Abu Ubaydah ibn Al-Jarraah-mtihani wake ulikuwa mzito !

Alikuwa na umbo la kuvutia, mwembamba na mrefu uso wake mwingi huwa na tabasamu na kuwa na ndevu ziliachana achana.  Alikuwa mkarimu sana mpole na mwenye haya.  Hata hivyo, katika mazingira magumu huwa mkakamavu na mkali mfano wa upanga.
Jina lake kamili ni Amr ibn Abdullah ibn Al-Jarraah.
 
Abdullah ibn Umar anasimulia:
 
“Watu watatu katika kabila la maquraysh walikuwa wanajulikana sana kuwa na tabia nzuri na wapole.  Wakiongea nawe hawakughilibu na ukiongea nao hawakusingizii uongo:  Abubakar Siddiq, Uthman ibn Affan na Abu Ubaydah ibn Al-Jarraah.”
 
Abu Ubaydah ni miongoni mwa watu wa mwanzo kusilimu.  Yeye na Abubakar wamepishana kwa siku moja tu.  Na kupitia kwa Abubakar ndiko kulikomfanya kusilimu. Abubakar aliwachukua yeye, Abdurrahmaan ibn Awf, Uthman ibn Madh-uun na Al-arqam ibn Abil Arqam kwenda kwa Mtume (SAW) ambapo wote kwa pamoja wakakubali ukweli na dini ya haki.  Hawa wanahesabika kuwa mihimili ambayo uislam ulikuja kujengewa baadae.
 
Kama walivyokuwa waislam wa Makka, Abu Ubaydah pia alipata taabu sana kwani alikuwa ni miongoni mwa waislam wa mwanzo.  Taabu, shida, matusi, vipigo na huzuni vyote hivi vilikuwa ni majaribu yaliyowapata na ni imani thabiti kwa Mwenyezi Mungu (SW) ndiyo iliyomsaidia. Na katika mtihani mkubwa uliomfika ni majaribu aliyoyapata katika vita vita vya Badr.
 
Alikuwa ni miongoni wa wapiganaji wa jeshi la kiislam na alipigana kwa ari moja kama mtu asiyegopa kabisa kifo.  Majeshi ya kiquraysh yalimfahamu vyema na mara nyingi yalimwepuka, lakini kulikuwa na mtu mmoja alikuwa akimfuata kila aendako naye akajitahidi wasikutane.
 
Hata hivyo, yule mtu  akawa anamrandia na alipopata nafasi akaanza kumshambulia.  Abu Ubaydah bado hakuwa tayari kupigana naye, aliendelea kujihami tu.  Lakini yule mtu akawa kikwazo kwake kuendelea kupigana kwani kila akijaribu kumuepuka humkalia mbele yake mpaka wakawa uso kwa uso.  Abu Ubaydah hakustahamili tena akampiga pigo moja la nguvu na kumuua.
 
Mwenyewe utaweza kufahamu ni nani kwani ulikuwa ni mtihani wa aina yake kati ya uislam na ukafiri na ubaba ua umwana.  Alikuwa ni baba yake mzazi Abdullah ibn Al-Jarraah!
 
Abu Ubaydah hakutaka kumuua baba yake lakini kwenye vita kati ya uislam na ukafiri chaguo lilikuwa moja tu. Chaguo lenyewe ni majaribu makubwa na ya kuzingatia sana mpaka baadhi wakasema hakumuua baba yake bali alichoua ni ukafiri uliomo kwenye mwili wa baba yake.
Na kuhusu tukio hilo aya ya Suratul Mujaadalah/22 iliteremka
 “Huwakuti watu wanaomuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho kuwa wanawapenda wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake hata wakiwa ni baba zao,au watoto wao ,au ndugu zao,au jamaa zao.Hao ameandika katika nyoyo zao imani na amewapa nguvu kwa roho itokayo kwake. Na atawaingiza katika mabustani ipitayo mito kati yake.Humo watakaa daima.Mwenyezi Mungu awe radhi nao na wao wawe radhi nae.Hao ndio kundi la Mwenyezi Mungu.Hakika kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kufanikiwa” 
Na athari za kukutana na baba yake vitani zilimfanya awe na imani zaidi kwa Mwenyezi Mungu na uchamungu wa hali ya juu kwa ajili yake.
 
Imehadithiwa na Muhammad ibn Jaafar (RA) kwamba ujumbe wa wakristo ulikuja kwa Mtume (SAW) na kusema, “Ewe Abul Qasim, (wakimaanisha Mtume) tunamtaka mmoja wa masahaba wako aje pamoja nasi, mtu ambaye wewe mwenyewe uko radhi naye, ili atahukumie baadhi ya mas-ala yetu kuhusu vitu ambavyo sisi wenyewe tumekhtalifiana. Kwani nyinyi waislam tunakuheshimuni sana.”
 “Njooni jioni, nitakupeni mtu mmoja ambaye ni thabit na mkweli” akajibu Mtume (SAW) 
Umar ibn Khattab aliyasikia haya na baadaye kusema:
“Nilikwenda mapema kusali nikitaraji labda mimi ndiye niliyesadifu yule mtu aliesifiwa na Mtume (SAW).
 
Mtume (SAW) alipomaliza kusali akaanza kutazama kulia na kushoto, nikajiinua kidogo na kujishughulisha ili Mtume (SAW) apate kuniona.  Mtume (SAW) aliendelea kutafuta mpaka alipomuona Abu Ubaydah akamwita na kumwambia, “Nenda nao na wahukumie kwa haki yale wanayotofautiana.”  Hivyo ndivyo alivyochaguliwa Abu Ubaydah.
 
Sifa hii ya uadilifu ya Abu Ubaydah, aliweza kuitekeleza kwa amana katika kutekeleza majukumu yake na hayo kuthibitishwa na matukio tofauti.
 
Siku moja, Mtume (SAW) alipeleka kundi la masahaba kwenda kukutana na msafara wa maquraysh.  Alimteua Abu Ubaydah kuwa Amir (kiongozi) na kuwapa kigunia cha tende kama chakula chao.  Abu Ubaydah akawa anampa kila sahaba mmoja tende moja kila siku.  Alikuwa akiila ile tende na kuinyonya kama mtoto mchanga anavyonya ziwa la mama yake.  Kisha akanywa maji na hii kumtosheleza kwa siku nzima.
 
Siku ya vita vya Uhud, pale waislam walipokuwa wanapigwa, mmoja katika makafiri alikuwa akisema kwa sauti kubwa, “ Nionesheni Muhammad, nionesheni Muhammad” Abu Ubaydah alikuwa miongoni mwa waislam kumi waliomzunguka Muhammad kumkinga na makafiri.
 
Vita vilipomalizika, ilibainika moja ya jino lake Mtume (SAW) la gego limevunjika, kipaji chake kimejeruhiwa na vipande vya vyuma viwili vya ngao yake kupenya kidogo kwenye mashavu yake.  Abubakar akataka kumtoa Mtume (SAW) lakini Abu Ubaydah akamwambia:
“Niachieni mie”
Aliogopa kuvivuta vile vipande vya nyuma kwa mkono kuchelea kumzidishia maumivu Mtume (SAW).  Hivyo akaamua kuvitoa kwa meno, akavibana na akavivuta kwa nguvu kwa bahati mbaya jino lake la nabu likatoka  akimshughulikia Mtume (SAW).  Ikabidi kile kipande cha chuma chengine  akitoe kwa kwa jino lake jengine la nabu nalo pia likatoka, Abubakar akasema kwa mzaha;
“Abu Ubaydah ni mtaalam wa kun’goa jino la nabu!”
 
Baada ya Mtume (SAW) kufariki, waislam walikutana ili kumchagua Khalifa.  Mkutano huu ulifanyika Saqifa sehemu ya mkutano ya Banu Saadah siku hii inajulikana katika historia kama siku ya Saqifa.  Umar ibn Khattab akamwambia Abu Ubaydah, “Lete mkono ili niape kiapo cha utii kwako kwani nilimsikia Mtume (SAW) akisema, Kila umma una Amir (msimamizi) na wewe ni Amir wa umma huu”
 
“Wala sitofanya, kujitanguliza mbele ya mtu ambaye Mtume (SAW) aliamrisha atuongoze kwenye sala naye akatuongoza mpaka kufa kwa Mtume (SAW)” akajibu Abu Ubaydah akimaanisha Abubakar Siddiq.
 
Alikuwa mshauri wa karibu wa Abubakar enzi za ukhalifa wake na kufanya hivyo hivyo kwa Umar.  Hakuwahi kutofautiana kwa lolote lile isipokuwa jambo moja ambalo alitofautiana na Umar ibn Khattab.
 
Tukio hilo lilitokea wakati Abu Ubaydah yupo Syria akiongoza jeshi la waislam mpaka kuweza kuikamata Syria yote na kuwa chini ya himaya ya kiislam.
 
Yakaja kuingia maradhi ya mlipuko (kuambukiza). Mlipuko ambao haujawahi katokea na watu wengi kuathirika.  Umar akamtuma mjumbe kumpelekea salamu Abu Ubaydah akiwa na barua isemayo:
 
“Nina shida na wewe muhimu sana.Ukiipata tu barua hii hata kama usiku, nnakushauri kuanza safari hata kabla ya alfajiri  haijaingia na kama utaipata mchana, haraka fanya safari hata kabla ya jioni haijaingia.”
 
Alipoipata barua, Abu Ubaydah akasema, “nnajua kwa nini Amirul Muumiinin ananihitaji.  Anataka kuhakikisha uhai wa mtu na hata hivyo utamalizika.”
Hivyo akajibu,
 
“Ninajua kama unanihitaji.  Lakini nipo ndani ya jeshi la waislam na wala sina hamu yoyote ya kujiokoa nafsi yangu na haya majanga yanayotupata.  Sitopendelea kutengana nao mpaka pale Mwenyezi Mungu atakapotaka.  Hivyo ikikufika barua hii (ukubali udhuru wangu) niachie kutoka kwenye amri yako na uniruhusu niendelee kubaki.”
 
Umar alipoipata barua na kuisoma alitokwa na machozi mpaka wale waliokuwepoo wakauliza;
“Vipi Amirul Muuminiin, Abu Ubaydah amefariki?”
Umar akajibu, “Hapana, lakini kifo kipo karibu naye.”
 
Na kama alivyosema Umar haukupita muda maradhi yakamkumba Abu Ubaydah na kabla ya kufariki alitoa wasia kwa jeshi lake na kusema:
 
“Ngojeni nikupeni wasia ambao utakufanyeni muwepo katika njia ya kheri:”
 
“Simamisheni Sala, fungeni Ramadhani, toeni sadaqa, tekelezeni ibada ya Hijja na Umrah, na kuweni pamoja. Msiiruhusu dunia ikuharibuni kwani mtu hata akiishi miaka elfu mwishowe atafikia kama hapa ambapo mimi nipo.”
 
“Amani iwe kwenu na rehema za Mwenyezi Mungu.”
 
Abu Ubayadah akamgeukia Muadh ibn Jabal na kumwambia, “ewe Muadh, wasalishe watu” na hapo hapo roho kumtoka.
 
Muadh akasimama na kusema, “Enyi watu mmefikwa na msiba wa kufiwa na huyu mtu, sikumbuki kama nimemuona mtu aliye na moyo safi na kuwa mbali sana na maovu na kuwa mkweli kwa watu wake kuliko yeye.  Muombeni Mwenyezi Mungu amjaze rehema zake na Inshaallah Mwenyezi Mungu atakurehemuni.”