022 - Hadiyth Ya 22: Kuhifadhi Undugu Wa Kiislamu, Haki, Heshima, Kutokufanyiana Uadui, Chuki Na Kudharauliana


 
عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه)  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اللَّه (صلى الله عليه و آله وسلم)  ((لاَ تَحَاسَدُوا وَلاَ تَنَاجَشُوا وَلاَ تَبَاغَضُوا وَلاَ تَدَابَرُوا ولاَ يَبِعْ بَعْضُكُمْ عَلَى بَيْعِ بَعْضٍ, وَكُونُوا عِبَادَ اللَّهِ إِخْوَانًا. الْمُسْلِمُ أَخُو الْمُسْلِمِ لاَ يَظْلِمُهُ وَلاَ يَخْذُلُهُ وَلاَ يكذبه ولاَ يَحْقِرُهُ.  التَّقْوَى هَاهُنَا)) وَيُشِيرُ إِلَى صَدْرِهِ ثَلاَثَ مَرَّاتٍ  ((بِحَسْبِ امْرِئٍ مِنْ الشَّرِّ أَنْ يَحْقِرَ أَخَاهُ الْمُسْلِمَ. كُلُّ الْمُسْلِمِ عَلَى الْمُسْلِمِ حَرَامٌ دَمُهُ وَمَالُهُ وَعِرْضُهُ)) رواه مسلم
 
Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah (رضي الله عنه) amesema:  Mtume wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Msihusudiane, wala msipandishiane bei [katika biashara pasina kuwa na haja ya kununua], wala msibughudhiane, wala msikatane, wala msiingie katika biashara waliyokwishaingia wenzenu, nyote kuweni ni waja wa Allaah ndugu moja.  Muislamu ni ndugu wa Muislamu, hamdhulumu, wala haachi kumsaidia, wala hamdanganyi, wala hamdharau. Taqwa ipo hapa)) akaashiria kifuani mwake mara tatu. ((Yatosha kuwa shari mtu kumdharau nduguye Muislamu. Kila Muislamu juu ya Muislamu mwenziwe ni haramu damu yake, mali yake, na heshima yake)).[1]
 
Mafunzo Na Hidaaya:
 
  1. Uislamu unasisitiza kuchunga haki na heshima baina ya watu, na unatahadharisha kudharauliana. [Rejea Hadiyth namba 88, 89, 96 126].
 
  يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا يَسْخَرْ قَوْمٌ مِّن قَوْمٍ عَسَىٰ أَن يَكُونُوا خَيْرًا مِّنْهُمْ وَلَا نِسَاءٌ مِّن نِّسَاءٍ عَسَىٰ أَن يَكُنَّ خَيْرًا مِّنْهُنَّ ۖ وَلَا تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ ۖ بِئْسَ الِاسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ ۚ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ ﴿١١﴾
 
Enyi mlioamini! Watu (wanaume) wasiwadharau watu (wengineo, kwani) huenda (waliodharauliwa) wakawa bora kuliko wao. Na wala wanawake (wasiwadharau) wanawake (wengineo), huenda (waliodharauliwa) wakawa bora kuliko wao. Na wala msikashifeni, na wala msiitane majina ya utani (mabaya). Uovu ulioje wa jina la ufasiki baada ya iymaan.  Na yeyote asiyetubu, basi hao ndio madhalimu[2]
 
  1. Uislamu unakataza kuudhiana [Al-Ahzaab 33: 58] na kutendeana uadui bali kushirikiana kwa wema [Al-Maaidah 5: 2]. 
 
  1. Waislamu wote ni ndugu [Al-Hujuraat: 49: 10].
 
  1. Uhasidi, bughudha na chuki, ni miongoni mwa maradhi ya moyo yanayomhatarisha Muislamu siku ya Qiyaamah kufika mbele ya Allaah (سبحانه وتعالى) akiwa na moyo usiosalimika [Ash-Shu’araa 26: 88-89].
 
  1. Uislamu unasisitiza kuungana si kutengana au kukatana undugu [Muhammad 47: 22-23].
 
  1. Kuuana ni miongoni mwa madhambi makubwa, nayo yanahusiana na haki ya mtu [An-Nisaa: 92-93].
 
  1. Taqwa ipo moyoni, na inadhihirishwa kwa vitendo vyake, kukhofu kutenda uovu na kutenda mema.
 
  1. Muislamu anafaa achunge sana asije kuingia katika haramu kwa kuvunja heshima ya nduguye, kumwaga damu yake au kula mali yake.
 
  1. Hii ni Hadiyth ‘adhimu yenye kutufunza mahusiano mema na maingiliano mazuri baina ya Waislamu wao kwa wao na wanaadamu wote duniani.



[1]  Muslim.
[2]  Al-Hujuraat (49: 11).