Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu)

Khalifa wa pili aliyeongoka

Jina na nasaba yake

Jina lake ni Umar bin Al Khatwaab bin Nufail bin Abdul Uzza bin Riyah bin Abdullah bin Qarat bin Razah bin Uday bin Kaab bin Luay bin Ghalib Al Qurashi Al Adawi, aliyekuwa pia akijulikana kwa jina la Abu Hafs.
Jina la mama yake ni Hantamah binti Hashim bin Al Mughiyrah bin Abdullah bin Umar bin Makhzum.
Imepokelewa kuwa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alisema;
"Nilizaliwa miaka minne kabla ya vita vikubwa vya Al Fujaar.", na vita hivi vilipiganwa kabla ya kupewa utume Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa miaka 30.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ananasibiana na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) upande wa baba katika babu yao wa saba, na upande wa mama wanakutana katika babu yao wa sita.

Wanawe na wakeze


Watoto wa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) walikuwa Abdullah na Abdul Rahman (mkubwa) na Hafsa, wote hawa alizaa na mkewe wa mwanzo Zeinab binti Madhaun bin Habib bin Wahab bin Hudhafa bin Jumah.
Alikuwa na binti mwengine Ruqayah aliyezaa na mkewe mwingine ambaye ni Ummu Kulthum binti wa Ali bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) na Bibi Fatima binti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
Na alikuwa pia na watoto wengine wawili Zeid na Ubeidullah, na mama yao alikuwa Ummu Kulthum binti Jarwal bin Malik, na wawili hao walipigana katika vita vya Siffin wakiwa upande wa Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Alikuwa pia na mtoto mwengine aliyempa jina la Asim pamoja  na Abdul Rahman (wa kati), na mama yao alikuwa Jamila binti Thabit na alikuwa na Abdul Rahman (mdogo)  na mama yake akiitwa 'Um Walad', na alikuwa pia na mtoto aliyempa jina la Fatima, na mama yake ni Hakim binti al Harith bin Hisham na alikuwa na binti mwengine aliyempa jina la Zeinab na huyu ni mdogo wa watoto wote wa Umar na mama yake ni Fakiha na alikuwa pia na Iyadh bin Umar na mama yake ni Atika binti Zeid bin Amr bin Nufeil.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alilibadilisha jina la mamake Asim aliyekuwa akiitwa 'Aasiya' na maana yake ni (mwenye kufanya maasi). Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamwambia;
"Hapana, bali wewe ni Jamila."

Umbo lake


Umar bin Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mrefu, unapomuona kwa mbali utadhani amepanda mnyama, na alikuwa na kipara sehemu ya mbele ya kichwa chake, na rangi ya ngozi yake ilikuwa nyekundu kupita kiasi, mwenye ndevu nyingi, na alikuwa mtumiaji wa mkono wa kushoto (mashoto) na alikuwa akitembea kwa haraka sana.

Maisha yake


Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliishi miaka 65. Miaka 30 katika ukafiri na miaka 35 katika Uislamu, na kabla ya kusilimu kwake alikuwa akifanya kazi ya kuchunga kondoo na ngamia wa baba yake Al Khatab bin Nofeil.
Mara baada ya kusilimu, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alibadilika akawa mmoja katika watu adhimu walioushangaza ulimwengu kwa kipaji cha uhodari wake, hekima ya hali ya juu, pamoja na elimu iliyochimbuka ghafla katika kifua chake.
Aliposhika ukhalifa aliweza kuziangusha dola kubwa za Kirumi na Fursi zilizokuwa na nguvu nyingi wakati ule, akaweza kuikomboa Baytul Maqdis na kuwafukuza Mayahudi nje ya bara ya Arabuni, na nchi nyingi moja baada ya nyingine zilikuwa zikisalimu amri mbele ya majeshi yake.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni katika watu wanaokushangaza kila unaposoma sira yake na kukufanya uihisi haiba yake na kujiona kama unaishi naye katika wakati wake, katika uadilifu wake, katika ushujaa wake, katika uaminifu wake, katika hekima aliyokuwa nayo na katika ukali wake. Ukali ulomfanya mwalimu wake na mwalimu wa ulimwengu Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aseme;
"Mkali wenu katika Uislam Umar bin Khatab".
Imam Ahmad na Ibni Hibban

Yupo mtumishi kuliko mimi?


Siku moja katika siku za joto kali sana Othman bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akichungulia dirishani pake, akamuona Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) anakwenda mbio nyuma ya ngamia aliyekata kamba, akamuuliza;
'Kuna nini ewe Umar?"
Akamwambia;
"Ngamia wa zaka amekata kamba."
Othman (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
"Umar, si ungetuma watumishi tu wamfuatilie?"
Umar akajibu:
"Kuna mtumishi kuliko mimi?"
Kuwa Khalifa wa Waislamu, kwake yeye maana yake ni kuwa mtumishi wa Waislam, kuwatumikia Waislamu, kuwahurumia Waislam, kulinda haki za Waislam, kuwalinda Waislam na kuulinda Uislam.

Kila mtu huko anakula chakula hiki?


Siku moja Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliletewa zawadi ya halwa nzuri sana kutoka kwa mmoja wa magavana wake katika nchi ya Azerbijan, akamuuliza mjumbe aliyepewa haluwa ile;
"Kwani kila mtu huko anakula chakula hiki?"
Mjumbe akajibu:
"La, sivyo ewe Khalifa wa Waislamu, hiki ni chakula cha watu wakubwa tu".
Umar akaghadhibika sana, akamuuliza;
"Yu wapi ngamia wako? Chukua chakula hiki umrudishie aliyekupa, kisha umwambie;
"Umar anakuamrisha; Usijishibishe chakula mpaka washibe kwanza Waislamu wote chakula hicho".

Waislamu wanazistahiki zaidi


Siku moja mkewe alitamani halwa, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
"Ziwapi pesa za kununulia halwa?"
Mkewe akamjibu;
"Mimi ninazo, nimeweza kudunduliza katika pesa zetu za chakula zinazozidi".
Umar akamwambia;
"Kama katika pesa zetu za chakula zipo zinazoweza kuzidi, basi wapo Waislamu wanaozistahikia, kwa hivyo nenda kazirudishe katika hazina ya Waislam."

Umehukumu ukafanya uadilifu ukaweza kulala


Siku moja aliwasili Madina mjumbe wa Kaisar mfalme wa Warumi aliyetumwa kuonana na Umar.
Akauliza;
"Yuko wapi Umar?"
Akaambiwa;
"Yule pale Umar aliyelala chini ya mti ule."
Akamtizama Umar aliyekuwa amelala chini ya mti, kisha akawatazama Waislam waliokuwa wakipita mbele yake bila kujali, kila mmoja anakwenda katika shughuli zake, akakumbuka alikotoka namna wafalme wao wanavyoishi ndani ya ngome zinazolindwa na maaskari kila mahala, Mrumi yule akatamka kauli yake maarufu akasema;
‘Umehukumu, ukafanya uadilifu, ukaweza kulala ewe Umar’.

Mwenyezi Mungu ametutukuza kwa Uislamu


Siku ile majeshi ya Kiislamu yalipoingia Palestina na kuuteka mji wa Jerusalem pamoja na msikiti wa Baytul Maqdis kutoka mikononi mwa manasara, maaskofu wa kanisa kuu walikataa kuzitoa funguo na kuwapa wafunguzi hao, wakataka ahudhurie Khalifa wa Waislamu mwenye sifa maalumu zilizoandikwa ndani ya vitabu vyao ili wamkabidhi funguo hizo.
Akafikishiwa habari hizo Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyefunga safari ndefu kutoka Madina hadi Palestina akifuatana na mtumishi wake. Ngamia wa mtumishi alikufa njiani akabaki ngamia mmoja waliyekuwa wakimpanda kwa zamu, mara mtumishi na mara anampanda Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na mara anakwenda bila kupandwa, na walipowasili Baytul Maqdis ilikuwa zamu ya mtumishi kupanda ngamia, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaingia akiwa anatembea kwa miguu wakati mtumishi wake yupo juu ya ngamia.
Wakuu wa majeshi ya Kiislam waliokuwepo Jerusalem walipomuona Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akiwasili akiwa katika hali ile, wakamzunguka na kumtaka yeye ampande ngamia huyo badala ya mtumishi wake, maana haitokuwa vizuri kuwakabili wakubwa wa manasara akiwa anatembea kwa miguu.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawaambia;
“Mwenyezi Mungu ametutukuza kwa Uislam, na iwapo tutautafuta utukufu kwengine na sio katika Uislam, basi Mwenyezi Mungu atatudhalilisha”.

Huyu ndiye Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyewashangaza waandishi wa historia na kuushangaza ulimwengu mzima kwa hekima na busara yake, uadilifu wake, ujasiri na ushujaa wake.
Huyu ndiye Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa akikesha wakati Waislam wamelala, aliyejinyima ili Waislam wapate, aliyebaki na njaa ili Waislam washibe, aliyejitolea maisha yake pamoja na maisha ya Masahaba wenzake (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa ni mhanga ili neno la Mwenyezi Mungu liwe juu na neno la wale waliokufuru liwe chini.

 

Mwenyezi Mungu utie nguvu Uislamu kwa kumsilimisha Umar bin Khatwaab


Wakati wa ujahilia (kabla ya Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuanza kuteremshiwa Wahyi) Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mpiganaji mieleka maarufu katika Soko la Ukadh, mahali walipokuwa wakikutana Waarabu kila mwaka kwa ajili ya kufanya biashara na kufanya michezo mbali mbali na mashindano ya mashairi na mengine.
Miongoni mwa mashindano hayo yalikuwa ni mieleka, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa bingwa wa kupigana mieleka. Alikuwa akitumia mkono wake wa kushoto na alikuwa 'akipiga anaumiza', kama walivyokuwa wakimsifia.
Alikuwa akijulikana kwa sifa zifuatazo:
'Akisema anasikilizwa, akitembea anakazana na akipiga anaumiza.'
Hakuwa akimuogopa mtu yeyote, na alikuwa anapoanzisha jambo hupenda kulikamilisha. Hapendi kufanya mambo nusu nusu kisha akaacha na kurukia mengine. Hakuwa akiyachukulia mambo kwa wepesi. Kila kitu alikuwa akikipa umuhimu wake, na yaliyomo moyoni mwake huyadhihirisha katika ulimi wake. Hajuwi kuficha wala kujificha.
Kwa sababu hizi ndiyo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamuomba Mwenyezi Mungu kwa kusema:
"Mwenyezi Mungu utie nguvu Uislamu kwa (kumsilimisha) Umar bin Khatab".
Al Hakim
Anasema Abdillahi bin Masaood (Radhiya Llaahu ‘anhu):
"Tuliendelea kuwa na nguvu tokea aliposilimu Umar. Kusilimu kwake kulikuwa ufunguzi, kuhama kwake (kwenda Madina) kulikuwa ushindi, na Ukhalifa wake ulikuwa huruma. Tulikuwa hatuwezi kusali panapo nyumba (ya Al Kaaba) mpaka aliposilimu Umar".

Namna Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alivyosilimu


Siku moja wakati wa adhuhuri Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) alitoka nyumbani kwake panga mkononi akielekea nyumba ya Al Arqam bin Abil Arqam, ambayo ndani yake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pamoja na Sahaba zake (Radhiya Llaahu ‘anhu) walikuwa wakikutana na kujifunza Qurani tukufu.
Alipokuwa njiani, Umar alikutana na mtu aitwaye Naeem bin Abdullah, aliyemuuliza;
"Unaelekea wapi ewe Umar?"
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
"Nakwenda kwa huyu anayewabadilisha watu na kuwatenganisha Makureshi na kuitukana dini yao pamoja na miungu yao. Nakwenda kumuua".
Yule mtu akamwambia;
"Uelekeaji mbaya unaoelekea na mwendo mbaya unaokwenda".
Umar akadhani kuwa huyu naye keshasilimu, akamuuliza;
"Isiwe na wewe washakubadilisha? Ikiwa ni hivyo basi bora nikuanze wewe".
Kwa uwoga mkubwa yule mtu akamwambia;
"Umar, Jua ya kuwa dada yako keshasilimu pamoja na mumewe Said bin Zeyd na wamekwisha iacha dini yako".
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akageuza njia na kuelekea nyumbani kwa dada yake Fatima bint Al Khatab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa wakati huo yuko pamoja na mumewe na Sahaba mwengine aitwae Khabbab bin Al Arat (Radhiyallahu anhum), na wote walikuwa wakisoma na kuidurusu Qurani tukufu.
Alipowasili aligonga mlango kwa kishindo kikubwa.
"Nani?"
"Mimi Umar!"
Khabbab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliruka na kujificha chini ya kitanda huku akimuomba Mwenyezi Mungu amsalimishe. Ama Fatima dada yake Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), yeye aliwahi kuzificha kwa kuzishindilia kifuani pake zile karatasi zilizoandikwa Qurani tukufu.
Wakamfungulia mlango na kumkaribisha huku nyuso zao zikionesha dalili ya uoga.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawauliza;
"Ni yepi haya maneno niliyoyasikia mkiyasoma nilipokuwa nje kabla ya kuingia humu?"
Wakajibu ;
"Si kitu ni mazungumzo na hadithi tu."
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Nasikia nanyi pia mumebadilisha dini yenu?"
Said (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu;
"Umar! unaonaje ikiwa ukweli upo katika dini nyingine….?"
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakumuacha amalize maneno yake, akamrukia kwa nguvu za ajabu na kumwangusha chini kwa kishindo kisha akamkalia juu ya kifua chake, na dada yake alipojaribu kuja kumsaidia mumewe alipigwa kofi la nguvu usoni na damu zikaanza kumtoka, jambo lililomfanya apige ukelele mfano wa baragumu au radi huku akimkabili Umar na kumwambia:
"Ewe adui wa Mwenyezi Mungu! Unanipiga kwa sababu nimemuamini Mwenyezi Mungu mmoja? Basi fanya utakavyo mimi natamka;
"Ash hadu an laa ilaaha illa Llah wa anna Muhammadan Rasuulu Llah".
Ndani ya sauti kali na ushupavu wa dada yake, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaiona nuru ya Uislamu. Hajapata hata siku moja kumsikia dada yake akimkabili na kumjibu, kwani Fatima alikuwa akimuogopa sana Umar,  lakini leo dada yake huyu anamnyanyulia sauti na kumjibu kwa ukali na kwa ushupavu bila uoga? Bila shaka pana jambo tukufu sana lililombadilisha na kumgeuza na kuuingiza ushujaa ule moyoni mwake.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuwa akipenda kuzitumia nguvu zake kwa ajili ya inda tu, bali alikuwa  mtu anayependa kuyaweka mambo sawa. Hapo mwanzo alidhani kuwa dada yake anapotea, akataka kumuongoza katika haki,  lakini alipogundua kuwa dada yake yupo katika haki, na yeye ndiye aliyepotea, akaikubali haki na kuifuata.
Akainuka kutoka juu ya kifua cha Said (Radhiya Llaahu ‘anhu), na alipoziona zile karatasi alozificha dada yake kifuani pake zikijitokeza, akamwambia;
"Nipe hizo karatasi."
Dada yake akamwambia;
"Sikupi kwani hawazigusi hizi isipokuwa waliotahirikia. Nenda kaoge kwanza ili ujitahirishe."
Umar(Radhiya Llaahu ‘anhu) akenda kuoga kisha akarudi haraka huku ndevu zake zikiwa bado zinatiririka maji, akazichukua karatasi zile kutoka kwa dada yake na kuanza kuzisoma, na ndani yake ilikuwa imeandikwa Surat Twaha - kuanzia aya ya mwanzo hadi ya kumi na sita:

"TWAHA! .
Hatukukuteremshia Qur'ani ili upate mashaka.
Bali ni mawaidha kwa wenye kunyenyekea.
Materemsho yatokayo kwa aliye umba ardhi na mbingu zilizo juu.
Arrahmani, Mwingi wa Rehema, aliyetawala juu ya Kiti cha Enzi.
Ni vyake vyote vilivyomo mbinguni na vilivyomo katika ardhi, na vilivyomo baina yao, na vilivyomo chini ya ardhi.
Na ukinyanyua sauti kwa kusema...basi hakika Yeye anajua siri na duni kuliko siri.
Mwenyezi Mungu! Hapana Mungu isipokuwa Yeye.
Yeye ana majina mazuri kabisa.
Na jee! Imekufikia hadithi ya Musa?
Alipouona moto, akawaambia watu wake: Ngojeni! Mimi nimeuona moto, huenda nikakuleteeni kijinga kutoka huo moto, au nikapata uongofu kwenye moto.
Basi alipoufikia akaitwa: Ewe Musa!
Hakika Mimi ndiye Mola wako Mlezi! Basi vua viatu vyako.
Kwani upo katika bonde takatifu la T'uwa.
Nami nimekuteua wewe; basi sikiliza unayo funuliwa.
Hakika Mimi ndiye Mwenyezi Mungu. Hapana Mungu ila Mimi tu.
Basi niabudu Mimi, na ushike Sala kwa ajili ya kunikumbuka Mimi.
Hakika Saa itakuja bila ya shaka. Nimekaribia kuificha, ili kila nafsi ilipwe kwa iliyoyafanya.
Basi wasikuzuwie na (kuyaamini) hayo wale wasio yaamini na wafuatao matamanio ya nafsi zao.Usije ukaangamia."

Kwa moyo mkunjufu, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akazikumbatia karatasi hizo na kuzibusu huku akisema;
"Haipaswi kwa mwenye aya kama hizi kuwa na mshirika anayeabudiwa pamoja naye, - Nipelekeni kwa Muhammad!".
Hapo ndipo Khabbab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa amejificha chini ya kitanda alipojitokeza na kusema;
"Bishara njema ewe Umar, Wallahi Mwenyezi Mungu ameikubali dua ya Mtume wake".
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akatoka na kuelekea nyumba ya Al Arqam (Radhiya Llaahu ‘anhu) iliyopo karibu na mlima Safaa, na Hamza (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomuona Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akija na uso mkunjufu, akasema;
"Huyo anakuja, iwapo Mwenyezi Mungu anamtakia kheri basi atasilimu, ama iwapo hamtakii hivyo, basi kifo chake kitakuwa mikononi mwetu leo".
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akatoka na kumuendea Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), akamkabili kwa kumshika na kumkunjakunja nguo zake pamoja na ala ya panga yake huku akimwambia;
"Hivyo utangoja ewe Umar mpaka Mwenyezi Mungu atakapoteremsha aya juu yako zikikulani kama alivyoteremshiwa Al Walid bin Mughiyra? - Mola wangu, huyu Umar bin Khatab! Mwenyezi Mungu ipe nguvu dini kwa kumuingiza Umar katika dini yako"
Hapo ndipo Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliposilimu na kuzitamka shahada mbili;
"Ash- hadu an Laa ilaaha illa Llah wa ash - hadu annaka Rasulu llah."
Alisilimu akiwa na umri wa miaka ishirini na sita na wakati huo walikuwa wamekwisha kusilimu watu thelathini na tisa na yeye akawa wa arubaini kusilimu.
Kwa kauli hii, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alibadilika na kutoka katika ushirikina wa kuabudu masanamu na kuingia katika ibada ya Mwenyezi Mungu mmoja asiye na mshirika, na kutoka katika uadui mkubwa dhidi ya Uislamu na kugeuka kuwa mlinzi mkubwa wa Uislamu, na kutoka katika nguvu na ushujaa usio na mwongozo na kuingia katika nguvu na ushujaa ulio na mwongozo wenye nuru inayoongozwa na kitabu kinachon'gara, kitabu cha Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala.
Ushujaa na nguvu zake alizokuwa akizitumia dhidi ya Uislamu akavigeuza na kuvitumia katika kuulinda na kuuendeleza mbele Uislamu.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa na tabia ya kuipenda haki na kuitetea mara anapoiona na kuijua, na mara baada ya kusilimu kwake alimwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kumuuliza;
"Sisi si tuko katika haki katika kuishi kwetu na kufa kwetu ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamjibu:
"Ndiyo ewe Umar. Naapa kwa Yule ambaye nafsi zetu zimo mikononi mwake, nyinyi mumo katika haki katika maisha yenu na katika kufa kwenu".
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema:
"Kwa nini basi tunajificha? Naapa kwa Yule aliyekuleta kwa haki, utoke, na sisi tutoke pamoja na wewe."
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akakubali kutoka pamoja na Waislamu, wakawa wanatembea katika barabara za Makkah mistari miwili, msitari mmoja ukiongozwa na Umar na mwengine ukiongozwa na Hamza (Radhiya llahu anhum)
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa hastarehe bila ya kukamilisha kile alichokianzisha, akaapa akisema:
"Wallahi kila mahali nilipokaa nikiutetea ukafiri lazima nikakae tena kuutetea Uislamu".
Akafanya kama alivyokula kiapo, kisha akamwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kumwambia:
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, nini kinachotufunga ndani tu? Wallahi mimi nishakwenda kila mahali nilipokuwa nikikaa kuutetea ukafiri na badala yake nikawa nautetea Uislamu bila ya kuwaogopa, na kutoka sasa ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu tusimwabudu tena Mwenyezi Mungu kwa kificho".
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akalikubali pendekezo lake.

Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye anatamani apigwe kama ndugu zake


Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa mtu wa ajabu sana alikuwa akiona uchungu kila anapowaona Waislamu wenzake wakipigwa wakati yeye hapana anayethubutu kumsogelea. Akaamua kumuendea Abu Jahal nyumbani kwake na kumgongea mlango. Alipoufungua na kumuona Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) amesimama mbele yake akamwambia;
"Wewe!?" Kisha akaufunga mlango mbele ya uso wake.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaondoka na kuziendea nyumba nyingine za washirikina, akawa anawagongea milango moja baada ya nyingine, lakini hapana aliyethubutu kumtokea.
Akaamua kuwaendea panapo Al Kaaba mahali wanapokusanyika, huku akijua kuwa itakuwa vigumu kwao kumuacha atambe mahali hapo, na itawabidi wapigane nae.
Hebu tumsikilize Umar mwenyewe akituhadithia yaliyomkuta siku hiyo. Anasema Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu):
"Watu wakaanza kunizunguka na kupigana na mimi, wakawa wananipiga na mimi nawapiga, mpaka alipokuja mjomba wangu na kusimama panapo Hijr Ismail na kusema:
'Umar mtoto wa dada yangu yumo ndani ya himaya yangu,'
Kwa kauli yake hiyo watu wakaacha kunipiga, lakini nilipowatazama ndugu zangu na kuwaona wakiendelea kupigwa wakati mimi hapana anayethubutu kunigusa, nikamwendea mjomba wangu na kumwambia:
"Himaya yako nakurudishia mwenyewe"
Akaniambia:
"Usifanye hivyo ewe mwana wa dada yangu"
Nikamwambia:
"Bali nairudisha fanya utakavyofanya "
Nikawa naendelea kupambana nao mpaka Mwenyezi Mungu alipotutukuza kwa Uislamu".

Anasema Khalid Muhammad Khaled katika kitabu chake kiitwacho 'Khulafaa Rasuul':
"Mwanamume aliyefanya yote haya mara tu baada ya kusilimu kwake, tutakutana naye tena akiwa Khalifa wa Waislamu, huku majeshi yake yakibomoa makasri ya Kisra, mfalme wa Wafursi na Kaisar mfalme wa Warumi, lakini juu ya ushindi mkubwa aliokuwa akiupata pamoja na nguvu zake zote hizo, mtu huyu huyu tutamuona akipanda juu ya membari baada ya kuwaita Waislamu ili akutane nao, kisha anawambia:
"Enyi watu, mimi kazi yangu ilikuwa kuchunga kondoo wa shangazi zangu katika kabila la Bani Makhzum na malipo yangu yalikuwa gao la tende au zabibu", na baada ya kusema maneno  hayo anateremka akiwa amewashangaza watu, na Abdurahman bin Auf (Radhiya Llaahu ‘anhu) anapotangulia na kumuuliza:
"Kwa nini ukafanya hivyo ewe Amiri wa Waumini?"
Akajibu:
"Ole wako ewe mwana wa Auf, nilikaa peke yangu nikitafakari na  kujiuliza;
'Wewe ndiyo ushakuwa Khalifa wa Waislamu, na hapana aliye juu yako isipokuwa Mwenyezi Mungu, NANI ALIYE BORA KULIKO WEWE? Nikaona bora  niijulishe nafsi yangu kadiri yake (nikivunje kiburi changu)".

Hijra yake


Anasema Sayiduna Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Wote waliohama kutoka Makka kwenda Madina walihama kwa kificho isipokuwa Umar bin Khatab. Yeye alipotaka kuhama aliuvaa upanga wake kiunoni na kubeba ngao yake, akachukua mikuki mkononi mwake kisha akenda moja kwa moja mpaka mbele ya Al Kaaba mahali wanapojikusanya washirikina, akatufu mara saba mbele yao kisha akaelekea Maqamu Ibrahim na kusali rakaa mbili, kisha akaanza kuyaendea makundi yaliyojikusanya hapo moja baada ya moja huku akiwaambia;
‘Zimedhalilika nyuso zenu. Yeyote kati yenu anayetaka mamake amkose na wanawe wawe mayatima na mkewe awe kizuka, basi na akutane nami nyuma ya bonde hili”.
Anasema Sayiduna Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Hapana hata mmoja aliyethubutu kumfuata isipokuwa wanyonge wachache waliokuwa wakionewa, hao ndio waliomfuata. Akawafundisha na kuwaongoza kisha akaendela na safari yake”.
Alipowasili Madina, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokelewa na wenzake waliotangulia kabla yake nao ni Masa ab bin Umair na Ibni Ummi Maktoum (R Anhum) na wengine.
Waislam waliobaki Makkah wakaendelea kuhamia Madina makundi kwa makundi na hatimaye akahamia Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na dola ya Kiislam ikaanzishwa hapo Madina chini ya misingi iliyo thabit na yenye nguvu. Mapambano mengi yakatokea na vita vingi baina ya nuru ya haki na viza vya batil.

 Baadhi ya nishani alizopewa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)


Zifuatazo ni baadhi tu ya sifa nzuri nzuri alizopewa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na Mtume Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) zilizonukuliwa kutoka katika hadithi sahihi:

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema;
"Mwenyezi Mungu ameijaalia haki katika ulimi wa Umar na katika moyo wake. Miongoni mwa waliokuja kabla yenu walikuwepo watu wenye kufunuliwa bila ya wao kuwa mitume. Ikiwa katika umma wangu wapo wenye mfano wao, basi huyo atakuwa Umar".
Bukhari- Muslim na Attarmidhiy

Na akasema;
"Niliota nimo Peponi, nikamwona mwanamke anatawadha karibu na kasri, nikauliza ;
'Kasri ya nani hii?'
Nikajibiwa;
'Kasri ya Umar'
Nilipokumbuka wivu wa Umar nikarudi haraka kule kule nilikotoka."
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliposikia maneno hayo, alilia sana na kusema;
"Nikuonee wivu wewe ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?"
Bukhari na Muslim

Na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema;
"Nilipokuwa nimelala nikaota nimeletewa mbele yangu watu wakiwa wamevaa kanzu, wamo miongoni mwao waliovaa kanzu (fupi) zinazowafika vifuani pao, wengine (fupi) juu zaidi kuliko hapo, kisha nikaletewa Umar akiwa amevaa kanzu inayoburura"
Akaulizwa ;
"Nini tafsiri ya ndoto hiyo ?"
Akajibu;
"Dini"
Bukhari na Muslim

Na akasema;
"Nilipokuwa nimelala niliota nimeletewa birika la maziwa, nikanywa na kumpa Umar yaliyobaki".
Akaulizwa :
"Nini tafsiri yake?"
Akajibu;
"Elimu"
Bukhari

Myahudi mmoja anayeitwa Zeyd bin Sana alitaka kusilimu, na hii ni baada ya kuzijua alama zote za Utume alizokuwa nazo Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) isipokuwa mbili, nazo ni ‘Upole wake’ na ‘Ustahamilivu wake’.Akataka kujihakikishia juu ya alama mbili hizo.
Tumwache Zeyd mwenyewe atuhadithie;
"Nilipoipata fursa nilimwendea Mtume alipokuwa akenda mazikoni pamoja na sahaba zake na kumkunja nguo zake huku nikimkunjia uso wangu na kumwambia;
"Wallahi sikujua kama nyinyi wana wa Abdul Muttalib mnachelewesha kulipa madeni ya watu namna hii."
'Umar akawa ananitazama huku macho yake yanamzunguka kama nyota, akaniambia';
"Wewe adui wa Mwenyezi Mungu, unamwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu haya ninayosikia  na kutenda haya ninayoyaona?  Wallahi ingekuwa siilindi heshima yake, basi ningeikata shingo yako kwa panga langu".
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akawa anamwangalia Umar kwa utulivu uliojaa mapenzi, kisha akatabasam na kusema;
"Mimi na huyu mtu tunahitajia yaliyo bora kuliko hayo ewe Umar, ilikuwa uninasihi mimi niwe mlipaji mzuri wa deni lake na umnasihi yeye adai kwa njia bora kuliko hii. Nenda ewe Umar kamlipe deni lake na mwongezee pishi ishirini za tende".
Zeyd akasilimu.
Al Hakim

Siku moja baada ya kugonga mlango na kupewa idhini ya kuingia nyumbani kwa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam), Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaingia na kumkuta Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akicheka.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
"Mwenyezi Mungu akujaalie uwe na furaha siku zote ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu."
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamwambia:
"Nimeshangazwa na hawa wanawake waliokuwa pamoja nami, walikuwa wakizungumza, na mara ulipoingia wakanyamaza na kujifunika gubi gubi (kwa kukuogopa)".
Umar(Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
"Wewe ndiye unayestahiki wakuogope zaidi ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu".
Kisha akawageukia wale wanawake na kuwaambia;
"Enyi maadui wa nafsi zenu, mnaniogopa mimi na hamumwogopi Mtume wa Mwenyezi Mungu?"
Wakamwambia;
"Ndiyo! Wewe ni mkali kuliko Mtume wa Mwenyezi Mungu".
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema;
"Eeh! Mwana wa L Khataab we, naapa kwa Yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake; Lau kama shetani atakuona unatembea katika njia yake, basi atageuza njia na kukukimbia".
Bukhari – Muslim - Ahmad

Utamwambia nini kesho Mola wako ewe Umar?


Anasema Dr. Khaled Mohd Khaled;
“Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) angelikuwa mtu mwenye ghururi basi ingejitokeza ghururi hiyo mara baada ya kusilimu kwake au baada ya kuwa Khalifa wa Waislamu, maana mara tu baada ya kusilimu kwake, Uislamu ulipata nguvu, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alielewa vizuri kiasi gani Waislamu walivyokuwa wanyonge na wenye kuogopa kabla ya hapo, alikuwa akiona namna walivyoanza kupata nguvu mara tu baada ya kusilimu kwake, wakawa wanasali panapo Al Kaaba bila uwoga. Na alikuwa akiona pia namna walivyokuwa wakitembea na kupiga kelele za Takbir katika mji wa Makka bila ya uwoga.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akimsikiliza rai zake, na mara nyingi akimkubalia, bali mara nyingine Mwenyezi Mungu huteremsha aya zinazounga mkono rai zake.
Kwa mfano katika hadithi iliyosimuliwa na Bukhari na Muslim, anasema Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Mwenyezi Mungu amenikubalia mara matatu;
Niliposema ‘Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu ungefanya mahali alipokuwa akisimama Ibrahim pawe panasaliwa; Ikateremshwa aya;
“Na mahali alipokuwa akisimama Ibrahim pafanyeni pawe pa kusalia”.
Al Baqarah – 125
Na aya ya Hijabu, nilimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam); ‘Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ungeliwaamrisha wakezo wajifunike, kwa sababu miongoni mwa wanaozungumza nao wamo wema na wamo waovu’. Ikateremshwa aya ya Hijabu;
“Nanyi mnapowauliza (wakeze) waulizeni nyuma ya pazia. Kufanya haya kutasafisha nyoyo zenu na nyoyo zao.”
Al Ahzab – 53
Na pale wake wa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) waliposhirikiana kwa wivu wao dhidi ya Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam), Nikawaambia (akiwemo Bi Hafsa(Radhiya Llaahu ‘anhu) – mwanawe ambaye pia ni mke wa Mtume(Swalla Llahu alayhi wa sallam)),  ‘Akikupeni talaka, Mola wake atampa badala yenu wake wengine walio bora kuliko nyinyi’; Ikateremshwa aya;
“(Mtume) akikupeni talaka, Mola wake atampa badala yenu wake wengine walio bora kuliko nyinyi; wanaofuata nguzo za Imani, watii, watubiao wanapokosa, wafanyao ibada, wafanyao mambo mengi ya kheri, waliopata kuolewa na wasiopata kuolewa.’
At Tahriym – 5
Bukhari na Muslim
Na baada ya kufariki Abubakar Al Siddiq (Radhiya Llaahu ‘anhu), Khalifa wa mwanzo wa Waislamu, akapewa ukhalifa Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyejaaliwa kupata ushindi mkubwa dhidi ya maadui wa Mwenyezi Mungu.
Yote haya yanaweza kumfanya mtu wa kawaida awe na kiburi pamoja na majivuno, lakini Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akijulikana kwa kutojivuna kwake hata baada kupata mafanikio yote hayo.

Juu ya nguvu na ushujaa na ukali wake, Umar alikuwa mtu ambaye ukitaka kumtisha umwambie:
"Utasema nini kwa Mola wako kesho Ewe Umar."
Utamwona anavyolia kama mtoto mdogo.”

Sidai wala sidaiwi


Siku moja Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu), alimuuliza Abu Musa Al Ash- ariy (Radhiya Llaahu ‘anhu) :
"Ewe Aba Musa, utafurahi  ikiwa kule kusilimu kwetu pamoja na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kuhama kwetu pamoja naye, na shahada yetu pamoja na matendo yetu mema, vyote turudishiwe wenyewe na badala yake tufutiwe dhambi zetu tuwe hatudai wala hatudaiwi?"
 Abi Musa AL Ash ary (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu:
"La Wallahi, ewe Umar, kwani sisi tumepigana Jihadi, tukasali, tukafunga, tumefanya mema mengi na wamesilimu mikononi mwetu watu wengi kwa hivyo sisi tunategemea thawabu za amali hizo."
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu huku machozi yakimlenga:
"Ama mimi naapa kwa yule ambaye nafsi yangu ipo mikononi mwake, natamani nirudishiwe yote hayo, kisha nisalimike nisidai wala nisidaiwe".

Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) mara nyingi alinukuliwa akisema;
‘Iwapo nitaambiwa kuwa watu wote wataingia Peponi isipokuwa mtu mmoja tu, basi ningeogopa mtu huyo asiwe mimi’.
Haya ni mafundisho aliyoyapata kutoka kwa mwalimu wake na mwalimu wa ulimwengu mzima, Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam), kwani siku moja Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) alipomuona akisali mpaka miguu yake ikivimba alimuuliza:
"Kwa nini unafanya yote hayo wakati wewe umeshasamehewa madhambi yako yote yaliyotangulia na yanayokuja?"
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamjibu:
"Basi nisiwe mja mwenye kushukuru?"

Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akijinyima vyakula vizuri akiogopa siku ya Kiama asije akaambiwa kuwa amekwishajifurahisha navyo hapa duniani.
Imepokelewa kuwa siku moja Hafs bin Abil Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuja kumtembelea Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamkuta anakula, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamkaribisha, lakini Hafs (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipouona mkate mkavu alokuwa akila Umar huku akichovya ndani ya mafuta, akakataa kulipa taabu tumbo lake, akamshukuru Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) lakini hakukikaribia chakula hicho.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
“Kwa nini hutaki kula na mimi?”
Hafs (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Chakula unachokula ni kikavu na kigumu wakati mimi sasa hivi nitarudi nyumbani na kula chakula laini nilichokwishatayarishiwa.”
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia:
“Unadhani mimi nashindwa kuamrisha nikachinjiwa kijibuzi kidogo kikachunwa ngozi yake kisha nikaamrisha iletwe ngano nyepesi nipate kupikiwa mikate laini, kisha niamrishe ziletwe zabibu zitupwe juu ya samli inayokaangiwa nyama hiyo, kisha yamiminwe maji juu yake mpaka yageuke rangi yake na kuwa nyekundu mfano wa damu ya paa, kisha nikala hii (mikate na nyama) na kunywa ile (supu)?”
Hafs (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu:
“Wewe ni mjuzi wa vyakula vizuri ewe Amiri wa Waumini”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaendelea;
“Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mikononi mwake; Ingelikuwa siogopi kupunguza thawabu zangu, ningekula kama mnavyokula nyinyi, na kama ningetaka ningeishi maisha bora kuliko mnayoishi, lakini kila nikiikumbuka Siku ambayo kila anayenyonesha atamsahau anayemnyonesha na kila mwenye mimba ataizaa mimba yake, nikaamua kuvibakiza vizuri vyangu mpaka siku hiyo, kwani nimemsikia Mwenyezi Mungu akisema;
“Mlipoteza vitu vyenu vizuri katika maisha yenu ya dunia (basi hamtavipata leo hapa) nyinyi mlijifurahisha navyo (huko)..”
Al Ahqaf – 20
Juu ya kuwa si haramu kula vyakula vizuri, lakini huyu ni Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye hata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alisema juu yake;
"Mkali katika dini ya Mwenyezi Mungu kupita wote ni Umar."
Attirmidhy - Ibni Majah na wengine

 Ukhalifa


Katika tukio la Saqifa, siku aliyofariki Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikaribia kuwa Khalifa wa Waislamu wakati Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipomwambia;
“Lete mkono wako tufungamane nawe ewe Umar”.
Lakini Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa akauvuta mkono wake nyuma kwa nguvu na kusema;
“Bali wewe ndiye tutakayefungamana naye, kwani wewe ni bora kuliko mimi, haiwezekani mimi kuwa Khalifa wa watu, Abubakar akiwa ndani yao.’
Abubakar(Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Wewe una nguvu kuliko mimi ewe Umar”
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu;
“Ama Nguvu zangu ziko chini ya amri yako kwa ajili ya ubora wako”.
Akaunyanyua mkono wa Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kufungamana naye na Waislam wote mmoja baada ya mwengine wakafungamana naye mahali hapo. Lakini Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokuwa akifariki dunia, alimchaguwa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) awe Khalifa wa Waislamu baada yake, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akakubali kwa sababu Waislamu walikuwa na haja ya uongozi wa mtu wa nguvu zake na hekima yake.

Mali hiyo si ya Umar wala si ya watu wa nyumba ya Umar


Siku moja uliwasili Madina msafara uliopitia nchi mbali mbali, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawauliza watu wa msafara huo juu ya yale waliyokumbana nayo na kuyasikia wakiwa njiani, wakamwambia;
“Ama katika mji fulani watu wanakuogopa sana kwa ukali wako, na katika mji mwingine tumewaona watu wakikusanya mali nyingi na kujitayarisha kuja hapa kukuletea, lakini katika mji fulani tumewaona watu wacha Mungu wanakuombea dua wakisema ;
“Mola wetu tunakuomba umghufirie Umar madhambi yake na umnyanyue daraja yake”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Ama wale wanaoniogopa, ingelikuwa wananitakia kheri basi wasingeniogopa, na mali hiyo inayokusanywa si ya Umar wala si ya watu wa nyumba ya Umar, bali ya baitul maal ya Waislamu, na mimi sina chochote ndani yake, ama wale mlowasikia wakiniombea dua bila mwenyewe kuwajua, hayo ndiyo ninayotarajia".
Alikuwa anapomuona mtoto mdogo njiani humshika na kumwambia;
‘Niombee dua kwa Mwenyezi Mungu, kwani wewe ni mdogo na bado huna dhambi, na dua yako inakubaliwa’.

Kifo cha mnafiki


Abdullahi bin Ubey bin Salul, alikuwa kiongozi wa wanafiki pale Madina, na aya nyingi ziliteremshwa kuwajulisha Waislamu juu ya unafiki wake. Lakini Abdillahi huyu alikuwa na mwanawe aitwae Abdillahi bin Abdillahi bin Ubey bin Salul (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliyekuwa kipenzi cha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), kinyume na babake.
Hebu tumsikilize Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) akituhadithia namna ilivyokuwa siku aliyofariki mnafiki huyo;
‘Alipokufa Abdullahi bin Ubey, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliwaita watu waje kumsalia na yeye alisimama mbele yetu, na alipotaka kuanza kumsalia nikasimama mbele yake na kumwambia;
‘Unamsalia adui wa Mwenyezi Mungu?' Nikawa namkumbusha kila ubaya aliomtendea, huku Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akitabasamu. Na aliponiona nazidi kusema, akaniambia;
‘Nipishe ewe Umar, mimi nimehiyarishwa na nikachagua, Mwenyezi Mungu ameniambia;
‘Ewe Mtume! Waombee msamaha (hao wanafiki) au usiwaombee; (yote sawa sawa) Hata ukiwaombea msamaha mara sabini, Mwenyezi Mungu hatawasamehe.’
At Tawba –80
Na kama nikijua kuwa nikiongeza zaidi ya mara sabini atasamehewa, basi ningeongeza".
Kisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamsalia na akalifuata jeneza lake na kusimama kaburini pake.
‘Nikashangazwa kwa kumwendea kwangu Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), lakini Wallahi haujapita muda ikateremka aya ifuatayo;
‘Wala usimsalie kamwe mmoja wao yoyote yule akifa, wala usisimame kaburini kwake (kumuombea dua).’
At Tawba -84
Hii ndiyo tabia ya Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), ambaye anapohisi pana makosa hujaribu kuyasahihisha, lakini Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) mwingi wa huruma alimhurumia Abdillahi bin Ubay akamsalia na kumwombea dua huenda Mola wake akamsamehe. Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alijaribu kusema, lakini alinyamaza akatii na kusali nyuma yake baada ya Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kushikilia kuwa lazima amsalie.

Mwaka wa Ramada


Siku moja katika mwaka wa Ramada, mwaka maarufu wa ukame na njaa kali iliyouwa watu wengi pale Madina, waliletwa ngamia kutoka nchi ya Sham, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaamrisha wachinjwe na kugawiwa nyama yake.
Baada ya kumaliza kusimamia uchinjaji na ugawaji wa nyama hiyo, na kurudi nyumbani kwake, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaletewa na mtumishi wake vipande vizuri vya nyama vilivyochaguliwa kwa ajili yake.
Umar akauliza;
‘Imetokea wapi nyama hii?’
Akaambiwa;
‘Katika wanyama waliochinjwa’
Akasema, huku akiisogeza upande nyama hiyo;
‘Ole wangu! Nitakuwa amiri gani mimi ikiwa nitakula vipande vizuri vya nyama vilivyochaguliwa na kuwaachia watu kula mabaki yake?’
Akamwita mtumishi wake Aslam na kumwambia;
‘Ewe Aslam, ondoa chakula hiki na uniletee mkate wangu na mafuta ya kutolea’.
Baada ya juhudi kubwa aliyoifanya ya kusimamia uchinjaji na ugawaji wa nyama siku ile, Umar alistahiki kula vipande vizuri vya nyama ile, lakini yeye hakuona hivyo, bali aliona kuwa Waislam ndio wenye kustahiki.

 

Alikuwa mkali zaidi kwa watu wa nyumba yake


Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mkali zaidi kwa watu wa nyumba yake kuliko kwa wengine kwa kuhofia watu wasije wakasema kuwa Umar anawapendelea jamaa zake.
Alikuwa anapoweka kanuni mpya akiwakusanya watu wake wa nyumbani na jamaa zake na kuwaambia;
‘Mimi nimewakataza watu kufanya hivi au vile, na watu wanakutazameni mfano wa ndege wanavyoitazama nyama. Mkianguka na wao wanaanguka na mkinyanyuka wananyanyuka. Na mimi Wallahi nikiambiwa kuwa mmoja wenu ametenda katika yale niliyoyakataza, basi nitamtia adabu mara mbili zaidi kuliko watu wengine. Kwa hivyo atakaye na afanye na atakaye na aache.”
Kwa hivyo kuwa jamaa yake Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakukuwa na maana kuwa mtu anaweza kufanya atakalo kisha akasalimika, bali kinyume cha hivyo Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akiwanyima jamaa zake baadhi ya haki wanazopata watu wengine kama ilivyokuwa katika kisa cha Abdillahi bin Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa akijulikana kwa ucha Mungu wake.
Siku moja Umar(Radhiya Llaahu ‘anhu), alipokuwa akitembea akaona ngamia wanene, waliohitilafiana na wengine kwa uzuri wao.
Akauliza;
‘Ngamia wa nani hawa?”
Akaambiwa;
‘Ngamia wa Abdillahi bin Umar’.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alitetemeka huku akishangaa, akasema;
‘Ole wako ewe mwana wa Amiri wa Waislamu’.
Akatuma watu wamwitie Abdillahi (Radhiya Llaahu ‘anhu), na alipowasili akamwambia;
‘Vipi ngamia hawa ewe Abdillahi’
Mwanawe akajibu;
‘Hawa ni ngamia wangu, nimewanunua kwa pesa zangu mwenyewe na kuwapeleka malishoni ili wanenepe na ili nipate kuwauza kama wanavyofanya biashara Waislam wengine’.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu kwa ukali;
‘Ndiyo! Na watu watasema ngamia hawa wa mtoto wa Amiri wa Waislamu kwa hivyo wachungeni vizuri na walisheni majani mazuri, na kwa njia hii ngamia wako watanenepa na ngamia wa wenzio watakonda, na wewe utapata faida kubwa kuliko wenzio’.
Kisha akasema;
‘Abdullahi, chukua ngamia wako nenda kawauze na uchukuwe rasilmali yako tu uliyonunulia ngamia hawa na pesa zilizobaki zirudishe katika Baytul mal ya Waislam’.
Huyu ndiye Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa akimuogopa Mwenyezi Mungu asije akamhesabia siku ya Kiama kuwa aliwapendelea wanawe au jamaa zake na kwamba walikuwa wakiitumilia fursa ile kwa kujineemesha wakati wenzao hawakuwa wakiipata fursa kama ile.

Huyu ndiye Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye siku moja alipokuwa akipokea mali kutoka katika miji mbali mbali ya Kiislamu, binti yake Hafsa (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimtania kwa kumwambia;
‘Usitusahau watu wako, maana Mwenyezi Mungu ameusia juu ya nasaba’.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
‘Mwanangu, haki ya nasaba katika mali yangu, ama hii ni mali ya Waislamu, inuka nenda nyumbani kwako’.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alijifunza haya kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), aliyemuona mara nyingi akimwambia kipenzi chake, Fatima l Batool (Radhiya Llaahu ‘anhu);
‘La ewe Fatima, wapo Waislam wanaohitajia zaidi mali hii.’

Hotuba yake ya mwanzo


Baada ya Waislam kufungamana naye na kumkubali kuwa Khalifa wao, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipanda juu ya membari na kutoa hotuba yake ya mwanzo akasema;
“Ninasikia kuwa kuna watu wanauogopa ukali wangu na ugumu wangu. Wanasema; 'Umar alikuwa mkali wakati Mtume wa Mwenyezi Mungu alipokuwa nasi, kisha akawa mkali zaidi wakati Abubakar alipokuwa  Khalifa wetu. Atakuwaje leo wakati amri yote ipo mikononi mwake?'
Anayesema hayo amesema kweli, kwani mimi nilikuwa msaidizi na mtumishi wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ambaye hapana anayeweza kuufikia upole wake na huruma zake na alikuwa kama alivyosema Mwenyezi Mungu;
‘Kwa walioamini ni mpole na mwenye huruma’
Na mimi nilikuwa kwake mfano wa upanga ulionolewa nikingoja amri zake. Nikaendelea kuwa naye katika hali hiyo mpaka Mola wake alipomchukua akiwa ameridhika nami. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili hiyo, na nina furaha sana kwa ajili hiyo.
Kisha Abubakar akapewa Ukhalifa, na alikuwa kama mnavyomjuwa ukarimu wake na upole wake, na mimi nilikuwa mtumishi wake na msaidizi wake nikichanganya ukali wangu kwa upole wake na nilikuwa mfano wa upanga wake ulionolewa nikingoja amri zake, na nikaendelea kuwa naye katika hali hiyo, mpaka Mola wake alipomchukua akiwa ameridhika nami. Namshukuru Mwenyezi Mungu na nina furaha sana kwa ajili hiyo.
Kisha nikakabidhiwa mimi Ukhalifa, basi mjue kuwa ukali ule umeongezeka, lakini utakuwa kwa wale madhalimu na wanaokiuka mipaka. Ama wale watu wa usalama na dini na mwenendo mwema, mimi nitakuwa laini kwao kuliko ulaini wao baina yao, na sitomuacha mtu amdhulumu mwenzake au apindukie mipaka katika kuwaudhi wenzake. Na atakayefanya hivyo nitauchukua uso wake na kuuweka juu ya ardhi mpaka aikubali haki, kisha baada ya ukali wangu huo nitauweka uso wangu mimi juu ya ardhi kwa wale walio wapole na wasiopindukia mipaka.
Na kwangu mimi kuna haki zenu zisikilizeni vizuri;
Juu yangu nisikuchukulieni chochote katika haki zenu ila kwa haki yake. Na ni juu yangu kila kinachoingia mkononi mwangu, kisitoke isipokuwa pale panapostahiki. Ni juu yangu kujitahidi ili mapato yenu yaongezeke Inshaallah, ni juu yangu kuziba pengo zenu (kuondoa shida zenu). Na ni juu yangu nisikutieni katika maangamizo, na mnapokuwa vitani basi mimi ni baba wa watoto wenu mpaka mtakaporudi…..
Kwa hivyo mcheni Mungu na munisaidie katika nafsi zenu na munisaidie katika nafsi yangu katika kuamrisha mema na kukataza maovu na kuninasihi katika yale aliyonipa Mwenyezi Mungu katika kukuongozeni.”

 Nitamlipia kisasi chake


Katika kila msimu wa Hija, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), alikuwa akiwatangazia mahujaji wanaokuja kutoka sehemu mbali mbali za ulimwengu, kwa kuwaambia;
"Enyi watu! Mimi siwatumi magavana kwenu kwa ajili ya kukupigeni wala siwaleti ili wachukue mali zenu, bali nawaleta wakufunzeni dini yenu na mafundisho ya Mtume wenu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Kwa hivyo yeyote aliyetendewa kinyume na hayo alete malalamiko yake kwangu. Na mimi Wallahi nitamlipia kisasi chake".
Mmoja katika Masahaba (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
"Iwapo mmoja katika magavana uliowaweka kampiga mtu, ndiyo kweli utalipa kisasi cha aliyepigwa?"
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu;
‘Ndiyo! Nitafanya hivyo, kwani mimi nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisema;
"Kama yupo kati yenu niliyempiga mgongoni pake, basi mgongo wangu huu hapa na aje kulipa kisasi chake."
Na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) huwa anakusudia yale anayoyasema, kwa sababu siku moja alipotembelewa na watu kutoka mji wa Hims – Syria, aliwauliza juu ya gavana wao huko aitwaye Abdullah bin Qurt (Radhiya Llaahu ‘anhu), wakasema;
‘Ni mtu mwema isipokuwa amejijengea jumba la fahari’
Jumba la fahari! anajifaharisha mbele ya watu kwa kujijengea jumba la fahari wakati Waislam wanatafuta tonge ya kuzuwia njaa?
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamtuma mjumbe kwenda mji wa Hums na kumwambia;
"Kahakikishe juu ya jambo hili, na ikiwa ni kweli basi ianze hiyo nyumba, choma moto mlango wake, kisha njoo naye Amiri huyo".
Mjumbe akaifunga safari mpaka mji wa Hums na kurudi na Abdillahi bin Qurt (Radhiya Llaahu ‘anhu) mpaka kwa Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekataa kumkabili gavana huyo muda wa siku tatu, kisha akamtaka akutane naye panapo zizi la ngamia na kondoo wa sadaka.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamtaka Amiri huyo avue nguo za thamani alizovaa na badala yake avae nguo za wachungaji, kisha akampa bakora na kumwambia;
‘Nguo hizi ni bora kuliko alizokuwa akivaa baba yako na fimbo hii ni bora kuliko ile ulokuwa ukiichungia kondoo. Wafuate ngamia hawa na wachunge ewe Abdullah’.
Baada ya kupita siku tatu akamwita na kumuuliza;
"Kwani mimi nilikupa ugavana na kukupeleka huko kwa ajili ya kujijengea majumba na kujiimarisha? Rudi katika kazi yako lakini usirudie tena uliyofanya".
Alimetendea haya gavana ambaye watu wake walishuhudia kuwa ni mtu mwema isipokuwa tu alijijengea jumba zuri la fahari kwa ajili ya nafsi yake.

Mimi ni bora kuliko wewe


Huyu ndiye Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye siku moja alipopata mashtaka kutoka kwa kijana wa Kimisri aliyekuwa katika dini ya Kinasara kuwa alipigwa bakora na Muhammad mwana wa Amru bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) gavana wa Misri kwa sababu alimshinda katika mashindano ya mbio, na baada ya kumtandika bakora akamwambia;
‘Mimi ni bora kuliko wewe’.
Amr bin Al Aas huyu (Radhiya Llaahu ‘anhu), ndiye aliyekuwa mkuu wa majeshi ya Kiislam yaliyoiteka nchi ya Misri na hatimaye akapewa yeye ugavana wa nchi hiyo.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamtaka Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) aje Madina, yeye pamoja na mwanawe Muhammad.
Hebu tumsikilize Anas bin Malik (Radhiya Llaahu ‘anhu), akituhadithia jinsi mambo yalivyokuwa siku hiyo. Anasema Anas (Radhiya Llaahu ‘anhu);
‘Wallahi tulikuwa tumekaa kwa Umar, mara Amru bin Aas akatokea akiwa amevaa saruni na nguo ya juu, na Umar akawa anageuka huku na kule kumtafuta mwanawe Muhammad aliyekuwa nyuma ya baba yake.
Umar akauliza;
‘Yuko wapi Mmisri?’
Mmisri akasema;
“Mimi niko hapa ewe Amiri wa Waislamu.”
Umar akamwambia;
“Chukua bakora hii umtandike huyo ‘Aliye bora'
Akamtandika bakora huku Umar akimwambia;
“Endelea kumpiga huyo ‘Aliye bora”
Kisha Umar akamwambia yule kijana wa Misri;
“Sasa mtandike bakora baba yake, kwa sababu mwanawe asingekupiga isipokuwa kwa kuwa anaendekezwa na baba yake”.
Yule Mtu wa Misri akasema;
“Ewe Amiri wa Waumini, nimekwisha piga na kulipiza kisasi changu kiasi cha kutosha kwa kumpiga yule aliyenipiga”.
Umar akamgeukia Amru na kumwambia;
“Ewe Amru, tokea lini mnawageuza watu kuwa watumwa na hali wamezaliwa na wazee wao wakiwa huru?”
Huyu ni Amru bin Al Aas mkuu wa jimbo kubwa kabisa katika majimbo yanayohukumiwa na dola ya Kiislamu, na mwanawe hajaweza kuepukana na uadilifu wa Umar bin Khatwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu), bali hata yeye mwenyewe aliponea chupu chupu kutandikwa bakora, na hii ni kwa sababu ya kusamehewa na yule aliyeonewa.

Matumizi yake


Anasema Abdullahi bin Amer bin Rabia (Radhiya Llaahu ‘anhu);
Nilifuatana na Umar bin Khatwaab kutoka Madina hadi Makka katika safari ya Hija kisha nikarudi naye. Wallahi sikumwona akipigiwa hema la fahari wala akikaa ndani ya jengo, bali alikuwa akijikinga na jua kwa kutandaza kitambaa juu ya mti na kulala chini yake.
Ama Bashaar bin Namir (Radhiya Llaahu ‘anhu) yeye anasema;
“……Kisha Umar akaniuliza;
‘Kiasi gani tulichotumia katika Haji yetu?’
Nikamjibu;
‘Dinari kumi na tano’
Akasema;
‘Tumefanya israfu katika mali hii’

Walipotambua kuwa inambidi Umar akope ili aweze kuendesha maisha yake vizuri, masahaba wakubwa kama Othman, Ali, Talha na Al Zubeir (RAnhum) wakakutana na kuamua kumtuma binti yake Hafsa (Radhiya Llaahu ‘anhu) amshauri na kumkinaisha baba yake akubali kuongeza mshahara wake kutoka nyumba ya mali ya Waislam.
Umar akamuuliza binti yake;
‘Nani aliyekutuma?’
Bibi Hafsa akamwambia;
‘Mimi naona hivyo.’
Umar akamwambia;
‘Bali kuna watu waliokutuma.’
Kisha akamuuliza mwanawe;
‘Mwanangu wewe ulikuwa mke wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), nyumbani kwake alikuwa akivaa nini?.
Akasema;
‘Nguo mbili tu alikuwa nazo’
Akasema;
‘Na kipi katika vyakula vizuri mlichokuwa mkila?’
Akajibu;
‘Mkate wa ngano tukiivuruga ndani ya mafuta au samli."
Akamuuliza tena;
‘Kitambaa gani cha thamani alichokuwa nacho nyumbani Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)?
Akajibu;
‘Nguo moja nzito, tulikuwa tukiitandika chini siku za joto na katika siku za baridi tukiigawa kwa kuitandika nusu chini na nusu nyingine tukijifunikia’.
Kisha akasema;
‘Ewe Hafsa, waambie waliokutuma kuwa; mfano wangu na mfano wa sahibu zangu wawili Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), ni mfano wa watu watatu waliotembea njia moja, wa kwanza amewasili pamoja na zawadi alizotakiwa achukuwe, na wapili akapita njia hiyo hiyo na akawasili pamoja na zawadi inayotakikana, kwa hivyo wa tatu wao akiifuata njia ya wawili hao na kuridhika na zawadi kama yao basi atakutana nao. Ama akifuata njia nyengne isiyokuwa yao hatokutana nao’.

Mashauriano (Shura)


Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akipenda kushauriana na kusikiliza rai za wengine katika kila dogo na kubwa, wala hakuwa akipenda kuwahukumu watu kwa mabavu.
Alikuwa akitumia hekima ya hali ya juu na kusikiliza ushauri wao katika mambo yote ya kimaisha, isipokuwa katika mambo mengine hasa yale aliyokuwa akimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akiyatenda. Hayo alikuwa akiyafuata bila kurudi nyuma hata kama alikuwa haijui hekima iliyo ndani yake.
Alikuwa kwa mfano akilibusu jiwe jeusi la Al Kaaba huku akiliambia;
‘Najua wewe ni jiwe tu, hudhuru wala hunufaishi, na lau kama nisingemuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akikubusu basi nisingekubusu’.
Anapotufu alikuwa akienda mbio huku akiliacha wazi bega lake la upande wa kulia huku akisema;
‘Sisi tulikuwa tukikimbia na hatukuwa tukiyafunika mabega haya wakati wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliyetutaka tufanye hivyo kwa ajili ya kuwaonesha makafiri kuwa hatuna maradhi waliyokuwa wakitusingizia, na kuwaonesha kuwa sisi tuna nguvu za kutosha. Lakini sasa Uislamu ushaenea na ukafiri ushaondoka, juu ya hayo siwezi kuacha jambo tuliokuwa tukilitenda wakati wa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam).”
Alikuwa anapoisoma kauli ya Mwenyezi Mungu;
‘Wa dhaariati dharwa falhaamilati wiqra,’ akisema;
"Wadhaariati dharwa, maana yake ni Upepo, na kama nisingemsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisema hivyo basi nisingesema. Falhaamilati wiqra, maana yake ni Mawingu, na kama nisingemsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisema hivyo basi nisingesema.”

Alikuwa akihuzunika anapoona watu wanaogopa kumtoa makosa anapokosea au kumnasihi pale anapohitajia nasaha.
Siku moja Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akimsikitikia sahaba Hudhaifa (Radhiya Llaahu ‘anhu) juu ya uamuzi alioutowa wa kutowapa ardhi za kilimo wapiganaji Jihadi, hasa zile ardhi za kilimo zilizotekwa na Waislam katika nchi ya Fursi (Iran) baada ya kutekwa kwa nchi hiyo. Alitaka zibaki vile vile zikimilikiwa na wenye ardhi zao watakaokuwa wakitoa malipo maalumu yatakayokwenda katika Nyumba ya mali ya Waislam, na kwa njia hiyo watu watafaidika zaidi.
Alikuwa akiona pia kuwa kuwagawia ardhi wanaopigana Jihadi kutawafanya waiache kazi hiyo muhimu na kujishughulisha na mambo ya kidunia.
Baadhi ya watu hawakuridhika na rai hiyo, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipotaka ushauri wa watu wanaojulikana kwa hekima, wote wakamuunga mkono Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) katika uamuzi wake.
Jambo hilo lilimhuzunisha Umar(Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyedhani kuwa watu wanaogopa kutoa rai zao, ndipo alipomwita Hudhaifa (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumsikitikia, na Hudhaifa (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
“Wallahi kama tukikuona umeiacha haki na kwenda upande, basi sisi tutakurudisha tena katika haki ewe Umar”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alifurahi sana kwa kauli hiyo akasema;
“Namshukuru Mungu kuwa nina marafiki watakaonirejesha katika haki iwapo nitaiendea kombo.”

Siku moja alipanda juu ya membari na kuhutubia watu akisema;
“Enyi Waislam, mtasema nini iwapo nitakigeuzia dunia kichwa changu hivi?" Mtu mmoja akainuka na kutangulia mbele huku akiunyosha upanga wake na kuutikisa huku akimuambia;
“Ukifanya hivyo, basi na sisi tutakwambia kwa panga zetu hivi”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
‘Unanikusudia mimi maneno hayo?’
Yule mtu akasema;
“Naam ni wewe niliyekukusidia”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema:
“Mwenyezi Mungu akurehemu, Namshukuru Mwenyezi Mungu aliyejaalia miongoni mwenu atakayeniweka sawa pindipo nikienda upande”.

Umar(Radhiya Llaahu ‘anhu), hakuwa akitamka haya kwa ajili ya kujionesha tu, kwani alikuwa na nguvu pamoja na kuaminika kiasi ambacho hakuwa na haja ya kufanya mambo kwa kutaka kujionesha, bali huu ulikuwa ni mwenendo wake wa kweli, na tabia yake ya kweli ya kuipenda haki.
Alikuwa pale anapokosolewa, hupenda kuitamka kauli maarufu ifuatayo;
‘Mwenyezi Mungu amrehemu mja aliyenipa zawadi makosa yangu’
Kwake yeye, anapotolewa makosa huona kama amepewa zawadi, na kwa ajili hiyo humshukuru yule aliyemkosoa na kumuombea rehema kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Siku moja alipanda juu ya membari, na baada ya kumtukuza Mwenyezi Mungu na kumsalia Mtume wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam), akaanza kuhutubia kwa kusema;
“Sikilizeni, Mwenyezi Mungu awarehemu”
Mmoja katika Waislam waliohudhuria akainuka na kusema:
“Wallahi hatukusikilizi Wallahi hatukusikilizi”
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
“Kwa nini hunisikilizi ewe Suleiman?”
Suleiman (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Kwa sababu umejipendelea nafsi yako, umetugawia kila mmoja wetu kitambaa kimoja na wewe umejichukulia viwili”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), akawa anatafuta baina ya watu, kisha akauliza:
“Yu wapi Abdullahi bin Umar” (mwanawe).
Abdillahi bin Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akainuka na kusema;
“Ni mimi hapa ewe Amiri wa Waislam”.
Umar, akasema:
“Mimi kama mjuavyo ni mrefu, na kitambaa nilichopata hakijanitosha, na Abdullahi mwanangu akanipa kitambaa chake nikakiunganisha na changu”.
Suleiman (Radhiya Llaahu ‘anhu), akasema huku machozi yakimlenga:
“Alhamdulillah, sasa tutakusikiliza ewe Amiri wa Waumini”.
Hapana mfalme wala kiongozi yeyote duniani aliyewapa watu uhuru kama huu, akaruhusu kuhojiwa hata juu ya nguo aliyovaa mbele ya umma kama ule na kwa lugha kali kama ile juu ya kuwa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakati huo hakuwa akiitawala Bara ya Arabu peke yake, bali alikuwa Khalifa wa Dola ya Kiislamu inayotawala Bara ya Arabu yote na sehemu kubwa ya Asia na Afrika.
Na kwa nini asifanye hivyo wakati yeye ni mwanafunzi wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) aliyemuona siku moja akiambiwa na mbedui;
“Nipe, kwani mali hii si mali yako na ufalme huu si wako”
Na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alitabasamu kisha akamwambia mbedui yule:
“Umesema kweli, kwa hakika mali hii ni ya Mwenyezi Mungu”.
Na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipotaka kumvamia mbedui yule, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamzuwia na kumwambia;
“Mwache ewe Umar, mwenye haki yake ana haki ya kusema”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliupenda na kuufuata mwenendo huu wa kipenzi chake, mbora wa viumbe vyote, Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
Aliupenda na kuufuata, na akawajulisha umma kuwa kushauriana ndiyo njia ya kunyanyuka kwa Umma.
Na wao walifahamu vizuri kuwa kiongozi wao alikuwa akikusudia kuwapa uhuru wa kutoa rai zao, na kwamba hilo halikuwa jambo la mzaha au la kupita njia.

Huyu ndiye Khaula bint al Hakim


Siku moja Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokuwa akitembea akiwa amefuatana na Al Jaarod, alitokea bibi mmoja aliyemwita Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa sauti kubwa huku akisema;
“Tembea taratibu ewe Umar ili niweze kukufikia na kukuambia maneno machache”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akageuka kumtazama bibi huyo, na alipomuona alisimama na kumsubiri huku akitabasamu.
Bibi akasema;
“Umar, mimi nakujua wewe tokea ulipokuwa ukiitwa Umayr (kwa kulidogosha jina la Umar), ulipokuwa ukipigana mieleka katika soko la Ukhadh, hazikupita siku ukawa unaitwa Umar, kisha hazikupita siku nyingi ukawa unaitwa Amiri wa Waislamu, kwa hivyo Muogope Mwenyezi Mungu katika raia zako…..”
Al Jarood aliyekuwa amefuatana na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia yule bibi;
“Umevuka mpaka katika maneno yako na Amiri wa Waislamu.”
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), akamwambia;
“Muache aseme, kwani wewe humjuwi nani huyu? Huyu ndiye Khaula bint Al Hakim ambaye Mwenyezi Mungu ameyasikia maneno yake akiwa juu ya mbingu Zake saba alipokuwa akijadiliana na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) juu ya mumewe, Basi Umar ni nani hata akatae kusikiliza kauli yake?”
(Kwa ajili ya bibi huyu Mwenyezi Mungu hapo mwanzo aliteremsha aya nne za mwanzo za Suratu l Mujadilah “Qad samia”).

Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliupa umma kila tumaini, kila nafasi na kila haki ili watu wajue kuwa wanao uhuru na kwamba kila mmoja anayo haki ya kusema na ya kutoa ushauri na kumkosoa yeyote katika viongozi, hata kama kiongozi huyo ni Amiri wa Waislamu. Hii ni kwa sababu uhuru ni jambo jepesi kabisa; nalo ni kila mtu kuipata haki yake na awe na uhuru wa kuidai haki hiyo popote alipo.
Na kwa vile haki haimilikiwi na mtu mmoja au kundi fulani, au haijulikani na mtu mmoja tu au na kundi Fulani, kila mmoja alikuwa na haki ya kuifuata njia hiyo.

Siku moja mtu mmoja alikuwa akijadiliana na Umar huku akiwa ameshikilia hoja yake kuwa ni sawa na kwamba hoja ya Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) haikuwa sawa. Akawa anamwambia:
“Ittaqi llah yaa Umar – (Muogope Mwenyezi Mungu ewe Umar).” Akawa anayakariri maneno hayo, huku wenzake wakimwambia;
“Basi inatosha, unazidisha tena kubishana na Amiri wa Waislamu”.
Umar akasema;
“Mwacheni aseme. Hamtakuwa na kheri iwapo hamtosema, na hatutakuwa na kheri iwapo hatutasikiliza”.
Na hii ni kauli ya haki kabisa, kwani watu hawatakuwa na kheri ikiwa wataogopa kusema ukweli, na viongozi hawatakuwa na kheri ikiwa watakataa kusikiliza.

Kuupanua msikiti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)


Siku moja Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimwendea Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) ami yake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamwambia;
“Niliwahi kumsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akisema kuwa anataka kuupanua msikiti, na kwa vile nyumba yako ipo karibu zaidi na msikiti basi naona bora ujitolee ili tuweze kuifanya kazi hii, na badala yake tutakupa ardhi kubwa zaidi”.
Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Sitofanya hivyo”
Umar akamwambia;
“Kwa hivyo itanibidi nikulazimishe.”
Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Huna haki ya kunilazimisha. Tumtafute mtu ahukumu baina yetu kwa haki”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
“Unamchagua nani atuhukumie baina yetu?”.
Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Hudhaifa bin Al Yamani”.
Umar na Al Abbas (R Anhum), wakamwendea Hudhaifa nyumbani kwake ili ahukumu baina yao, na kwa ajili hiyo ufalme wa Hudhaifa (Radhiya Llaahu ‘anhu) utakuwa mkubwa zaidi kupita ule wa Amiri wa Waislamu kwa sababu watalazimika yeye na Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuukubali uamuzi wowote atakaouamua.
Kwa msemo wa kisasa tutasema; Hudhaifa atakuwa kadhi baina ya mtu anayeiwakilisha Serikali ambaye ni Umar, dhidi ya mmoja kati ya wananchi ambaye ni Al Abbas (Radhiyallahu anhum).
Baada ya kuwakaribisha na kusikiliza maneno ya pande zote mbili Hudhaifa (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Nilisikia kuwa Nabii Daud (AS) alitaka kuupanua msikiti wa Baytul Maqdis na kulikuwa na nyumba ya yatima karibu na msikiti huo. Nabii Daud (AS) akataka kuichukua nyumba hiyo kwa nguvu ili aibomoe na kuiunganisha na msikiti, lakini Mwenyezi Mungu akamfunulia wahyi kuwa;
'Nyumba iliyotakasika na dhulma ni nyumba yangu,' Nabii Daud (AS), akaamua kumrudishia yatima huyo nyumba yake."
Al Abbas akamtazama Umar na kumuuliza;
‘Bado unataka kuichukua nyumba yangu?’
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“La, sitaki tena.”
Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Sasa kwa hiari yangu nakupa nyumba yangu ili uweze kuupanua msikiti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)."

Mwenye kipaji na hekima


Mwenye kupewa hekima basi amepata kheri nyingi sana, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema;
"Miongoni mwa waliokuja kabla yenu walikuwepo watu wenye kufunuliwa bila ya wao kuwa ni mitume. Ikiwa katika umma wangu wapo wenye mfano wao, basi atakuwa Umar".
Bukhari- Muslim na Attarmidhiy

Katika kauli zake za hekima, ni pale alipomsikia mtu akimsifia mwenzake kuwa ni madhubuti na mwaminifu, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
“Ushawahi kusafiri naye?”
Akasema;
“La, sijawahi”
 “Uliwahi kugombana naye?”
“La, sijawahi”
“Uliwahi kumwaminisha mali?”
“La”
"Basi usimpe mtu sifa ya umadhubuti ikiwa hukumshuhudia akipapambana na mitihani."

Usiku umekuwa mrefu


Inajulikana kuwa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akipenda kutoka nyakati za usiku kwa ajili ya kuchunguza hali za raia wake, na usiku mmoja alipokuwa katika hali hiyo alimsikia mwanamke akiwa nyumbani kwake akihuzunika huku akisema kwa sauti kubwa;
“Usiku umekuwa mrefu na mume wangu hayupo, Wallahi ningekuwa simuogopi Mwenyezi Mungu ningekitingisha kitanda changu hiki kila pembe. Lakini kumuogopa Mola wangu na wingi haya zangu pamoja na kuilinda heshima ya mume wangu kunanizuwia nisifanye hivyo”.
Kisha mwanamke huyo akaendelea kusema;
“Hivyo Umar anaona ni jambo jepesi kunifarikisha na mume wangu?”
Asubuhi iliyofuata Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akenda moja kwa moja mpaka nyumbani kwa binti yake Hafsa (Radhiya Llaahu ‘anhu), akamuuliza;
“Ewe Hafsa, mwanamke anaweza kustahamili kuwa mbali na mumewe kiasi cha muda gani?”
Hafsa (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Mwezi, miezi miwili, mitatu, mwezi wa nne subira inaanza kutoweka”.
Kuanzia siku hiyo Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaweka kanuni ya kuwa askari yeyote aliyekuwa mbali na nchi yake kwa ajili ya kupigana jihadi, aruhusiwe kurudi nyumbani kwake kila baada ya miezi mine.

Na alipomsikia mtu mzima mmoja akisikitika kuwa siku nyingi zishapita hajamuona mwanawe wa pekee aliyekwenda kupigana Jihadi, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaamrisha mwanawe huyo arudishwe haraka kwa mzee wake, na akaweka kanuni kuwa asiruhusiwe mtu yeyote kwenda kupigana Jihadi iwapo ana wazee wawili watu wazima, au hata mmoja, isipokuwa baada ya idhini yao.
Umar ni kipaji cha hekima kinachofanya kazi kimaumbile na kinachoweka kanuni zinazonasibiana na hali za watu.

Namna ya kuhukumu baina ya watu


Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimuandikia Abu Musa Al Ash ary (Radhiya Llaahu ‘anhu) yafuatayo akimfundisha hekima za kuhukumu baina ya watu kwa uadilifu;
“Kutoka kwa Mja wa Mwenyezi Mungu Amiri wa Waislamu, kwa Abdullahi bin Qays, kwa hakika kuhukumu baina ya watu ni fardhi iliyo wazi na mwenendo unaowajibika kufuatwa. Sikiliza vizuri na ufahamu pale unapotolewa ushahidi, na uamue unapokubainikia ukweli, kwani uamuzi bila ya haki hauna faida. Wapoze watu katika vikao vyako. Mwenye kudai anawajibika kutoa ushahidi, na mwenye kukanusha anawajibika kula kiapo.
Suluhu ni bora baina ya Waislamu, lakini isiwe suluhu inayohalalisha haramu na kuharamisha halali.
Usije ukakuzuwia uamuzi uliouamua jana, kisha Mwenyezi Mungu akakuongoza ukatambua kuwa ulikosea katika uamuzi ule, ukakufanya uogope kuiweka sawa haki, kwani haki ni haki na haibatilishwi na chochote. Na kuirudisha haki kwa wenyewe ni bora kwako kuliko kuendelea kuinyamazia batili.
Ushahidi wa Waislamu baina yao ni haki, isipokuwa yule aliyewahi kuhukumiwa kupigwa mjeledi kwa kosa kubwa au aliyewahi kutoa ushahidi wa uwongo au anayetiliwa shaka kwa sababu ya kumpendelea mshitaki au mshitakiwa kwa ajili ya undugu wa nasaba, (hawa ushahidi wao haukubaliwi). Mwenyezi Mungu ndiye ajuwaye siri za moyoni.
Usiwatishe watu au kuingiza uoga nyoyoni mwao, kwani yule anayeihusisha nia kwa ajili ya kumridhisha Mwenyezi Mungu basi Mwenyezi Mungu anamtosheleza. Ama mwenye kuamua kinyume na haki kwa ajili ya kutaka kujipendekeza kwa watu, Mwenyezi Mungu humuacha alivyo, na iko siku atamfedhehesha. Unaonaje si bora mtu azikimbilie thawabu za Mola wake na Rehema Zake?
Wassalaam”.

Mtu wa aina hii, muadilifu, mcha Mungu, mwaminifu, mwenye kipaji cha hekima na nguvu pamoja na kuwa yeye ni khalifa wa Waislamu anayehukumu Mashariki ya ardhi na Magharibi yake, asiyechaguwa pa kukaa, bali hukaa popote inapomalizika safari yake, analala popote, ikiwa ni juu ya mchanga, chini ya mti au juu ya rundu la majani. Anakula anachokipata, ikiwa ni kipande cha mkate kwa nyama au mara nyingine hutolea mafuta au samli.
Huwa na furaha anapomsikia mtoto au mtu yeyote akimwita kwa jina lake;’Ewe Umar’.
Hufurahi pale anapomuona mzee akijaribu kubeba mzigo mzito kisha akatangulia yeye na kumbebea mzigo ule mpaka nyumbani kwake kisha mzee yule akasema;
“Mwenyezi Mungu akujaze kheri ewe mwanangu, wewe unastahiki kuwa Khalifa kuliko Umar”.
Jambo ambalo wafalme wangelilisikia basi wangemuonea husuda.

Mpe habari sahibu yako kuwa amepata mtoto wa kiume


Usiku mmoja alipokuwa katika matembezi yake ya kusikiliza shida za raia alifika sehemu za nje ya mji wanapoishi mabedui, na akawa anasikia sauti ya mwanamke akilia kwa maumivu. Alipoelewa kuwa kinachomliza ni uchungu wa uzazi na kwamba hana mtu wa kumsaidia isipokuwa mumewe, Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akarudi nyumbani kwake na kumwambia mkewe Ummu Kulthum binti wa Imam Ali bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Tuna chochote nyumbani mwetu?”
Mkewe (Radhiya Llaahu ‘anhu) akauliza;
“Kuna nini?”
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Mwanamke mbedui anazaa na hana wa kumsaidia”.
Ummu Kulthum (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Naam tunacho ukitaka.”
Umar na mkewe (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakaanza kukusanya unga, samli, sukari na baadhi ya mahitaji, kisha wakaondoka na kufuatana mpaka penye hema la mzazi, na Ummu Kulthum (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaingia ndani ya hema na Umar akabaki nje pamoja na mume wa mzazi, akawasha moto kwa ajili ya kuwapikia kitakachoweza kumsaidia mzazi huku mume wa mzazi akimshukuru.
Bada ya mzazi kujifungua, Ummu Kulthum (Radhiya Llaahu ‘anhu) akachungulia nje na kumwambia Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Ewe Amiri wa Waislamu, mpe habari sahibu yako kuwa amepata mtoto wa kiume.”
Kauli hii ilimsitua mbedui aliyeinuka kwa mshangao huku akionesha kuona haya huku akijaribu kutamka neno lolote lile baada ya kujua kuwa Khalifa wa Waislamu pamoja na mkewe ndio waliokuwa wakiwatumikia usiku kucha.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
“Baki hapo hapo ulipo wala usisituke."
Kisha Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akinyanyua chungu kilichokuwa na chakula na kukisogeza mlangoni na kumwita mkewe;
“Ewe Ummu Kulthum nipokee chungu hiki ili umlishe mama na mwache ashibe sawa sawa”.
Ummu Kulthum (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamlisha mama yule na baada ya kushiba akakirudisha chungu kile kwa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliyekiweka mbele ya baba na kumwambia;
“Kula, maana wewe umekesha usiku kucha na bila shaka una njaa”.
Kisha akaondoka yeye na mkewe kurudi nyumbani huku akimwambia yule mtu;
“Kesho njoo mjini ili niamrishe upewe katika mali kiasi cha kukusaidia wewe, na ili mtoto mchanga awe analipwa haki yake”.

Kifo chake


Ilikuwa siku ya Ijumaa wakati Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipopanda juu ya membari akampwekesha Mwenyezi Mungu na kumsalia Mtume wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kisha akasema;
“Nimeota ndoto, na sioni tafsiri nyengine isipokuwa ajali yangu imeshakaribia. Nimeota jogoo mwekundu ananidokoa mara mbili kichwani pangu.”
Kisha akazungumza juu ya Khalifa atakayekuja baada yake, akasema;
“Watu wananitaka nimchague Khalifa, na Mwenyezi Mungu hataipoteza dini yake wala Ukhalifa wake kwa kuondoka kwangu mimi duniani, Ushauriano juu ya nani atakayekuwa Khalifa baada yangu uwe kati ya watu hawa sita ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipokufa alikuwa radhi nao. Na yeyote kati yao mtakayefungamana naye basi lazima mumsikilize na kumtii, nami najua kuwa wapo watakaonilaumu juu ya uamuzi wangu huu, watu hao mimi nilipambana nao kwa upanga wangu huu hata wakaingia katika Uislamu”.
Hotuba hiyo ilikuwa siku ya Ijumaa na aliuliwa siku ya Jumatano na mmajusi mmoja (mwenye kuabudu moto) aitwaye Abu Luu lua Al Majusiy, wakati alipokuwa akisalisha watu Sala ya Alfajiri.
Abu Luu lua huyu aliyekuwa na jambia alilolipaka sumu, aliingia msikitini akijificha kwa kiza wakati wa Sala ya Alfajiri na wakati ule hakukuwa na taa za kutosha kama ilivyo hivi sasa, na Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakati huo alikuwa kesha funga Sala na kuanza kusoma baadhi ya Sura, na Abu Luu lua akamsogelea na kumpiga jambia mara tatu, moja wapo chini ya kitovu, na hiyo ndiyo iliyomuuwa Simba huyu wa Waislamu (Radhiya Llaahu ‘anhu) katika uwanja wake wa Ibada.
Abu Luu lua akafanikiwa kuwauwa masahaba wengine saba na kuwajeruhi sita walipojaribu kumkamata na hatimaye mmoja katika Masahaba aitwaye Huttan Al Tamimi (Radhiya Llaahu ‘anhu) alifanikiwa kumrushia guo lake usoni na kumfunika nalo, na alipoona kuwa kesha wezwa akajiuwa mwenyewe kwa kujipiga na jambia lake aliyolipaka sumu.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokuwa akianguka alimvuta nguo Abdulrahman bin Auf (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa nyuma yake na kumtaka akamilishe Sala.
Anasema mwanawe Abdillahi bin Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
“Kabla ya kufariki kwake, kichwa cha babangu kilikuwa juu ya paja langu, akaniambia;
‘Abdullah! kiweke kichwa changu juu ya ardhi huenda Mola wangu akikiona juu ya ardhi akanionea huruma’.

Kiongozi mfano wa Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyeweza kuzivunja vunja nguvu za Warumi na Wafursi, dola mbili kubwa za wakati huo, pamoja na kuweza kuwatoa Mayahudi nje ya Bara ya Arabu. Kwa sababu hizi mamilioni ya watu wakaingia katika dini hii ya Mwenyezi Mungu. Mtu wa aina hii hakosi kuwa na maadui katika kila pembe ya ulimwengu wanaochukizwa na mafanikio yake.
Hakukuwa na jeshi lolote lililoweza kusimama mbele ya majeshi yake, lakini makhabithi waliweza kuwachomeka watu wao katika sehemu mbali mbali ili kuizuwia nguvu hiyo, na juu ya hayo, juu ya kifo cha Shahada alichotunukiwa na Mola wake, Makhalifa waongofu waliokuja baada yake waliweza kuiendeleza kazi hiyo na kuinyanyua bendera ya Laa ilaaha illa Llah.

Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye ni bin ammi yake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwepo alipokuwa Umar akikata roho akamwambia;
“Mwenyezi Mungu akurehemu ewe Abu Hafs (Umar bin Khatwaab) kwani Wallahi ulikuwa Mlinzi wa dini ya Kiislamu, makimbilio ya mayatima, mahali pa imani, mlinzi wa madhaifu. Ukiwasaidia watu na kuisimamia haki, mfunguzi wa miji, na kwa hivyo ukafanikiwa akawa anatajwa Mwenyezi Mungu kila wakati katika kila pembe ya dunia”.
Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamuuliza;
"Utashuhudia hayo mbele ya Mwenyezi Mungu?"
Ali bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa karibu yake akamshika mkono Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumwambia;
"Shuhudia, na mimi nitakuwa shahidi wako."
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia Umar;
"Nitashuhudia."

Maziko yake


Alipotambua kuwa wakati wa kuonana na Mola wake umeshafika, alimtuma mwanawe Abdillahi (Radhiya Llaahu ‘anhu) ende kwa Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) na kumuomba akubali azikwe karibu na Sahibu zake wawili ambao ni Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na Abubakar Al Siddiq (Radhiya Llaahu ‘anhu) waliozikwa ndani ya chumba cha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha).
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akasema;
“Wallahi mahali hapa baina ya Mume wangu na Baba yangu nilijiwekea mwenyewe, lakini kwa vile Umar ameniomba, basi sitomkatalia ombi lake. Mmwambie nimekubali”.

Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) alifurahi sana kusikia hayo, lakini alimwambia na kumsisitiza mwanawe kuwa;
“Kabla sijazikwa nenda kamtake tena ruhusa Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha), na iwapo atakubali ndiyo munizike hapo, kwa sababu huenda ikawa amenikubalia hivi sasa bado ningali hai kwa kunionea haya au kwa kuniheshimu nikiwa Khalifa wa Waislamu, lakini huenda akataka kubadilisha nia yake baada ya kufa kwangu.”

Mwenyezi Mungu akurehemu ewe Umar. Hata unapokuwa baina ya uhai na mauti, kipaji chako kina fanya kazi yake sawa sawa. Nguvu zako zinafanya kazi sawa sawa, na hekima yako inafanya kazi yake na UchaMungu wako unafanya kazi yake bali hata kuwapenda kwako Sahibu zako kunafanya kazi yake.
Mwenyezi Mungu amswalie Mtume wetu Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na awe radhi nao Sahaba zake pamoja na Umma wote wa Kiislamu - Aamin.