Suhayl ibn Amr-mwana diplomasia

Suhayl ibn Amr-mwana diplomasia

 
Kati kati ya vita vya Badr, Suhayl (kipindi hicho bado ni kafiri) akajikuta ndani ya mikono ya waislam mateka.  Umar ibn Khattab akamwambia Mtume (SAW):
 
“Ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Niachie mimi nimng’oe meno yake mawili ya mbele ili asiweze tena kusimama na kuweza kusema chochote dhidi yako baada ya hii leo.”
 
“Hapana Umar.  Sitomfanyia mtu yoyote ubaya asije Mwenyezi Mungu akanifanyia na mimi hata kama ni Mtume,” akamtahadharisha.  Akamwita Umar karibu yake na kumnong’oneza,
  “Umar! Labda  Suhayl atakuja kufanya jambo siku za usoni litakuja kukufurahisha.” 
Suhayl ni mtu mmoja maarufu katika maquraysh.  Alikuwa mzungumzaji mzuri na mara nyingi maoni yake hupewa kipaumbele.  Alifahamika zaidi kama ‘Khattaab’ msemaji mkuu wa maquraysh.  Umuhimu wake ulikuja kuonekana zaidi katika kukhitimisha ule mkataba maarufu wa Hudaybiya.
 
Mwishoni mwa mwaka wa sita Hijriya, Mtume (SAW) na kiasi cha masahaba elfu moja na mia tano walitoka Madina kuelekea Makka kutekeleza ibada ya Umra. Kuonesha kwamba hawakukusudia vita, waislam hawakuwa na silaha zozote ila panga zao tu viunoni.  Pia walichukua wanyama kwa ajili ya kuchinja kuonesha nia yao ni kuuzuru msikiti mtukufu wa Makka.
 
Maquraysh walipopata habari ya ‘ugeni’ huu, haraka wakajiandaa kwa vita.  Wakaapa kutowaruhusu waislam kuingia Makka.  Akatumwa Khalid ibn Walid (alikuwa bado kusilimu wakati huo) na jeshi la farasi kwenda kuwazuia. Jeshi la Makafiri likawasubiri sehemu moja iitwayo Karral Ghamim.
 
Mtume Muhammad (SAW) alipata habari za Khalid mapema kama anawasubiri. Licha ya kuwa na uhasama dhidi yao, muda huu Mtume (SAW) hakuwa tayari na vita hivyo akauliza:
“Kuna mtu yoyote anayejua njia nyengine ya kufika Makka ili kuepukana na Maquraysh.
 
Mtu mmoja wa kabila la Aslam akasema anaijua na kuwapitisha waislam njia nyengine ya taabu kwenye milima ya Warrah na hatimaye kuukaribia Makka kutoka upande wa kusini.  Khalid alipogundua kwamba amepigwa chenga akatahayari na kujirudia zake Makka.
 
Mtume (SAW) akapiga kambi Hudaybiya na kuwaashiria kwa maquraysh yuko tayari kwa suluhu kama watataka.  Maquraysh wakamtuma Badil ibn Warqa pamoja na watu wengine wa kabila la Khuzaa kuulizia nini lilikuwa lengo la ujio huu.  Alikutana na Mtume (SAW) na baadaye kurudi kwa Maquraysh na kuwataarifu nia njema ya Mtume (SAW) na masahaba zake.  Hawakumuamini wakisingizia Banu Khuzaa ni masahiba wa Muhammad wakauliza:
 
“Hivi anakusudia kuja na jeshi lote hili kufanya Umra tu?  Waarabu watasikia ametujia na kuingia Makka kwa nguvu wakati hali ya kivita bado ipo baina yetu.  Wallahi hilo halitotokezea bila ya rukhsa yetu.
 
Maquraysh wakapeleka ujumbe mwengine chini ya Halis ibn Alqamah, mkuu wa kabila la Ahabish, masahiba na Maquraysh.  Mtume (SAW) alipomwona Halis anakuja akasema, “Huyu mtu anatoka katika watu wanaothamini kuchinja wanyama. Watangulizeni wanyama wote ili apate kuwaona.  Hilo likafanyika, Halis akapokewa na waislam kwa talbiya:
 
“Labbayka llahumma Labbayka” na alipowajibu akasema kwa mshangao, “Sub-hana Allah watu  hawa hawana sababu ya kuzuiliwa kuingia Makka ikiwa wenye wagonjwa ya ukoma na punda wanaruhusiwa kuhiji iweje mtoto wa Al Muttalib azuiwe kuizuru nyumba ya Mwenyezi Mungu (SW)?”
 
Wallahi, Mola wa Alkaaba waache Maquraysh wahilikishwe.  Hawa watu wamekuja kutekeleza ibada ya Umra.”
 
Aliporudi na kuwataarifu maquraysh wakamrudi, “hebu kaa chini wewe ni mbedui tu wa kiarabu, hujui lolote juu ya mbinu wala njama?”
 
Akatumwa mjumbe mwengine Urwah ibn Masoud mkuu wa kabila la Atthaqaf toka Tail.  Alipofika akamwambia Mtume Muhammad (SAW):
“Ewe Muhammad umewakusanya watu wote hawa na kurudi sehemu uliyozaliwa.  Maquraysh wameapa kwa Mungu kwamba Makka hutoingia kwa nguvu. Nnaapa hawa watu wote watakuasi.”  Abubakar kusikia vile akamwendea Urwah na kumbeza, “Tumuasi Muhammad? Adhabu iwe juu yako.”
 
Wakati Urwah akiongea alimgusa Mtume (SAW) ndevu zake. Mughira ibn Shubah akamkwapua mkono wake, “ondoa mkono wako hapa!”
Urwah akajibu :”Adhabu iwe juu yako mtu katili sana wewe, ” Mtume (SAW) akatabasamu.  Urwah akauliza, “ni nani huyu yaa Muhammad?”
“Ni binamu yako Al-Mughira”
“Hana adabu” Urwah akaendelea kumwagia matusi.”
 
Urwah akaanza kuwakagua masahaba wa Mtume (SAW) akagundua wakipewa amri, hutii tena kwa haraka.  Akitaka kutawadha au kuoga, masahaba kushindana kila mtu akitaka kumpelekea maji.  Wakiongea mbele yake, huongea kwa sauti ya chini chini na hata hawamuangalii usoni kwa kumheshimu.
 
Naye aliporudi, akaelezea jinsi alivyovutiwa nao:
 
“Enyi Maquraysh!  Nilikwenda kumtembelea Chosroes  kwenye milki yake, nilimuona Qaysar (Caesar) mtawala wa kibizantini kwenye kilele cha utawala wake, lakini sijawahi kumuona mfalme mbele ya watu wake kama Muhammad mbele ya masahaba.  Nimewaona watu ambao hawana hata nia ya kumuasi seuze dhamira ya kumgeuka.  Fikirieni sana msimamo wenu huu amekuleteeni mwongozo wa haki, kubalini alichokuleteeni, ushauri wangu unatoka ndani ya moyo wangu……….
Sidhani kama mtapata ushindi dhidi yake milele!”
“Usiseme hivyo,” Maquraysh wakadakia, “Tutamwambia arudi zake Madina na aje mara nyengine wakati ujao.”
 
Wakati huo huo, Mtume Muhammad (SAW) akamtuma Uthman ibn Affan kwa Maquraysh kuwafahamisha lengo na madhumuni ya safari yake Makka, na pia kuwaomba wawaruhusu kwani wanataka pia kuwakagua jamaa zao.  Uthman pia alikuwa na lengo la kuwashajiisha wale dhaifu wa Makka waliobaki na kutofanya Hijra na kuwataarifu kwamba fat-h inakuja karibu……
 
Uthman akafikisha salamu za Mtume (SAW) kwa Maquraysh na bado wakashikilia msimamo wao wa kutoruhusu kuingia Makka.  Wakamwambia Uthman kwamba anaweza kufanya Tawwaf Al kaabah.  Uthman akawajibu kwamba hilo halitowezekana kwani hatoweza yeye kutufu wakati Mtume wa Mwenyezi Mungu anakatazwa.  Wakamkamata Uthman na kumsweka ndani mahabusu. 
 
Uvumi ukazuka kwamba tayari ameuwawa.  Mtume aliposikia akabadilika ghafla.   Akasema:
 
“Hatutoondoka mpaka tupigane.”
 
Akawatolea khutba na kuwataka wafanye bay-ah- kiapo cha utii cha kuwa tayari kupigana.  Wakakusanyika watu pale Mtume alipokaa na wote kuapa kuwa tayari kwa vita.  Muda mfupi baadaye, Mtume (SAW) akathibitisha kwamba ulikuwa ni uvumi tu.
 
Kufikia hali hii ndipo Maquraysh wakamtuma Suhayl ibn Amr.  Ujumbe wake ni mfupi tu:
“Mtume arudi Madina.”  Uteuzi wa Suhayl kwa shughuli hii ulikuja kutokana na sifa zake za kuwa msemaji na mzungumzaji mzuri na mpatanishi wa kutegemewa.
 
Mtume Muhammad (SAW) alipomuona Suhayl anakuja akajua kwamba msimamo wa Maqurash unaelekea kubadilika,
 
 “sasa wanataka upatanishi ndio maana wamemtuma mtu huyu.”
 
Mazungumzo yalikuwa marefu na hatimaye wakafikia makubaliano ya kimsingi.  Umar na baadhi ya masahaba hawakufurahishwa na masharti ya makubaliano hayo wakiona kama kwamba hayatawasaidia waislam na ni ushindi kwa makafiri.  Mtume (SAW) akawahakikishia kwamba hivyo wanavyodhani sivyo, kwani Mtume (SAW) hawezi kubisa kwenda kinyume na amri ya Mwenyezi Mungu (SW) na Mwenyezi Mungu mtukufu hatomuacha mkono.  Akamwita Ali ibn Talib aandike masharti ya mkataba:
 
“Andika Bismillahir Rahmanir Rahiim.”
 
Suhayl akaruka, “siijui hii.”
 
“Andika badala yake, Bismika Llahumma.”
 
Mtume akakubali, kasha akasema andika haya yafuatayo:
  “Ndivyo walivyokubali kati ya Muhammad mjumbe wa Mwenyezi Mungu na Suhayl ibn Amr………….. 
Suhayl hakukubaliana naye, “kama nikishuhudia ya kwamba hakika wewe ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu nisingelipigana nawe.  Andika badala yake jina lako na la baba yako.” Na hili pia Mtume (SAW) akalikubali, na kumuagiza Ali aandike:
 
“Haya yafuatayo ndivyo walivyokubaliana kati ya Muhammad ibn Abdullah na Suhayl Ibn Amr………..
 Kusimamisha vita kwa muda wa miaka kumi ambapo watu waishi kwa amani na kujiepusha kudhuriana.
Kwamba, yoyote miongoni mwa Maquraysh akija kwa Muhammad bila ya idhini ya walii wake, Muhammad amrudishe na yoyote ambaye yuko na Muhammad akienda kwa Maquraysh wao hawatomrudisha…..
 
Suhayl aliweza kuwafanya Maquraysh wawe na pahala pa kuweka uso wao kwani ni dhahiri kwamba alivutia upande wa Maquraysh huku Mtume (SAW) akimvumilia.
 
Miaka miwili baada ya mkataba wa Hudaybiya katika mwaka wa nane Hijiriya Maquraysh wakakiuka masharti .  Waliwaunga mkono Banu Bakr katika umwagaji wa damu dhidi ya Khuzai ambao walikuwa wakimuunga mkono Mtume (SAW)
 
Mtume (SAW) akaitumia nafasi hii kufanya safari ya Makka lakini lengo halikuwa kulipiza kisasi.  Waislam elfu kumi walifanya safari hii na kuingia Makka ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhani Maquraysh walipoliona jeshi la waislam hawakuwa na ubavu wa kulizuia na mji wa Makka kusalimu amri kwa Mtume Muhammad (SAW).  Mtume (SAW) akatangaza msamaha na kuwaita viongozi wa Maquraysh:
 “Enyi Maqurysh, mnafikiri nitakufanyeni nini?” 
Suhayl ibn Amr akajibu, “Tunafikiria utatutendea wema.”
Tabasamu likatanda kwenye uso wa Al-habib Mustafa (SAW) kisha akasema,
  “Idh-habuu….wa antum attulaqaa. ( Nendeni mko huru)” 
Kusikia habari hii ya kuachiwa huru tena bila ya kutarajia, Suhayl ibn Amr akatangaza kusilimu kwake pale pale.  Bila ya shaka imani yake wakati ule haikuwa imani ya mtu alieshindwa na kukata tamaa bali kama itakavyokuja kuonekana baadaye, ilikuwa kwa ajili ya uislam na kwa ajili ya upendo kwa Al-habib Mustafa (SAW).
 
Wale wote waliosilimu siku ya Fat-h Makka walipewa jina la ‘attulaqaa’ walioachiwa huru.  Waliona  jinsi walivyokuwa na bahati na wengi wao wakijitolea kwa hali na mali kwa ajili ya uislam ambao muda wote walikuwa wakiukandamiza.
Miongoni mwao ni Suhayl Ibn Amr.
 
Uislam ulimjenga upya.  Sifa zake zote alizokuwa nazo zikapata msukumo mpya na kuwa bora na bora zaidi.  Kwa ufupi tu sifa zake zinaweza kutajwa kama ifuatavyo: mkarimu, mpole, mtekelezaji sala, mfungaji, msomi wa Quran na kadhalika. Huyu ndie Suhayl aliekuja fahamika.  Licha ya kuchelewa kusilimu, Suhayl alibadilika na kuwa mcha mungu na mpiganaji jihadi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mtukufu.
 
Habari za kufariki kwa Mtume (SAW) zilipofika Makka ambapo Suhayl alikuwa akiishi, waislam waliingiwa na mtafaruku Madina na hata Makka.  Abubakar Siddiq alijitahidi kutuliza hali hii Madina kwa usemi wake maarufu.
“Yoyote aliyekuwa anamuabudu Muhammad, basi Muhammad amekufa.  Na yeyote anaemuabudu Mwenyezi Mungu basi Mwenyezi Mungu (SW) yuhai na wala hatokufa milele.”
 
Mjini Makka, Suhayl akawa na jukumu hilo hilo la kuwatuliza waislam.  Akawaita waislam na kuwapo taarifa za kifo cha Mtume Muhammad (SAW) na kuwahakikishia kwamba Muhammad alikuwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu (SW) na kama amefariki basi atakuwa tayari amekamilisha ile kazi aliyopewa ya kuwalingania watu na kuitangaza dini ya Mwenyezi Mungu mtukufu.  Na ni wajibu wa waislam kuiendeleza kazi hii baada ya kufa kwake na kuyachukua maisha yake yote kwa ‘Qudwah’ ruwaza na mfano wa kuiendeleza kazi hii.
 
Siku hii ndiyo ile siku aliyoitabiri Mtume Muhammad (SAW) pale alipomwambia Umar alipotaka kumng’oa jino Suhayl, “Mwachie, labda kuna siku atakuja kukufurahisha.”
Habari hizi za ‘khutba’ nzito ya Suhayl kwa waislam wa Makka zilipofika Madina, Umar ibn Khattab akamkumbuka Mtume (SAW).  Ni ile siku ambayo meno mawili ya mbele ya Suhayl yaliyotaka kutolewa naye yamefaidisha umma wa Mtume Muhammad (SAW).
 
Aliposilimu Suhayl alijiwekea nadhiri ifuatayo kwa ufupi:
 
Kuzidisha juhudi kuutumikia uislam, kwa uchache basi kama alivyofanya alipokuwa kafiri, alipokuwa akimshirikisha Mwenyezi Mungu alipoteza muda wake mwingi mbele ya masanamu.  Akawa anatumia muda wake mwingi pamoja na waumini mbele ya Mungu mmoja tu, akisali na kufunga.
 
Kabla ya kusilimu, Suhayl alishiriki kwenye vita vingi dhidi ya Uislam.  Sasa akawa dhidi ya ukafiri na alipigana kwa moyo mmoja dhidi ya waajemi Persia na ukandamizaji uliokuwa ukifanywa na utawala wa Kibizantini.
 
Akawa na ari, alitoka kuelekea Syria pamoja na waislam na kushiriki kikamilifu kwenye vita vya Yarmuk vita viliyokuwa vikubwa na vya kutisha katika histora ya kiislam.
 
Suhayl alikuwa akikupenda sana Makka.  Hata hivyo, baada ya ushindi wa waislam Syria akakataa kata kata kurudi Makka huku akisema:
“Nilimsikia mjumbe wa Mwenyezi Mungu (SW) akisema,
 
‘mtu yoyote anaetoka fi sabili Ilah kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa muda wa saa moja tu basi ni bora kwake kuliko shughuli za maisha yake yote alizojishughulisha akiwa nyumbani kwake.”
 
Akaahidi, “Nitakuwa ‘muraabit’ (niliyejifunga) kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mpaka kufa kwangu na sitorudi tena Makka.
 
Naam! Maisha yake yote, Suhayl alithibitisha ahadi yake hii.  Alikufa huko Palestina kwenye kijiji kidogo cha Amawas karibu na Jerusalem.