Hakim ibn Hazm- rafiki wa Mtume (SAW)





Hakim ibn Hazm- rafiki wa Mtume (SAW)
 
Historia inanukuu kwamba Hakim ni mtu pekee aliyezaliwa ndani ya Al-Kaabah!
 
Mama yake, akiwa pamoja na marafiki zake, siku hiyo waliitembelea Al –Kaaba ilikuwa wazi kwani kulikuwa na sherehe enzi za Ujahiliya.  Akapatwa na uchungu na hata kushindwa kwenda wala kusogea pahala pengine. Likaletwa busati na kujifungua Hakim hapo hapo.  Baba yake ni Hazm ibn Khuwaylid, ndugu yake aliekuwa mke wa Mtume (SAW) bi Khadija bint Khuwaylid (RA).
 
Alikuwa katika utajiri na neema hasa kutokana na nasaba yake kuwa yenye hadhi na heshima. Alikuwa mstaarabu na mwenye khulka nzuri mpaka kuweza kuheshimiwa na watu wa rika tofauti.  Alikabidhiwa jukumu la ‘rifada’ kitengo maalum cha kuwasaidia wenye shida na waliopoteza mali zao msimu wa Hijja.  Alifanya kazi hii kwa uadilifu na ikhlaas mpaka wakati mwengine alikuwa akitoa katoka mfuko wake mwenyewe.
 
Hakim alikuwa rafiki wa karibu wa Mtume (SAW) kabla ya kupewa utume.  Ingawa alimzidi umri Mtume (SAW) kwa takriban miaka mitano, alikuwa akitumia muda wake mwingi pamoja na Muhammad ibn Abdullah.  Uhusiano wao huu ulikuja pata nguvu zaidi pale Mtume (SAW) alipomuoa shangazi yake, Bi Khadija bint Khuwaylid.
 
Kilichoshangaza zaidi, licha ya kuwa na urafiki wa karibu na Mtume (SAW), lakini hakusilimu mpaka Makka ilipofunguliwa, ikiwa ni zaidi ya miaka ishirini baadaye.  Mtu kama Hakim mstaarabu na mwenye busara na kuwa na karibu sana na Mtume (SAW) angelihesabika katika miongoni mwa watu wa awali kusilimu, lakini hali haikuwa hivyo.
 
Kama waislam walivyoshangaa Hakim kuchelewa kuingia uislam, Hakim mwenyewe naye pia alijishangaa hasa baada ya kuonja tamu ya imani, akajuta kwa kila muda katika maisha yake alioupoteza akimshirikisha Allah (SW) na kumkataa Mtume Muhammad (SAW).
 
Siku moja, mwanawe alimuona baba yake akilia na kumuuliza, “kwanini  unalia baba?”
 
“Vitu vingi tu mwanangu mpenzi” alijibu Hakim huku akindelea:
 
“Zaidi ni kuchukua muda mrefu mpaka kusilimu kwangu, ningeliwahi kungelinisaidia kupata wasaa wa kufanya mambo mengi mema ambayo nimeyakosa hata kama ningelipewa dhahabu kuitumia kwenye ardhi.  Nilinusurika vita vya Badr na pia vita vya Uhud, baada ya vita vya Uhud nikajisemea sitowasaidia tena maquraysh dhidi ya Muhammad (SAW) na sitoondoka tena Makka.”
 
Aliendelea, “Ikinijia kutaka kusilimu, huwaangalia watu wengine miongoni mwa maquraysh, watu waliokuwa na nguvu na upeo wa mambo na kusimama kidete kwenye hadhara na vitendo vya kijahiliya.  Basi hurudi nyuma na kuungana nao na majirani zao….. Allah! (SW) najuta kwa nini sikusilimu, na kufuata wazee na mababu zetu tu bila ya kuwa nadhari; kwanini nisilie mwanangu?”
 
Hata Mtume Muhammad (SAW) alishindwa kumwelewa Hakim ilikuwa kuwaje mpaka uislam ukawa umejificha kwake?  Mtu mwenye hekima, busara na haiba kubwa kama Hakim nini chengine anahitaji kuuona ukweli na haki?
 
Kwa muda mrefu Mtume(SAW) alikuwa akitamani kundi la watu fulani kuingia uislam.  Siku ya kukombolewa Makka, Mtume Muhamad (SAW) alisema kuwaambia Masahaba:
 “Kuna watu wane Makka ambao ninawachukulia kutojishughulisha na shirk, na ningependelea kama wangesilimu.”
Masahaba wakauliza, “Ni nani hao, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu?.
 Ibn Usayd, Jubayr ibn Mutim, Hakim ibn Hazm na Suhayl ibn Amr” 
Kwa rehma zake Mwenyezi Mungu wote hawa walikuja kusilimu pale Muhammad (SAW) alipoingia Makka na kuikomboa kutoka katika ukafiri, ujinga na ujahili na alitoa kinga kwa kusema:
“Yoyote atakayetamka ‘Ash-hadu ana-laa ilaha ill  allah wahdahuu laa sharika lahu wa ana Muhamaad Abuduhu warasuuluhu” basi yuko salama.” “Yoyote atakayebaki Al kaaba na kuweka silaha chini basi yuko salama.  Yoyote atakayekwenda nyumba ya Abu Sufiyan, basi yuko salama. Na yoyote  atakayekwenda nyumba ya Hakim ibn Hazm, yuko salama…….. 
Hakim alitamka ‘kalima’ bila ya kinyongo na kuapa kwamba zile juhudi zote alizokuwa akizitumia kuupiga vita uislam sasa atazitumia kwa ajili ya uislam.
 
Hakim alimiliki ‘Darun nadwa’ lililokuwa jengo la kihistoria Makka kwani lilikuwa ‘ jengo la bunge’ ambapo maquraysh hukutana zama za ujahiliya kupanga njama za kumpiga vita Mtume (SAW).
 
Aliamua kuachana nalo kabisa jengo hilo na kukata mawasiliano yake yote nalo na hatimaye kuliuza kwa Dirham laki moja, mpaka kijana mmoja wa kiquraysh akamhoji, ‘umeuza’ kitu cha  thamani na hadhi na historia ya waquraysh!”
 
“Njoo mwanangu; hadhi na utukufu wote umekwisha na chote kilichobaki cha thamani ni taqwa.  Mimi nimeuza jumba hili ili nikapate nyengine peponi. Wallahi fedha yote niliyoipata kwa kuliuza nimezitoa zitumike kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (SW)” akamjibu Hakim.
 
Hakim alitekeleza ibada ya Hijja na alikwenda na ngamia mia walio bora na wote kuwachinja ili apate kuwa karibu na Mwenyezi Mungu na Hijja iliyofatia alisimama Arafa akiwa pamoja na watumwa wapatao mia, kila mmoja akampatia nishani ya fedha ambayo imeandikwa ‘Uko huru kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kutoka kwa Hakim ibn Hazm’
Ilipokuja Hijja ya tatu, alikwenda na kondoo elfu moja na na akawachinja wote Mina ili kuwalisha maskini na yote hayo alifanya ili apate kuwa karibu na Allah (SW).
 Ingawa alikuwa mkarimu mno na kutumia mali zake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (SW).  Hata hivyo, alipenda na yeye kuwa na kingi.   Baada ya vita vya Hunayn, alimuomba Mtume (SAW) ngawira aliyokuwa akiigawa na akapewa, akaomba aongezwe, akaongezwa.  Kwa kuwa Hakim alikuwa mwanagenzi katika uislam, Mtume (SAW) alikuwa mkarimu zaidi kwa wanagenzi ili kuwazoea nyoyo zao.  Hakim akapata ngawira nyingi sana lakini Mtume (SAW) akamwambia kwa kumkumbusha; “Ewe Hakim! Hakika utajiri ni mtamu na unapendeza. Yoyote atakaeuchukua kwa uchu hatorehemewa nao, itakuwa kama mtu anakula bila ya kutosheka, mkono ulio juu bora kuliko mkono ulio chini (ni bora kutoa kuliko kupokea). 
Maneno haya ya hekima na busara kutoka kwa Mtume (SAW) yalimwingia Hakim vizuri sana akilini mwake na hapo kumwambia Mtume (SAW);
“Ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu ambaye amekutuma kwa haki sitoomba tena baada yako  kitu chochote.”
 
Enzi za Ukhalifa wa Abubakar, Hakim aliitwa mara kwa mara kwenda kuchukua ruzuku yake kutoka Baytul-Mal lakini alikataa na enzi za Umar pia akaendelea na msimamo wale mpaka Umar akawahutubia waislam:
“Nnashuhudia kwenu enyi waislam kwamba nimemwita Hakim kuchukua ruzuku yake lakini anakataa.”
 
Hakim akawa mkweli kwa ahadi yake kwani hakuchukua kitu chochote, alipata funzo kubwa kutoka kwa Mtume (SAW) kwamba kukinai ni utajiri usiokuwa na mfano!