Abu Al Asi Ibn Alrabiy - Alieahidi na Akatekeleza


(Kutoka katika kitabu صور من حياة الصحابة


cha Muandishi Dr, Abdurrahman Raafat Al-basha)



Kimefasiriwa na Ustaadh Talib Juma Ali


A
likuwa Abu Al-‘Asi ibn Alrabiy Alabshamy kijana mzuri aliye mrembo mwenye mvuto kwa mwenye kumuangalia, aliyezungukwa na neema, na mwenye nasaba iliyo bora. Hivyo alielekea kuwa ni miongoni mwa mashujaa wa kiarabu kwa kila maana iliyoibeba neno hili, akiwa ni mwenye murua na ahadi, na mwenye kila alama ya kujivunia urathi wa wazee na mababu.
Alirithi Abu al- ‘Asi kutoka kwa wazee, mapenzi ya biashara yaliyomo katika misafara miwili ya “miongo ya kiangazi na kipupwe”.
Havikuwa vipando vyake vyenye kukosekana au kuchoka kuwemo katika safari ya kwenda au kurudi baina ya Makka na Sham. Msafara wake ulikuwa ni wenye kukusanya baina ya watu wafikao mia mbili. Watu walikuwa ni wenye kumpa mali zao kufanyia biashara, ziada ya mali yake, nayo ni kwa sababu ya uzoefu wake, ukweli na uaminifu aliokuwa nao. 
Khala  (Shangazi) yake, bibi Khadija mkewe Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) alimfanya mfano wa mwanawe ndani ya nafsi yake na aliwacha nyumba yake kuwa wazi na kumkaribisha kwa furaha na mapenzi.Na hayakuwa mapenzi ya Mtume  (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) kwa Abu Al ‘Asi ni madogo kuliko ya bibi Khadija.
Siku zikawa ni zenye kwenda haraka na kupita katika nyumba ya Muhammad ibn Abdillah na mtoto wake mkubwa Zainab akawa tayari ameingia katika utu uzima na uwa la uzuri kuchanua na kupelekea nafsi za watoto wa nyumba bora za Makka kuvutiwa nae. Kwa nini isiwe hivyo?, wakati yeye ni mtoto bora wa nasaba miongoni mwa watoto wa kike wa kikureish na mwenye baba na mama watukufu na ni mwenye adabu na tabia njema? Lakini watampataje? Wakati Khala yake (Abu-al ‘Asi) amesimama mbele yao kuwa ni kizuizi naye ni Abu Al‘Asi ibn Al rabiy kijana miongoni mwa vijana wa Makka.
Haukupita muda baada ya ndoa ya wawili hawa Zainab bint Muhammad na Al-‘Asi isipokuwa nuru ya imani ya Allah Subhaanahu Wata’ala ikaangaza Mji wa Makka na Allah  Subhaanahu Wata’ala akamtuma Mtume wake Muhammad (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) na dini ya uongozi na ya haki na akamuamrisha kuwahadharisha jamaa zake wa karibu na akawa wa mwanzo kuamini miongoni mwa wanawake ni mkewe bibi Khadija bint Khuwaylid na watoto wake Ruqayyah, Ummukulthum na Faatimah licha ya kwamba Faatimah alikuwa ni mdogo.
Bahati mbaya mkwewe Abu al ‘Asi alichukia kuacha dini ya mababa na mababu zake. Hivyo akapinga kuingia (dini) aliyoingia mkewe, bibi Zainab, licha ya kwamba alikuwa ni mwenye kumpenda sana, mapenzi yaliyo safi na ya kweli.
Mivutano ilipozidi baina ya Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) na makureshi walisema baadhi yao wakiambizana: “kwa nini mnamsaidia Muhammad kwa kukubali vijana wenu wa kiume kuwaowa watoto wa Muhammad, laiti mngeliwaacha na kumrejeshea mwenyewe angekuwa ni mwenye kuwashughulikia wao baada yenu”.
Wakasema Hakika ni rai bora hiyo mliyoiyona wakamwendea Abu al ‘Asi na kumwambia: “muache mkeo ewe Abu al-‘Asi na mrejeshe nyumbani kwa baba yake. Nasi tutakuozesha mwanamke yeyote umtakae katika watoto wazuri wa kikureish”. Akawajibu; "hapana wallahi; mimi simwachi, mke wangu na mimi sina nimpendae katika wanawake wote wa dunia zaidi yake”.Ruqayyah na Ummukulthum wao wakaachwa na kurejeshwa kwake Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) alifurahishwa kwa hilo, na alitamani laiti Abu al-‘Asi nae angefanya walivyofanya rafiki zake. Na hakuwa na nguvu za kumlazimisha kumuacha kwani ilikuwa bado hakujateremka amri ya kuharamisha ndoa baina ya muislam mwanamke na mshirikina.
Alipohama Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) kwenda Madina na shauku kumzidi juu ya mtoto wake, na makureshi wakatoka kwa ajili ya kupambana na Mtume katika Badri, Abu al-asi alilazimika kutoka nao, sio kwa lengo wala hamu ya kupambana na waislamu au kwa kutaka chochote kile, bali ni kutokana na nafasi na cheo chake katika kaumu yake ndiyo iliyompelekea kuwa ndani ya msafara huo.
Vita vya Badr vilimalizika kwa kushindwa makureshi vibaya sana, vita ambavyo vilivunja kiburi vya shirki na kuvunja ufedhuli wao. Miongoni mwao wakauwawa na wengine kutekwa na wengine wakatoroka.
Miongoni mwa waliotekwa ni Abu-al ‘Asi mume wa Zainab bint Muhammad (Salallahu ‘Alayhi Wasallam). Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam), aliwawekea mateka wa vita hao fidya kwa ajili ya kuzikomboa nafsi zao. Fidya hiyo ilikuwa ni baina ya dirham elfu hadi elfu nne kulingana na hali na utajiri wa mateka huyo katika familia yake.
Ujumbe ukawa ni wenye kuja na kurudi baina ya Makka na Madina, ukiwa umebeba mali za kukombolea mateka wao. Bibi Zainab alituma nae mjumbe wake Madina akiwa amebeba fidya ya kumkombolea mumewe Abu-alasi. Nayo ilikuwa ni mkufu aliopewa zawadi na mama yake Bibi Khadija siku aliyoolewa.
Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) alipouona mkufu ule, vazi la huzuni liliugubika uso wake mtukufu na akamtamani na kumhurumia sana mwanawe, hapo hapo aliwaambia masahaba wake;
“Hakika Zainab ametuma mali hii ili kuwa ni kikombolea cha Abu al‘Asi mkihisi kumwachia huru Abu al ‘Asi na mkamrejeshea Zainab mali yake basi fanyeni". Masahaba wakajibu papo hapo: "Hakika hilo ni ombi bora kutoka kwako Mtume wa Allah".
Lakini Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) alimshurutishia Abu al ‘Asi kuachiliwa kwake. Lazima kuambatane na kumrejeshea mtoto wake haraka haraka bila ya kuchelewa. Abu al-‘Asi hakuingia Makka isipokuwa alianza kutekeleza ahadi yake. Akaamrisha bibi Zainab ajitayarishe kwa safari na akamwambia msafara wa wajumbe wa Mtume hawapo mbali na Makka wanamsubiri akamtayarishia mizigo na mnyama wake na akamwakilisha ndugu yake ‘Amru ibn Al-rabiy kufuatana nae na kumfikisha kwa wajumbe hao mkono kwa mkono.  ‘Amru bin Al-rabiy akaitia pinde, mishale alani, na kuvaa mabegani mwake na kumpandisha bibi Zainab ndani ya khawdaj[1] tayari kwa safari na alitoka mchana mchana mbele ya macho ya makureshi, watu wakaja juu na kumfuata na kuanza kumtisha na kumtia hofu.
Hapo ‘Amru alitoa upinde wake na kutia mshale wake, akasema: “yeyote atakayejaribu kumsogelea Zainab basi nitauachia mshale shingoni mwake”. Na ‘Amru alikuwa mwenye shabaha asiekosea.
Abu Sufiyan alikuwa ndio kwanza anafika alisema kumwambia ‘Amru: “Ewe mtoto wa ami yangu rejesha mshale dhidi yetu tuzungumze na akarejesha"  na Abu Sufiyan akasema:
“Hakika hujafanya jema kwa tendo lako hili kwani umetoka na Zainab mbele ya macho ya watu, wakati waarabu wote wanajua kushindwa kwetu na yaliyotufika kwenye mikono ya Muhammad. Ikiwa utatoka na mwanawe mbele ya macho ya watu kama ulivyofanya makabila yatatusema kwa woga na watatushusha hadhi na kutukebehi na kutudharau. Basi rejea nae na mwache kwa mumewe siku mbili tatu watu wakianza kusema kwamba tumemzuia kutoka, hapo toka nae kifichoficho (kwa kujificha?) na mpeleke kwa baba yake. Hakika sisi hatuna haja nae.”
‘Amru alikubali hayo na kurudi nae Makka. Baada ya siku kupita akatoka nae usiku na kumfikisha kwa wajumbe wa Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) mkono kwa mkono kama alivyousiwa na kaka yake. Abu al-‘Asi alikaa Makka baada ya kufarakana na mkewe hadi ilipokaribia Fat-h (kukombolewa) Makka kwa muda mchache. Alitoka kwenda Sham kwa ajili ya biashara. Alipokuwa akirejea Makka akiwa na wanyama (ngamia) wafikao mia na watu wasiopungua mia na sabini walitokewa na kikosi miongoni mwa vikosi vya Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) kikiwa karibu ya Madina vikateka wanyama na watu wake lakini Abu al‘Asi aliwahi kukimbia bila ya kutekwa.
Kiza kilipoingia Abu al ‘Asi alijificha na kuingia Madina kinyemela  mpaka akafika alipo Zainab na akaomba himaya na akampa.
Alipotoka Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) wakati wa alfajiri kwa sala na akawa tayari mihrabuni na analeta takbira ya kuhirimia na watu wakaleta takbira, sauti kali ya Zainab iliita toka safu za wanawake ikisema:“Enyi watu mimi ni Zainab bint Muhammad na nimempa himaya Abu al ‘Asi hivyo mlindeni.”
Baada ya Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam ) kusali alisema: “Mmeyasikia niliyoyasikia" wakasema: “ndiyo ewe Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam)”. Akasema: “Naapa na yule ambae nafsi yangu imo mikononi mwake (Allah) hakika sikuwa na habari yoyote ya haya mpaka pale niliposikia mliyoyasikia. Hakika muislamu anamlinda yule aliye chini yake”.
Kisha akaondoka kuelekea nyumbani kwake na akamwambia mwanawe:
“Mkirimu Abu al‘Asi lakini tambua hakika wewe sio halali yako akawaita walioteka mali yake na kuwaambia: “Hakika ni miongoni mwetu kama mjuavyo nanyi mmechukua mali yake. Mkimtendea wema na kumrejeshea mali yake itakuwa ni katika tuyapendayo ama ikiwa hamkurejesha itakuwa ni jumla ya - ngawira- ambayo Allah Subhaanahu Wata’ala ameruhusu kwenu na mtakuwa ni wenye haki".
Wakasema: “Bali tutamrejeshea mali ewe Mtume wa Allah” . Alipokuja kuchukua mali yake walimwambia: “Ewe Abu al ‘Asi hakika wewe ni mbora katika makureshi na ni mtoto wa ami yake Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam). na mkwewe jee huoni bora usilimu nasi tutakurejeshea mali zako zote upate kutononeka na neema na mali za watu wote wa Makka halafu wewe ubakie nasi Madina?" Akajibu: “Hakika ni wazo baya mlilonipa kuanza dini mpya kwa woga.
Abu al ‘Asi alitoka na wanyama wake na mali zake kuelekea Makka na alipofika alimpa kila mwenye haki, haki yake na akasema: "Enyi makureshi jee yuko aliebaki na haki yake kwangu hajaichukua?"
Wakasema: “Hapana Mungu akujaze kheri na kila wema hakika wewe ni muaminifu na mkarimu". Akasema: “Ama maadam nimetekeleza amana zenu na haki zenu, basi nashuhudia kwamba hakuna anaestahiki kuabudiwa kwa haki ila Allah na Muhammad ni Mtume wake. Wallahi hakuna kilichonizuia na uislamu kwa Muhammad Madina isipokuwa ni hofu yangu kwamba mtanidhania kuwa nilitaka kula mali zenu. Ama Allah Subhaanahu Wata’ala alipozirejesha kwenu na kujitakasa basi sasa nimesilimu".
Kisha akatoka na kuelekea hadi kufika kwa Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam) na akakirimiwa na kurejeshewa mkewe akawa anasema Mtume (Salallahu ‘Alayhi Wasallam): "Amesema akawa mkweli, akaniahidi akanitekelezea ahadi yangu".

 

[1] kijumba kidogo kinachowekwa juu ya ngamia