Ammaar bin Yaasir Pepo Ilikuwa na Hamu Naye





Ammaar bin Yaasir 

Pepo Ilikuwa na Hamu Naye




Alitoka baba yake Ammaar, Mzee Yaasir Yemen kuja Makkah kumtafuta kaka yake. Na baadae akapafanya Makkah ndiyo makaazi yake akiwa chini ya Hudhyafah Ibn Mughiyrah. Na ni Hudhayfah aliemshauri Yaasir kumuoa mmoja wa wajane aliokuwa nao Sumayyah bin Khiyaat. Na katika ndoa hii alizaliwa ‘Ammaar.
Familia hii ilikuwa ni miongoni mwa familia za mwanzoni kusilimu pale alipowalingania Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam dini na kuongoka katika kufuata dini ya haki.
Tatizo lililokuwepo Makkah wakati huo ni kuangaliwa aliesilimu anatoka katika ukoo wa aina gani. Wakiwa miongoni mwa koo zenye nguvu na zinazoheshimika hutumia njia ya kuwaonya na kuwatisha kama alivyokuwa akisema Abu Jahl:

تركت دين آبائك وهم خير منك.. لنسفّهنّ حلمك، ولنضعنّ شرفك، ولنكسدنّ تجارتك، ولنهلكنّ مالك"

“Umeacha dini ya baba zako ambayo ni bora kwako na tutaivunja ndoto yako na kuiondoa hadhi yako na kuzigomea biashara zako na kuangamiza mali zako”
Na kama walitoka katika ukoo usiokuwa na hadhi  pamoja na maskini na wasiokuwa na uwezo hawa ndio walichokiona cha moto. Familia ya Yaasir ilikuwa ni miongoni mwao
Kabila la Bani Makhzuum ndilo lillilopewa jukumu la kuiadhibu familia hii yote Yaasir,Sumayyah na mtoto wao ‘Ammaar. Na adhabu waliyokuwa wakiipata si rahisi kuisimulia kwani kipindi hichi uislamu ulikuwa bado hauna nguvu.
Adhabu waliyoipata ilifikia hadi ya kushindwa kuvumilia huku wakisema kumwambia Mtume Salla Allah ‘Alayhi Wasallam:

يا رسول الله.. لقد بلغ منا العذاب كل مبلغ"..                                    

Yaa Rasuulu Llah ! Adhabu tunayopewa imetufikia kikomo(hatuwezi kuvumilia tena)”
 Mpaka kumfanya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kila siku kutoka kwenda kuwapa pole na kuwausia kwa kusema:

" صبرا آل ياسر ان موعدكم الجنة                                              

Vumilieni Aali Yaasir kwani  hakika mmeahidiwa pepo
Adhabu waliyokuwa wakiipata inasimuliwa katika hadithi tofauti kutoka kwa masahaba kama anavyosema Amr bin Haakim : “ Ammaar alikuwa akiadhibiwa mpaka akawa hajui anachokisema”
Yaasir baba yake ‘Ammaar – Allah awawie radhi wote – alikuwa akiwa matesoni. Mkewe, Sumayyah  mama yake Ammaar akamtolea maneno ya ukali Abu Jahal, maneno haya yalimkera na kumchoma Abu Jahal. Akaamua kumchoma mkuki mbeleni na kumuua mbele ya mwanawe. Historia ya Uislamu haiandikiki bila ya kumtaja bibi huyu, kwani yeye ndiye mtu wa kwanza kuuawa shahidi katika Uislamu. Baada ya kifo cha baba na mama yake, Ammaar alizidishiwa adhabu maradufu. Wakati walimuadhibu kwa kumlaza katika mchanga wa jangwani na kumuwekea jiwe kubwa kifuani, mara nyingine wakimuunguza kwa moto na huku wakimuambia : Hatutakuachilia mpaka umtukane Muhammad na uwataje kwa wema lata na uzzah (Waungu wa kisanamu wa Maquraish wakati huo). Akafanya kama wanavvotaka kutokana na adhabu kali. Na ‘Ammaar, bila ya kujijua, akawa akiyakariri haya maneno anayoambiwa
Adhabu ilifikia hadi mpaka ‘Ammaar alikuwa akipoteza fahamu na wakati mmoja walimuadhibu mpaka hakujijua . Alipozinduka na kukumbuka aliyokuwa akiyasema aliingiwa na majuto huku akijua ni kosa kubwa kuyatamka na alipokutana na Mtume alikuwa akilia kwa majuto na Mtume alikuwa akimfuta machozi na kumwambia usiwe na wasiwasi. Wakija tena na kukutaka utamke wanayokutaka uyatamke wakubalie kisha akamsomea aya ya Quraan Annahl /106

         إِلاَّ مَنْ أُكْرِهَ وَقَلْبُهُ مُطْمَئِنٌّ بِالإِيمَانِ                  

Isipokuwa aliye lazimishwa na hali ya kuwa moyo wake umetulia juu ya Imani
Tokea wakati huo ‘Ammaar hakuhuzunishwa wala kujutia kwani alijua kwamba Allah Subhaanahu Wata’ala amemhakikishia kwamba ataziangalia nyoyo na si matamshi yanayotoka vinywani wakati moyo unayasuta.
Baada ya waislamu kuhamia Madina na dola la kiislamu kuasisiwa , ‘Ammaar alikuwa ni miongoni mwa masahaba waliokuwa na hadhi kubwa kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kwani alikuwa akipendwa na Mtume huku Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam hukaa na kumsifia juu ya imani yake na uongofu wake. Mpaka siku moja palipotokea kutoelewana kati yake na Khalid ibn Waliyd, Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam akasema :

   من عادى عمارا، عاداه الله، ومن أبغض عمارا أبغضه الله"                   

Yeyote mwenye kumfanyia uadui ‘Ammaar basi  Allah atamfanyia  uadui na yeyote mwenye kumbughudhi ‘Ammaar basi  Allah atambughudhi.
Ilimbidi Khalid kwenda kumuomba radhi ‘Ammaar.
Mapenzi haya ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kwa ‘Ammaar hayakuja kwa bahati bali ni jinsi imani yake,uongofu wake , mateso aliyoyapata kwa ajili ya dini, mitihani aliyoipata ya kujaribiwa katika imani yake ni mambo yaliyoifanya itikadi yake kuwa thabiti isyo na shaka wa kutetereka. Uongofu huu alikuwa akiuusia Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kwa kusema :

" اقتدوا بالذين من بعدي أبي بكر وعمر... واهتدوا بهدي عمّار             

“Wafuateni baada yangu kina Abu Bakr na ‘Umar…. Na igeni uongofu wa ‘Ammaar”
Imani ya ‘Ammaar haikumalizika kwa kufariki kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam bali alikuiwa mstari wa mbele katika kupigana vita vya Jihadi na kuzidi kulitangaza kalima yake Allah Subahaahu Wata’ala kuwa juu. Alikuwa ni mwanajihadi shujaa, asiyeogopa wala kubadilisha msimamo.
Enzi za Ukhalifa wa ‘Umar Ibnul Khattaab aliteuliwa kuwa Amiri katika mji wa Kufa na ‘Abdullah ibn Masoud kuwa  waziri wake na mwalimu wa kuwafundisha waislamu dini yao. Wakati watu wakiteuliwa Maamiri huzidi kuwa na nguvu au kuzidiwa na kibri lakini kwa ’Ammaar ilikuwa kinyume chake kwani alikuwa dhalili mpaka watu wakashangazwa na Amiri walieletewa. Anasema Ibn Abu Huzayl ambae alikuwepo Kufa wakati ‘Ammaar ni Amiri:

        رأيت عمّار بن ياسر وهو أمير الكوفة يشتري من قثائها، ثم يربطها بحبل ويحملها فوق ظهره، ويمضي بها الى داره"..!                                                                                                             

Nilikuwa nikumuona ‘Ammaar bin Yaasir wakati akiwa Amir wa Kufa akinunua vitu vyake akivifunga kwa kamba na kisha kuibeba mgongoni mwake akielekea nyumbani kwake”
Hakuwa mtu mwenye mambo makubwa kwani hata siku moja alijiwa na mmoja katika wenye hadhi na jina katika mji wa Kufa ili kuomba jambo kwa Amiri na kutokana na nafasi yake alikuwa na hakika kwamba Amiri angelimkubalia. Hata hivyo ‘Ammaar alimkatalia na kukasirika mpaka kudiriki kumrushia shutuma na matusi Amiri kwa kumwambia:

                                                    :" يا أجدع الأذن

“Mtizame aliekatika sikio!”
Sikio moja la ‘Ammaar lilikuwa limekatika alipopigana vita vya Yamaamah ambavyo ushujaa wake ulikuwa ni changamoto ya kuweza kuwatia morali waislamu na hatimaye kushinda. Mpaka ilifikia kusimama wakati tayari ameshakatwa sikio na kusema kwa sauti ya ukali “Mnaikimbia pepo? Niangalieni mimi ni ‘Ammaar bin Yaasir nifuateni nifuateni”
Amiri hakukasirishwa na kauli ile bali alijibu tu kwa kusema:

                              خير أذنيّ سببت.. لقد أصيبت في سبيل الله

Umelitukana sikio langu lililo bora kwani lilikatwa (wakati nnapigana) kwa ajili ya Allah”
Uadilifu wa ‘Ammar ulikuja dhihirika zaidi wakati ilipokuja fitna kubwa katika Uislamu na huku tayari akiwa ni mzee wa miaka zaidi ya tisini. Naam mzee wa miaka tisini aliweza kuikamata na kuibeba bendera ya vita ambavyo viliwagawa waislamu wasijue nani aliye kwenye haki kati ya Sayyidna ‘Ali bin Abi Talib akiwa kama ni khalifa na Mu’awiyah ibn Abu Sufyaan. Siku hiyo alisimama na bendera na kusema :

" والذي نفسي بيده.. لقد قاتلت بهذه الراية مع رسول الله صلى الله عليه وسلم، وهأنذا أقاتل بها اليوم..



والذي نفسي بيده. لو هزمونا، لعلمت أننا على الحق، وأنهم على الباطل".                              .

Kwa Yule ambae nafsi yangu iko kwenye mikono yake Nilipigana kwa ajili ya bendera hii pamoja na Mtume Salla ‘Allahu ‘Alayhi Wasallam na hivi leo nnapigana tena kwa ajili ya bendera hii.
Kwa Yule ambae nafsi yangu iko kwenye mikono yake hata kama wakitushinda basi bado nnnajua kwamba sisi ndio tuliokuwa katika haki na wao wako kwenye batili.”
Hii ndiyo siku aliyopigana ‘Ammaar kwa ajili ya haki na watu kumfuata mpaka akauwawa shahidi kama walivyokufa mashahidi wazazi wake wawili ambao walisiimamia haki.
Mzee wa miaka zaidi ya tisini anauwawa shahidi katika kuisimamia haki ambayo ndiyo msimamo wa kila muislamu. Alizikwa katika eneo pamoja na mashahidi katika nguo zake alizozivaa huku Khalifa Ali bin Abi Talib akiuchukua mwili wake na kuuhifadhi huku Pepo ikiwa tayari ikimsubiri na kama alivyowahi kusimulia Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam katika moja ya hadithi zake kwamba pepo ilikuwa na hamu sana na ’Ammaar.