watu wa Syria walisoma kwa mujibu wa mapokezi ya Ubay bin
Ka’b
Hudhayfah alichelea tofuati hizo, hivyo alikwenda kwa ‘Uthmaan Khaliyfah na kumwambia:
“Ewe
Jemedari wa Waumini! Okoa hili taifa kabla hawajatofuatiana wao kwa wao
juu ya Kitabu chao, kwa sababu Mayahudi na Wakristo walitofuatiana
kuhusu vitabu vyao.”
‘Uthmaan alitoa khutbah ambapo alisema:
“Enyi
watu! Miaka michache imepita tangu Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam) amefariki dunia, na mwatofautiana kuhusu Qur-aan,
nasema: “Haya ni masimulizi ya Ubay na yale ni masimulizi ya ‘Abdullaah,
kwa hiyo miongoni mwao watasema” WaLlaahi, huzisoma vizuri Aayah kadhaa
wa kadhaa. Kwa hiyo, nawaalika kila mmoja wenu kuileta, endapo mna
sehemu ya Kitabu cha Allaah.”
Watu walileta vipande vya karatasi au vipande vya ngozi vilivyoandikwa juu yake mpaka akikusanya vya kutosha.
Kisha ‘Uthmaan aliwaita walioleta ngozi na vipande vya karatasi na alimwuliza kila mmoja”
“Je uliisikia hii kutoka kwa Mjumbe wa Allaah na je, alikusomea?”
Mtu alijibu: “Ndiyo” Baada ya kusema hayo, alisema, “Nani mwandishi mzuri?”
Walijibu “Sa’iyd bin Al-‘Aasw.”
‘Uthmaan alisema:
“Sa’iyd atoe Imla na Zayd aandike.”
‘Uthmaan
alimtuma Hafswah bint ‘Umar mkewe Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam) amletee hati iliyokunjwa inakiliwe kwenye Msahafu,
kisha alirejeshewa.
Hati
zilizokunjwa ziliandikwa wakati wa ukhalifa wa Abu Bakr baada ya vita
ya Al-Yamamaah wakati Maswahaba wengi waliohifadhi Qur-aan walikufa
shahidi.
Wakati
huo ‘Umar alimwambia Abu Bakr, “Maswahaba wengi waliohifadhi Qur-aan
waliuawa siku ya Al-Yamaamah, nachelea kusije kupotea kitu katika
Qur-aan. Kwa hiyo nakutaka uamuru ukusanyaji wake.
Kwa
matokeo hayo, Abu Bakr alimwambia Zayd bin Thaabit akusanye kutokana na
ngozi, kutoka Al-Asab (matawi ya mtende yaliyoondolewa majani yake,
ambapo sehemu ya Qur-aan iliandikwa juu yake na kutoka mioyo ya Ummah na
Kiislamu. Zile hati zilizokusanywa alikuwa nazo Abu Bakr na kisha ‘Umar
alipofariki dunia zilitunzwa na Hafswah bint ‘Umar. Kisha ‘Uthmaan
alizichukua na alimwamuru Zayd bin Thaabit, Abdullaah bin Az-Zubayr,
Sa’iyd bin Al-Aasw, ‘Abdur-Rahmaan bin Al-Haarith bin Hishaam azinakili
katika Mus-haf.
Kwa hiyo ‘Uthmaan aliwapa maelekezo yafuatayo:-
“Endapo mtatofuatiana juu ya kitu chochote, kiandikeni kwa mujibu wa lugha ya Kiquraysh kwa sababu ilishushwa kwa lugha hiyo.”
Hivyo
walifanya, baada ya kunakili hati zilizokunjwa (scrolls), ‘Uthmaan
alizirejesha kwa Hafswah na kisha akapeleka nakala ya Msahafu kwa kila
jimbo na aliamuru aina nyengine ya Mus-haf ichomwe moto. Ulimwengu wa
Kiislamu unashukuru kwa kitendo hiki cha ‘Uthmaan.
Iwapo
tungeorodhesha aliyofanya ‘Uthmaan katika njia ya Allaah tungeweza
kutengeneza orodha kamili. Hapa inatosha kutaja matukio matatu ambayo ni
ushahidi ulio wazi juu ya utoaji wake mkubwa kwa ajili ya Allaah.
Kutoa Katika Njia ya Allaah
Kuliandaa jeshi kwa Vita ya Taabuuk
Vita ya Taabuuk inaitwa ‘Vita ya majonzi baada ya kauli ya Allaah. (9:117).
“Allaah
Amekwishapokea toba ya Nabii na Wahajiri na Ansari waliomfuata katika
saa ya dhiki, pale baada ya kukaribia nyoyo za baadhi yao kugeuka. Basi
akapokea toba yao, kwani hakika Yeye kwao wao ni Mpole na ni Mwenye
kuwarehemu.” (9: 117)
Mtume
(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwataka watu kuelekea
vitani na aliwafahamisha sehemu waliyokuwa wakienda ili wajiandae.
Aliwanasihi watu wa Makkah na makabila ya Kiarabu kupigana na akawataka
watu kutoa sadaka na akawataka watoe katika njia ya Allaah. Watu wengi
waliitikia kwa kutoa mali nyingi kama sadaka.
Wa kwanza kutoa sadaka yake alikuwa Abu Bakr ambaye alitoa mali yake yote iliyofikia Dirham 4000.
’Umar alitoa nusu ya mali yake.
‘Abdur-Rahmaan bin ‘Awf alitoa wakia (ounce) 200 za dhahabu na fedha.
‘Aaswim bin ‘Adiy wasaqi 70 za tende.
‘Uthmaan alitoa zana kwa thuluthi ya jeshi (1/3), ngamia 950 na farasi 50.
Ibn
Is-haaq alisema: “‘Uthmaan alitoa kiasi kikubwa kwa kulipa jeshi zana
za kivita. Hapana aliyetoa zaidi yake katika njia hii. Alipeleka dinari
elfu moja na kuziweka juu ya paja la Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam). Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
alisema: “‘Uthmaan hawezi kudhuriwa na chochote kuanzia siku ya leo.”
(At-Tirmidhiy).
Ukarimu Wake
Tumeona
jinsi ambavyo ‘Uthmaan alivyokuwa tayari kutoa katika njia ya Allaah.
‘Uthmaan hakukoma hapa. Hakuwa kama mvua iliyonyesha katika muda
mwafaka. Alifahamika kwa kusaidia masikini na yeyote aliyehitaji msaada
wake. Imesimuliwa kwa mamlaka ya Ibn ‘Abbaas.
Ibn ‘‘Abbaas alisema:
Wafanya
biashara walifika nyumbani kwa ‘Uthmaan na kubisha hodi. Alitoka nje na
joho lake ametungika mabegani, aliwauliza, “Mna shida gani?” Walijibu.
“Tumepata habari ya kuwa kuna msafara unakuja kwako, una ngano na
vyakula. Tuuzie ili tuweze
kuwasaidia masikini wa Madiynah.” ‘Uthmaan aliwajibu. “Ingieni ndani
nyote.” Waliingia na kushangaa. Kulikuwa na mizigo elfu moja
iliyopakuliwa nyumbani kwa ‘Uthmaan. Aliwaambia,”Mtanilipa kiasi gani
kama faida? Walijibu, “Kumi kwa kumi na mbili.“ Aliwambia, “Nimepewa
zaidi.” Wakasema, ”Kumi kwa kumi na nne.” Akasema,”Nimepewa zaidi.” Wakamwambia,
“Kumi kwa kumi na tano.” Akasema, “Nimelipwa zaidi.” Wakamwambia, “Nani
mwingine aliyekulipa zaidi? Wafanya biashara wote wa Madiynah tuko
hapa?” Akasema. “Kila dirham nimelipwa, mara kumi. Je, mnanyongeza
yoyote?” Wakajibu. “Hapana.” Akawaambia, ”Nyie ni mashahidi kuwa nimetoa
sadaka kwa masikini wa Madiynah.”
Kujinyima Anasa za Dunia
‘Uthmaan
alikuwa mfano wa mtu aliyejinyima anasa za dunia na mcha-Mungu. Aliishi
maisha ya kawaida. Alikula chakula cha kawaida, na hakufanya israfu
katika mavazi na kufuja mali. Alijua ya kuwa Allaah hakujishughulisha na
umbile la nje la mtu bali umbile la ndani na nia yake.
‘Abdul-Malik bin Shaddad bin Al-Had alisema.
“Nilimwona
‘Uthmaan Ijumaa moja juu ya mimbari amevaa nguo ya Aden isiyo na
thamani zaidi ya dirham nne au tano na kilemba cha Kufi kitochotiwa dai.[1]
Pamoja na kuwa alikuwa Khalifa alilala mchana Msikitini juu ya changarawe.
Al-Hasan
aliulizwa juu ya wale wanaolala mchana Msikitini. Alijibu, ”Nilimwona
‘Uthmaan bin ‘Affaan akilala mchana Msikitini. Alikuwa Khalifa wa
Waislamu wakati huo. Alipoamka kutoka usigizini alikuwa na alama za
kokoto kwenye ngozi yake. Watu walisema,”Huyu ni jemadari wa Waislamu.
Huyu ni jemadari wa Waislamu.”
Kwa
hiyo, tunaona ya kuwa kujirahisisha na kuipa nyongo dunia ilikuwa hali
yake ya kawaida. Aidha alipanda mnyama wa kawaida sio farasi dume.
Imeelezwa kwa mamlaka ya Maymuun bin Mahran:
“Al-Hamdaan aliniambia ya kuwa alimwona ‘Uthmaan akipanda farasi jike na mtumwa wake alipanda nyuma yake.”[2]
Kujitambua
Alikuwa mcha-Mungu na akiogopa Siku ya Malipo.
Kwa mamlaka ya Hani, mtumwa aliyemwacha huru:
“Kila
‘Uthmaan aliposimama mbele ya kaburi, alilia mpaka ndevu zake zikalowa.
Aliiogopa Siku ya malipo kwa sababu ni siku ambayo hapana ‘amali
zitakazofanywa na kumbukumbu zitakuwa zimefungwa.”
‘Uthmaan alikuwa akisema:
“Kama
ningekuwa kati ya Pepo na Moto bila kujua nitaamuriwa kwenda wapi,
ningechagua kufanywa jivu kabla ya kujua nitaamriwa kwenda wapi.”[3]
Abul-Fusayt alisema:
“Siku
moja, ‘Uthmaan alimwambia mtumwa wake, “Kwa hakika, mara moja
nilikufinya sikio lako, hivyo lipiza kisasi.”Kisha akamwambia yule
mtumwa, “Nifinye kwa nguvu kwa kulipiza hapa duniani kunavumilika ya Akhera hayavumiliki.”[4]
Kujitambua
kwake kulimzuia kusimulia Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam) Japokuwa alikuwa mtu wa karibu sana. Alikuwa mume wa
mabinti mawili wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
Ruqayyah na Ummu Kulthum. ‘Amr bin Sa’ad bin Abi Waqqaas alisema ya kuwa
alimsikia ‘Uthmaan akisema, “Kinachonizuia kusimulia Hadiyth za Mtume
(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ni kuogopa kuwa sikuwa
msikivu. Nilisikia Hadiyth isemayo: “Yeyote anayezua neno, na akalihusisha nami, atapata makazi yake Motoni.”[5]
Ukhalifa
Baada
ya ‘Umar kuchomwa kisu, aliambiwa: “Teua (mrithi) Ewe Jemadari wa
Waumini!” ‘Umar alijibu. “Hapana wanaostahiki zaidi katika suala hili
kundi hili la watu aliowafia. Aliwataja majina; ‘Aliy,
‘Uthmaan, Az-Zubayr, Twalhah, Sa’ad na ‘Abdu-Rahman.”
Aliendelea kusema: ‘Abdullaah bin ‘Umar (mwanae) awe shahidi (katika uchaguzi) nazingatia ya kuwa hahusiki na kadhia hii.”
Lile kundi lililochaguliwa walimchagua ‘Uthmaan kuwa Jemadari wa Waumini na mrithi wa ‘Umar.
Ushindi Katika Utawala Wake
Vita
nyingi zilipiganwa na kupatikana ushindi katika sehemu zote, baharini
na nchi kavu. Ushindi huo ulidumu kwa miaka kumi mpaka uliposimamishwa
na Al-Fitnah (zahama).
Maadui
wa Uislamu kwa makusudi kabisa waliendelea kufanya fujo na kusita
kutekwa na mipaka yao kuingizwa katika ardhi ya Waislamu na majaribio
mengi yalisitishwa.
Kabla
ya kipindi cha ‘Uthmaan, Waislamu waliteka majimbo mengi na kuongeza
maeneo mazuri katika dola ya Kiislamu. Waislamu hawakuweza kuacha idadi
kubwa ya wanajeshi katika miji na sehemu walizozifungua kwani Waislamu
wakati huo walikuwa ni wachache.
‘Umar
alipouawa, wakazi wa majimbo ya jirani walidhani Waislamu wamekuwa
dhaifu. Walidhani sasa ulikuwa muda mwafaka kuanzisha mashambulizi.
Walivunja mikataba waliokubaliana na Waislamu, na ‘Uthmaan kama Khalifa,
alipambana nao kwa nguvu. Alikusanya majeshi chini ya makamanda
wazoefu, na jeshi lilimudu kuleta utulivu kwa mara ya pili huko Persia
(Iran), Khurasan, Babul Al-Abwaab, Afrika na Armenia.
‘Uthmaan hakufanikiwa kuwashinda maadui tu bali aliongeza ardhi mpya katika dola ya Kiislamu baada ya kushinda vita nyingi.
Nchi zifuatazo ziliongezwa katika dola ya Kiislamu.
1. Katika Afrika, eneo la kuanzia Tripoli mpaka Algeria.
2. Cyprus (Kuprus) katika Maditerranean.
3. Mashariki ya Uturuki.
4. Armenia, na kaskazini mwa Daghustan.
5. Kapol, na Sind.
Vita hivi havikuwa rahisi. Vilikuwa vikali kama ilikuwa baharini au nchi kavu. Inatosha kutaja mfano mmoja tu.
Vita inaitwa Dhatus-Sawari (vita ya mlingoti uliosimikwa). Constantina,
mtoto wa Hercules akiwa kamanda katika mwaka wa 31 wa Hijriyah,
akitarajia kulipiza kisasi kwa Waislamu, walimshinda katika Afrika.
Waislamu wengi waliuawa. Makafiri wasio na idadi pia waliuawa, lakini
siku hiyo Waislamu walikuwa na uvumilivu usio na kikomo, na Allaah
Aliteremsha ushindi kwa Waislamu.
Ustawi wa Jamii Wakati wa Utawala Wake
Dola
ya Kiislamu ilipanuka sana enzi za Ukhalifa wa ‘Uthmaan Zama zake
zilikuwa za ustawi wa jamii na wingi na mali; watu wake walifurahia
maisha mazuri na anasa. Muhammad bin Sina alisema”
“Utajiri
(mali) uliongezeka wakati wa utawala wa ‘Uthmaan. Mjakazi aliweza
kuuzwa kwa kupimwa kwa fedha, farasi kwa dirhamu laki moja na mtende kwa
dirham elfu moja.
Al-Hasan alisema: “Chakula kilikuwa kingi wakati wa Ukhalifa wa ‘Uthmaan.”[6]
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) Akimsifu Wakati Wote.
‘Uthmaan
alikuwa mwenza wa kudumu wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa
sallam). Ingekuwaje kinyume chake? Alikuwa mume wa Ruqayyah na kisha Umm
Kulthum baada ya kifo cha Ruqayyah. Alikuwa Swahaba mcha-Mungu na
mwenye soni na alipendwa sana na kuwavutia watu wengi. Vipi isingekuwa
hivyo, ambapo alitumia mali zake nyingi katika njia ya Allaahambapo
hapana aliyekuwa sawa naye katika hili.
Kama
uthibitisho wa mapenzi hayo, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa
sallam) alikuwa akimwombea sana ‘Uthmaan kwa Allaah kwa du’aa:
”Allaah
Akusamehe Ewe ‘Uthmaan kwa yale uliyoyatenda, utakayoyatenda na
utakayoyaficha, uliyoyadhihirisha, na yale yatakayokuwepo mpaka Siku ya
Hukumu.”
Anas alisimulia ya kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisema,
“Mtu
mkarimu zaidi katika ummah wangu kwa ummah wangu ni ‘Abu Bakr, Mkali
zaidi katika Dini ya Allaah ni ‘Umar na mwenye soni ya kweli ni
‘Uthmaan.”
Aidha Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimzungumzia kwa ‘Aaishah.
“Hutaki nione haya mbele ya mtu anayeonewa haya na malaika?”
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliendelea kusema: “Ewe Allaah! Nimeridhishwa na ‘Uthmaan na nakusihi uwe radhi naye pia.”[7]
Na pia alisema,
“‘Uthmaan ni mwenye soni zaidi na mkarimu zaidi katika ummah wangu.”[8]
Na pia alisema:
“Mwenye haya zaidi katika ummah wangu ni ‘Uthmaan.”[9]
Rai za Maswahaba Kuhusiana Naye
Kuna
masimulizi sahihi kuwa wakati ‘Abu Bakr akimsomea wasia wake ‘Uthmaan
kuhusu mrithi wake, alitaja jina la ‘Umar kuwa khalifa wa kumrithi,
kisha Abu Bakr alipoteza fahamu.
‘Uthmaan
aliandika: “Umar”. Abu Bakr alipozinduka, aliuliza: “Kumeandikwa nini?”
‘Uthmaan alisema: “Umar” Abu Bakr alisema,”Utukufu kwa Allaah ambaye
ameutawala mja wake.”
Mutarrifu alimsifu ya kuwa alikutana na ‘Aliy ambaye alimwambia: “Ewe Abu ‘Abdullaah! Kitu
gani kilichokuchelewesha? Ni mapenzi kwa ‘Uthmaan? Iwapo unakubali
niliyosema (kuhusu kumpenda ‘Uthmaan), utakuwa sahihi kwa sababu alikuwa
na shauku ya kuwaunganisha jamaa zake, na anamwogopa sana Allaah”[10]
Ibn
‘Umar aliripoti, “Wakati wa uhai wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa
aalihi wa sallam) tuliwataka watu wachague kati ya Abu Bakr, ‘Umar na
‘Uthmaan, na watu walimchagua Abu Bakr, ‘Umar na kisha ‘Uthmaan.[11]
Ibn Sirin alisema:
“Aliyekuwa na elimu zaidi juu ya ibada za Hijjah alikuwa ‘Uthmaan na kisha Ibn ‘Umar.[12]
‘Uthmaan alipochaguliwa kuwa Khalifa, Ibn Mas’uud alisema”
“Tumemchagua mbora wa wote walio hai, na hatukufanya hiyana.”
‘Abdullaah bin ‘Umar alisema:
“Wanaume
watatu wa Kiquraysh ni wenye sura nzuri zaidi, wenye mwenendo mwema na
wenye soni zaidi (sana) Wanapokuambia kitu, basi ni kweli Na ukizungumza
nao, hawatokudanganya. Watu hao ni: Abu Bakr, ‘Uthmaan bin ‘Affaan na
Abu ‘Ubaydah bin Al-Jarraah.”[13]
Masruuq alikutana na Al-Ashtar na kumwambia, “Umemwua ‘Uthmaan?” Alijibu, “Ndiyo” “WaLlaahi, umemuua na wakati wote alikuwa anafunga na kuswali.”
Kufa Shahidi
Maadui
wa ‘Uthmaan walieneza uvumi wa uongo ili watu wawe dhidi yake.
Walimshutumu kwa kuwapendelea jamaa zake na kuwa aliwapa vyeo katika
ofisi za dola badala ya Maswahaba wengine wa Mjumbe wa Allaah. Walitumia
fursa ya hali ya uvumilivu wa ‘Uthmaan na kufululiza kujaribu
kuwaridhisha raia wake badala ya kuwa mkali kwao.
‘Abdullaah bin Saba alikuwa mstari wa mbele katika hujuma hii.
Kikundi
kilitoka Misri kilikwenda kwa ‘Uthmaan huko Madiynah wakimlalamikia
Amir wao, ‘Abdullaah bin Sa’da bin Abi Sarh. Aliwapokea na akakubaliana
nao kuwa Amir atauzuliwa. Alipofikisha ushauri wao wakamteua Muhammad
bin Abi Bakr na akatoa agizo kuhusiana na hilo. Walianza safari ya
kurejea kwao Misri. Njiani walimwona kijana aliyepanda farasi huku
akimpiga sana. Walimwuliza, kulikoni? Yule kijana aliwajibu:
“Mimi ni tarishi wa Kamanda wa Waumini, amenituma niende kwa Amir wa Misri.”
Walipofika walikuta barua (iliyoghushiwa) kutoka kwa ‘Uthmaan kwenda kwa ‘Abdullaah bin Sa’d bin Abi Sarh ikisema:
“ Iwapo fulani na fulani watakuja kwako, waue kwa kughushi, puuza barua yao, na endelea na madaraka yako mpaka taarifa nyingine itakapokufikia.”
Lile
kundi lilihamanika na kurejea Madiynah walipomhoji ‘Uthmaan aliapa kwa
jina la Allaah kuwa hakuandika barua ile. Baadaye ilithibitika kuwa
Marwaan ndiye aliyeghushi barua ile. Walipomtaka ‘Uthmaan awakabidhi
Marwaan, alikataa kwa kuchelea kuwa wangemuua.
Lile kundi likasema”
“Ama tupatie Marwaan au jiuzulu Ukhalifa.”
‘Uthmaan
alikataa, hivyo walimzingira na kutaka kumuua. ‘Aliy aliwatuma watoto
wake wawili Hasan na Husayn ili wamlinde. Az-Zubayr alimtuma mtoto wake
‘Abdullaah, Twalhah na Maswahaba wengine wa Mtume (Swalla Allaahu
‘alayhi wa aalihi wa sallam) pia walituma watoto wao kwa lengo hilo
hilo, lakini maasi walipanda ukuta wa nyumba. ‘Uthmaan alikuwa akisoma
Qur-aan aliyoipenda sana. Alipokuwa akisoma kimya na unyenyekevu,
walimuua. Alikufa na Mus-haf mikononi.
Aliuawa tarehe 18 Dhul –Hijjah, mwaka wa 35 H, na alizikwa Al-Baqi’i. Alikuwa na umri wa miaka 82.
[1] Hilyat Awliya’ 1/60
[2] Hilyat Awliya’
[3] Hilyat Awliya’
[4] Ar-Riyaadh An-Naadirah.
[5] At-Taariykh Al-Kabiyr 2191
[6] Ar-Riyaadh An-Naadirah
[7] Muslim
[8] Muslim
[9] Hilyat Awliyaa’
[10] Swifatus-Safwah.
[11] Al-Bukhaariy 2655
[12] Imeripotiwa na Ibn ‘Asakir