Saad ibn Abi Waqaas - Shujaa wa Qadisiyyah

Saad ibn Abi Waqaas - Shujaa wa Qadisiyyah

 
Alikuwa kijana mfupi na aliyejengeka kimwili na nywele nyingi. Watu wa Makka walimfananisha na simba mtoto. Nae pia anatoka katika ukoo wa kitajiri na kuheshimika. Ni mtu wa karibu sana kwa wazazi wake na alimpenda sana mama yake.  Muda wake mwingi aliupoteza kutengeneza mishale na pinde na kufanya sana mazoezi ya kurusha mishare kama kwamba anajiandaa na vita vikubwa.
 
Saad hakuwa na furaha katika mfumo mzima wa maisha ya Maquraysh wa Makka. Alihisi kwamba imani zao na miungu wanayoiabudu ina upungufu aina fulani bila ya kuujua hasa ni upi.  Tabia za Maquraysh nazo pia hazikumpendeza wala kumridhisha.
 
Siku moja alitembelewa na Abubakar Siddiq na kuzungumza naye.  Abubakar alimfahamisha kuhusu Muhammad ibn Abdullah mtoto wa marehemu dada yake kwa mjomba na shangazi, Amina bint Wahab kwamba ameteremshiwa Wahy na kutumwa kutangaza dini ya haki na uongofu.
 
Baadae Abubakar alienda naye kwa Muhammad (SAW). Ilikuwa ni jioni na Mtume ndio kwanza amemaliza kusali.  Baada ya kusikia wito na yeye mwenyewe tangu mwanzo kuwa na wasi wasi na imani ya kiquraysh alikubali hapo hapo na kutamka shahada.
 
Mtume alifurahishwa sana na kusilimu kwa Saad kwani tokea utotoni wake alama za kuwa mtu wa busara tayari zilijitokeza. Vile vile kusilimu kwake kungepelekea vijana wengine pia nao kuja katika uislamu.
 
Ingawa Mtume (SAW) alifurahishwa sana na kitendo cha Saad kuingia katika uislamu, kuna watu wengine walichukizwa sana na tendo hilo akiwemo mama yake Saad. Saad anasimulia:
 
 “Wakati mama yangu alipopata habari kwamba nimesilimu aliingiwa na hasira na alikuja kwangu huku ameghadhibika na kunikaripia, ‘Ewe Saad mwanangu, nini kimekusibu kuacha dini ya baba na mama yako na kufuata dini gani hii…..? Naapa ima uachane na dini yako hii mpya au nitajifungia kula na kunywa mpaka nife.  Moyo wako utaemewa kwa huzuni na majuto kukukumba na watu kukuapiza milele kwa jinsi ulivyomtendea mama yako.’
 
Saad akajibu, “usifanye hivyo, ewe mama yangu, hakuna kitu chochote kitakachonifanya niachane na dini yangu.”
 
Hata hivyo, mama yake hakumsikiliza na kuanza mgomo wake wa kutokula wala kunywa. Akaanza kudhoofika na Saad alijitahidi kumbembeleza na kumsihi mama yake huku akimletea chakula.  Mama yake alikataa kata kata na kurudia usemi wake ule ule, “achana na dini yako na mimi nitakula, ila hivyo, niache nife.”
 
Saad akamwambia, “ewe mama yangu nina mapenzi makubwa kwako kama mama yangu ulienizaa, lakini mapenzi yangu kwa Mwenyezi Mungu (SW) na Mtume wake ni makubwa zaidi, Wallahi, lau hata roho elfu moja na moja zitaondoka (kwa kunitaka nirudi dini yangu ya zamani) kamwe sitorudi dini yangu.”  Mama yake kuona msimamo wa mwanawe haujatetereka wala kuyumba licha ya kitisho kizito alichomtisha akaona hakuna haja tena ya kuendelea na mgomo na kuanza kula.
 
Ni kwa tukio hili adhimu la msimamo wa Saad kwa mama yake; aya za 14-15 za Surat Luqman ziliteremka:
 
“Na tumemuusia mtu kwa (kuwatendea wema) wazazi wao wawili, mama yake alibeba mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu na kumwachisha ziwa baada ya miaka miwili. (Tumemuusia) Nishukuru mimi na wazazi wako. Ni kwangu mimi ndio marudio.    Na pindi wakikushikilia kunishirikisha na ambayo huna elimu nayo basi usiwatii. Lakini kaa nao kwa wema duniani. Na ishike njia ya anaye elekea kwangu. Kisha marejeo yenu ni kwangu na mimi nitakuambieni mliokuwa mkiyatenda”
 
Katika siku za mwanzo wa Uislam, Mtume (SAW) aliwaasa waislam kuwa na tahadhari sana na Maquraysh wasije wakakasirika kwani bado Uislam haukuwa na nguvu za kuweza kuhimili vishindo vyao.  Wakati huo walikuwa wakitoka kwa vikundi kwenda kando kando ya mji wa Makka kufanya ibada. Siku moja baadhi ya makafiri waliwaona waislam wakisali na wakawabughudhi na kuwafanyia inda.
 
Subira ya waislam ilifika kikomo na wakavamiana nao na kuanza kupigana.  Saad alikamata bufuru la ngamia na kumpiga mmoja wao na kumjeruhi. Ilikuwa ni damu ya kwanza kumwagika kati ya vita vya waislam na makafiri vita ambavyo ilikuja kuwa kubwa na kujaribu imani za waumini na kuwatia katika mitihani.
 
Hata hivyo, baada ya tukio hili, Mtume (SAW) bado alisisitiza pale pale kuwa na subira na uvumilivu na kuwakumbusha kuwa hiyo ilikuwa ni amri ya Mwenyezi Mungu mtukufu na wakati bado haujawa muafaka.  Suratul Muzamil /10-11
 “Basi kuweni na subira na yale wanayoyasema na jitengeni nao kwa vizuri. Na niacheni mimi peke yangu niwashughulikie wale wanaokadhibisha , walioneemeka, basi wastahamilie kidogo”   
Miaka ilipita na rukhsa ya kupigana Jihadi ilipotoka Saad alikuwa na umuhimu mkubwa hasa katika vita vilivyotokea wakati wa Mtume (SAW) na baada ya kufariki kwake.
 
Alipigana vita vya Badr pamoja na mdogo wake Umayr ambaye aliomba aruhusiwe kuungana na jeshi japokuwa alikuwa na umri mdogo.  Saad alirudi peke yake Madina kwani Umayr ni mmoja katika mashahidi kumi na wane waliouwawa.
 
Katika vita vya Uhud, Saad alichaguliwa pamoja na Zayd, Saib ibn Othman bin Maazun kwani walikuwa warusha mishale stadi.  Alipigana kwa moyo na nguvu zake zote katika kumlinda Mtume (SAW) hasa pale baadhi ya waislam waliopangwa milimani kuondoka sehemu zao. 
 Mtume (SAW) alikuwa akimpa moyo huku akimwambia, “rusha, rusha yaa Saad… Fidaaka Abi wa Umm.” 
Ali ibn Abitalib anasema hajawahi kumsikia Mtume Muhammad (SAW) akiahidi kulipa kwa mtu yoyote isipokuwa Saad.
 
Katika historia ya kiislam Saad atakumbukwa kuwa sahaba wa kwanza kurusha mishale kwa ajili ya kuuhami Uislam na Mtume (SAW) akamuombea dua:
 “Ewe Mola uongoze mshale wake na umkubalie dua zake” 
Naam! Saad alijaaliwa utajiri na hakuwa maarufu kwa ushujaa tu bali pia alikuwa mkarimu.  Wakati wa Hijjatul Widaa – Hijja ya kuaga- akiwa pamoja na Mtume Muhammad (SAW) aliugua. Mtume (SAW) akaja kumkagua na Saad akasema, “Ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu, nimejaaliwa mali na nimebahatika kuwa na mtoto mmoja tu wa kike atayenirithi, Je! Niitoe thuluthi mbili ya mali yangu kama sadaqa?
 
Mtume (SAW) akasema, “Hapana”
 
Akauliza tena, “nusu je?”
 
Mtume akamkatalia tena, “hapana.”
 
“Je! Thuluthi?”
 
“Naam na bado thuluthi ni nyingi kwani kuwaacha warithi wako katika hali nzuri ni bora kuliko kuwaacha masikini wakiomba watu…….” Mtume alimjibu.
 
Saad alijaaliwa kupona ugonjwa na kubarikiwa na watoto wengine wengi tu.
Alikuwa maarufu zaidi kama kamanda wa jeshi la kiislam lililotumwa na Khalifa Umar ibn Khattab kwenda kupigana na waajemi (Persians) katika vita vya Qadisiyya.  Khalifa alitaka kuung’oa utawala wa Sasania (Ctesphon) uliokuwa ukitawala kwa karne nyingi. 
 
Kazi hii haikuwa rahisi kwani waajemi walikuwa wapiganaji stadi na wenye nidhamu ya hali ya juu.  Hivyo lilihitajika jeshi lililotimia katika maeneo yote. Khalifa akatuma wajumbe katika miji ya waislam iliyokombolewa kutangaza wito wa Jihadi na kukusanya wale wote wenye uwezo, utaalam, mbinu na mikakati kujiandaa na vita hivi adhimu.
 
Naam! Wanajihadi wakaitikia wito na kukusanyika Madina kutoka ila kona ya miji ya waislam. Kutokana na ukubwa wa jeshi la kiislam na uzito wa kazi yenyewe, Khalifa ikambidi afanye shura kuhusu nani atakuwa kiongozi wa jeshi. Ushauri wake Khalifa ulikuwa kuliongoza yeye mwenyewe kwani kazi ilikuwa nzito na kama ni Amirul Muuminin ni wajibu wake kuwaongoza waislam.  Sayyidina Ali hakuunga mkono wazo hilo na kumfahamisha Khalifa kwamba waislam walikuwa wanamuhitaji sana Khalifa kubaki Madina kuliko kwenda kuhatarisha maisha yake vitani.
 
Baada ya kupita shura, Saad akachaguliwa. Mmoja katika masahaba wakongwe Abdulrahman ibn Awl akampongeza Khalifa na kusema, “umejua kuchagua! nani mwengine zaidi ya Saad?”
Sayyidina Umar akasimama na kulitakia kila la kheri jeshi la kiislam na kumpa nasaha Saad kwa kumwambia:
 
“Ewe Saad! Usikubali maneno yoyote yatakayosemwa kwamba (umechaguliwa kwa sababu) ni mjomba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SW) au ni sahaba wa mjumbe wa Mwenyezi Mungu (SW), Mwenyezi Mungu (SW) haondoshi jambo baya kwa ubaya bali huondosha baya kwa jambo jema”
 
“Ewe Saad! Hakuna mahusiano yoyote kati ya Mwenyezi Mungu (SW) na mtu yoyote isipokuwa kwa kumtii yeye Allah (SW).  Kwa mtazamo wa Mwenyezi Mungu watu wote ikiwa ni mheshimiwa au mtu wa kawaida, ni sawa sawa.  Mwenyezi Mungu ni Mola wao, wote ni waja wake wanaotafuta kunyanyuliwa kwa taqwa na kutii.  Mkumbuke mjumbe wa Mwenyezi Mungu alivyokuwa akiwafanyia waislam na wewe ufanye hivyo hivyo!”
 
Amirul Muuminiin aliweka bayana kwamba vita hivi si kwa ajili ya mtu kupata umaarufu wala kutawala bali ni kulifanya neno la Mwenyezi Mungu “Laa Ilaha Ill allah” kuwa juu.
 
Watu elfu thelathini wakaanza safari kuelekea Qadisiyya wakiwemo tisini na tisa waliopigana Badr na zaidi ya mia tatu walioshuhudia suluhu ya Hudaybiya, pia wakiwemo takriban mia tatu wengine waliokuwamo katika jeshi la kuifungua Makka.  Wakiwemo watoto wa masahaba na wanawake waliokwenda kuwashajiisha na kama wauguzi.
 
Walipiga kambi Qadisiyya katika mji wa Hira, Waajemi walijiandaa na vita hivi na jeshi la watu laki moja na ishirini elfu wakiongozwa na kamanda wao shujaa Rustum.
 
Amirul Muuminiin alimuagiza Saad kumpelekea habari kwa kila kitakachotokea kwa waislam na makafiri.  Saad akamwandikia Amirul Muuminiin juu ya ukubwa wa jeshi lao na zana walizonazo.
 
Amirul Muuminiin akajibu, “Usitishike wala kushtushwa na utakayoyasikia kuhusu jeshi lao na mbinu watakazozitumia dhidi yenu.  Omba msaada kwa Mwenyezi Mungu na uwe na imani. Peleka ujumbe wa watu wenye busara, hekima na walio madhubuti wamlinganie kuingia Uislam na jitahidi kuniandikia kila siku.”
 
Saad alifanya kama alivyoagizwa na kutuma ujumbe mzito kwanza kwa Yazdaqird na baadaye kwa Rustum, wote kuwataka kuingia katika uislam na kulipa jizya (ushuru) ili wahakikishiwe usalama wao na kuishi kwa amani vyenginevyo wachague vita baina yao.
 
Ujumbe wa mwanzo wa waislam ulibezwa na kudharauliwa na kiongozi wa Waajemi, Yazdaqird.  Uliongozwa na Bin Nuum ibn Muqarrin. Ujumbe wa pili ukiongozwa na Rubiiy ibn Aamir kwa Rustum, ulikwenda moja kwa moja kambi ya Rustum. Huku akiwa na mkuki mkononi, Rubiiy akampa ujumbe  na Rustum akauliza:
 
“Rubiiy! Nini unataka kutoka kwetu?” ukiwa unataka utajiri, tutakupeni, mkitaka chakula tutakulisheni mpaka mkinai. “ Aliendelea kusema,
 
 “Tutakupeni nguo na kukufanyeni muwe matajiri na wenye furaha, tazama Rubriiy! Nini unaona kwenye majlis yangu hii,? Hapana shaka huoni alama za utajiri, mazulia ya fahari, mapazia ya kupepea, kuta zilizonakishiwa dhahabu, huna hata hamu basi tukikutunukia vyote hivi tulivyonavyo!”
 
Rubiiy alitulia na kumsikiliza Rustum akijifaharisha na kumwambia, “Sikiliza, Mwenyezi Mungu ametuchagua sisi na kutoka kwetu sisi kizazi chake ambacho mwenyewe Mwenyezi Mungu (SW) amemtaka ili kututoa kutoka kuabudu masanamu kwenda kwenye Tauhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu) na kututoa kutoka kwenye wale wote wanaojishughulisha na dunia (kusahau akhera), na kututoa kutoka watawala dhalimu dhidi ya uislam.” Aliendelea kusema,
 
“Na yeyote atakayetukubalia wito wetu tuko tayari kumkaribisha kwa mikono miwili na yoyote atakayeamua kupigana nasi, sisi tutapigana na mpaka ahadi ya Mwenyezi Mungu (SW) itakapotimia.
 
Rustum akauliza,
 
“Kitu gani amekuahidini Mungu wenu?”
 
“Pepo kwa wataokufa shahidi na ushindi kwa watakaoishi.” Alijibu Rubiiy.
 
Hata hivyo, Rustum kwa kujiona wo ni bora zaidi hakuwa tayari kuzingatia maneno haya hasa kwa mtu mwenyewe anayesema kuonekana dhalili na kwa kuwa karne nyingi, watu hawa walikuwa wakiwatawala na kuwajua kama walikuwa katili na wajinga.
 
Vita hivyo vikawa vinanukia, Saad alitokwa na machozi kwani kupindi hiki alikuwa mgonjwa hata kushindwa kusimama sawa sawa.  Aliona dalili zote kwamba vita hivi vitakuwa vikubwa, hatari na damu nyingi itamwagika. Akawa akisema moyoni Lau………….. Lakini hapo hapo akaikumbusha nafsi yake kwamba Mtume (SAW) amefundisha waislam kutosema Lau… kwani humaanisha ukosefu wa dhati na azma ya kufanya na kuona kwamba lau hali ingelikuwa tofauti si tabia ya kiislam.
Akajikongoja na kusimama mbele na kuanza kuwahutubia wanajihadi.  Alianza kwa aya ya 105 katika Quraan Suratul Anbiyaa,

“ Na hakika tulikwisha andika katika Zaburi baada ya kumbukumbu,ya kwamba ncha watarithi waja wangu walio wema” 
Baada ya kumaliza khutba ya kuhuisha nyoyo na kuwatia mori wanajihadi, wakasali sala ya adhuhuri jamaa na kuwageukia tena baada ya sala na kuwapa amri ya kupigana kwa kutamka  kilio cha kivita,
 
“Allah Akbar, Allah Akbar, Allah Akbar, Allah Akbar”  mara nne na kuamrisha washambulie huku akiwatia moyo kwa kusema, “Hayya ala barakatillah”, (haya wavamieni kwa baraka za Mwenyezi Mungu)
 
Kwa siku nne mfulululizo vita vilipigwana huku Saad akiwa kwenye hema lake akiongoza mashambulizi na kupanga mikakati na kuwatia mori wanajihadi,
 
“Allahu Akbar, Laa haula walaa Quwwata illaa Billahi.” 
 
Waislam walipigana kwa moyo wao wote na ufundi wakijua ima ni ushindi au shahada tu.  Baadhi ya wanajihadi mashujaa walitafuta mbinu mpaka kuweza kumfikia kamanda Rustum kwenye ngome yake. Hapo ikazuka piga nikupige ya aina yake kwani ni vumbi tu lililokuwa likitimka ndilo lililoonekana na paa la ngome ya Rustum kutupwa ndani ya mto. Kuona patashika hiyo Rustum alijaribu kukimbia lakini hakufika mbali na alikamatwa na kuuwawa.
 
Baada ya kuuwawa kwa kamanda wao majeshi ya Kiajemi yalianza kusambaratika na kukimbia huku na kule wasijue la kufanya na huku wanajihadi wa kiislam wakiwashambulia.
 
Vita hivi viliweka historia ya damu nyingi sana kumwagika kwani kwa siku nne tu zilizopiganwa vita hivi takriban watu elfu thelathini waliuwawa, na katika siku moja tu waislam elfu mbili walikufa shahidi na makafiri elfu kumi kupoteza maisha yao.
 
Vita vya Qadisiyyah vilileta ushindi muhimu sana kwa waislam.  Vilimaliza kabisa na kuondoa utawala wa kisasania kama vilivyokuwa vita vita vya Yarmuk kuumaliza utawala wa kibizantini.
 
Miaka miwili baadaye na kuwa na hali nzuri ya kiafya Saad alikwenda kuutwaa mji mkuu wa SasanCtesiphon, waliweza kuutwaa mji huu baada ya kuuvuka mto Tigris wakati wa mafuriko.
 
Shujaa wa Qadisiyyah kama alivyojulikana baada ya vita hivi, Saad, aliishi na kufariki akiwa na umri wa miaka themanini.  Kabla ya kufariki alimwita mwanawe na kumuomba afungue sanduku ambalo alikuwa amelihifadhi mwenyewe muda wote.  Ndani yake kulikuwa na juba la sufi na kumuusia mwanawe, “Nitakapokufa nikafinini kwa juba hili kwani ndilo nililokuwa nimevaa nilipokutana na makafiri siku ya vita vya Badr na ningependelea kukutana na Mwenyezi Mungu nikiwa nalo.”