ABU AMMAAR
Kadhia
ya fatwa kwa siku za karibuni limekuwa suala tata hasa kwa kupatikana rai,
maoni na hukumu tofauti kwa mas-ala yanayolingana.
Pia
kumejitokeza utitiri wa mufti na tunaona fataawa na majibu ya masuala
takriban katika maredio,T.V, magazeti na kwenye mitandao ambayo kwa kiasi
kikubwa imesaidia kuelimisha waislamu na kupata majibu ya mas-ala
yanayowatatiza. Hatuna budi kuwapongeza mamufti na wanazuoni wanaojitahidi kufutu
mas-ala katika hukumu za kisheria. Hata hivyo na kwa sababu hii hii pia
kukithiri kwa fatawa tofauti kumewatatiza waislamu wengine kujiona wana
majibu yanayotofautiana katika masail yanayolingana na kutopata maelekezo
mazuri ya fatwa ipi kuifuata na ipi kuiacha.
Tatizo
hili la kuwepo fataawa tofauti ni la kihistoria na limejitokeza
kutokana na kuwa na madhehebu tofauti, kuwepo katika mazingira yanayofanya
baadhi ya fatwa kubadilika, masheikh kufutu mas-ala kwa kutegemea na jinsi ya
muulizaji na pia wakati mwengine pasina kufanyiwa utafiti wa kina kwa
mas-ala kabla ya kupatiwa hukmu yake. Na sababu nyengine ni kuandikwa kwa
fatwa.Tutakuja kulifafanua hili kwa kirefu.
Maana ya karibu ya neno Fatwa ni maoni ya kielimu ya
Ulamaa katika kutoa hukumu ya kisheria katika jambo la kidini.Na wengine
huitafsiri kama kupiga muhuri kwa hukumu ya jambo ambalo Allah
Subhaanahu Wataala alipaswa alitolee hukmu. Imam Ibnul Qayyim anasema katika
kitabu chake cha I’ilaamul Muwaqi’iyn kwamba: “Kila muislamu atakaebebeshwa jukumu
hili awe na hadhari na nadhari na aelewe uzito wa jukumu lenyewe na wala
kusiwe na chochote moyoni mwake kitakachomzuia kutosema ukweli na
kuuusimamia, kwani Allah Subhaanahu Wataala pekee ndie atakaemlinda na
kumuongoa……..”
Moja
katika jambo zuri la kuandikwa fatwa ni kwamba tunaweza kuzitumia kama ni rai
au hukmu katika mas-ala yatakayojitokeza na pia kuitumia kama dira katika
kutupa mwanga wa kulitolea hukmu ya jambo kama litakuwa linalingana katika
baadhi ya sehemu zake.Hapa tuna mfano mzuri wa kitabu maarufu cha Fataawa za
Sheikhul Islam Ibnu Taymiyah ambacho kina hazina ya faida ya kielimu na vipi
mufti anaweza kufikia kulipatia jambo hukmu ya kisheria.
Mfano
mzuri kwa upande wa kimataifa ni hukumu ya kuwaunga /kutowaunga mkono
Hizbullah katika mapambano yao na adui mkubwa wa kiislamu - mayahudi.
Masheikh na mamufti wameonesha tofauti zao kuhusu kadhia hii wengine
wakijuzisha kuwaunga mkono mashia kwa hili tu kwa sababu ya kigezo cha
kuondosha uovu - Dar-ul Mafaasid. Wengine wamekataa katakata kuunga mkono kwa
sababu tayari mashia ni kundi potofu lililokengeuka kiitikadi hivyo haipaswi
kwa muislamu kushirikana nalo kwa chochote. Na kauli nyengine ni kuwaunga
mkono moja kwa moja kwani ni waislamu na wametamka Shahada na tofauti
zilizopo haziathiri kutowaunga mkono.
Katika
masaail ya kifiqhi pia tunaona masaail mengi sana kuwa na rai na miono
tofauti kati ya Maulamaa. Kama suala la kuandama kwa mwezi ambalo kila mwaka
hukutana nalo na waislamu kutafuta njia za kuweza kutafuta njia za kuondosha
tofauti hizi bila ya mafanikio. Kwani katika nchi moja inawezekana waislamu
wakaanza kufunga Ramadhan katika siku tatu tofauti huku kila mmoja akiona
kwamba rai yake ni sahihi na nyengine si sahihi kwa jinsi ya vigezo na dalili
zinazotumika.
Pia
katika ibada ya Hijja kupatikana rai na maoni tofauti kwenye vipengele vya
Hijja na ‘Umrah, kama kujuzu/kutojuzu kufanya Tawaaful Widaa’i kwa wenye
kufanya ‘Umrah. Au kuweza kufanya ibada ya ‘Umrah zaida ya mara moja katika
safari moja na kadhalika.
Na
hata kwenye vyakula pia hukutana na rai tofauti kuhusu uhalali na uharamu wa
chakula. Kama siki – vinegar ambayo uhalali/uharamu wake hutegemea na jinsi
ilivyotengenezwa.Na masuala mengi kuulizwa kuhusu uhalali/uharamu wake.
Tunaweza
kuona baadhi ya mifano tofauti ya kuweza kubadilika fatwa kutokana na
mazingira au hali kama ilivyotokea kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam
أنه جاءه شيخ كبير فقال له: أيقبّل الصائم؟ قال : (نعم)،ثم جاءه شاب
فتيّ فأعاد عليه
((.(السؤال،
فقال له : (لا))
Alijiwa na mtu mzima na kumuuliza “Je mwenye kufunga anaweza
kubusu?” Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam akamjibu: “ndiyo”. Kisha akajiwa
na mtoto wa kiume baleghe akauliza suala hili hili na akajibiwa ; “hapana”
Pia
Abdullah ibn ‘Abbass – Allah awawie radhi -
أنّه
جاءه رجل محمرّ العينين، منتفخ الودجين، تلوح عليه علامات الانتقام؛ فقال له: يا
ابن عبّاس، هل للقاتل من توبة؟، قال له: لا... ثمّ جاءه رجل آخر خافض الطرْف،
منكّس الرأس، قد بدت عليه علامات الحزن والندم، فقال: يا ابن عبّاس، هل للقاتل
من توبة ؟ قال:
نعم
Alikuja mtu huku macho yake yamewiva na huku akionesha kuvinjari
kulipa kisasi na kusema Ewe Ibnu ‘Abbaas ? mwenye kuua anaweza kutubu? Ibnu
‘Abbaas akamjibu;“hapana”. Kisha akajiwa na mtu mwengine ambae anaonekana
mnyonge huku amejiinamia kichwa chake na anaonesha alama za majuto na huzuni
na kusema Ewe Ibnu Abbaas Mwenye kuua anaweza kutubu? Ibnu ‘Abbaas akajibu
;”ndiyo”
Katika
matukio haya mawili la kwanza kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam
kumkubalia mtu mzima na kumkatalia mtoto ni kutokana na hali kwani mtu mzima
anaweza kuimiliki nafsi yake, tofauti na mtoto ambaye ndio kwanza baleghe -
haimudu nafsi yake na matamanio.
La
pili ni mazingira aliyekuja nayo muulizaji wa kwanza moja kwa moja yalimfanya
Ibnu ‘Abbaas kumkatalia kuwepo tawba kwa mwenye kuua kwani lengo lake
lilionekana ni kutaka kulipiza kisasi kisha kutumia mlango wa toba kama njia
. Wa pili alionekana kujuta na tendo lake lile hivyo amekuja kwa Ibnu ‘Abbaas
kutaka kujua kwamba anaweza kutubu kwa kosa lake.
Sasa
tuangalie athari za fatwa kama hizi kama zitaandikwa. Alhamdulillah enzi za
Mtume Salla Alahu ‘Alayhi Wasallam na masahaba –Allah awawie radhi –
hili halikuwa tatizo kwani kupata ufafanuzi wa jambo lolote haikuwa taabu
kwani Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam alikuwepo na masahaba
walikuwa karibu. Pia tunaona vipi Khalifa ‘Umar ibnul Khattaab, Allah
amuwie radhi, alivyobadilisha hukumu baada ya kupata kauli kinyume na jinsi
alvyohukumu kutoka kwa sahaba kama pale alipotaka kuzuia ughali wa mahari na
ikatoka sauti ya mwanamke ikimkumbusha aya ya Qur’aan inayoruhusu hivyo. Hali
hii iliendelea mpaka kwa watangu wema – salafun saalih.
Ieleweke
kwamba hukumu yoyote ya kisheria huwa ni thabiti na wala haibadiliki ikiwa
hali na mazingira yatakuwa yanalingana. Hubadilika kwa kubadilika hali na
mazingira kulingana na jinsi matukio yanavyojitokeza. Na wenye uwezo wa
kuyaona mabadiliko haya ni wanazuoni na maulamaa walio na upeo katika elimu
ya dini kwa kuzingatia misingi mikuu ya dini yetu kama ilivyokuja katika
Quraan na Sunna za Mtume wetu Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam
Katika
athari za kuandikwa fatwa:
1
Inaweza kutumiwa katika mazingira
yasiyolingana
Ingawa
ni fatwa sahihi isiyo na kosa lolote. Mazingira itakayotumiwa itaweza
kuleta madhara zaidi kuliko manufaa. Kwani kwa muislamu atakaenukuu fatwa ya
Mufti inawezekana hakuangalia kwa undani mazingira ya fatwa ya awali
ilipotolewa. Aliangalia zaidi natija ya fatwa.
Hapa
tutachukua mfano wa hukumu ya kuvuta sigara:
Masheikh
waliopita walifutu kwamba kuvuta sigara ni makruhu. Hukumu hii iliendelea kwa
muda mrefu na baadhi ya waislamu kuitumia hadi hii leo kwamba ndiyo hukumu
sahihi. Mamufti wa karibuni wamefutu kwamba kuvuta sigara ni haramu kwa
sababu ya madhara makubwa yanayosababisha upotevu wa mali, maradhi ya
saratani (cancer) kuudhi watu wengine na kadhalika.
Masheikh
waliofutu kwamba sigara ni makruhu si kwamba walikosea bali mazingira ya
wakati ule ambapo sayansi na teknolojia ilikuwa duni hawakuweza kuyaona
madhara haya yaliyokuja kuonekana baada ya kuendelea kwa sayansi na
teknolojia. Hivyo fatwa ilienda sambamba na mazingira ya wakati wao. Sasa kwa
muislamu kubaki na kusisitiza fatwa ile ni sahihi na hii ya sigara kuwa ni
haramu ni batili ni moja katika athari za kuandikwa fatwa hii na wengine
kuitumia kama hadidu rejea.
Sasa
tukitumia fatwa kwamba sigara ni makruhu tunaona hapa madhara makubwa
yatayowapata waislamu kuliko manufaa kwa kigezo tu kwamba tayari fatwa hii
ipo na imeshatolewa.
2
Inaweza kutumika katika wakati na pahala
pasipolingana.
Kwa
kuandikwa fatwa, kama tulivyosema, huangalia zaidi natija ya fatwa bila ya
kuangalia hali halisi iliyofanya kutolewa kwa fatwa hii. Hivyo Mufti anaweza
kufutu mas –ala na kwa kuwa yamendikwa muislamu mwengine kuja kuichukua
hukumu ile bila ya kuangalia kwa undani kwamba si mahala pake kutumika.
Mfano
Katika
nchi za joto imewahi kutoka Fatwa kwa wanaofunga Ramadhan kufunga siku moja
na kuacha siku moja kwa sababu ya joto kali linalofanywa waislamu wakifunga
kuwa hatarini katika afya zao.
Muislamu
mwengine anaweza kuathirika na kutumia fatwa hii kama kigezo lakini pahala
alipo si sehemu ya joto kali wala waislamu kutokuwa hatarini kwa afya zao.
Kwa kigezo tu kwamba fatwa hii tayari imeshatolewa na ipo.
3
Inaweza kuwa ni ya muda tu lakini ikachukuliwa kama ndio hukmu ya kudumu.
Hapa
kama kuna jambo limejitokeza ambalo lingehitaji Fatwa kwa wakati ule tu kwa
dharura iliyojitokeza na kuondoka kwa dharura pia humaanisha kufutika kwa
Fatwa.
Mfano.
Hukmu
aliyoitoa Khalifa - Amiirul Muuminiin - Umar ibnul Khattaab, Allah amuwie
radhi, alipokataza wezi kukatwa mikono kipindi kilichozuka njaa katika mji wa
Madina. Fatwa hii ilitolewa kwa dharura ya njaa tu na pale dharura
ilipomalizika hukmu ikarudi palepale.
Hata
hivyo muislamu ambae maarifa ya dini yake bado machache anaweza kuikuta fatwa
hii na kuichukua kama ni hukmu huku akimnukuu Khalifa wa Mtume Salla Allahu
‘Alayhi Wasallam kwamba alifanya jambo hili.
Au
mfano wa baadhi ya Mamufti kuruhusu kuweka pesa katika mabenki yanayoendeshwa
kwa riba ikiwa pahala hapana kabisa Benki inayoendeshwa kiislamu. Mfano kama
Uingereza ya enzi hizo. Ila fatwa hii tayari imefutwa kwa sababu ya tayari
kuwepo Benki za kiislamu au Benki zinazoruhusu kuweka pesa pasina kuwepo
riba.
4
Muislamu anaweza kujiamulia kufuata fatwa “poa”
Hii
ni pia ni athari mojawapo ambapo muislamu wa kawaida anaweza akautumia
uchochoro huu kutafuta fatwa inayolingana na shida na mahitaji yake na
kuifuata. Kwani amejikuta katika hali ya kuwa na fatwa tofauti huku uwezo
wake wa kielimu ni mdogo kuweza kuzichambua dalili zilizotumika kufikia
hukmu. Si kila muislamu ana uwezo wa kielimu kuweza kuzichambua na kuzihakiki
dalili na hoja zilizotumika hivyo kuamua kufuata fatwa “poa” katika zilizopo
kwa kukosa vigezo vya kutumia tatizo hili lkijitokeza.
5
Inawezekana Mufti hakupata ufafanuzi wa kutosha kwa aliyeuliza au kutofanywa
utafiti wa kina kabla ya kutolewa Fatwa.
Katika
masharti ya ziada ya Mufti ni kwamba atatakiwa awe na uwezo wa kuona mbali ,
mwenye busara na kuwafahamu vizuri watu janja , hila na mbinu zao , awe
na msimamo madhubuti katika dini yake na asikubali lawama , asiathirike na
khofu wa vitisho vitakavyoelekezwa dhidi yake, asitetereke na awe ni mtu asiyependa
makuu na amuogope Allah (Subhaanahu Wata’ala) kwa kila jambo alifanyalo
Hivyo
yawezekana Mufti kutopata maelezo ya kutosha hasa katika masuala
yanayofikishwa kwa maandishi- kwa mfano- ambayo huwa si rahisi kwa Mufti
kupata hali halisi ya suala lenyewe. Na hivyo utafiti kuwa si wa kina katika
kujibu suala alilopelekewa.
Ikumbukwe
hapa kwamba fatwa mara nyingi huwa ni rai au uoni wa sheikh au mufti kwa
jinsi alivyolifahamu jambo alilopelekewa na inawezekana ikawa sahihi au ikawa
si sahihi. Hivyo tunaona nyengine hukubaliwa na baadhi ya fatwa zikihojiwa na
kutiwa alama za kuuliza na nyengine kukataliwa moja kwa moja. Nyengine
huzusha mjadala ndani yake. Na mara nyingi huwekwa mwisho wa maelezo “Allah
ndie ajuae zaidi” ikiwa ni hatua ya tahadhari ikiwa mufti ameteleza katika
fatwa yake.
Nini
cha kufanya kwa muislamu wa kawaida atakapoona mas- ala lina fatwa
zinazotofautiana?
Muislamu
wa kawaida, tunaemkusudia, ni yule asie na uwezo wa kielimu ya dini ya kuweza
kuzichambua na kuzihakiki dalili na hoja zilitumika hadi kupatikana hukmu ya
mas-ala. Kwani kinachozingatiwa zaidi kwenye fatwa ni dalili na jinsi
zilivyotumika kama ni Qur’aan, Sunna, Ijmaa au Qiyaas. Inawezekana kutumika
kwa dalili vilivyo lakini jinsi ilivyotumika ikawa kidogo kuna mtihani.
Kwa
kuwa fatwa ni maoni ya mwanachuoni kwa mujibu wa alivyofahamu na kuzitafsiri
hukumu katika sheria ya dini ya kiislamu; kukubalika kwa fatwa kutategemea
zaidi jinsi ya uwezo alionao katika kuzichambua na kuzihakiki dalili na
kuzitumia vilivyo.Hivyo elimu ya mwanachuoni au ‘Alim ni kigezo muhimu cha
kukiangalia kabla ya kuikubali au kuikataa fatwa yake.
Maulamaa
wametofautiana kwa muislamu mchache wa elimu katika kuzitumia fatwa katika
katika kauli tatu zifuatazo:
1
Achague atakayoona inafaa katika
hizo.
2
Afanye jitihada na hatimae
kuchagua kauli ya mwenye elimu zaidi miongoni mwa waliotoa fatwa.
3
Achague rai iliyokuwa na nguvu
miongoni mwa rai zilizotolewa.
Ukiziangalia
kauli zote tatu unazikuta zina udhaifu kidogo katika matumizi.
Kwani
kumuachia mchache wa elimu kuchagua rai atakayoona inafaa anaweza kuathirika
na rai au hoja atakayoiona ni rahisi au yenye mvuto kwa jinsi ilivyopangwa au
inalingana na jinsi atakavyo kwa sababu hana sifa na uwezo wa kuweza
kuzichambua hoja zilizotolewa wala dalili zilizotumika.
Jitihada
ya kuchagua rai ya mwenye elimu miongoni mwao angalau inaweza kuwa ni rai
nzuri iwapo mchache huyu wa elimu ataweza kupata C.V za wanazuoni wote au
kupitia watu wengine wanaowafahamu na kuweza kusema huyu anaonekana ni mwenye
elimu zaidi. Na pia katika utoaji fatwa zake huonekana kuzingatia zaidi
dalili za kimsingi Qura’an na Sunnah. Lakini pia inaweza kujenga dhana kwamba
kila asemalo mwanazuoni huyu litakuwa ni sahihi na mengineyo si sahihi. ‘Alim
huyu ni mujtahid (mwenye kujitahidi) na kisheria atalipwa ujira mara mbili
akipatia hukmu ya jambo na kulipwa ujira mara moja akikosea.Pia inawezekana
ikaendeleza ile dhana ya Taqlid- kufuata tu – ambako nako pia kunakuwa na
mtihani wake.
Kuweza
kuitambua rai yenye nguvu miongoni mwa rai zilizotolewa pia ni mtihani kwa
mchache wa elimu kwani kila mufti anaweza kudai kwamba rai yake ndio yenye
nguvu au karibu na sahihi kwa jinsi ya alivyotumia vigezo anavyowafikiana
navyo. Hivyo daraja hii itahitaji muislamu mwenye upeo katika kuijua dini
yake na kuweza kuzijua na kuzihakiki vilivyo dalili na vigezo alivyotumia
mufti kama vinaweza kukubalika na hivyo rai yake kuwa na nguvu kuliko
nyenginezo.
Kwa
muono wangu, wallahu a’alamu, rai ya kuchagua mwenye elimu miongoni
mwao,licha ya kuwa na udhaifu kidogo katika matumizi, ni rai nzuri na
muwafaka katika kutafuta fatwa ipi ataweza kuitumia muislamu mchache wa elimu
kwa sababu zifuatazo:
1
Kwa kutokuwa na uwezo wa kielimu
moja kwa moja daraja yake huwa ya ittiba’a - mwenye kufuata na kuelekea
daraja ya chini ya taqleed - mwenye kuiga na kila mwenye kufuata taqleed
hupaswa kuwafuata walio na elimu. Suuratu Nnahl/43
فَاسْأَلُواْ أَهْلَ
الذِّكْرِ إِن كُنتُمْ لاَ تَعْلَمُونَ
"Basi waulizeni wenye ukumbusho kama nyinyi hamjui"
2
Elimu ni kigezo muhimu kwani ikiwa
elimu ya mufti ina walakini ,fatwa yake pia inaweza kuwa na walakini ingawa
si lazima.
3
Uwezo wa kuzichambua dalili
unahitaji elimu katika nyanja tofauti za dini hivyo kwa aliebobea ataweza
kuwa na nafasi nzuri ya kutumia elimu yake kuzichambua dalili kwa kituo na
ushuhuda.
4
Upeo na uelevu wa mambo
ukichangiwa na elimu sahihi ya dini humfanya mufti kuweza kutoa rai madhubuti
katika mas-ala kwani kutalenga katika kuangalia vigezo anavyotumia kama ni
sahihi au vyenginevyo.
5
Matumizi ya dalili za kisheria ni
kigezo cha kufuata hata kama kuna ugumu au wepesi. Na ikiwa jambo lenyewe
lina rai tofauti basi mwenye elimu ataweza kutupa picha halisi ya jinsi
vigezo alivyotumia kufikia hukmu na jinsi vilivyotumika kwani tumeagizwa
tuangalie zaidi dalili katika hukmu na si vyenginevyo.
Wallahu A’alamu – Allah ndie ajuae
zaidi.
|
Fatwa kwa Mchache wa Elimu
Subscribe to:
Posts (Atom)