Jinsi ya Kujifunza Eimu ya Dini



Katika vigezo vya kuviangalia katika kujifunza elimu ya dini.

1            Kutokuwa na pupa.

Muislamu hujifunza na kufundishwa pole pole na kwa ya uwezo wake na hali yake. Anasema Ali ibnu Abi Talib Allah amuwie radhi katika Hadithi mauquuf (ambayo haikutajwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi wasallam imesita kwa sahaba tu) ilivyopokewa na Bukhari katika mlango wa kubagua katika elimu nani wa kumsomesha na wa kutomsomesha kuogopea kutofahamu kwamba:

                   حدثوا الناس بما يعرفون، أتحبون أن يكذب الله ورسوله   
   
Zungumzeni(elimisheni) na watu kwa yale wanayoyajua kwani mnapendelea kukadhibishwa Allah na Mtume wake?

Kujifunza pole pole na kwa mpangilio humsaidia mwenye kutafuta elimu kufahamu aliyofundishwa kwanza kabla ya kupata maelezo ya kina. Vyenginevyo athari zake zinaweza kuwa kama alivyosema mmoja katika mataabi’i Azzuhriy pale aliposema:

                                     جُمْلَةً فَاتَهُ جُمْلَةً مَنْ طَلَبَ الحَدِيثَ      

Mwenye kuitafuta hadithi zote kwa mpigo basi hupitwa na zote kwa mpigo.

Kwanza ni vizuri kupata msingi kwa kusoma vitabu vidogo vidogo kabla ya kuendelea na vitabu vikubwa.

2            Kutazama unapoitafuta na kuichukua elimu

Mwenye kuitafuta elimu anapaswa kuangalia vizuri wapi anaipata elimu hii. Hili limekuwa suala muhimu katika ulimwengu wetu wa leo kwa jinsi elimu ilivyoenea. Si kila linaloandikwa au kuzungumzwa kuhusu uislamu ni elimu na pia kuwa na tahadhari kama alivyosema Imaam Muhammad ibn Sireen Allah amrehemu:

"Hii ni elimu ya Dini, kwa hivyo kuwa muangalifu ni kutoka kwa nani unaichukua Dini yako."

3          Kuitafuta kutoka vyanzo vilivyo na uhakika

Elimu tuliyonayo inakuja katika hali tofauti. Enzi za zamani tulikuwa tukimtegemea sana Ustaadh au Mwalimu kutufundisha. Enzi hizi nafasi ya kusoma kutoka kwa walimu imekuwa ndogo sana na hivyo kutegema elimu kutoka katika vyanzo ambavyo vinahitaji utafiti kwanza kujua uhakika wake kama mitandao,tovuti, televisheni, kaseti, Dvds na kadhalika.

Walimu wamegawika aina mbili walimu wadarisishaji na na walimu watendaji. Mdarisishaji ni mwenye kuelimisha bila ya yeye mwenyewe kuathirika nayo na hivyo kutoyatekeleza yale anayoyafundisha. Mwalimu mtekelezaji ni mwenye kufundisha na kuonekana athari ya elimu yake katika mwenendo na murua wake,vitendo na tabia zake, kauli na matamshi yake. Walimu wa aina hii hujulikana kama Rabbaaniyiin – walimu walezi. Kwani tukichukua elimu kutoka kwa walimu wa aina hii hufaidika kinadharia na kivitendo. Tofauti na mwalimu mdarisishaji ambae husomesha bila ya kuathiri. Kigezo hichi alikuwa nacho Mtume wetu kama pale bibi Aishah Allah amuwie radhi alipowahi kuulizwa kuhusu tabia ya Mtume  صلى الله عليه وسلم
 akasema tabia yake ilikuwa (kama) Qur’aan.   

Kutegemea nyenzo za kisasa katika kujielimisha pia tunatakiwa tuwe na uhakika na nyenzo hizo kama ni za kutegemewa au laa. Makala yaweza kuonekana ni nzuri lakini kumbe chanzo chake si cha uhakika. Dvd yawezekana kuwa ni maridadi na mhadhiri anazungumza kimahiri lakini kauli zinazotoka kwake zina mushkeli.

4          Kujiepusha na tofauti za Maulamaa

Kwa mwenye kuanza kutafuta elimu lengo ni kuwa na maarifa na si kujua Sheikh fulani kasema kitu gani na sheikh huyu mbona kasema hivi. Daraja hii si kwa wanaoanza na wale ambao bado msingi wao wa elimu ni mdogo. Ikiwa msingi wa kuanzia ndio huu basi lengo hapa huwa si kutafuta elimu bali ni kujitapa mbele ya Maulamaa na kushindana nao au kujilabu mbele ya wasiokuwa na elimu na kuwabeza. Mwenye kutafuta elimu hujifunga katika fani moja au mbili mpaka aielewe vilivyo na si busara katika hali – mustawaa – huu kujaribu kupitia vitabu tofauti kwani si wakati wake. Au kuanza kutafuta tofauti kati ya Maulamaa na kuanza kuwatia dosari na makosa na kuwapongeza wengine.
Elimu yetu ya dini imegawika sehemu mbili. Kwanza ni elimu wanayopaswa kusomeshwa waislamu wote kwa ujumla kwani hakutokuwa na madhara yoyote endapo itasomeshwa. Na kila mtu ataipokea atasikiliza na kunufaika nayo. Na elimu nyengine ni maalum kwa waliokuwa na upeo miongoni mwa waislamu. Elimu hii kufundishwa kwake huenda kukaleta madhara zaidi kuliko faida mpaka mwenye kuitafuta afikie sifa za kuweza kuifahamu vyema na kuweza kujua wapi pa kuitumia na wapi isitumike..
Kuna baadhi ya mas-ala katika elimu yetu ya dini huwa si busara kuwekwa  wazi au kujadiliwa kwa mapana na marefu kwani kufanyika hivyo kunaweza kuleta madhara  na fitna  kuliko faida.