Sehemu ya Pili

Abubakar As Siddique  (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Khalifa wa kwanza aliyeongoka

Makubaliano ya Hudaibia


Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikua akimfahamu na akimuelewa vizuri sahibu yake (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kupita Masahaba wote (Radhiya Llaahu ‘anhu), na alikuwa na uhakika kuwa yote anayoyasema ni Wahyi utokao kwa Mola wake Subhanahu wa Taala.
Katika mwaka wa tano baada ya kuhamia Madina, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na Masahaba wake (Radhiya Llaahu ‘anhu) waliondoka Madina kuelekea Makkah kwa nia ya kufanya Umra. Wakapiga kambi karibu na mji wa Makkah mahali panapoitwa Al Hudaibiyya, kisha wakamtuma Othman bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu) ende Makkah kuwajulisha Makureshi juu ya nia yao hiyo na kwamba hawakuja kwa nia ya kupigana vita.
Makureshi wakapeleka majeshi yao kutaka kuwazuia, na baada ya majadiliano marefu yaliyopita baina yao, wakaamua kumtuma mjumbe wao aitwaye Suhail bin Amr, aliyeweza kufikia makubaliano na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), yaliyokuja kujulikana kwa jina la Makubaliano ya Al Hudaibiyya.

Yafuatayo ni baadhi ya shuruti za makubaliano hayo;
· Waislamu warudi Madina mwaka huu na wafanye Umra mwaka ufuatao.
· Waislamu wanalazimika kumrudisha kwa Makureish yoyote atakayeingia katika dini yao na kukimbilia Madina, lakini Makureshi hawalazimiki kumrudisha atakayetoka katika Uislamu na kukimbilia Makkah.
· Wasipigane vita kwa muda wa miaka kumi, na wawe wanaendeana watakavyo.

Kabla ya mkataba huo kutiwa sahihi (saini), Waislamu walistukia kijana mmoja aitwae Aba Jandal aliyesilimu lakini alikuwa akiishi Makkah akipitishwa mbele yao akiwa amefungwa minyororo shingoni huku na kubebeshwa jiwe kubwa akipiga kelele akiwaomba Waislamu wenzake wamuokoe kutokana na adhabu hiyo.
Kijana huyu Aba Jandal ni mwana wa Suhail, mjumbe wa Makureish katika sulhu hiyo.
Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), alimuonea huruma kijana huyo, akamtaka Suhail amruhusu wamchukuwe kwa sababu mkataba ulikuwa bado haukutiwa saini wala haukupigwa mhuri, lakini baba yake alikataa na kutishia kuuvunja mkataba na kuanzisha vita ikiwa  watajaribu kumchukua kwa nguvu.
Abu Jandal alikuwa akipiga kelele huku akisema;
"Enyi Waislamu wenzangu! mnaniacha nirudi kwa washirikina hawa na mimi nataka himaya yenu?"
Mtume(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)  akamwambia ;
"Kuwa na subira, na Mwenyezi Mungu atakujaalia utoke katika janga hilo".
Omar bin Khattab (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuweza kuyastahamilia haya, akamuendea Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na kumuuliza;
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, wewe si Mtume wa Haki?"
Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamjibu;
"Ndiyo, ewe Omar".
Akauliza tena;
" Kwa nini basi tunakubali kujidhalilisha?"
Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia;
"Ewe Omar, mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, siwezi kumuasi, na Yeye ndiye atakayetunusuru".
Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akauliza;
"Si ulituahidi kuwa tutakwenda Makkah na tutatufu katika nyumba kongwe?"
Mtume(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akajibu;
"Nilikwambia kuwa ni mwaka huu ewe Omar?"
Omar akajibu;
"La hukusema hivyo."
Mtume(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akasema;
"Utakwenda Makkah ewe Omar na utatufu penye nyumba."
Omar pamoja na baadhi ya Masahaba (R.Anhum) hawakuridhika na baadhi ya masharti yaliyokuwemo ndani ya mkataba ule, wao waliona kuwa Waislamu wamekubali kujidhalilisha kwa kuyakubali masharti yote ya makafiri, na hii ni kwa sababu dhahiri yake mkataba huo si mzuri juu ya Waislamu, lakini kwa anayeona mbali mkataba huo ulikuwa ni ufunguzi mkubwa kwa Waislamu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu katika Suratul Fat-h aya ya mwanzo;
"Bila shaka tumekwishakupa kushinda kuliko dhahiri"
Mwenyezi Mungu katika aya hii anatujulisha kuwa kuukubali mkataba huo ni ushindi mkubwa kwa Waislamu, juu ya kuwa dhahiri yake ni kukubali masharti yote ya makafiri, na hii ni inatokana na sababu zifuatazo;
1)           Kutokana na suluhu hiyo, makafiri walifungika wasiweze kupigana vita dhidi ya Waislamu muda wa miaka Kumi.
2)           Katika muda wote huo Waislmu wakawa na uwezo wa kujishughulisha na kuieneza dini yao miongoni mwa makabila mengine ya Bara arabu, pamoja na nchi za Sham.
3)           Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alituma ujumbe kwa wafalme mbali mbali
4)           Wale waliosilimu wasioruhusiwa kukimbilia Madina kwa ndugu zao Waislamu, ni bora kwao kubaki Makkah kwa ajili ya kuwalingania watu katika dini ya Kiislam huko Makkah.
5)           Makafiri watakaorudi Makkah iwapo watatoka katika Uislam, hawataudhuru Uislam.
Sababu hizi na nyinginezo ambazo si wasaa wake huu kuzitaja ni dalili kuwa mkataba huo undani wake ulikuwa na manufaa makubwa kwa Waislamu, juu ya kuwa dhahiri yake ni kusalimu amri na kukubali masharti yote ya Makureshi.
Na hii ndiyo sababu iliyomfanya Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) asiridhike nao, wala asisimame hapo. Kwani alimwendea pia Abubakar Al Siddiq (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumuuliza tena masuali yale yale;
"Ewe Abubakar, Muhammad si Mtume wa Haki?"
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu); "Ndiyo"
Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu); "Tukipambana nao makafiri hawa, si atakayekufa upande wetu ataingia Peponi na wao wanaingia Motoni?"
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu); "Ndiyo".
Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu); "Kwa nini basi tunakubali kujidhalilisha?"
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Ewe Omar, yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na hawezi kumuasi, na Mwenyezi Mungu ndiye atakayemnusuru, kamatana naye kwani Wallahi yupo katika Haki".
Majibu yale yale ya Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kayapata kwa Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), na Mwenyezi Mungu akawateremshia Waislamu utulivu nyoyoni mwao.
Mwenyezi Mungu anasema;
"Yeye ndiye aliyeteremsha utulivu katika nyoyo za Waislamu ili waongezeke imani juu ya imani yao".
Suratul Fat-h 4
Omar(Radhiya Llaahu ‘anhu) alisema baadaye;
"Nikatambua kuwa ile ndiyo Haki".
Mwaka wa tisa Hijri ndio mwaka ulioitwa 'Mwaka wa Wajumbe' na hii ni kutokana na wajumbe wa makabila mbali mbali ya kiarabu waliokuja kusilimu mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).

Vita vya Badr


Imani ya Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ilikuwa ikijitokeza na kueneza tumaini baina ya watu kila inapotokea shida au dhiki.
Katika vita vya Badr, jeshi dogo sana la Waislamu liliondoka mjini Madina kwa nia ya kuuteka msafara mdogo wa kibiashara ukiongozwa na Abu Sufyan unaotokea Syria na kuelekea Makkah, na Waislamu walitegemea kuwa bila shaka msafara huo utakuwa na watu wachache waliokwishachoka baada ya safari ndefu hiyo.
Mwenyezi Mungu akawataka Waislamu wauachilie mbali msafara huo na wende kupambana na jeshi kubwa la Makureshi lililokwishaondoka Makkah kuelekea Madina likiwa limejitayarisha kivita na limejizatiti barabara. Na Mwenyezi Mungu aliwaahidi Waislam kuwa watawashinda Makureshi hao juu ya wingi wao.
Idadi ya Waislam ilikuwa mia tatu na kidogo tu, na hawakuwa na silaha nzito isipokuwa panga zao.
Waislamu wakapiga mahema yao katika bonde la Badr na kumtaka Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) asiondoke hemani pake iwe itakavyokuwa.
Jeshi kubwa la makafiri likaanza kuhujumu kwa nguvu, na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akihuzunika kila anapoona Muislam anauliwa, na mambo yalipozidi kuwa magumu hata akawa anasikia sauti za panga na kelele na mayowe zikikaribia, akaamua kutoka nje ya hema huku akinyanyua mikono yake mbinguni na kumuomba Mola wake kwa hamasa akisema;
"Mola wangu ikiwa kundi hili litaangamizwa, hutoabudiwa tena ardhini, Mola wangu nipe ushindi ulioniahidi Mola……"
Aliendelea hivyo mpaka Sayiduna Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipomwendea na kuiweka sawa nguo ya kujifunikia ya Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) iliyokuwa ikimwanguka huku akimwambia;
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu inatosha kuomba, kwani Mola wako atakupa kile alichokuahidi".
Bila shaka Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) anaamini kuwa kila alichoahidiwa na Mola wake atakipata, bali hata kabla ya vita hivyo kuanza, yeye ndiye aliyewaonesha Masahaba (Radhiya Llaahu ‘anhu) mwahali watakapoanguka vigogo vya Makureshi. Aliwaonyesha mahali gani Abu Jahal atauliwa na kuanguka, na akawaonyesha mwahali gani watauliwa na kuanguka vigogo wengine mbali mbali wa Kikureshi, na  yote yalitokea kama alivyosema.
Lakini hisia yake juu ya uzito wa mzigo alioubeba na hofu yake katika pambano hili la mwanzo baina ya Imani na Kufru ndiyo iliyomfanya atoke nje ya hema lake na kunyanyua mikono yake juu akiomba kwa hamasa namna ile.

Imani ya hali ya juu


Imani ya hali ya juu kabisa ya Abubakar ilionekana pale alipofariki Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) .
Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipokuwa akiumwa maradhi yake ya mwisho, alimtaka Abubakar awe anasalisha watu. Siku moja baada ya kuwasalisha Waislam,  Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliingia chumbani kwa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na baada ya kuzungumza naye muda mrefu akamtaka ruhusa arudi nyumbani kwa ajili ya kukidhi haja zake.
Baada ya kumaliza haja zake na alipokuwa akijitayarisha kurudi msikitini, akasikia sauti za watu wanalizana, akazipokea habari za kufariki kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu huku anakimbia kuelekea msikitini na huku machozi yakimtoka huku akisema;
"Inna lillahi wa inna ilayhi raaji uun".
Ndani ya nyumba ya Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) watu walikuwa mfano wa waliorukwa na akili.
Hata Omar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu), mwenye nguvu, shujaa, alisimama mbele ya watu panga mkononi huku akisema:
"Wanafiki wanadai kuwa eti Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) amekufa, Mtume hajafa, bali amekwenda kwa Mola wake kama alivyokwenda Musa mwana wa Imran na atarudi. Sitaki kumsikia mtu akitamka kuwa Mtume amekufa., nikimsikia mtu anasema hivyo nitamkata kichwa chake kwa upanga wangu huu."
Ikiwa hii ni hali ya Omar, ilikuwaje basi hali ya walio chini yake? Waislam hawakutegemea kuwa Mtume wao, kipenzi chao, (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) siku moja atakuja kuwatoka, msituko ulikuwa mkubwa sana.
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliingia moja kwa moja chumbani alipolazwa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), akamfunua uso wake na kuubusu huku akisema;
"Uso wako unapendeza ukiwa u hai au umekufa. Ama kile kifo alichokuandikia Mola wako kimekwishakufikia".
Akaufunika uso wake na kutoka nje na kumkuta Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) angali anawasemesha watu. Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamtaka anyamaze lakini Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakunyamaza, na alipomuona hanyamazi akawaelekea watu na kuwaambia;
"Aliyekuwa akimuabudu Muhammad, basi Muhammad kesha kufa, ama aliyekuwa akimuabudu Allah, basi Allah yu hai na wala hafi."
Kisha akaisoma kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:
"Na hakuwa Muhammad ila ni Mtume tu. Wamepita kabla yake Mitume (wengi kabisa). Akifa au akiuawa ndiyo mtarudi nyuma (kwa Visigino vyenu), muwe makafiri kama zamani? Na atakayerudi nyuma kwa visigino vyake hatamdhuru Mwenyezi Mungu cho chote. Na Mwenyezi Mungu atawalipa wanaomshukuru."
Aali Imran- 144
Alipoisikia tu aya hiyo Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuweza kusimama, akakaa kitako mfano wa simba aliyenyeshewa mvua. Siku zilizofuata alisema:
"Ilikuwa kama kwamba ninaisikia aya hiyo kwa mara ya mwanzo, miguu haikuweza kunichukua nikajitupa chini na kukaa".
Bukhari.
Ama Ibni Abbas alisema;
"Wallahi ilikuwa kama hawaijui aya hii, na mara walipomsikia Abubakar akiisoma, watu wote waliipokea na kila aliyeisikia alikuwa akiisoma na kuirudiarudia".
Bukhari.
Huu ndio ushujaa wa Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), wakati kama huu, umma wote ulipobabaika na kutetereka, akiwemo Omar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu), Abubakar Al Siddiq alikuwa thabiti mfano wa jabali mbele ya kimbunga kilichouvamia umma siku hiyo, na aya aliyoisoma siku ile ikawa inarudiwarudiwa na kila mtu;
"Aliyekuwa akimuabudu Muhammad, basi Muhammad kesha kufa, ama aliyekuwa akimuabudu Allah, basi Allah yu hai na wala hafi."
Neno la Tawhid, neno la kuuamsha Umma, 'Ikiwa mnamuabudu Allah basi amkeni na muifanye bendera ya Laa ilaaha Illa llah ipepee kila mahali. Aamkeni muyaendeleze mapambano yaliyoanzishwa na Mtume wenu huyu mtukufu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)'.
Neno hilo liliwaamsha na kuwatanabahisha Waislamu, wakaanza kutimiza wajibu wao, wakamuosha, wakumshughulikia na kumsalia na kumuaga Mtume wao mtukufu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
"Je kusingekuwepo na Abubakar, hali ingekuwaje siku hiyo?"

Siku ya Saqifa


Hii ni siku aliyofariki Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na baadhi ya watu wa Madina walijikusanya mahali panapoitwa Saqeefat Bani Saaidah karibu na msikiti wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kwa ajili ya kufungamana na sahaba mmoja katika watu wa Madina aitwaye Saad bin Obada (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumchagua kuwa ni Khalifa wa Waislam.
Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu), alipopata habari hizo alimwendea Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumhadithia yanayotokea, na wote kwa pamoja wakifuatana na Abu Ubeidah Amer bin Jarrah (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakaelekea huko.
Abubakar wala Omar hawakuwa na tamaa ya Ukhalifa kama tutakavyoona, na hii ni kwa sababu walimsikia Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akimkatalia Ami yake Al Abbas, alipomuomba ampe ugavana wa mkoa mmojawapo, na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia;
"Sisi Wallahi hatumpi utawala mwenye kuuomba wala mwenye kuung'ang'ania" .
Na hii ni kwa sababu utawala, si neema wala raha hata mtu aung'ang'anie na kuutaka. Mwenye kuung'ang'ania utawala ni yule asiyeelewa jukumu lake,  ama sivyo asingeutaka. Na Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyajua hayo vizuri .
Wengi walibabaika baada ya kuzipokea habari za kifo cha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na miongoni mwao ni watu wa Madina  waliojikusanya mahali hapo panapoitwa Saqeefat Bani Saaidah, wakasema kuwa; lazima pafanywe haraka kumchagua kiongozi wa umma kabla hapajatokea machafuko, na wakataka kiongozi huyo atoke katika watu wao (awe mtu wa Madina), kwa sababu Madina ni mji wao, na kwa sababu ya fadhila zao nyingi katika kuunusuru Uislamu, na kwa ajili hiyo wakaamua kumchagua sahaba huyo aitwaye Saad bin Obada (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Mara baada ya kuwasili mahali hapo, Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akataka kuuhutubia mkusanyiko huo, lakini Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), alimvuta nyuma na kumuomba amwachie yeye ahutubie, akajisogeza  mbele na kusema;
"Enyi watu wa Madina, hakika hapana fadhila itakayowezwa kutajwa bila ya kutajwa nyinyi ….", akaendelea kuwapa sifa zao walizostahiki, kisha akasema.
"Lakini Khalifa wa Waislamu atoke kwetu sisi watu wa Makkah".
Katika kitabu chake kitukufu, Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala daima hutanguliza kuwataja watu wa Makka 'Al Muhajirin' kabla ya watu wa Madina 'Al Ansar'  .
Mwenyezi Mungu anasema;
"Na wale waliotangulia wakawa wa kwanza katika (Uislamu) Muhajiri na Ansari…".
At Tawba-100
Mmoja katika watu wa Madina aitwaye Al Khabbab bin Mundhir (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Kwetu atoke Amiri na kwenu Amiri".
Akainuka sahaba mwengine ambaye pia ni katika watu wa Madina aitwaye Bashir bin Mubarak (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kusema;
"Enyi Al Ansar (Watu wa Madina), ingawaje sisi tumeipigania dini hii kwa hali na mali, lakini haijuzu kwetu kujifanya bora kuliko wenzetu, sisi tulifanya hayo kwa ajili ya kutaka radhi za Mwenyezi Mungu na kumtii Mtume wetu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam). Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) anatokana na kabila la Kikureshi, na watu wake ndio wanaostahiki kutuongoza. Mwenyezi Mungu asinijaalie nikapingana nao. Muogopeni Mola wenu enyi watu wa Madina na msiwaendee kinyume Al Muhajirina (watu wa Makkah)".
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), akaunyanyua juu  mkono wa Omar na wa Abu Obaida Amir bin Jarah (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kusema;
"Huyu Omar bin Khattab ambaye Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alimuomba Mwenyezi Mungu kutokana naye autukuze Uislamu, na huyu Abu Ubaida ambaye Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alimsifia kuwa ni 'Mwaminifu wa Umma huu', mimi nimeridhika (achaguliwe) mmoja kati yao, (awe Khalifa)"
Omar aliuchomoa mkono wake kwa nguvu mfano wa mtu aliyeshika jinga la moto na Abu Ubaida akasema;
"La wallahi! Nina hiari nikatwe kichwa changu bila ya kutenda dhambi yoyote, lakini sikubali niwe kiongozi wa watu akiwemo Abubakar ndani yao. Ewe Abubakar, Mtume wa Mwenyezi Mungu alikutanguliza wewe utusalishe, na katika kila kubwa na dogo aliridhika na wewe, basi kwa nini na sisi tusiridhike na wewe? Utandaze mkono wako tufungamane nawe, ewe Abubakar".
Akautandaza, na katika riwaya zilizo sahihi, wa mwanzo kufungamana naye alikuwa Bashir bin Mundhir ambaye ni mtu wa Madina, kisha Omar kisha Abu Ubaida kisha wakamvamia masahaba wote mmoja baada ya mmoja wakifungamana naye (Radhiyallahu anhum).
Siku ya msiba mkubwa kupita yote iliyopata kuwatokea Waislamu ilimalizika kwa amani baada ya kuweza kuiondoa hitilafu iliyozuka baina yao, na baada ya kupata matumaini kwa kumuona Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ndiye aliyeshika hatamu, kwani Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) anapokuwa anaumwa au anapopatwa na udhuru wowote, alikuwa daima akimtanguliza Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) kusalisha watu, kuongoza misafara ya hija na kusimamia mambo mbali mbali.
Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipokuwa akiumwa katika maradhi yake ya mwisho, alimchagua Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) awasalishe watu, na bibi Ayesha (Radhiya Llaahu ‘anha) alipojaribu kumtaka Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kumpa Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) jukumu hilo badala ya baba yake kwa sababu Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mwingi wa kulia anaposalisha, Mtume(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alikasirika akamwambia;
"Mwambie Abubakar asalishe watu!"

Mimi si mbora wenu


Siku ya mwanzo ya utawala wake Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipanda juu ya membari ya msikiti wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kuwahutubia Umma aliopewa jukumu la kuwaongoza. Baada ya kupanda ngazi mbili alishindwa kuzikamilisha ngazi zote tatu alizokuwa akizipanda Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), maana aliona kuwa akizikamilisha ngazi zote atakuwa amejiweka daraja moja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Baada ya kuzipanda ngazi hizo akaanza kuhutubia kwa kusema;
"Enyi watu!
 'Mimi nimepewa uongozi juu yenu, lakini si mbora wenu.
Nikihukumu sawa, nisaidieni.
Nikihukumu vibaya nirakibisheni.
Hakika aliye dhaifu miongoni mwenu, kwangu mimi ni mwenye nguvu mpaka nimpatie haki yake, na hakika mwenye nguvu miongoni mwenu, kwangu mimi ni dhaifu mpaka niichukue haki ya watu iliyo kwake.
Nitiini iwapo nitamtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ama nikiasi (amri ya Mwenyezi Mungu) basi msinitii.
Umma unapoiacha Jihadi, hudhalilika.
Inukeni msali, Mwenyezi Mungu akurehemuni".
Hii ndiyo hutuba ya mwanzo ya Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu); hotuba fupi iliyoweka wazi jinsi gani atakavyohukumu.
Alisema;  
'Mimi nimepewa uongozi juu yenu, lakini si mbora wenu'.
Aliyasema haya ili kuujulisha Umma kuwa yeye si mfalme juu yao bali ni kiongozi tu, na hivi ndivyo uhusiano utakavyokuwa baina yake na Umma wake, Kiongozi, Mwalimu, Jemadari, Khalifa wao na Mwenzao.
Kwa njia hii aliwajulisha Umma wake juu ya Dhamana aliyopewa na juu ya kiongozi mwaminifu, vipi anatakiwa awe.
Pia alitaka kuondoa katika fikra zao kwamba, anayehukumu, yupo juu ya sheria, na kwamba anaweza akafanya atakavyo, na kwamba hakosi na wala hakosolewi.
Alitaka kuwajulisha kuwa Uongozi si cheo cha kujivunia bali ni dhamana, na Ukhalifa alopewa ni kazi na si kitu cha kujitakabaria mbele ya watu.
"Lakini si mbora wenu"
Katika kitabu chake kiitwacho 'Khulafaa a Rrasuul' Mwandishi maarufu Khalid Muhammad Khalid (Mwenyezi Mungu amrehemu) alisema;
"Huenda akawa Kweli si mbora wao kwa vile yeye ni mwenye kuhukumu, lakini alikuwa mwenye hekima kupita wao na hii ni kwa sababu yeye ni Al Siddiq, Aliyesadiki ambaye ndani yake amekusanya Kusadiki, Imani, Uaminifu na Uongofu ulomfanya astahiki kuwa Sahibu yake Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipokuwa pangoni.
Alikuwa mwenye hikima kwa sababu alijua kuwa hatokuwa huru mpaka Umma wake kwanza uwe huru.
Hatokuwa na nguvu mpaka Umma wake kwanza upate nguvu.
Hatokuwa na Amani mpaka Umma wake kwanza  upate amani"

Kupambana na waliortadi


Baadhi ya makabila yanayoishi mbali na mji wa Madina na ambayo yaliingia karibuni tu katika Uislamu, yalianza kufanya uasi na kurtadi mara baada ya kusikia habari za kifo cha Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Walirtadi baada ya kukataa kumpa Khalifa mpya wa Waislamu mali ya zaka kama walivyokuwa wakimpa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Walisema kuwa Mwenyezi Mungu katika aya ya 103 ya Suratu Tawba anasema;
"Chukua sadaka katika mali zao, ziwasafishe na kuwatakasa kwa ajili ya hizo (Zaka) kuwataja kwa vizuri (mbele yangu) na uwaombee dua. Hakika kuwaombea kwako kutawapa utulivu na Mwenyezi Mungu ndiye asikiaye na ajuaye."
Waasi hao wakasema:
"Tulitakiwa tutoe Zaka na kumpa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) apate kututakasa kwa ajili ya hizo Zaka na kutuombea dua, lakini sasa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kesha kufa na Abubakar hawezi kututakasa na kutuombea dua kama alivyokuwa akifanya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam). Kwa ajili hiyo hakuna tena haja ya kutoa Zaka."
Sayiduna Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaamua kuingia vitani na waasi hao kutokana na sababu mbili;
1-           Aliona kuwa huko ni Kurtadi, kwa sababu Zaka ni nguzo ya tatu ya Kiislamu na kukataa kuitoa ni kuikataa nguzo hiyo.
2-           Akaona pia kuwa kuyanyamazia mambo hayo kutasababisha kutokea uasi wa aina nyingine, maana watu watakapoona kuwa pana udhaifu katika uongozi, kila mmoja atataka kuiweka sheria mikononi mwake.
Umar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu) yeye aliona kuwa kwa vile watu hao wanaukubali Uislamu, bora wasiwapige vita, lakini Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa akijulikana kwa upole hakuikubali rai hiyo na akashikilia kupigana na waasi hao.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia; "Vipi unapigana vita na watu wanaoikubali shahada ya "Laa ilaaha illa llah" wakati Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alisema kuwa; atakayeikubali shahada hiyo itahifadhika mali yake na damu yake?
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu;
"Lakini si alisema kuwa ni lazima aipe haki yake (shahada hiyo)? Na Zaka ni katika haki zake." Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alisema baadaye kuwaambia watu:
"Kisha Mwenyezi Mungu alikifungua kifua changu kuikubali rai ya Abubakar".

Jeshi la Usama


Wakati haya yakitokea, Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliona ni bora kulianzisha tena jeshi la Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu), jeshi lililoundwa na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) mwenyewe chini ya uongozi wa Osama bin Zeid (Radhiya Llaahu ‘anhu), na jeshi hilo lilikuwa limekwishapiga kambi nje ya Madina likijitayarisha kwenda kupigana na Warumi, lakini kutokana na kushtadi kwa maradhi ya Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) jeshi hilo halikuondoka.
Baada ya kifo cha Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) jeshi hilo lilirudi tena Madina, na Waislamu wakahitilafiana juu ya kulianzisha tena jeshi hilo.
Baadhi ya Waislamu akiwemo Omar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu) waliona kuwa si fikra nzuri kulianzisha tena jeshi hilo hasa wakati huu ambapo mji wa Madina umo katika hatari ya kuvamiwa na makundi ya waliortadi.
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Lianzisheni tena jeshi la Osama, kwani Wallahi hata kama mbwa wa mwitu wataninyakua basi nitalianzisha tena kama alivyofanya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)."
Alipoona kuwa Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ameshikilia jambo hilo, Omar bin Khattab (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Kwa vile Osama ni kijana mdogo sana, basi angalau ungemweka mtu mzima aliongoze jeshi hilo".
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliruka kutoka pale aliposimama na kuzishika ndevu za Omar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu), akamwambia;
"Ole wako ewe Ibnil Khatab! Amepewa uongozi na Mtume wa Mwenyezi Mungu na wewe unanitaka mimi nimuondoe?"
Ndani ya jeshi hilo walikuwemo masahaba wakubwa kama vile Omar, Othman na wengine (R.Anhum), na lilipokuwa likiondoka mjini Madina, Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawa analisindikiza huku akitembea kwa miguu na Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu) akiwa amepanda farasi.
Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye umri wake haukuzidi miaka kumi na nane wakati ule akasema;
"Ewe Khalifa wa Waislamu, bora wewe panda juu ya mnyama huyu na mimi nitakwenda kwa miguu".
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
"Wallahi utabaki juu ya farasi na mimi nitatembea kwa miguu, kwani nitakuwa nimefanya jambo kubwa sana ikiwa nitaitia miguu yangu vumbi angalau kidogo katika njia ya Mwenyezi Mungu?."
Kwa vile Abubakar alikuwa akiuhitajia ushauri na msaada wa Omar katika uendeshaji wa mambo ya Waislamu, na kwa vile Omar alikuwa miongoni mwa wanajeshi chini ya uongozi wa Osama, ilimbidi Abubakar amuombe Osama ili amruhusu Omar abaki naye Madina. Akamnong'oneza sikioni pake na kumwambia;
"Itakuwa vizuri kama utakubali kuniachia Omar, maana namhitajia katika kuendesha mambo ya Umma".
Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu), akakubali.
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) angeweza kumuamrisha Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu) juu ya jambo hilo, lakini hakufanya hivyo kwa sababu Osama (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mkuu wa jeshi hilo na mwenye haki ya kutoa ruhusa hiyo, na kama Osama angelikataa, basi asingemlazimisha.
Na jambo hili la Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuliunda tena jeshi la Osama lilisaidia sana kuyavunja nguvu makundi ya walortadi na kuingiza uoga nyoyoni mwao, maana waasi hao walipoliona jeshi hilo likitoka nje ya Madina kuelekea Sham, walisema:
"Wallahi ungekuwa mji wa Madina uko katika udhaifu na hitilafu kama tunavyosikia, basi wasingeweza kulitoa nje jeshi kubwa kama hili kupambana na Warumi".
Baada ya kuwasindikiza mpaka nje kidogo ya mji wa Madina, Abubakar akalihutubia jeshi hilo na kulijulisha juu ya misingi ya jeshi la Kiislamu linavyotakiwa liwe.
Baada ya kumshukuru na kumpwekesha Mwenyezi Mungu, akasema:
"Msifanye khiyana wala msishambulie bila taarifa (ghadran), wala msikate kate maiti za adui, wala msiue mtoto wala mzee wala mwanamke, wala msiunguze mtende wala msikate mti unaotoa mazao wala msichinje mbuzi wala n'gome wala ngamia isipokuwa kwa ajili ya kula.
Na mtakutana na watu waliojitenga ndani ya hekalu zao kwa ajili ya ibada, basi waacheni hivyo hivyo walivyo."
Kisha akasema: "Nendeni kwa jina la Mwenyezi Mungu."
Haya ndiyo maamrisho ya Kiislamu, na hivi ndivyo alivyofundishwa Abubakar na Mwalimu wake Muhammad (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam). Na hivi ndivyo majeshi ya kiislamu yalivyokuwa yakifanya kupitia karne zote.
Na waisome historia ya ufunguzi wa Kiislamu kama watakuta yale waliyofanya wao huko Algeria, Bosnia Kosovo, Afghanistan na hivi sasa Palestina. Waislamu wanachinjwa kama mbuzi na kukatwa katwa maiti zao na wengine wamezikwa wakiwa wazima, na wake zao wameingiliwa kwa nguvu na kuharibiwa, kisha wanajidai kuwa wao ni mabingwa wa kugombania haki za binadamu.

Alipotoka kwenda sokoni


Siku ya pili baada ya kuwa Khalifa wa Waislamu, Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alitoka kuelekea sokoni huku akiwa amebeba rundu la nguo.
Omar bin Khataab na Abu Ubaida (Radhiya Llaahu ‘anhu) walipomwona katika hali hiyo wakamuuliza;
"Unakwenda wapi ewe Khalifa wa Mtume wa Mwenyezi Mungu?"
Akawajibu;
"Naelekea sokoni".
Omar akamuuliza;
"Unakwenda kufanya nini sokoni na umepewa u Khalifa juu ya Waislamu?"
Abubakar akajibu;
"Wanangu nitawalisha nini?"
Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akatoa akasema;
"Itakuwa bora kama tutashauriana na masahaba wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) waweze kumjaalia Khalifa wa Waislamu malipo maalum ili aweze kujihusisha na matatizo ya Umma".
Masahaba wote wakakubali ushauri huo.

Hali chakula cha haramu


Alikuwa akihiyari kufunga mawe tumboni pake, yamsaidie asihisi njaa kuliko kuingiza tumboni mwake chakula cha haramu.
Katika Sahihul Bukhari imeelezwa kuwa;
'Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa na mfanyakazi, kijana mdogo, na siku moja kijana huyo alikuja na chakula na kumkaribisha Khalifa wa Waislamu (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekipokea na kula.
Yule kijana akamuuliza Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
'Unajuwa kitu gani ulichokula ewe Khalifa wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)?"
Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu) akauliza;
'Kitu gani?"
Yule kijana akajibu;
"Hapo zamani, zama za ujahilia (kabla ya kuwa Muislamu), niliwahi kumtabiria mtu, na mimi sijui chochote kuhusu utabiri wakati huo, nilimdanganya tu, na tokea siku ile sijaonana na mtu huyo isipokuwa leo, akanipa zawadi yangu (malipo yangu), na.'zawadi yenyewe ni hicho ulichokula."
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaingiza mkono wake kinywani na kuanza kujitapisha kwa nguvu, na yule kijana akamwambia;
'Mungu akurehemu! Yote haya (unafanya) kwa sababu ya tonge moja tu?'
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
'Wallahi kama haiwezekani kukitoa mpaka niitoe roho yangu basi nitafanya hivyo, maana nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akisema; "Sehemu yoyote ya mwili iliyojengeka kwa mali ya haramu basi Motoni ndipo panapostahiki kuingizwa mwili huo, na mimi naogopa isiongezeke sehemu yoyote ya mwili wangu kwa tonge hili".

Wakati majeshi ya Waislamu yalipokuwa yakisonga mbele kuyashinda majeshi ya Kirumi na kuteka nchi baada ya nchi, huku mali nyingi za ngawira zikiletwa Madina, Abubakar hakuyumbishwa wala kubabaishwa na yote hayo, bali aliendelea kuhukumu kwa uadilifu na kuishi maisha yale yale na kuvaa nguo zile zile na kula chakula kile kile alichokuwa akila kabla ya kuwa Khalifa.
Alipofariki dunia Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliwacha vitu vifuatavyo;
Ngamia aliyekuwa akimbebea maji, chombo cha kukamulia maziwa ya mnyama, na jokho alokuwa akilivaa anapopokea wajumbe kutoka nje, na alipoviona vitu hivyo Omar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alilia sana kisha akasema:
"Wallahi umekwisha wapa taabu kubwa watakaokuja kuhukumu baada yako."
Alikuwa akisema;
Siku ile alipobashiriwa Pepo na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alisema;
"Wallahi siamini kuwa nitaepukana na adhabu ya Mwenyezi Mungu, hata kama mguu wangu mmoja utakuwa ushaingia Peponi, huenda nikawa nimemkosea huyu au yule, kisha uje kutolewa mguu wangu Peponi na kuingizwa Motoni."
Rabia Al Aslamiy (Radhiya Llaahu ‘anhu) anasema;
"Siku moja nilikuwa nikijadiliana na Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu), akaniambia neno lililonichukiza, kisha akajuta na kuniambia;
'Ewe Rabia nirudishie kama nilivyokwambia, upate kulipa kisasi chako'
'Nikamwambia;
Sitofanya hivyo'
Akenda kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na mimi nikamfuata, hata watu wakashangaa wakasema;
'Vipi huyu mtu, yeye anakukosea kisha anakwenda kukushitaki?"
Nikawambia, 'Huyu ni Abubakar ….'
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akaniuliza;
'Ewe Rabia, kuna nini baina yako na Abubakar?'
Nikamwambia;
'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, yeye aliniambia neno lililonichukiza akataka nimrudishie ili nimlipize kisasi, nikakataa'.
Mtume akaniambia;
'Ahsante (umefanya vizuri) ewe Rabia, usimrudishie, lakini sema;
'Mungu akusamehe ewe Abubakar'
Nikasema, ' Mungu akusamehe ewe Abubakar', Abubakar akaondoka huku analia".
Musnad Imam Ahmed
Khalid Mohammad Khalid katika kitabu cha 'Khulafaa Rasuul', anasema;
"Neno moja tu ulimi uliteleza akalitamka. Halikuwa neno ovu, kwa sababu Abubakar haiwezekani atamke neno ovu, lakini neno hilo lilimchukiza Rabia likamsituwa na kumhuzunisha Abubakar aliyeshikilia kuwa lazima alipizwe kisasi.
Na kwa nini asifanye hivyo wakati aliwahi kumuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akifanya hivyo hivyo siku ile alipokuwa akiwapanga majeshi ya Waislamu katika vita, na kwa bahati mbaya alimpiga mtu mmoja kwa nguvu tumboni  pake, na alipohisi kuwa pigo hilo limemuumiza mtu huyo, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipandisha nguo yake na kulifunua tumbo lake na kumtaka mtu yule amrudishie kama alivyompiga."

Mkamuaji maziwa


Kabla ya kupewa Ukhalifa, Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akipenda kwenda kuwasaidia masikini na wazee na vilema, akiwapikia na kuwaoshea vyombo vyao na hata kuwakamulia maziwa.
Siku moja baada ya kuwa Khalifa wa Waislamu, alikwenda kuwatembelea baadhi ya wale masikini aliokuwa akiwatumikia, na mara baada ya kugonga mlango wa mojawapo ya nyumba hizo mtoto mdogo alifungua, na alipoulizwa na mamake ;
'Nani anayegonga mlango mwanangu?'
Mtoto akajibu;
'Mkamuaji maziwa amekuja, mama'
Mama alipomwona Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akastuka na kusema;
'Mwanangu, sema 'Khalifa wa Waislamu'.
Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
'Mwache, kwani ameniita kwa jina ninalolipenda kuliko yote'
Alikuwa akiwapenda masikini na akipenda kuwatumikia, na alikuwa akiwapenda watumwa na aliwakomboa wengi kwa mali yake.
Alimkomboa Amer bin Fuhayra, Zubeir, Um Absi na mwanawe, na wengi katika Masahaba waliokuwa wakiteswa na makafiri wakati ule, na siku ile alipomkomboa Bilal bin Rabah (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliambiwa na kafiri aliyekuwa akimtesa na kumuadhibu;
'Ungenambia huna isipokuwa vijisenti kidogo tu, basi ningekuuzia'
Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
'Wallahi ungelitaka hata riali mia za dhahabu basi ningelikulipa'.
Huyu ndiye Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa mwingi wa huruma, mwingi wa kuona haya, hasa anaposifiwa mbele ya watu, alikuwa akisema;
"Mola wangu nijaalie niwe bora kuliko wanavyonifikiria na unisamehe kwa yale wasiyoyajua juu yangu na usinihisabie kwa wanayoyasema."
Na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alisema juu yake;
"Mwenye huruma kupita wote katika umma wangu Abubakar"
Imam Ahmed na Ibni Haban.

Kufariki kwake


Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa Khalifa wa mwanzo wa Waislamu na alikuwa amiri wa mwanzo aliyetumwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu kuongoza msafara wa Hija katika mwaka wa tisa wa Hijri, na alikuwa wa mwanzo kuikusanya Qur-ani na kuiandika katika kitabu kimoja baada ya hapo mwanzo kuwa iliandikwa ndani ya majani, mifupa, vigogo vya miti nk.
Alikuwa akiruhusiwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) yeye na Omar bin Khattab (Radhiya Llaahu ‘anhu) kutoa fatwa hata wakati wa uhai wake Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Alifariki dunia siku ya Jumatatu mwezi 13 Jamadil akher mwaka wa 13 wa Hijri mwafaka na mwezi wa Agosti mwaka wa 634 akiwa na umri wa miaka 63, na baba yake alifariki baada yake kwa kiasi cha miezi sita.