Barakah - Mama Mlezi wa Mtume



Barakah-mama mlezi wa Mtume Muhammad (SAW)

 
Hatuna data za uhakika kuweza kujua vipi huyu binti wa kihabashah aliishia Makka kuuzwa.  Hatumjui asili yake, wazazi na nasaba yake.  Kama walivyokuwa watoto wengi wa kike na kiume, waarabu na wasiokuwa waarabu walikamatwa na kuletwa kwenye soko la watumwa Makka.
 
Baadhi yao yaliwakumba mambo mengi tu kuishia kuwa chini ya wakubwa na ‘mabibi’ wakatili na kutumika kama punda bila ya kujali watu wakarimu na wanaojali.
Barakah, binti wa Kihabashah, alibahatika .   Alifika nyumba ya Abdullah ibn AbdulMuttalib.  Alikuwa mtumishi pekee nyumbani kwake na Abdullah alipomuoa bibi Aminah aliendelea pia kumhudumia.
 
Kwa mujibu wa Barakah, wiki mbili tu baada ya ndoa ya Abdullah na Amina, baba yake Abdullah, Bwana Abdul Muttalib alikuja nyumbani na kumtaka mwanawe aambatane na msafara wa biashara uliokuwa ukielekea Syria.  Bi Amina alisikitika sana na kuanza kulia:
 
“Mambo gani haya! Mambo gani haya! Vipi mume wangu aondoke na mimi ndio kwanza bi harusi na hata hina bado haijatoka mikononi mwangu?”
 
Kuondoka kwake kulikuwa pigo kubwa kwa Bi Amina, hakuweza kulistahamilia kwani hapo hapo alipoteza fahamu.  Barakah anaendelea:
“Nilipomuona bi Amina hana fahamu, nikalia kwa sauti kubwa na ya kusikitika; Ewe bibi yangu! Bi Amina akafungua macho huku akitokwa na machozi na kusema, nipeleke kitandani”
 
Bi Amina alibaki kitandani kwa muda mrefu na hakutaka kuzungumza na mtu yoyote, hakutaka kumuona mtu yoyote anayetembelea isipokuwa Abul Muttalib mkwewe.  Miezi miwili baada ya safari ya Abdullah, Bi Aminah akaniita siku moja alfajiri huku uso wake umejaa tabasamu na kuniambia:
“Barakah! Nimeota ndoto ya ajabu.”
“Kuna jambo zuri, bibi yangu.” 
Aliendelea “Nimeona nuru imetoka tumboni mwangu ikamurika milima, majabali na mabonde yanayoizunguka Makka.”
“Ni mja mzito nini bibi yangu.”
“Naam, Barakah! Lakini sijihisi kuumwa umwa kama wanavyokuwa wanawake wengine.”
“Utazaa mtoto ambaye ataleta kheri” akamalizia Barakah
 
Muda wote ambao Abdullah alikuwa safarini Bi Aminah  alikuwa mnyonge sana.  Muda wote Barakah alikuwa naye na kumliwaza huku akimchangamsha kwa riwaya na hadithi.
 
Bi Amina alisikitishwa zaidi pale mkwewe, Bwana Abdul Muttalib alipokuja siku moja na kumtaka aondoke nyumbani na kwenda milimani kama watu wote wa Makka wanavyofanya kwani mtawala wa Yemen alikuwa akijiandaa kuivamia Makka.
 
Amina alilalamika hali yake ya uja uzito na hana nguvu za kuelekea huko milimani.  Abdul Muattalib alikasirika sana lakini Bi Amina wala hakuwa na woga wowote.
Usiku na mchana, Barakah alikaa na Bi Amina.  Barakah anasema:
“Nilikuwa nikilala chini ubavuni mwa kitanda cha Bi Aminah na husikia kuugua kwake usiku huku akimtaja mumewe.  Akiugua hunifanya niamke na hujaribu kumliwaza na kumpa moyo.”
 
Kundi la kwanza, likarudi kutoka Syria na kupokelewa kwa hoi hoi na vifijo na familia za wafanya biashara Makka.  Barakah alikwenda kwa kujificha hadi nyumbani kwa Bwana Abdul Muttalib kujua habari za Abdullah.  Hakukuwa na habari zozote.  Akarudi kimya hadi nyumbani na wala hakumwambia lolote Bi Aminah asijea kazidi kuchanganyikiwa.  Baada ya kundi zima likarudi bila ya Abdullah.
 
Zilipofika habari za kufariki kwa Abdullah, Madina.  Barakah alikuwepo kwa Bwana Abdul Muttalib na anasimulia:
Nilipiga ukelele huo niliposikia na sikujijua tena nikatoka mbio hadi nyumbani kwa Bi Amina nikipiga kelele na kulalama kwa kuwa hatunae tena duniani.  Kulalama kwa kuwa kipenzi chetu ambaye tulikuwa tukimsubiri kwa muda mrefu, na kulalama kwa mmoja katika vijana watanashati wa Makka keshatutoka.
 
“Bi Amina alipopata habari akapoteza fahamu na nikakaa karibu naye akiwa katika hali ambayo si hai na wala si maiti.  Hakukuwa na mtu mwengine zaidi yetu.  Nikamuuguza usiku na mchana mpaka alipojifungua mtoto wake.
 
Alipozaliwa, Barakah ndiye aliempokea na kuwa mtu wa kwanza kumpokea mtoto.  Na alipokuja babu yake Abdul Muttalib akampa jina la Muhammad na akamchukua hadi Al-kaabah na wakaazi wote wa Makka wakafurahi kuzaliwa kwa Muhmmad.
 
Barakah akaendelea kukaa na Bi Amina pale Muhammad alipopelekwa ‘Badiyyah’ jangwani kulelewa na Bi Halima.  Aliporudishwa akiwa na umri wa miaka kama mitano hivi.  Mama yake alimpokea kwa furaha na upendo na Barakah kumkaribisha kwa hamu.
 
Muhammad alipokuwa na miaka sita mama yake akaamua kuzuru kaburi la mumewe Yathrib.  Barakah na Bwana Abdul Muttalib walijaribu kumshawishi asifanye safari hii.  Bi Amina hakukubali ushauri wao.  Siku moja asubuhi wakatoka Bi Amina, Muhammad na Barakah wakapanda ngamia, wakiwa ni miongoni mwa msafara mkubwa wa biashara ukielekea Syria.
 
Msafara ulichukua siku kumi kufika Yathrib.  Muhammad akabaki kwa wajomba zake wa Banu Najjar wakati Bi Aminah akifanya ziara kila siku katika siku chache alizokuwepo Madina, Bi Aminah alitembelea kaburi la mumewe huku akiwa na huzuni.
 
Na walipokuwa njiani kurudi Makka, Bi Aminah akapatwa na homa kali.  Walipofika Al-Abwa, mji uliopo kati kati ya Makka na Yathrib, walisimama.  Hali ya Bi Aminah ilizidi kuwa mbaya na joto lake kupanda.  Homa ikapanda kichwani, akamwita Barakah kwa sauti ya kukohoa kohoa.  Barakah anasimulia:
Akanieleza kwa sauti ya chini, “Ewe Barakah, ninaona kama karibu nitaondoka duniani.  Ninamuaacha mwanangu umlee.  Baba yake alikufa wakati yuko tumboni.  Hivi sasa hapa anampoteza mama yake mbele ya macho yake.  Uwe kama mama yake na usimwache kabisa!”
 
“Moyo wangu ukaishiwa na nguvu na nikaanza kulia kwa kwikwi mpaka mtoto akashtuka na yeye kuanza kulia.  Akajirusha na kumkumbatia mama yake kwa nguvu huku mama anakata roho.”
 
Barakah akarudi Makka na mtoto yatima, hana baba wala mama na kumpeleka kwa babu yake Bwana Abdul Muttalib.  Alikaa hapo kwa ajili ya kumlea na miaka miwili baadaye alipokufa babu yake alikwenda naye pamoja kwa  ami yake Abu Talib.
 
Aliendelea kumshughulikia mpaka akawa mkubwa na kuoa.  Barakah naye akamfuata Muhammad kwenye nyumba ya Bi Khadija.  “Sijawahi kumuacha na wala yeye hajawahi kuniacha,”  alisema.
 
Siku moja alikuja Muhammad (SAW) na kumwita
 “Ya, Ummah! (siku zote alimwita mama).  Mimi nimeshaoa na wewe bado hajaolewa.  Unaonaje akija mtu kukuposa.?” 
Barakah akamwangalia Muhammad na kusema, “Sitokuacha hata kidogo, hivi mama anamtupa mwanawe?”
Muhammad akatabasamu na kumbusu kwenye kichwa chake na akamtizama mkewe Bi Khadija na kumwambia.
  “Huyu ndiye Barakah.  Huyu ni mama yangu baada ya mama yangu.  Ni sehemu ya ukoo wangu.” 
Bi Khadija akamwambia Barakah, “Barakah! Umeupoteza ujana wako kwa ajili ya Muhammad naye sasa anataka kukulipa baadhi ya fadhila zako, kwa ajili yangu na yake, kubali uolewe kabla ya uzee kukufika.”
 
“Niolewe na nani mie?” Akauliza Barakah.
 
“Kuna Ubayd ibn Zayd wa kabila la Khazraj kutoka Yathrib amekuja kukuposa.  Tafadhali usikatae.”
 
Barakah alikubali na akaolewa na kwenda Yathrib kwa mumewe.  Akajaaliwa mtoto wa kiume na kumwita Ayman.  Tokea hapo watu wakamwita ‘Umm Ayman.”
Kwa bahati mbaya ndoa yake haikudumu kwani mumewe alifariki na yeye kujirudia zake Makka kwa ‘mwanawe’ Muhammad nyumbani kwa Bi Khadijah.   Katika nyumba hiyo pia walikuwepo Ali ibn Talib, Hindi (mtoto wa Bi Khadija kwa mumewe wa kwanza na Zayd ibn Harith.
 
Zayd ni mwarabu wa kabila la Kalb.  Alikamatwa alipokuwa mdogo na kuletwa Makka kuuzwa soko la watumwa.  Alinunuliwa na jamaa yake Bi Khadija.  Zayd akajikuta yupo karibu mno kwa Muhammad mpaka uhusiano wao ukawa kama wa baba na mwana.  Na pale baba yake Zayd alipokuja Makka kumtafuta mwanawe, Zayd alipewa jukumu la kuchagua kama kukaa na Muhammad au kwenda kwa baba yake. Majibu yake yalikuwa ni haya:
“Katu sitomwacha mtu huyu. Yale mambo aliyomtendea ni sawa na baba anavyomtendea mtoto wake. Hakuna hata siku moja niliyojihisi kama mtumwa.  Na amenishughulikia vizuri tu, ni mpole na mwenye upendo na kuhakikisha kwamba nipo katika furaha.  Ni mtu mmoja mpole wa ajabu na mbarikiwa katika viumbe.  Vipi nimwache ili niende na wewe?……..katu sitomwacha.
 
Baadae, Muhammad akamwambia uko huru.  Hata hivyo, Zayd aliendelea kuishi naye na kuwa sehemu ya familia. 
 
Wakati Mtume (SAW) alipoteremshiwa wahy.  Barakah na Zayd walikuwa ni miongoni mwa watu wa mwanzo kusilimu.  Walipata pia mikiki na mateso ya Maquraysh kama walivyokuwa waislam wa mwanzo.
 
Barakah na Zayd walikuwa na umuhimu wao mkubwa enzi hizo.  Walikuwa kama mashushushu kwani walijitolea kustahamili mateso na adhabu za Maquraysh ili kupata habari za mkakati na mbinu za Makafiri.
 
Siku moja, Makafiri wakafunga njia zote zinazoelekea kwa Al-Arqam ambapo Mtume Muhammad (SAW) huwakusanya masahaba na kuwafundisha dini ya kiislam.  Bi Khadija akawa na ujumbe muhimu kwenda kwa Mtume (SAW).  Akamtuma Barakah, Barakah akayahatarisha maisha yake kwa kuweza kupenya mtego huu wa Maquraysh na kufika kwa Mtume Muhammad (SAW) na kumfikisha ujumbe Mtume (SAW), Mtume akatabasamu na kumwambia:
 “Umerehemewa, Umm Ayman.  Bila ya shaka una pahala pako peponi.” 
Alipoondoka Mtume (SAW) akawauliza masahaba,
 “Ikiwa mtu anataka kuoa mwanamke katika watu wa peponi basi na amuoe Umm Ayman.” 
Masahaba wote wakanyamaza kimya na hakuna yoyote aliyesema kitu, Umm Ayman hakuwa mzuri wa sura wala hakuvutia.  Umri wake ulikuwa ni miaka Khamsini na keshaanza kuzeeka.  Licha ya hivyo Zayd ibn Harithah akajitokeza na kusema:
 
“Ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu mini nitamuoa Umm Ayman, ni bora yeye kuliko wanawake walio na uzuri na hadhi.”
 
Wakaoana na kujaaliwa mtoto wa kiume na wakamwita Usamah.  Mtume (SAW) alimpenda sana Usamah na alikuwa akicheza naye, akimbusu na kumlisha.  Tokea utotoni kwake Usamah alijitolea nafsi yake kwa ajili ya Uislam na baadaye akaja kupewa majukumu makubwa na Mtume (SAW).
 
Pale Mtume (SAW) alipohamia Yathrib ambayo ikaja kujulikana kama Madina, alimwacha Umm Ayman Makka kwenye nyumba yake kwa shughuli fulani.  Baadaye Umm Ayman akaifanya safari hii peke yake.  Ilikuwa safari ya taabu na mashaka akikata majagwa, majabali na milima.  Joto lilikuwa kali, mchanga unaunguza, vumbi linatimka na alistahamili yote hayo mpaka kuwasili Madina.  Alipofika miguu yake ilikuwa imevimba, uso wake hatuamaniki kwa vumbi na michanga.
 
“Ya Umm Ayman! Ya Umm Ayman! (Oo Umm Ayman, oo mama yangu)  Bila ya shaka una pahala peponi.” 
 
Alitamka Mtume (SAW) pale alipomuona Mtume (SAW) akamfuta uso wake na kumkanda miguuu na mabega.
 
Ummm Ayman alishiriki kikamilifu katika kuushughulikia Uislam Madina.  Katika vita vya Uhud, aliwashughulikia majeruhi na kuwagawia maji.  Alishiriki kwenye vita vya Khaybar na Hunayn pamoja na Mtume (SAW).
 
Mwanawe Ayman alikufa shahidi kwenye vita vya Hunayn. Mumewe Zayd alikufa shahidi kwenye vita vya Mut a huko Syria.  Kipindi hicho Barakah alikuwa na miaka sabini na muda mwingi alikuwepo nyumbani. Mtume (SAW) akifuatana na Abubakar na Umar humtembelea mara nyingi na humuuliza, “vipi hali yako hujambo?”
Naye hujibu, “sijambo, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu maadam uislam upo na unaendelea!
 
Alipofariki Mtume (SAW), Barakah alikuwa akionekana mara nyingi kutokwa na machozi na anapoulizwa kwa nini unali hujibu; “Wallahi, nilijua kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu atakufa lakini ninalia kwa sababu (kifo chake) ndio mwisho wa kuteremshiwa Wahy kwetu.”
 
Barakah alikuwa mtu mmoja muhimu sana kwani ni mtu pekee aliekuwa karibu na Mtume (SAW) katika maisha yake yote tokea kuzaliwa kwake mpaka kufariki.  Alifariki enzi za Ukhalifa wa Uthman.
 
 Ndio, asili yake haikujulikana lakini mahala pake peponi tayari amethibitishiwa.