Salman Al-Farisiy- mtafuta ukweli

Salman Al-Farisiy- mtafuta ukweli

 
Hiki ni kisa cha mtafuta ukweli. Na kwa kuanzia na tumsikilize mwenyewe Salman:
 
“Nilikuwa Isfahan katika kijiji cah Tayyan katika uajemi (Iran).  Baba yangu alikuwa ‘Dihqan’ mkuu wa kijiji chetu na alikuwa tajiri na alikuwa na nyumba kubwa.
Tokea utotoni baba alinipenda kuliko watoto wake wengine na ilifika wakati mapenzi yake yalivyokuwa makubwa aliogopa kwamba huenda nikapotea au kitu chochote kile kunifika, alinifungia ndani kama mfungwa au kama vile wasichana wari wanavyotawishwa.”
 
Anaendelea kueleza, “Dini ya kimajusi ikaniiingia kikwelikweli mpaka kufikia kupewa cheo cha mwenye kuulinda moto tuliokuwa tukiuabudu. Kazi yangu ni kuhakikisha moto ule unawaka bila  kuzimika mchana na usiku kila siku.
 
 Baba alikuwa na shamba kubwa ambalo lilitoa mazao ya kutosha na mwenyewe baba alilishughulikia na kusimamia mavuno.  Siku moja ‘Dihqan’ akiwa katika kazi zake aliniambia: “Mwanangu kama unavyoniona, nina shughuli nyingi sana leo na sitoweza kwenda shamba nendo leo kaangalie na kulikagua.”
 
Nikiwa njiani, nikapita njia moja ambako kuna kanisa na nilisikia sauti za maombi na yalinivutia. Sikujua chochote kuhusu ukristo, wala dini nyenginezo kwani nilikuwa ‘mtawa’ na nilipozisikia zile sauti nikaingia ndani kanisani kuona mwenyewe nini wanafanya watu hawa.
 
Nilipendezwa na jinsi wanavyosali na kuvutika na dini yao, nikajisemea, “Hii ni bora kuliko yetu, sitoondoka mpaka jua litue.”
Nilipouliza nikaambiwa dini hii asili yake ni Sham. Lile hasa nililotumwa na baba sikulifanya kwani sikufika shamba na ulipoingia usiku nilirudi nyumbani.  Baba aliponiuliza nikamfahamisha kukutana kwangu na wakristo na kumfahamisha jinsi nilivyovutiwa nao. Baba akanishangaa na kuniambia, “Mwanangu hakuna chochote kizuri katika dini yao, dini yako na wazazi wako ni bora zaidi.” Lakini mimi nikasisitiza, “hapana baba dini yao ni bora kuliko yetu.”
 
Baba hakufurahishwa na mtazamo wangu na akaingiwa na khofu kwamba nitaacha dini yangu. Kuona hivyo akaamua kunifungia na kunitia minyonyoro miguuni. Niliwahi siku moja kupenyeza ujumbe kuwambia wakristo wanipe habari za msafara wowote utakaoendea Syria.  Ilipokuwa tayari wakanipa habari niliweza kujifungua ile minyororo  niliyofungwa na kutoroka kwa kujificha mpaka nikajiunga na msafara. Na niliulizia kiongozi wao nikelekezwa kwa Askofu mmoja, nikenda kumuona na kusema:
“Ninataka kuwa mkristo na nitapenda kujifunga na kanisa na  nijifunze kutoka kwako na kusali pamoja na wewe.”
 
Askofu akanikubalia. Muda mchache tu baadae nikagundua kwamba Askofu huyu hakuwa mkweli  wala  hakuwa na uadilifu kwani alikuwa akiwaamrisha wafuasi watoe sadaka huku akiwaahidi kurehemewa.  Watu wanapotoa sadaka, Askofu badala ya kuzitumia kwa njia ya kheri kama kuwapa masikini na wanaohitaji, alikuwa akizitia mfukoni mwake.  Aliweza kujikusanyia fedha na dhahabu nyingi kwa njia hii. Alipokufa na walipotaka kumzika nikawaeleza wale wafuasi tabia mbaya ya Askofu wao .
 
Waliniomba niwaoneshe alipoficha sadaka hizo. Niliwaonesha na walipoona machupa yaliyojaa dhahabu waliingiwa na ghadhabu na kusema, “Hatukuziki tena na badala yake wakamsulubu na kumpiga mawe.”
 
Niliendelea kumtumikia mrithi wake na alikuwa tofauti na wa kabla yake kwani alikuwa mtu wa dini na  mwenye kuitafuta akhera. Alikuwa akiabudu mchana na usiku.  Nilipendezwa nae sana na kutumia muda mwingi pamoja naye. Alipokufa, nikajifunga na watumishi tofauti wa kanisa katika miji mbali mbali baada yake. Wa mwisho kukutana naye akanieleza kuja kwa Mtume Muhammad (SAW) katika ardhi ya waarabu ambao alikuwa mkweli na kukubali zawadi lakini kukataa kuitumia sadaka, Salman aliendelea.
 
Kundi la viongozi wa kiarabu wa kabila la Kalb lilipita Ammuriyah, niliwaomba wanipeleke ardhi ya waarabu na kuwalipa kiasi cha pesa nilichonacho. Walikubali na tulipofikia Wadil Qura (mji katikati ya Madina na Syria) walivunja ahadi yetu na wakaniuza kwa myahudi. Nikawa mtumwa wa kumfanyia kazi bwana wangu huyu ambaye naye akaniuza kwa jamaa yake kutoka Banu Quraydha, akanichukua Yathrib.
 
Kipindi hicho, Mtume (SAW) alikuwa akiwalingania watu dini ya kiislam Makka.  Siku moja nilikuwa juu ya mtende, wakati  bwana wangu alitembelewa na jamaa yake akasema:
 
“Mungu awaapize na kuwapiga vita Aws na Khazraj (makabila mawili makubwa ya madina).   Wanakusanyika Quba leo hii wakijiandaa kumpokea mtu mmoja kutoka Makka anaedai kuwa ni Mtume”
 
Niliposikia maneno haya niliingiwa na baridi ya ghafla na kuanza kutetemeka kwa nguvu mpaka niliogopa huenda nikamuangukia bwana wangu nikashuka na kumuuliza tena, “unasema nini?, Hebu rudia!
 
Bwana alikasirika na kunibamiza kibao na kuniambia, “inakuhusu nini wewe rudi nenda ukafanye uliyotumwa.”
 
Jioni yake nikakusanya tende kidogo na kwenda sehemu Mtume amefikia na kumwambia,
 
“Nimesikia wewe ni mtu mkweli na muadilifu na kwamba una masahaba ambao ni wageni na wanahitaji msaada hii basi ni sadaka yangu, nnahisi lakini wewe utahitajia zaidi kuliko wengine.
 
Mtume (SAW) akawapa masahaba na yeye hakula hata kidogo. Sifa ya uadilifu na yale maneno aliyoambiwa na maaskofu wa kikristo kuyathibisha mwenyewe Salman kwa Mtume (SAW) ni moja katika sababu zilizomfanya asilimu.  Mtume (SAW) alimkomboa pamoja na Salman mwenyewe kuingia mkataba na bwana wake kwamba akimpa cha kiasi fulani cha mitende angekuwa huru.
 
Mara nyingi akiulizwa yeye ni mtoto wa nani, hujibu “ni Salman mtoto wa kiislam kutokana na kizazi cha Adam”
 
Salman alikuwa na nafasi muhimu sana katika harakati za kupanuka kwa uislam. Katika vita vya Khandaq ni yeye aliyekuja na rai ya kuchimbwa Khandaq kuizunguka Madina.  Hata Abu Sufiyan alipoona mbinu hii alisema “waarabu hawajawahi kutumia mbinu hii kabla”
 
Alipokuwa Amir wa Al-Madain (Ctesiphon) karibu na Baghdad, Salman alikuwa akipata ruzuku ya Dirham 5000.  Zote hii huzitoa sadaka. Alijikimu mwenyewe kwa kilimo chake cha mitende mpaka baadhi ya watu wakasema, “wewe ni Amir na rizki yako ni ya uhakika kutoka baytul maal na bado unafanya kazi hii.”
 
“Ninapenda kujilisha kwa mikono yangu mwenyewe”, Salman aliwajibu. 
Inasemekana siku moja alimtembelea Abu Dardaa na kumkuta mkewe katika hali mbaya sana na akamuuliza “una kitu gani?”
“Ndugu yako hana habari kabisa na hii dunia akajibu, alipokuja Abu Dardaa alimkaribisha Salman chakula alipomwomba haya na tule basi, Abu Dardaa akasema, mimi nimefunga!”
 
“Wallahi na mimi sili mpaka na wewe ule.”
Salman alikaa siku hiyo hadi usiku na Abu Dardaa alipotaka kuamka kwa ajili ya ibada, Salman akamzuia na kumwambia:
“Ewe Abu Dardaa mola wako ana haki juu yako, Aila (Familia) yako ina haki juu yako na mwili wako una haki juu yako, kipe kila kimoja haki yake.”
 
Asubuhi yake walisali pamoja na baadaye kwenda kwa Mtume (SAW).  Mtume alimuunga mkono Salman.
 
Salman alibahatika kuwa mtu mwenye elimu, hekima na busara.  Ali ibn AbiTalib aliwahi kumfananisha Salman na Luqman.  Kaab Al-Ahbaar  naye anasimulia: “Salman alikuwa na elimu na busara kama mfano wa bahari isiyokauka.”
 
Alikuwa na elimu ya vitabu vya ukristo, Quran na pia majusi na aliwahi kutafsiri baadhi ya sura za Quran kwa lugha ya kifarsi wakati wa Mtume (SAW).  Anahesabika kama ni mtu wa kwanza kuifasiri Quran katika lugha isiyokuwa ya kiarabu.
 
Kwa mujibu wa riwaya za uhakika alifariki mwaka 35 Hijiria enzi za Ukhalifa wa Uthman huko Madain (Ctesiphon).