Fayruz Ad-Daylami-muuaji wa al-Aswad mkadhibishaji





Fayruz Ad-Daylami-muuaji wa  al-Aswad mkadhibishaji
 
Mtume Muhammad (SW) aliporudi Madina baada ya kutekeleza Hijjatul Widaai (hija ya kuaga) alianza kuugua, habari za kuugua kwake zikaenea bara arabu yote na waislam wa kweli kusikitishwa sana na kwa wengine wakaiona hii kama ni fursa ya kuonesha misimamo yao halisi dhidi ya Uislam na Mtume.  Kwani lile chaka la unafiki walilojivika nalo halikuwa na haja tena.
 
Huko, Al-yamama Musaylamah mnafiki na muongo akuaukana uislam.  Katika mji wa Asad, Tulayhah al-Asadiy akartadi na Yemen Al aswad al Ansi nae pia akartadi. Wazandiki hawa watatu hawakuishia hapo bali nao wakadai kwamba ni mitume wametumwa na Mwenyezi Mungu kwa kaumu zao kama alivyokuwa Muhammad (SAW) alivyotumwa kwa maquraysh.
 
Al-Asad alikuwa mwana mazingaombwe Hata hivyo, alijaaliwa kuwa na kipaji cha kusema na kuweza kuwadanganya watu kwa yote ayakayoyasema. Alikuwa na uwezo na nafasi katika jamii yake aliweza kuwavuta watu wa aina zote matajiri, masikini, wakubwa, wadogo, wanawake na wanaume.  Na alikuwa na kawaida ya kuvaa “niqaab” kizoro kuficha uso wake na kuwazidishia watu kumshangaa na kupumbaa.
 
Katika mji wa Yemen siku hizo, ukoo wa Abna ulikuwa ni moja katika koo maarufu na kutajika sana.  Abna ni mchanganyiko wa waajemi waliokuwa wakitawala Yemen ambao waliwaowa waarab wa kiyemen na kuchanganyika nao. Feyruz Ad-Daylam alikuwa ni mmoja wa hawa waabna.
 
Wakati wa kuja Uislam, Yemen ilitawaliwa na Wa-abna na Badhan alitawala Yemen kwa niaba ya Waajem1 wa kichosroes. Badhan aliposikia habari za Uislam zilimuingia vyema na kuzikubali pamoja na kumkubali Mtume (SAW) na risala yake.
 
Alijitenga na Wachosroes na kuingia Uislam na wafuasi wake wakamfuata na kuingia Uislam kwa wingi.  Mtume (SAW) akampa heshima ya kuendelea kutawala Yemen mpaka kufariki kwake muda mfupi kabla ya kuibuka kwa al-Aswad al-Ansi.
 
Ukoo wa Al-Aswad-Banu Mudh-hij- walikuwa wa kwanza kuukubali “utume”wa al-Aswad.  Akiungwa mkono na kabila lake lililokuwa na nguvu al Aswad alianza kuvamia miji ya karibu na kuanzia Sanaa ambako akamuua mtawala wake, Shah ibn Badhan na kumtwaa mkewe kwa nguvu. Akaendelea kuvamia miji mengine mpaka maeneo kutoka Hadhramawt mpaka Taif na kutoka Al-Ahsa mpaka Aden yakawa chini yake.
 
Al-Aswad alikuwa mjanja na mwerevu sana kuweza kuwadanganya watu na kuwatapeli kwa mbinu aina kwa aina.  Alidai kwamba alitembelewa na Malaika na kumteremshia wahy na kumpa bishara ya kuweza kuwajua watu na mambo yao. Kilichomsaidia ni mashushushu aliokuwa nao kila pembe ambao humletea habari zao, matatizo, siri, matarajio na wasi wasi wao.
 
Kwa mbinu hii akija mtu kwake na kuelezwa yale aliyokuwa nayo vile vile yalivyo hushangazwa sana na kuzidi kuchanganyikiwa na kumkubali. Alipata wafuasi wengi kwa ujanja wake huu.
 
Habari za al-Aswad, kurtadi na kudai utume zilipomfikia Mtume Muhammad (SAW), alituma ujumbe wa masahaba kumi wakiwa na barua rasmi, kwa masahaba wa Yemen ambao alikuwa akiwaamini. Akawahimiza kuikabili fitna hii ya Al-Aswad na kuzidisha imani.  Pia akawaamrisha wamuondoshe Al-Aswad kwa njia yoyote ile.
 
Wote waliobahatika kupata barua za Mtume (SAW) walianza mara moja kupanga mbinu za kuikabili fitna. Mmoja wapo wa watu hawa ni Fayruz.  Fayruz mwenyewe anaeleza:
 
“Mimi na wa-Abna waliokuwa pamoja na mimi hatukuwa na shaka hata mara moja kwa dini ya Mwenyezi Mungu.  Hakuna imani yoyote katika maadui wa Mwenyezi Mungu iliyoweza kutuingia katika nyoyo zetu bali tulisubiri na kutafuta wakati mwafaka wa kumkamata Al-Aswad na kumpoteza kwa njia yoyote”. Aliendelea kusema, “Na tulipopata barua kutoka kwa Mtume Muhammad (SAW) ilituzidishia imani yetu na kutupa nguvu zaidi na kila mmoja wetu akawa na ari kwa lile atakalolifanya.”
 
Baada ya kupata mafanikio katika mpango wake, jeuri na kiburi vikamuingia Al- Aswad mpaka akawa anaanza kumuonea choyo kamanda wake mwenyewe wa majeshi, Qays ibn Yaghuth na aliwahi kumwambia anaonekana kuwa na nguvu sana.  Qays alihisi moja kwa moja kwamba usalama wake uko hatarini hasa baada ya kuona mahusiano yake na Al-Aswad hayakuwa mazuri.
 
Anaendelea kusimulia Fayruz, “tukatoka mimi na bin ami yangu Dadhaway na kwenda kwa Qays. Tulimfahamisha kuhusu ujumbe wa Mtume (SAW) na tukamuomba ajumuike nasi tumfanye ‘asusa’ al-Aswad kabla ya al-Aswad hajamfanya yeye Qays ‘asusa’.  Alitukubalia na kuanza kutupa baadhi ya siri za al-Aswad.
 
Sote watatu tulikubaliana kukabiliana nae chini kwa chini kwani tulikuwa karibu naye na wenzake wengine kukabiliana nae kwa njia nyengine, tukielewa kwamba Dadha (Al-Aswad alimchukua kwa nguvu na baadaye kumuua mume wake) bin ami yetu nae pia angelituunga mkono. Tulikwenda kwake na Fayruz kumwambia Dadha, “ewe bin ami, umeona madhara na ubaya wa huyu mtu aliyoyafanya kwako na kwetu. Amemuua mumeo na kuwadhalilisha wanawake wote wa ukoo wako, amewauwa waume zao na kuwanyang’anya madaraka.”
“Hii ni barua kutoka kwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu (SW), kwetu sisi hasa na kwa watu wa Yemen kwe ujumla katutaka tuiondoe fitna hii.  Je! uko tayari kutusaidia?”Akauliza, “vipi nnaweza kusaidia?”Feyruz akajibu, “kumfanya aukimbie mji……….au hata kumuua.”
“Wallahi”, akasema Dadha, “mawazo yangu yote yako huko kumuua”. Aliendelea, “ila niliogopa kushauri hilo. Sijawahi kumuona mtu mbaya na mkatili kuliko huyu (al-Aswad), na Mwenyezi Mungu (SW) hajamuumba mtu mwengine anayechukiza zaidi yake isipokuwa shetani na nnaahidi kwa Mwenyezi Mungu (SW) aliyemtuma Mtume Muhammad (SAW) kutuamrisha mema na kutukataza mabaya, mimi sikuwa na shaka hata kidogo katika dini yangu”
 
Fayruz akauliza, “sasa vipi tutammaliza?” Baada ya kufikiri, akasema Dadha, “huyu mtu ana ulinzi wa hali ya juu.  Hakuna hata sehemu moja katika kasri yake hapajazungukwa na walinzi, ila kuna chumba kimoja kibovu na kimeelekea nje siku ya tatu tokea leo usiku, nendeni kwenye chumba hicho mtakuta silaha na mimi nitawasubiri…….”
 
Lakini Fayruz akalalama na kusema, “kupita kwenye kasri lenye ulinzi mkali mpaka kufika kwenye hicho chumba bila ya kuonekana na walinzi haitokuwa kazi rahisi.”
Dadha akajibu, “ni kweli lakini nina wazo”. Aliendelea, “mtumeni mtu kesho ambaye mnamuamini aje kama mfanyakazi, nitamfahamisha atengeneze njia kwenye chumba ya kuweza nyinyi kupita kwa urahisi” “Sasa umesema, hilo ni wazo zuri”, akamalizia Fayruz.
 
            Tukaenda kujiandaa na kuwafahamisha waumini wengine waliokubali kutusaidia nao pia wajiandae kwa ajili ya vita na tukawapa aina ya ishara tutakayotumia kuashiria kuanza kuvamia. Ulipoingia usiku na wakati kufika tulienda mimi na wenzangu wawili mpaka kwenye chumba tulichofahamishwa na kuingia ndani ya kasri.  Tukakuta silaha na kuzichukua tukielekea chumba cha adui wa Mwenyezi Mungu. Tulimkuta bin ami yetu Dadha akitusubiri na kutuonesha chumba alicholala Al-Aswad na tukaingia.  Tulimkuta amelala  fofofo huku akikoroma. Fayruz akatoa upanga na kumkata shingo yake kwa pigo mmoja tu na Al-Aswad kutoa mayowe kama fahali la ng’ombe linapochinjwa.
 
Walinzi waliposikia mayowe yale wakakimbilia chumba cha Al-Aswad na kumkuta Dadha mlangoni na walipomuuliza, “ kulikoni”, aliwajibu, “msiwe na wasi wasi, mnaweza kwenda, mtume wa Mwenyezi Mungu anapokea Wahy”. Kusikia kauli hii kutoka kwa mkewe walinzi hawakushughulika na wakaondoka kuendelea na lindo.
 
Ilipofika alfajiri, Fayruz akasimama kwenye ukuta wa kasri na kuanza kuadhini, “Allah Akbar, Allah Akbar na kuendelea mpaka alipofika Ash-hadu anna Muhammad Rasul Lllah! Kisha akaongeza Wa ash-hadu annal Aswad al Ans kadhaab!” na nnashuhudia kwamba Al-Aswaad ni muongo!
 
Hii ndiyo ilikuwa ishara waliyokuwa wakiisubiri wapiganaji jihadi wa kiislam waliokuwa nje wakisubiri. Wakaanza kulivamia kasri kila pembe na kuwapiga walinzi. Kwanza walinzi walishtushwa na adhana ndani ya kasri, halafu wakasikia takbira ‘Allah Akbar’ za waislam zikitokea kila kona.Wakaanza kukimbia wasijue la kufanya huku wanajihadi wakiwavamia.
 
Kulipopambazuka vita vilikwishamalizika na asubuhi yake tu Fayruz na masahaba wengine wakaandika barua yenye habari njema kwenda kwa Mtume (SAW) Madina, habari ya kuuwawa kwa mkadhibishaji na muongo mkubwa al-Aswad.
 
Kwa bahati mbaya ujumbe ulipofika Madina wa barua, wakakuta tayari Mtume Muhammad (SAW) amefarika usiku wake tu! Hata hivyo walifahamishwa kwamba Mtume (SAW) aliteremeshiwa wahy kufahamishwa kuuwawa kwa Al-Aswad siku ya tukio lilipotokea.
 
Miaka ikapita na Khalifa Umar ibn Al Khattab alimuandikia barua Fayruz, “nimepata habari kwamba umeshughulika na kula mkate na asali (akimaanisha hakuwa na harakati zozote).  Itakapokufika barua hii tafadhali uje na kwa rehema zake Mola, kujumuika nasi katika njia ya Mwenyezi Mungu.
 
Fayruz akatekeleza amri ya Amirul muuminiin na kwenda Madina. Alipofika akaomba kuonana na Umar na kuruhusiwa.  Kulikuwa na watu wengine pia wakitaka kumwona. Akatokea kijana wa kikuraysh na kumsukuma Fayruz na kutaka kuingia ndani.  Fayruz akampiga yule kijana na kumuumiza kwenye pua. Kijana alipofika kwa Khalifa na alipomuona tu akamuuliza:
“Ni nani aliyekupiga?” Akajibu kijana “ Fayruz, yuko mlangoni” Fayruz akaingia na Umar akamuuliza, “Fayruz nini tena hiki?” Akajibu, “Yaa Amirul Muuminiin uliniandikia barua na wala huyu kijana hukumuandikia, uliniruhusu niingie na wala hukumruhusu na alitaka kuingia kabla yangu, kisha nikafanya kama ulivyoambiwa.”
Umar akatoa hukumu pale pale, “kisasi!” akimaanisha maadam Fayruz amempiga yule kijana basi na yeye apigwe. Fayruz akauliza, “kwani ni lazima hicho kisasi?” Umar akajibu, “ni lazima”
 
Fayruzi akainama na kuweka magoti yake chini na kijana akajiandaa kurudisha lile pigo alilopigwa pale puani.  Wakati akijitayarisha kupiga, Umar akamwambia, “hebu subiri kidogo kijana!  Ngojea nikwambie kitu ambacho nilisikia kwa Mtume (SAW).  Nilimsikia jioni moja akisema,” “usiku huu al-Aswad al-Ans aliedai kuwa ni mtume ameuwawa.  Fayruz Ad-daylami muungwana na muadilifu amemuua” Kisha Umar akamuuliza yule kijana, “bado unajihisi kulipiza kisasi baada ya kusikia yale niyoyasikia kwa Bwana Mtume Muhammad (SAW)? Kijana akasema, basi nimemsamehe baada ya kuniambia haya maneno, kutoka kwa Mtume wa Allah (SW).
 
Fayruz hakuridhika bado na kumuuliza khalifa, “hivi unafikiri, kusalimika kwangu huku ni kwa mimi kukiri kosa na kwamba msamaha wake haukuja kwa kurubuniwa?”
“Naam”, Umar akajibu
“Nnakuzawadia upanga wangu, farasi wangu na elfu thelathini katika fedha zangu kama zawadi kwako”,akamwambia yule kijana.
Amirul muuminiin akapendezwa sana na tukio hili la Fayruz, ghafla kuwa hasira na papo papo kuwa takrima na kumwambia yule kijana wa kiquraysh, “unaona msamaha wako umezaa matunda, tayari uko tajiri sasa hivi.”