Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Khalifa wa nne
aliyeongoka
Babu Yake
Abdul Muttalib bin Hashim alikuwa mkuu wa kabila la
Kikureshi, mbora wao na kiongozi wao wanayemtii. Sifa zake zilienea katika eneo
lote la jangwa la (Bara ya) Arabuni kuanzia Kaskazini mpaka Kusini yake. Wote
walikuwa wakimheshimu na wakijua kuwa yeye ndiye aliyekichimba kisima cha maji
ya Zamzam kwa mikono yake. Kisima kinachoendelea kutowa maji yenye baraka mpaka
wakati wetu huu.
Majeshi ya Abraha Mhabeshi yalipotaka kuibomoa Al
Kaaba, Abdul Muttalib alitambua kuwa hana uwezo wa kupambana nayo. Aliwataka
watu wake wauhame mji na kupanda juu ya majabali. Akawakusanya kondoo zake na
kuondoka nao huku akimuomba Mola wake Mtukufu ailinde nyumba Yake hiyo ya Al
Kaaba.
Alipoulizwa kwa nini anakimbia pamoja na wanyama wake
na kuiacha Al Kaaba bila ulinzi, Abdul Muttalib alijibu:
"Lilbayti rabbun yah-miyhi", maana yake;
"Nyumba ina Mola wake mlezi mwenye kuilinda".
Alifurahi kupita kiasi alipoletewa bishara njema ya
kuzaliwa kwa mjukuu wake Muhammad bin Abdillahi bin Abdul Muttalib (Swalla
Llahu alayhi wa sallam). Akambeba kwa mikono yake miwili na kukimbia naye mpaka
ndani ya msikiti wa Al Kaaba huku akimuomba Mwenyezi Mungu na kumshukuru
akisema;
"Alhamdulillahi aliyenipa mtoto huyu mwema na
mzuri".
Akampa jina la Muhammad, na kabla ya kufariki kwake alimuusia
sana mwanawe
Abu Talib juu ya mtoto huyo na kumtaka amlee vizuri, akamwambia;
"Mwanangu huyu atakuwa na shani kubwa, kwa hivyo
umtunze vizuri, asije akafikiwa na dhara yoyote".
Abdullahi, baba yake Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) alifariki dunia kabla ya kuzaliwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam). Kwa hivyo Abu Talib akachukuwa jukumu la kumlea mtoto
huyo kama alivyousiwa na baba yake Abdul Muttalib, na hata pale Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) alipoanza kufunuliwa Wahyi na kuilingania dini ya Mola
wake, Abu Talib alimsaidia sana, akamlinda yeye pamoja na ujumbe aliokuja nao
juu ya kuwa yeye mwenyewe (Abu Talib) hakuingia katika dini hii tukufu.
Abu Talib alikuwa na heba na heshima kubwa mbele ya
waarabu kama aliyokuwa nayo baba yake. Pia
alirithi sifa na tabia njema za baba yake, akaweza kujulikana na kuheshimiwa na
Waarabu wote kama alivyokuwa akiheshimiwa baba
yake Abul Muttalib..
Alikuwa shujaa na mwenye uwezo wa kuongoza, na kwa vile
alikuwa mkubwa wa kabila la Makureshi aliweza kumlinda Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) asidhuriwe na Makureshi.
Katika ukoo huu uliokuwa ukiwaongoza Makureshi na
waarabu wote kwa hekima na heshima na utukufu mkubwa kupitia karne nyingi sana,
alitokea Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) mwana wa Abu Talib bin Abdul Muttalib bin
Hashim bin Abdu Manaf, aliyerithi kutoka kwa baba yake Abu Talib kila sifa
njema za ukarimu, ushujaa na ukweli.
Katika kitabu chake kiitwacho
'Abqariyat Imam Ali', na maana yake (Kipaji cha hekima cha Imam Ali), anasema
Abbas al Aqqad;
"Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
anajulikana kuwa ni mtu wa mwanzo katika kabila la Bani Hashim aliyezaliwa
kutokana na baba na mama wote wakiwa wanatoka katika ukoo wa Al Hashimiy. Baba
yake Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), jina lake ni Abu Talib bin Abdul Muttalib bin
Hashim bin Abdi Manaf na mama yake pia jina lake ni Fatima bint Asad bin Hashim
bin Abdi Manaf.
Inasemekana kuwa Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipewa na mamake jina la 'Haidarah', (na maana yake ni 'Simba'),
sawa na jina la babu yake (babake mamake) ambaye jina lake lilikuwa
'Asad', na maana yake pia ni Simba, lakini baba yake akalibadilisha na kumpa
jina la Ali."
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
mdogo wa ndugu zake, na mkubwa wake alikuwa Jaafar kisha Aqiyl kisha Talib (Radhiya
Llaahu ‘anhu). Inasemekana kuwa Aqiyl
alikuwa kipenzi cha baba yake, na hii ndiyo sababu pale Abu Talib alipokuwa
katika shida na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akifuatana na Hamza na Al
Abbas walipomwendea Abu Talib kwa ajili ya kumsaidia ulezi wa watoto wake,
akawaambia;
"Niachieni mimi Aqil na
wachukuweni muwatakao".
Al Abbas akamchukua Talib, Hamza
akamchukua Jaafar, na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamchukuwa Aliy (Radhiya
Llahu anhum).
Wake zake
Vitabu vya historia vinasema kuwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) hajawahi
kuoa mke mwengine wakati alipokuwa akiishi na bibi Fatima (Radhiya Llaahu
‘anha) binti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), lakini
baada kufariki, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alioa wake wafuatao:
1. Umama bint
Abul Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) binti yake bibi Zainab (Radhiya Llaahu ‘anha)
mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na Abul Aas
mume wa bibi Zainab alikuwa mtoto wa dada yake bibi Khadija binti Khuwaylid (Radhiya
Llaahu ‘anha).
2. Asmaa binti
Umais (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa mke wa Jaafar bin Abu Talib na
alipofariki Jaafar bibi Asmaa aliolewa na Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu), na
alipofariki Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaolewa na Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu).
3. Fatima Ummul
Baniyn.
4. Ummu Said
binti Urwa bin Masaud Al Thaqafiy
5. Khaula binti
Jaafar bin Qays
6. Al Suhabaa
binti Rabia
7. Laila binti
Masaud
8. Muhyaat binti
Mruul Qays
Inasemekana pia kuwa alioa wake wengine zaidi ya hawa.
Ewe Dunia Mtafute Mwengine!
Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipomtaka Dhirar bin Dhamira Al Kanaaniy azungumze juu ya sifa
za Aliy bin Abu Talib (RAnhum), Dhirar akasema;
"Ali bin Abu Talib alikuwa
Wallahi mtu mwenye kuona mbali, mwenye nguvu nyingi, anasema kwa utulivu na
anahukumu kwa uadilifu, elimu inabubujika kutoka katika kila sehemu yake, na
hekima inazungumza kutoka katika kila kitendo chake, hakuipa thamani yoyote
dunia wala mapambo yake.
Alikuwa akistarehe nyakati za
usiku (pale anaposali) ndani ya kiza chake. Aikuwa Wallahi mwingi wa mafunzo,
mwingi wa kufikiri, akipenda kupindua pindua viganja vya mikono yake pale
anapofikiri, akipenda kuvaa nguo zisizokuwa ndefu sana (hakuwa akipenda kuvaa
maguo mengi na makubwa yanayoburura), na alikuwa akipenda chakula kisichokuwa
laini (hakuwa akipenda vyakula vya fakhari), Alikuwa Wallahi akijiweka kama
mmoja wetu, tukimwendea anatusogelea na tunapomwita anatujia, na juu ya
kujikurubisha nasi kwake, hatukuwa tukimsemesha sana kwa sababu ya haiba aliyokuwa
nayo.
Alikuwa akiwatukuza wachaMungu na
akiwapenda maskini. Mbele yake, mwenye nguvu muovu hawi na tamaa ya kuitimiza
batili yake, na aliye dhaifu hakati tamaa ya kupata haki yake - Nashuhudia
mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa nilikuwa nikimuona wakati unapoingia usiku
akiuendea msala wake huku akizishika ndevu zake na kulia kwa huzuni kubwa sana huku akisema;
"Ya Rabbana ya Rabbana"
- huku akimnyenyekea Mola wake, kisha anasema kuiambia dunia;
"Hay-haata hay-haata (hayawi
hayawi). Ewe dunia mhadae mwingine, nimekwisha
kukuacha talaka tatu wala sitokurejea tena. Umri wako mdogo, kukaa nawe ni
hatari, na hatari zako zinakuja kwa wepesi, Aah! Aah! (nasikitika) kwa machache
niliyojitayarishia, na safari ni ndefu na njia ni ya hatari."
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akawa analia huku akijifuta machozi kwa kitambaa, na wote waliohudhuria hapo
siku hiyo wakawa wanalia.
Sali Ubavuni Mwa Bin Ami Yako
Siku moja Abu Talib alimuona mwanawe Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akisali nyuma ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa
sallam), na hii ilikuwa katika siku za mwanzo za Uislamu, na Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) hakuogopa wala kubabaika, na baada ya kumaliza kusali akamwendea
baba yake na kumwambia kwa ufasaha;
"Ewe baba yangu, nimemuamini Mwenyezi Mungu na
kumfuata Mtume wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam)".
Baba yake akamwambia;
"Yeye hakuiti isipokuwa ndani ya jambo la kheri.
Kuwa pamoja naye".
Na siku ile Abu Talib alipomuona Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) akisali nyuma ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
kuliani kwake huku mwanawe Jaafar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akiwa amesimama kwa
mbali kidogo akiwatazama, Abu Talib akamwita Jaafar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumwambia;
"Kamilisha ubawa wa Bin ammi yako, nenda kasali
upande wake wa kushoto".
Wa Mwanzo Kusilimu Katika Watoto
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
miaka minne wakati alipochukuliwa kulelewa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam), na alikuwa kesha timia miaka kumi pale wahyi ulipoanza
kuteremka. Na siku ile alipomuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi
wa sallam) akisali, alimuuliza;
"Unafanya nini?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akamwambia;
"Ninasali".
"Unamsalia nani?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akamwambia:
"Mola wa ulimwengu
wote".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akauliza;
"Nani huyu Mola wa ulimwengu
wote?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akamwambia:
"Ni Mungu mmoja asiye na
mshirika, aliyeumba, na mikononi mwake imo amri ya kila kitu, Naye ni Mweza wa
kila kitu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akazitamka shahada mbili na kuwa mtoto wa mwanzo kusilimu. Lakini juu ya udogo
wa umri wake, alikuwa miongoni mwa wale waliokuwa wakihudhuria darsi za Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) katika nyumba ya Al Arqam bin
Abul Arqam pamoja na masahaba wenye umri mkubwa kupita yeye kama vile Abubakar
na Uthmaan na Al Zubair na Twalha na Abdul Rahman bin Ouf na Saad bin Abi
Waqqaas na wengine (RAnhum) tokea siku za mwanzo za Uislamu.
Niulizeni Kisha Niulizeni
Hakuwa akisema uwongo siku ile
alipowaambia watu;
"Niulizeni, kisha niulizeni
kisha niulizeni mtakacho juu ya kitabu cha Mwenyezi Mungu, kwani Wallahi hapana
hata aya moja katika aya zake ila ninaijua iwapo imeteremshwa usiku au
mchana".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alilelewa katika nyumba ya Qurani, au tunaweza kusema kuwa alilelewa na yule
aliyekabidhiwa Qurani, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
Akawa anaipokea kutoka katika kinywa chake kitukufu ikiwa bado mbichi na mpya,
Qurani ambayo daima ni mbichi na mpya, maneno
yake yasiyokonga wala kuchosha.
Alikuwa akiwatangulia wenzake
katika kuisikia Qurani pamoja na siri zake, ikimtakasa huku ikibubujika kutoka
katika kinywa cha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
wakati akikumbana na taathira zake. Hii ndiyo sababu iliyomfanya Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) awe mtiifu wa Qurani maisha yake yote.
Hakusema uwongo siku ile
alipomuandikia Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumwambia;
"Mtume Muhammad ni ndugu
yangu na mkwe wangu
Na Hamza bwana wa mashahidi pia ni
ami yangu
Jaafar ambaye usiku na mchana
anaruka na Malaika ni mtoto wa mama yangu
Na binti wa Muhammad ni mke wangu
na utulivu wangu
Tumechanganya pamoja naye damu
yangu na nyama yangu
Wajukuu wawili wa Mtume kutoka
kwake, nao pia ni wanangu
Yupi kati yenu mwenye sehemu kubwa
kuliko yangu?
Nimetangulia katika Uislamu kabla
kubalighi kwangu.
Uadilifu Wake (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Siku moja aliipoteza ngao yake,
naye wakati huo alikuwa Khalifa wa Waislamu. Alipokuwa akipita sokoni akaiona
ikiwa mikononi mwa Myahudi aliyekuwa akitaka kuiuza.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alimwendea Myahudi huyo na kumwambia;
"Ngao hii ni yangu imenianguka usiku wa siku fulani mahali
fulani."
Myahudi akasema;
"Bali
hii ni ngao yangu na imo mikononi mwangu ewe Amiri wa Waumini".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Hii ni ngano yangu na mimi
sikuwahi kumuuzia mtu yeyote wala kumpa zawadi mtu yeyote hata ikaweza
kukufikia wewe".
Myahudi akasema;
"Atakayehukumu baina yetu ni
kadhi wa Kiislamu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Sawa! twende kwa
kadhi".
Wakaondoka pamoja na kuelekea kwa
kadhi Shuraih, anayejulikana kwa uadilifu wake na kwamba ni mtu asiyemuogopa
yeyote mbele ya haki.
Shureih akasema;
"Unasemaje ewe Amiri wa
Waislamu?"
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Nimeiona ngao yangu hii kwa
mtu huyu, na mimi ilinianguka usiku kadha na mahali kadha (akapataja mahala
ilipomuanguka). Nashangaa vipi imekuwa yake wakati mimi sikupata kumuuzia mtu
wala kuigawa".
Shureih akasema kumuuliza Myahudi;
"Unasemaje na wewe?"
Akajibu;
"Ngao ni yangu na imo
mikononi mwangu na mimi simtuhumu Amiri wa Waumini kuwa anasema uongo".
Shureih akamgeukia Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) na kumwambia;
"Mimi sina shaka yoyote kuwa
maneno yako ni kweli tupu ewe Amiri wa Waumini, na kwamba ngao hii ni yako kama ulivyosema, lakini huna budi kuleta mashahidi wawili
watakaoshuhudia juu ya madai yako".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Ndiyo nitawaleta, nitamleta
aliyekuwa mtumwa wangu niliyemuacha huru Qambar na mwanangu Al Hassan, nao watashuhudia
juu ya ukweli wa madai yangu".
Kadhi Shureih akasema:
"Lakini ushahidi wa mwana kwa
ajili ya babake haukubaliwi ewe Amiri wa Waisalmu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Subhanallah! Mtu katika watu
wa Peponi ushahidi wake haukubaliwi! Kwani hukumsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) akisema;
"Al Hassan na Al Hussein ni
mabwana wa vijana wa Peponi?".
Shureih akasema;
"Naam! nimemsikia ewe Amiri
wa Waislamu, isipokuwa mimi siukubali ushahidi wa mwana kwa ajili ya
babake".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamgeukia Myahudi yule na kumwambia;
"Ichukue! kwani sina
mashahidi wengine isipokuwa hao'.
Myahudi akasema;
"Lakini mimi nashuhudia kuwa
ngao hii ni yako ewe Amiri wa Waislamu".
Kisha akaongeza kusema;
"Ya Allah! Amiri wa Waislamu
anahukumiwa na kadhi wake, na kadhi huyo anahukumu dhidi yake? Nashuhudia
kwamba hapana Mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Allah, na kwamba Muhammad
ni Mtume wake. Nakujulisha ewe kadhi kuwa ngao hii ni ya Amiri wa Waumini na
kwamba mimi nilikuwa nikimfuata alipokuwa akenda na jeshi lake mpaka alipofika
mji wa Siffiyn na hapo ndipo ngao hiyo ilipomuanguka kutoka juu ya ngamia wake
na mimi nikaiokota".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamwambia;
"Kwa vile umesilimu, basi
nakupa wewe ngao hii kama ni zawadi yako na
pia nakupa zawadi farasi wangu huyu".
Anayependwa na Mwenyezi Mungu na Mtume Wake
Kutoka kwa Abul Abbas Sahal bin
Saad Al Saidiy (Radhiya Llaahu ‘anhu), amesema kwamba siku ya vita vya Khaibar,
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alisema;
"Kesho nitampa bendera mtu
ambaye kwa mikono yake Mwenyezi Mungu atatupa ushindi. Mtu huyo anampenda
Mwenyezi Mungu na Mtume wake na anapendwa na Mwenyezi Mungu na Mtume
wake".
Anaendelea kusema Sahal (Radhiya
Llaahu ‘anhu);
"Usiku kucha watu walikuwa
wakiwaza kwa kutaka kujua ni nani huyo mwenye kupendwa na Mwenyezi Mungu na
Mtume wake atakayepewa bendera hiyo. Asubuhi yake watu wote wakaamkia kwa Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Kila mmoja akitamani apewe
yeye bendera siku hiyo".
Imepokelewa kuwa; Umar (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alisema;
"Hakuna siku niliyotamani
kupewa bendera kuliko siku hiyo".
Baada ya watu kujikusanya mbele
yake, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akauliza;
"Yuwapi Aliy bin Abu
Talib?"
Akajibiwa;
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu,
Aliy anaumwa macho".
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akasema;
"Niitieni"
Akaitwa, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) akamtemea mate machoni pake huku akimpangusa na kuomba
dua. Hapo hapo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akapona na kukabidhiwa yeye bendera
hiyo.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akauliza;
"Nipigane nao mpaka wawe kama sisi?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akamwambia;
"Nenda mpaka utakapofika
katika mji wao. Kisha waite katika Uislamu na uwajulishe juu ya yale Mwenyezi
Mungu anayotaka kutoka kwao…."
Imeelezwa kuwa Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipoufikia mlango wa Khaibar (mji wa Mayahudi), alipiga ukelele
na kusema;
"Mimi Aliy Bin Abu
Talib".
Anasema Khalid Muhammed Khaled
katika kitabu cha 'Khulafaa Rrasuul';
"Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alikuwa akielewa namna gani jina hilo
linavyoingiza khofu ndani ya nyoyo za makafiri, kwani mara baada ya kulitaja
jina lake, kwa ghafla alishambuliwa na kupigwa pigo la nguvu mpaka ngao yake
ikamuanguka, na mbele yake akawaona walinzi wa mlango huo waliokuwa
wakimshambulia wakijitayarisha kummaliza, na yeye akiwa amelala chini bila ya
kuwa na hata ngao ya kujikinga.
Akasema moyoni mwake;
"Leo ama nitaonja yale
yaliyomkuta Hamza au Mwenyezi Mungu atanipa ushindi".
Akainuka na kuwaendea walinzi hao
na kuanza kuwasukuma huku na kule kwa nguvu zake zote. Ikisha akauendea mlango
wa ngome hiyo ya Khaibar na kuung'oa kwa mikono yake".
Anaendelea kusema Dr. Khaled;
"Watu kabla hawakujua nini
kinachotendeka walistukia Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akitoa takbir kwa sauti
kali; "Allahu Akbar", na kumuona keshaubeba mlango huo kwa mikono
yake miwili.
Anasema Abu Raafi-a (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ambaye alikuwa katika kikosi cha Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Tulijaribu mimi na wenzangu
saba kuubeba mlango huo tukashindwa".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) pamoja
na majeshi yake wakawa wanashambulia huku wakiingia ndani ya mji wa Khaibar.
Haukupita muda mrefu wakafanikiwa kuuteka mji huo.
Alipoletewa habari za kutekwa kwa
mji huo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akasema;
"Allahu Akbar! ishaangamia Khaibar – Hakika sisi tunaposhuka uwanja wa
watu itakuwa asubuhi mbaya kwa wale walioonywa (wasionyeke)".
Bukhari na Muslim
Askari Mwenye Adabu
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
askari mwenye wingi wa adabu na heshima. Na kwanini asiwe hivyo wakati
amelelewa katika nyumba ya mwalimu wa adabu Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) aliyefundishwa adabu na Mola wake Subhanahu wa Taala.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) amesema;
"Amenifundisha Mola wangu na
amenifundisha vizuri".
Katika vita vya Uhud, Abu Saad bin
Abi Twalha aliyekuwa msitari wa mbele katika majeshi ya makafiri alipaza sauti
yake juu akimwita Aliy bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) kumtaka apambane
naye. Aliy akauitikia mwito huo kwa kujisogeza mbele mpaka wakawa uso kwa uso
na mapambano makali yakaanza baina yao.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alifanikiwa kumpiga Abu Saad pigo la nguvu na kumuangusha chini huku akilia
kutokana na maumivu makali, lakini alipounyanyua upanga wake juu tayari
kumuuwa, nguo ya Abu Saad ikafunuka na utupu wake ukawa unaonekana.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akafumba macho huku akigeuka na kurudi nyuma kuelekea msitari wa mbele wa jeshi
la Waislamu akimwacha adui yake huyo amelala chini.
Alipoulizwa;
"Kwa nini hujamuua?"
Akajibu;
"Alinikabili kwa utupu wake
nikamuonea huruma".
Si hivyo tu, bali hata baada ya
majeshi ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) kushinda katika vita vya Al Jamal, na
kabla ya vita vya Siffiyn kuanza, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipata habari
kuwa watu wawili katika jeshi lake na majina yao ni Hajar bin Uday na Umar bin
Al Hamaq walikuwa wakimtukana Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa
dhahiri, jambo lililomkasirisha sana Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyewaita na
kuwataka waache matusi yao.
Wakamuuliza;
"Ewe Amiri wa waumini, kwani
sisi si tupo katika haki?"
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akajibu;
"Ndiyo, naapa kwa Mungu wa Al
Kaaba (kuwa sisi tupo katika haki)".
Wakamuuliza;
"Sasa kwa nini basi
unatukataza tusiwatukane?"
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akawaambia;
"Sipendi muwe watukanaji
wanaopenda kulaani watu. Bora mseme;
"Mola wetu zuwia damu yetu na
damu yao isimwagike na utupatanishe, na uwatowe
kutoka katika makosa yao
mpaka waijuwe haki na batil ili wasijiingize ndani yake (batili hiyo)".
Anasema Dr. Khalid Muhammad
Khalid;
"Huyu ni mpiganaji mwenye
heshima ya hali ya juu, na huu ni ushujaa wa hali ya juu usiopatikana isipokuwa
kwa mwanamume wa kweli, na unaofaa kuigwa na wanaume wa kweli".
Abu Sufyan
Abu Sufyan alitumwa na makafiri wa
Makka kwenda Madina kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
kumuomba msamaha baada ya wao Makureshi kuvunja baadhi ya masharti ya mkataba
wa Hudaibia. Alipowasili Madina hapana hata Muislamu mmoja aliyekubali kukaa au
kuzungumza naye.
Alipoamua kwenda nyumbani kwa
binti yake Umm Habiba Ramlah bint Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye ni
mke wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), binti yake huyo
alikataa kumuacha baba yake akae hata juu ya tandiko la mumewe, akalikunja na
kumuacha baba yake akae chini.
Alipomuuliza binti yake:
"Kwa nini hutaki nilikalie
tandiko hili?"
Akamwambia;
"Kwa sababu wewe ni
mshirikina na kwa ajili hiyo hustahiki kulikalia tandiko la Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)".
Aliporudi Makka Abu Sufyan
akawahadithia Makureshi yaliyomkuta Madina, akasema;
"Nikamwendea mwana wa Abi
Quhafa (Abubakar Al Siddiq (Radhiya Llaahu ‘anhu)) lakini sikupata msaada
wowote kutoka kwake. Kisha nikamwendea Ibni l Khattab (Umar (Radhiya Llaahu
‘anhu)) nikamuona amegeuka kuwa adui mkubwa., akanambia;
"Unataka mimi nikakuombeeni
msamaha kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu? Wallahi lau kama
sitapata kitu cha kukupigeni isipokuwa punje ndogo ndogo basi nitapigana nanyi
jihadi kwa punje hizo", kisha nikamwendea Ali, nikamuona ni mwenye huruma
kupita wote".
Vita Vya Al Ahzab (Khandaq)
Makabila mbali mbali ya
washirikina yaliungana na kuunda jeshi kubwa la watu wapatao elfu kumi kwa
ajili ya kuwapiga vita Waislamu hapo Madina, na hii ilikuwa baada ya
washirikina hao kuchochewa na Mayahudi wa mji huo.
Riwaya nyingine zinasema kuwa
jeshi hilo
lilikuwa la watu wapatao elfu ishirini na nne, na idadi hii ilikuwa kubwa
kuliko idadi ya watu wote wanaoishi Madina wakijumuishwa na wanawake na watoto
wa mji huo.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) aliitisha baraza la ushauri kuzungumzia mpango wa
kuuhami mji wao kutokana na uadui huo, na baada ya mashauriano na rai mbali
mbali, wakakubaliana juu ya rai ya Salman Al Farsiy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
aliyesema:
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu,
katika ardhi ya Wafursi tulikuwa pale tunapozungukwa tukichimba handaki lenye
kuuzunguka mji wetu".
Anasema Al Mubarak Furriy katika
kitabu cha 'Al Rahiyq al Makhtum;
"Haya yalikuwa maarifa mazuri
ambayo Waarabu kabla ya hapo hawakuwa wakiyajua".
Wachache sana miongoni mwa
makafiri akiwemo Amr bin Abd Wud Al Amry aliyekuwa mpiganaji mwenye nguvu
nyingi anayejulikana kwa ujabari na ukhabithi wake waliweza kuvuka na kuwafikia
Waislamu waliokuwa upande wa pili wa handanki hilo kwa kupitia njia ndogo
iliyojibana.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alipambana na Amr na akaweza kumuuwa, na Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alipambana na Nofel bin Abdullahi al Mughiyra al Makhzumiy naye pia akafanikiwa
kumuua.
Fathul Bari (Sharhi ya Sahih al
Bukhari).
Imepokelwa katika Mustadrak ya Al
Hakim hadithi iliyo sahihi kwa shuruti zilizowekwa na Maimam Bukhari na Muslim
inayosema kuwa;
"Miongoni mwa walioweza
kulivuka handaki hilo
kupitia njia iliyojibana alikuwa Amr bin Abdu Wud Al Amry aliyewahi kupigana
katika vita vya Badr akaumizwa mguu, na hakuwahi kupigana vita vya Uhud.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamtokea na kumwambia;
"Ewe Amr, niliwahi kukusikia
pale penye Al Kaaba ukisema kuwa mtu akikuita katika mambo mawili utakubali
moja wapo".
Akasema;
"Ndiyo"
Akamwambia;
"Basi mimi nakwita utoe
shahada ya 'Laa ilaaha illa Llah wa anna Muhammadan rasuulu Llah' na nakwita
katika Uislamu".
Amr akasema;
"Sina haja na yoyote katika
mawili hayo".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamwambia;
"Basi nakwita tupambane mimi
na wewe".
Akasema;
"Mimi sitaki kukuua".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Lakini mimi nataka
kukuua".
Wakapambana na Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akamuua Amr."
Msitari wa Mbele
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
msitari wa mbele katika kila anachowaamrisha au kuwanasihi Waislamu.
Alikuwa msitari wa mbele katika
ucha Mungu, katika kupigana jihadi, katika mwenendo na tabia njema, katika
kutoa, katika ustahamilivu, katika kuikinai dunia na katika kila nyanja ya
maamrisho ya Kiislamu.
Siku moja alipokuwa katika mji wa
Al Kufa na baada ya kuwasalisha Waislamu Sala ya Alfajiri, alikaa kimya muda
kidogo huku uso wake ukionesha dalili ya huzuni nyingi.
Aliendela kukaa akiwa katika hali
hiyo huku watu wakimuangalia na kuuheshimu ukimya wake huo mpaka jua
lilipochomoza vizuri na miale yake kuenea katika kuta za msikiti, kisha
akainuka na kusali raka-a mbili kisha akatikisa kichwa chake kwa masikitiko na
kuvipindua pindua viganja vya mikono yake huku akisema;
"Wallahi nimewaona Masahaba
wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na wala simuoni
kati yenu yeyote anayefanana nao. Walikuwa wakati wa asubuhi zinaonekana juu ya
nyuso zao dalili ya kukesha kwao huku wakifanya ibada na kusoma Qurani na kurukuu
na kusujudu. Na wanapokuwa wakimdhukuru Mwenyezi Mungu, utaviona vichwa vyao
vimeinama kwa unyenyekevu mfano wa miti inavyoinama siku za upepo mkali huku
macho yao
yakibubujika machozi mpaka nguo zao kuroa".
Anasema Khalid Muhammed Khalid
katika kitabu chake 'Khulafaa Rrasuul';
"Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
anatujulisha hapa juu ya hali ilivyokuwa katika zama tukufu kupita zote, siku
za Wahyi na utume, siku ambazo nafsi ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ingali
inaishi ndani yake na akawa anaendelea kuishi ndani yake katika maisha yake
yote. Hata wakati ukisonga mbele namna gani, hawezi kuusahau utukufu ule na
mapenzi yake juu ya Masahaba wa Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ambao pia
ni Sahibu zake. Hawezi kuiondoa heshima yake juu yao, wala kuwasahau, na hawezi pia kuuondoa
utukufu na mapenzi yake juu ya siku hizo ndani ya moyo wake, ndani ya dhati
yake, kwa sababu huo ndio mwenendo wake na hayo ndiyo makimbizi yake".
Maneno ya Hekima
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
mwingi wa hekima, na zifuatazo ni baadhi ya kauli zilizonukuliwa kutoka kwake;
"Jifunzeni ilimu ili muwe watu wake. Jueni
kuwa dunia tunaiacha nyuma na akhera tunaikabili, na kila moja kati ya nyumba
mbili hizo ina watu wake. Basi kuweni watu wa akhera na wala msiwe watu wa
dunia.
Wale waloikinai dunia, wameijaalia
ardhi yake kuwa busati lao, udongo kuwa tandiko lao, na maji kuwa pambo lao.
Mwenye kuipenda akhera lazima
ajiweke mbali na matamanio, na mwenye kuuogopa moto ajiweke mbali na
yaliyoharamishwa.
Mwenye kuitaka Pepo akimbilie
kumtii Mwenyezi Mungu, na aliyeikinai dunia hayapi umuhimu wowote masaibu yake.
Jueni kuwa Mwenyezi Mungu ana waja
wake, amewahifadhi wasifanye shari, nyoyo zao za huzuni, nafsi zao zimekinai,
matakwa yao machache, wamesubiri siku chache ili wapata raha za milele".
Anapomsikia mtu akiitukana dunia
alikuwa akimwambia;
"Dunia ni nyumba ya ukweli,
mahali panapoteremka Wahyi, msikiti wa Mitume, mahala pa kufanya biashara (na
Mwenyezi Mungu) kwa wanaomjua (Mwenyezi Mungu). Kwa hivyo ndani ya dunia
chumeni rehema za Mwenyezi Mungu ili muipate Pepo Yake".
Hakubadilika hata kidogo (Radhiya
Llaahu ‘anhu) tokea utoto wake mpaka ukubwani. Na hata katika zama za hatari,
zama za vita, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akiuweka mbele ucha Mungu
wake. Hakuwa akiongoza watu kwa akili zake, na hekima yake ya hali ya juu peke
yake, bali kwa ucha Mungu wake pia. Hakuwa akitaka chochote kutoka kwao
isipokuwa wawe wacha Mungu, kwa sababu anayemuogopa Mola wake, ndiye askari wa
kuaminika.
Na siku ile ya mapamabano baina
yake na Muawiya (Radhiyallahu Anhuma), alipoambiwa na bin ammi yake Abdullahi
bin Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu), ambaye naye pia ni mcha Mungu;
"Tumia hadaa, kwa sababu vita
ni hadaa".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamjibu;
"Abadan, sitoiuza dini yangu kwa dunia".
Anasema Khalid Muhammed Khalid;
"Mtu adhimu aliyekuwa
akiufundisha ulimwengu uaminifu, utakatifu, na utiifu kwa Mola wake".
Hotuba yake ya mwanzo alipowasili mji wa Al Kufa
Katika hutoba yake ya Ijumaa ya
mwanzo aliyowahutubia Waislamu mara baada ya kuwasili mji wa Al Kufa, Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alianza hotuba yake kwa kuwausia Waislamu katika kumcha Mwenyezi
Mungu, akasema;
"Nakuusieni waja wa Allah
kumuogopa Allah, kwani Taqwa ni jambo bora la kunasihiana baina ya waja wa
Allah, na ndiyo amali anayoridhika nayo Mwenyezi Mungu kutoka kwa waja wake.
Mumeamrishwa kumcha Mungu na kwa
ajili ya wema mumeumbwa, kwa hivyo ogopeni yale Allah aliyokutahadharisheni
nayo, kwa sababu amekutahadharisheni na adhabu kali kabisa.
Muogopeni Mwenyezi Mungu kuogopa
kwa kweli na tendeni matendo yenu bila ya kujionesha kwa watu wala kutaka sifa
au umaarufu, kwani mwenye kufanya amali yoyote ile kwa ajili ya kujipendekeza
kwa mwengine asiyekuwa Allah, basi Mwenyezi Mungu humsukumiza nazo amali zake
kwa huyo aliyemfanyia amali hiyo.
Ogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu,
kwa sababu hajakuumbeni kwa upuuzi, na wala hakuacha chochote kiende ovyo.
Keshataja athari zenu na keshajua siri zenu na kuzihesabu amali zenu na
kuziandika ajali zenu. Kwa hivyo dunia isikubabaisheni kwani inawaghururisha
watu wake, na ameghurika yule atakayebabaishwa nayo.
Na jueni ya kuwa Akhera ndiyo
makazi ya milele".
Siku moja kabla majeshi yake na
majeshi ya Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) kupambana katika vita vya Siffiyn,
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuwahutubia majeshi yake kwa maneno ya hamasa,
bali aliwahutubia kwa kuwaambia maneno yanayohitalifiana kabisa na maneno
yanayosemwa na majemadari katika hali kama
hiyo.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alisema;
"Kesho mtapambana na kaumu,
kwa hivyo usiku wenu ufanyeni uwe mrefu kwa kusali na zidisheni katika kusoma
Qurani na muombeni Mwenyezi Mungu akupeni subira, maghufira na afya."
Katika wakati wa amani au katika
wakati wa vita, anapokuwa ameshinda au anapokuwa katika shida yoyote ile,
hapana kinachomshughulisha isipokuwa kumcha Mola wake Subhanahu wa Taala.
Isipokuwa vita vya Tabuk
Huo ndio msimamo wake, na namna
hii ndivyo alivyokuwa akivikabili vita vyote alivyoshiriki.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alishiriki katika vita vyote vilivyopiganwa wakati wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) isipokuwa vita vya Tabuk, wakati Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipomuamrisha abaki Madina kwa ajili ya
kuwalinda watu wa nyumba yake. Jambo hilo lilimhuzunisha sana Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu), kwa sababu katika vita hivi hapana aliyebaki Madina isipokuwa wanawake,
wazee, watoto wadogo, na wanafiki waliokuwa wakijulikana kwa unafiki wao, na
walibaki pia Wale Watatu Waliongojeshwa ambao kisa chao kimetajwa katika Suratu
al Tawba.aya ya 18 na kuendelea mbele.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam);
"Unaniweka mlinzi juu ya
wanawake na watoto?"
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akamjibu mbele ya Masahaba wake wote (RAnhum) kwa kumwambia;
"Haikuridhishi kuwa wewe
kwangu mfano wa Harun alivyokuwa kwa Musa, isipokuwa hapana tena Mtume baada
yangu?"
Khalifa na mfano mwema
Mwenyezi Mungu amejaalia Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) awe Khalifa katika wakati mgumu sana, wakati ambao hapana mwengine
katika wakati wake angeliweza kuumudu, na Waislamu walikuwa na haja kubwa sana
ya uongozi wa mcha Mungu mfano wake, muadilifu pamoja na hekima yake, kwa
sababu wakati wa utawala wake yalizuka masaibu na matatizo mengi magumu sana
pamoja na fitna nyingi baina ya Waislamu, lakini mwanafunzi huyu ambaye ni
miongoni mwa wanafunzi wa mwanzo wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) alisimama imara mbele ya kimbunga hicho kilichomkabili yeye,
pamoja na umma wa Kiislamu.
Katika maamuzi yake alikuwa daima
akikumbuka jinsi Ustadhi wake Mtume wa Mwenyezi Mungu Muhammad (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) alivyokuwa akiyakabili kwa hekima kubwa mitihani mingi
iliyokuwa ikimkuta, alikuwa akikumbuka maneno aliyowahi kumsikia akimuambia
Ammi yake Abu Talib pale alipomshauri kuacha kuulingania Uislamu kutokana na
mateso na maudhi aliyokuwa akiyapata kutoka kwa Makureshi, na Mtume (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) akamjibu;
"Wallahi lau kama wataliweka jua katika mkono wangu wa kulia na mwezi
mkono wangu wa kushoto, basi sitoicha amri hii mpaka Mwenyezi Mungu
atakapoidhihirisha au nife kwa ajili yake".
Hakuisahau pia siku ile ya 'Fat'hi
Makka', siku Waislamu walipouteka mji wa Makka, na hakuzisahau zile nyuso za
makafiri wa Makka waliokuwa kabla ya hapo wakiwatesa na kuwauwa Waislamu,
wakiwadhulumu na kuwadhulumu kila walichokimiliki. Na pia katika vita vya Uhud
namna walivyomuuwa ami yake, Hamza (Radhiya Llaahu ‘anhu) bwana wa Mashahidi.
Siku hiyo Makureshi waligeuka wao
kuwa mateka wa majeshi ya Kiislamu, wakakusanywa upande mmoja wakingojea hukumu
kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) itakayoamua
mustakbali wao; hukumu kwa walivyokuwa wakitaraji kuwa hawatosalimika.
Akakumbuka pia namna gani siku ile
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alivyosimama mbele ya
mateka hao na kuwahutubia akiwauliza;
"Mnadhani nitakufanyeni
nini?"
Wakajibu;
"Kheri, ewe ndugu mkarimu na
mwana wa ndugu mkarimu".
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akawaambia;
"Nendeni, nyote mko huru".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
hakuisahau pia siku ile ami yake Al Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipomwendea
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kumuomba ampe
ugavana katika mojawapo ya wilaya za Kiislamu. Juu ya kuwa Al Abbas (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ni ami yake Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) tena ni mtu
muadilifu, mcha Mungu na shujaa, lakini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) alimjibu kwa kumuambia;
"Sisi Wallahi ewe ammi yangu,
hatumpi kazi hii mwenye kuiomba wala hatumpi mwenye kuichunga ".
Alikuwa akipenda kujikumbusha
maneno na maamuzi ya hekima pamoja na uvumilivu na ushujaa wa Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na kuyafanya kuwa dira yake na mfano
wake bora wa kuufuata.
Mwanzo wa kuhukumu kwake
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
mwingi wa hekima na hodari wa kutoa hukumu. Mara nyingi Abu Bakar (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipokuwa khalifa wa Waislamu alikuwa akimwendea kutaka msaada
wake huku akimwambia;
"Tupe fatwa juu ya jambo hili
ewe Abal Hassan (baba wa Hassan)".
Umar bin Khattab (Radhiya Llaahu
‘anhu) naye pia mara nyingi alikuwa akimwendea Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
kutaka ushauri wake, na aliwahi kumwambia;
"Lau kama si Ali, basi Umar angeangamia".
Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alipokuwa khalifa naye pia mara nyingi alikuwa akimwita Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) na kumtaka ushauri wake katika matatizo mbali mbali,na hili si jambo la
kushangaza kwani Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
aliwahi kusema;
"Mbora wenu katika kutoa
hukumu ni Ali."
Ibni Majah – Sehemu ya (1) mlango
wa fadhila za Masahaba
Abu Yaala
Sayuty katika Jameal Saghiyr
-mlango wa herufi ya hamza, na wengine
Jukumu lake la kuhukumu lilianza
pale waasi waliokuwa wameizunguka nyumba ya Uthmaan bin Affan (Radhiya Llaahu
‘anhu) waliporudi mara ya pili baada ya kukubali ushauri wa Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) hapo mwanzo wa kuondoka kuelekea makwao.
Waasi hao walirudi baada ya
kuikamata barua inayowataka magavana wa Misri na AlKufa kuwauwa waasi hao wote
mara watakapowasili huko.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alijaribu tena kuwataka waasi hao waondoke na kurudi makwao, lakini mara hii
walikataa. Juu ya kuwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikanusha, na sisi
tunaamini kuwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) amesema kweli alipokanusha, kwani
huyu ni mtu ambaye Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
amesema juu yake kuwa hata Malaika wanamsitahi.
Kwa hivyo ikajulikana kuwa waasi
hao hawakurudi mara hii isipokuwa kwa sababu ile ile iliyowaleta hapo mwanzo
nayo ni kumuuwa Khalifa wa Waislamu Uthmaan bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Katika riwaya iliyopokelewa na
Shaddad bin Aus (Radhiya Llaahu ‘anhu) anasema;
"Baada ya kutambua hayo, Aliy
(Radhiya Llaahu ‘anhu) akatoka nyumbani kwake akiwa amevaa kilemba cha Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na kuubeba upanga wake akielekea
moja kwa moja nyumbani kwa Khalifa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), akiwa
amefuatana na mwanawe Al Hassan na Abdullahi bin Umar bin Khattab pamoja na
baadhi ya Masahaba watu wa Makka na wa Madina (RAnhum). Akaingia nyumbani kwa
Khalifa na kumsalimia kisha akamwambia;
"Naona watu hawa
hawataridhika isipokuwa kukuuwa, kwa hivyo tuamrishe tupigane nao".
Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akasema;
"Nakuombeni kwa jina la
Mwenyezi Mungu ikiwa yupo kati yenu anayemshuhudia Mwenyezi Mungu kikweli na
akaelewa kuwa mimi nina haki yoyote ile juu yake, basi arudishe upanga ndani ya
ala yake na aondoke na isimwagike damu kwa ajili yangu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akarudia tena na tena kumwambia maneno hayo, lakini Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) akaendelea kukataa., kwa hivyo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akatoka na
kuelekea msikitini, na Sala iliposimamishwa watu wakamtaka Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) awasalishe, wakamwambia;
"Ewe Abul Hasan, tangulia
usalishe watu".
Akawajibu;
"Sitakusalisheni wakati
nyumba ya Khalifa wa Waislamu imezungukwa, nitasali peke yangu".
Akasali peke yake. Kisha akatoka
na kuelekea nyumbani kwake akiwaacha wanawe wawili pamoja na baadhi ya Masahaba
(Radhiya Llaahu ‘anhu) waulinde mlango wa nyumba ya Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu).
Waasi walielewa kuwa kila
wakikawia kuutimiza uadui wao, mambo hayatakuwa mazuri upande wao. Yakatokea
yaliyotokea, na Khalifa wa Waislamu Uthmaan bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akauliwa kwa njia ya kikhabithi, na mkewe Bibi Naila (Radhiya Llaahu ‘anha)
alipokuwa akijaribu kumkinga akakatwa vidole vya mkono wake pamoja na sehemu ya
kiganja, na hapo ndipo uti wa mgongo wa mwanzo wa Waislamu ulipovunjika.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) anaukataa Ukhalifa mara tatu
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
ameketi msikitini pamoja na watu wapatao kumi zilipomfikia habari za kuuliwa
kwa Khalifa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), akaondoka haraka kuelekea nyumba ya
Khalifa na alipowasili akaanza kwa kuwapiga wanawe Al Hassan na Al Hussein huku
akiwaambia;
"'Tabban lakum' (Mtaangamia),
vipi anauliwa Khalifa wa Waumini na nyinyi mpo mlangoni pake?".
Mji wa Madina ulibaki bila ya
khalifa muda wa siku tano, na katika siku zote hizo aliyekuwa akitamba mjini
hapo na kutoa amri alikuwa Al Ghafiqiy bin Harb mtu aliyemuuwa Khalifa wa
Waislamu Uthmaan bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Wamisri waliokuwa wengi wa waasi
hao walimuendea Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) mara mbili wakimtaka awe Khalifa wa
Waislamu lakini Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa. Wakamwendea Twalha (Radhiya
Llaahu ‘anhu) naye pia akakataa, kisha wakatoka na kumwendea Al Zubair (Radhiya
Llaahu ‘anhu) naye pia akakataa, kisha wakamwendea Abdillahi bin Umar (Radhiya
Llaahu ‘anhu), naye akakataa na mwisho wakamwendea Saad bin Abi Waqaas (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ambaye pia alikataa, na walipomrudia tena Aliy bin Abu Talib (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akakataa tena .
Hapana aliyethubutu kubeba jukumu
la ukhalifa wakati umma umekabiliwa na tatizo kubwa kama hilo, na nani atakayethubutu ikiwa Aliy mwenyewe
(Radhiya Llaahu ‘anhu) ameukataa?
Wote walioukataa walikuwa
wakihofia yale yatakayotokea baadaye, kwani atakayeshika uongozi itambidi
awahukumu wauaji wa khalifa wa tatu wa Waislamu Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
kwa kifo kwa ajili ya kitendo kiovu hicho.
Lakini wakati huo huo lazima
ajitokeze mtu wa kuiongoza dola ya Kiislamu. Lazima achaguliwe Khalifa kwa
sababu kila wakati unaposogea na nchi kuwa bila ya Khalifa, hatari inayotokana
na wenye tamaa inaongezeka. Hatari inayoweza kuiparaganya dola ya Kiislamu,
kuutawanya umma na kuupotezea mustakbali wake.
Anasema Dr.Khalid Mohammad Khalid;
"Watu waliitambua hatari
hiyo, pamoja na hatari ya waasi ambao baada ya kumuuwa Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) wakawa wanaeneza chuki, bughudha pamoja na uongo mwingi juu ya Khalifa
huyo mtukufu (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Wote waliitambua hatari ambayo
mfano wake ilikuwa kama kimbunga
kitakachouangamiza umma wote. Wakatambua kuwa lazima awepo kiongozi madhubuti
atakayezishika hatamu na kuuongoza umma na kuwavusha nje ya bahari hii
iliyochafuka.
Wakakusanyika watu wema katika
watu wa Makka na wa Madina na kumwendea Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), na baada
ya mazungumzo ya hekima kupita baina yao,
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akakubali kufungamana ili awe Khalifa wao.
Hapakuwa katika Masahaba wa Mtume (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wakati ule aliyestahiki kuwa Khalifa kupita Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu), na hapakuwa na mtu aliye na kipaji, uwezo, hekima na ushujaa kupita
yeye. Wakati huo ukhalifa wenyewe haukuwa kitu chenye manufaa yoyote ya
kidunia, bali ulikuwa ni mzigo mkubwa kwa yule atakayeubeba na ulikuwa ni
hatari kubwa kwa mwenye kumuogopa Mola wake".
(Mwisho wa maneno ya Dr. Khalid).
Wa mwanzo kufungamana naye
Wa mwanzo kufungamana naye,
aliyeuingiza mkono wake ndani ya mkono wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) siku hiyo
alikuwa ni Twalha bin Ubaidullah (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyefungamana naye kwa
mkono wake wa kulia uliokatika katika vita vya Uhud pale alipokuwa akipigana
kwa ajili ya kumkinga Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
aliyekuwa amezungukwa na maadui .
Anasema Ibn Kathir katika 'Al
Bidaya wal Nihaya;
"Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akatoka moja kwa moja na kuelekea msikitini. Akapanda juu ya membari akiwa
amevaa nguo zake pamoja na kilemba huku akiwa amekamata bakora yake. Akasimama
akiwa ameiegemea bakora hiyo, na watu wote wakafungamana naye hapo. Hiyo
ilikuwa ni siku ya Jumamosi tarehe kumi na tisa mwezi wa Dhul Hijjah.
Wa mwanzo kufungamana naye alikuwa Twalha (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kwa mkono wake uliokatwa siku ya vita vya Uhud, na yule
aliyemuuwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipoona vile akasema (kwa kejeli);
"Inna lillahai wa inna ilayhi raajiun". Na wa pili kufungamana naye
alikuwa Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) kisha wakafuatilia Waislamu wote
kufungamana naye mmoja baada ya mmoja".
Anaendelea kusema Ibni Kathir;
"Na katika hotuba yake ya mwanzo siku hiyo, Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alimshukuru Mwenyezi Mungu akampwekesha, kisha akasema;
"Hakika Mwenyezi Mungu ameteremsha kitabu
kinachotujulisha nini kheri na nini shari. Kwa hivyo ifuateni kheri na
epukaneni na shari. Mwenyezi Mungu ameharamisha mengi, akaitukuza heshima ya
Muislamu na kuifadhilisha kupita kila kitu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawataka Waislamu
waheshimiane na wawe na ikhlasi katika amali zao na katika Tauhid pamoja na
kuhurumiana na kupendana, na akawajulisha kuwa Mwislamu mwema ni yule ambaye
Waislamu wenzake watasalimika na ulimi wake pamoja na mkono wake na kwamba si
halali kwa Muislamu kumuudhi Muislamu mwenzake.
Akasema; "Kumbukeni kuwa watu wapo mbele yenu na
akhera ipo nyuma yenu (inakuja). Mnapoiona kheri, ifuateni, na mnapiona shari,
iepukeni, na kumbukeni pale mlipokuwa wachache madhaifu mlipokuwa mkionewa juu
ya ardhi".
(Mwisho wa maneno ya Ibni Kathir).
Kuwalani wauaji wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Atakayechunguza maisha ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ataona
kuwa yale matatizo na mapambano mbali mbali aliyokuwa akikabiliana nayo tokea
utotoni mwake, pamoja na hekima na busara kubwa iliyojificha ndani ya dhati
yake, ilikuwa muda wote huo ikimlea Khalifa huyu mtukufu kwa ajili ya
kumtayarisha na mitihani mbali mbali atakayopambana nayo katika wakati huu
mgumu kupita nyakati zote katika historia ya Waislamu.
Kuanzia siku ya mwanzo ya utawala wake baadhi ya Masahaba (Radhiya
Llaahu ‘anhu) walimwendea nyumbani kwake wakimtaka awakamate wauaji wa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) na kuwahukumu, lakini Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliwaambia;
"Wakati bado haujafika, kwani waasi hawa ni wengi sana na idadi yao
inapindukia watu elfu kumi. Kwa hivyo itakuwa bora kama
tutasubiri mpaka pale nitakapojimakinisha barabara."
Maneno hayo yaliwakasirisha masahaba hao (Radhiya Llaahu
‘anhu), wakatoka kwa ghadhabu huku wakimtuhumu Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa
hataki kuwakamata waasi.
Miongoni mwa waliochukuwa msimamo mkali sana katika jambo hili walikuwa Twalha, Al
Zubair na Muawiya bin Abu Sufyan (Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote).
Anasema Ibni Jariyr;
"Mara baada ya watu kufungamana na Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu), Naila, mke wa Uthmaan bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimwita Al
Noaman bin Bashir (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumpa nguo ya Uthmaan iliyojaa damu
aliyokuwa ameivaa siku aliyouliwa, pamoja na vidole vyake (Bibi Naila) kikiwemo
kiganja chake kilichokatwa na waasi pale alipokuwa akimkinga mumewe, na kumtaka
Al Noaman avipeleke nchi ya Sham kwa Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu
‘anhu).
Muawiya alilia sana alipoviona vitu hivyo, akavichukuwa na
kuvipeleka moja kwa moja mpaka ndani ya msikiti wa Damascus na kuvitundika juu
ya membari ya msikiti ili kila mtu aweze kuviona na kuhamasika katika kudai
kisasi cha kuuliwa Khalifa huyo wa tatu wa Waislamu .
Akapanda juu ya membari na kuwahutubia watu waliokuwa
wakilizana kwa uchungu mkubwa sana
na kwikwi kila anapovinyanyua vitu hivyo ili wavione, na akaendela na kazi hii
ya kuhamasisha watu muda wa karibu mwaka mzima.
Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye aliwahi kumuomba Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ampe ugavana wa mji wa Al Kufa, na Twalha (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akataka apewe ugavana wa Basra
ili waweze kukusanya watu wengi na kutayarisha jeshi kubwa la kupambana na
wauaji wa Khalifa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), lakini Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) akawataka msamaha na kuwaambia;
"Mtanisamehe sana,
lakini kwa wakati huu jambo hili haliwezekani kutendeka".
Masahaba hao hawakuridhika na msimamo huo. Wakaondoka kwa
ghadhabu, jambo lililosababisha kuvunjika kwa mfupa wa pili wa mgongo wa
Kiislamu.
Chanzo cha tukio la ngamia (Waqa'at al Jamal)
Kilichozidi kuharibu mambo na kuyafanya yawe magumu zaidi kwa
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), ni kule kujiunga kwa Bibi Aisha (Radhiya Llaahu
‘anha) pamoja na wale wanaodai kisasi cha kuuliwa kwa Khalifa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu).
Wakati Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipouliwa, Bibi Aisha
pamoja na wake wenzake wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) walikuwa Makka kwa ajili ya kufanya Umra, na pia kwa ajili ya kuwa
mbali na uasi ulioanza kudhihiri wakati ule dhidi ya Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu), na Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) alipata msituko mkubwa aliposikia
habari za mauaji hayo.
Al Zubair bin Al Awaam na Twalha (RAnhum) waliondoka Madina
baada ya kuruhusiwa na Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), ingawaje baadhi ya Masahaba
(Radhiya Llaahu ‘anhu) walimshauri Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) asiwaruhusu
kuondoka wakihofia wasije kuungana na Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kusababisha upinzani mkubwa dhidi yake.
Masahaba wawili hao (Radhiya Llaahu ‘anhu) pamoja na maelfu
ya watu waliokuwa nao waliungana na Bibi Aisha (Radhiyallahu anha), na wote kwa
pamoja wakaondoka kuelekea mji wa Basra
kwa ajili ya kujaribu kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huo.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye aliondoka Madina kuelekea Al
Kufa akiwa na kundi kubwa la watu, na katika kila mji aloupitia watu wengi wa
miji hiyo waliungana naye, isipokuwa alistushwa sana alipopata habari za
kujiunga kwa Bibi Aisha (Radhiyallahu anha) na kundi la wanaotaka kisasi cha
damu ya Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kilipwe kwa haraka.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa na uhakika kuwa Bibi
Aisha, Al Zubair na Twalha (Radhiya Llaahu ‘anhum), wote hao wanaelewa vizuri
kuwa yeye hawaungi mkono wauwaji wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), na kwamba
wakati utakapofika atawakamata na kuwahukumu, lakini kilichomhuzunisha ni ule
uamuzi wao wa kutoka na makundi makubwa ya watu kwa ajili ya kuharakisha
kukamatwa kwa wauaji hao. Habari zilizomfikia zilisema kuwa kundi hilo linaelekea Basra kwa
nia ya kuwajumuisha watu wema wa mji huo, pamoja na wa nchi yote ya Iraq
na kukusanya jeshi kubwa kwa ajili ya mapamabano.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa vile yeye ndiye kiongozi na
mtu wa mwanzo kulibeba jukumu la kulipa kisasi hicho, bila shaka hatokubali
dhulma kubwa kama hiyo ipite bila ya yule
aliyedhulumu kutiwa adabu. Lakini kilichomhuzunisha ni kule kutoachwa yeye kama ni mkuu wa dola hiyo ya Kiislamu kutumia hekima zake
na uwezo wake katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hili.
Baadhi ya Masahaba wakubwa kama vile Abdullahi bin Omar,
Osama bin Zaid, Saad bin Abi Waqqaas, Muhammad bin Muslamah na wengineo
(RAnhum) walikataa kujiunga na kundi lolote katika hayo mawili wakihofia
visitokee vita vya wenyewe kwa wenyewe, na Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alipokuwa akiondoka kuelekea Basra walikataa kuungana naye, wakamwambia;
"Mwenyezi Mungu ametuamrisha kupigana vita na
washirikina, ama vita hivi vikitokea baina ya Waislamu wenyewe kwa wenyewe,
sisi hatupendezewi kuitia mikono yetu ndani yake."
Hata hivyo walimjulisha Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa wao
wanatambua kuwa yeye yupo upande wa haki, lakini hawakutaka kunyanyua panga zao
na kuzielekeza katika vifua vya Waislamu wenzao.
Hakika kuuliwa kwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
kulisababisha fitna kubwa sana
baina ya Waislamu.
Katika kambi ya pili, Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha)
aliwahutubia watu na kuwajulisha ubaya wa waasi hao waliomuuwa Khalifa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) tena ndani ya mwezi ulioharamishwa umwagaji wa damu ndani yake na
katika mji ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
aliharamisha kupigana vita ndani yake, kisha wakakikata kiganja cha mkono wa
Bibi Naila (Radhiya Llaahu ‘anha) mke wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kuvikata vidole vyake pamoja na kuiba mali yao.
Watu wengi wakaungana na Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha), huku
wakimwambia;
"Popote utakapokwenda sisi tuko nyuma yako".
Kabla ya Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) kuondoka Makka,
hitilafu ilitokea kati ya wake za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi
wa sallam). Wapo miongoni mwao waliotaka kwenda moja kwa moja mpaka Madina
kumtaka Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) awakamate wauaji hao na kuwahukumu, na
wengine wakataka wende Basra
kukusanya jeshi kubwa kwa ajili ya kupambana na wauaji hao.
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) aliunga mkono rai ya kwenda
Basra, na walipokuwa njiani, wao pia wakaungwa
mkono na baadhi ya watu, na idadi yao
ikafika kiasi cha watu wapatao elfu tatu. Wakaondoka huku Bibi Aisha (Radhiya
Llaahu ‘anha) akiwa amebebwa ndani ya hema linalofungwa juu ya ngamia (Hawdaj).
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye alipowasili mji wa Al Kufa
alipata wafuasi wengi waliokuwa na hamasa kubwa ya kutaka kupigana vita kwa
ajili ya kumnusuru Khalifa wao mpya ambaye ni mtoto wa ammi yake Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
Alipoona hamasa zao zinaongezeka, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
aliwatuliza kwa kuwaambia kuwa; haki haipatikani kwa mapambano peke yake, bali
hupatikana kwa njia nyingi na kwamba kupigana vita kuwe ni jambo la mwisho la
kulitegemea.
Akamwita Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumtaka ende Basra kwa Mama wa
Waislamu Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) na kuzungumza naye ili mambo haya
yamalizike kwa amani.
Mazungumzo baina ya makundi mawili
Alipowasili mji wa Basra,
Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikwenda moja kwa moja kuonana na Bibi Aisha
(Radhiya Llaahu ‘anha) kwa ajili ya mazungumzo ya kutafuta amani akamwambia:
"Ewe Mama wa Waislamu, kipi kilichokuleta mji huu?
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akasema;
"Kupatanisha baina ya watu".
Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Na wewe Twalha na Zubeir, kipi kilichokuleteni?"
Nao pia wakasema;
"Kupatanisha baina ya watu".
Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Hebu niambieni, mtu vipi anaweza kusuluhisha baina ya
watu?"
Twalha na Al Zubeir wakasema;
"Kwa kulipa kisasi cha kuuliwa kwa Uthmaan kwa kuwauwa
waliomuuwa, kwa sababu tukiwaacha tutakuwa tumekwenda kinyume na mafundisho ya
Qurani."
Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Kwanini hamuukubali udhuru wa Aliy wa kuchelewesha
kuwakamata wauaji hao, wakati mnaelewa kuwa waliomuuwa wanao wafuasi wengi sana, tena kwa maelfu, na
kwamba kitendo cha kuwauwa wauaji hao hivi sasa kitasababisha umwagaji mkubwa
wa damu. Nyinyi wenyewe huko mlikotoka mliwauwa (baadhi ya) wauwaji wa Ali, na
mkajikuta mnapambana na watu wapatao elfu sita wenye silaha, hatimaye mkaamuwa
kuwaacha. Isitoshe, Aliy hakuwasamehe wauaji hao, isipokuwa anasubiri mpaka
pale fursa nzuri itakapopatikana, hapo atawakamata na kuwahukumu. Lakini wakati
huu umma upo katika hali mbaya, watu wanakhitalifiana, na maelfu ya watu
wamejikusanya ili waanzishe vita vikali baina yao. Msitupoteze!, umma utaangamia!"
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akasema;
"Nini rai yako ewe Qaa qaa?"
Al Qaa qaa (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Mimi naona kuwa bora tuyatulize mambo hivi sasa, na
nyinyi mfungamane na Ali, kwani kufungamana kwenu naye ni dalili ya kheri.
Lakini mkikataa na mkaendelea kufanya upinzani, hii itakuwa ni dalili ya shari
na kutoweka kwa ufalme, na mimi naogopa ikiwa mtashikilia kuifuata njia hii ya
shari mtakuja dhurika nyinyi pamoja na sisi. Naogopa Mwenyezi Mungu asije
akatuteremshia ghadhabu yake. Kwa hivyo kuweni funguo za kheri kama ilivyo kawaida yenu, na tusijiingize katika balaa
mpaka ikatusibu. Bora tuyatulize mambo".
Mazungumzo yakaishia hapo na wakakubaliana kuwa Al Qaa qaa
atakuja pamoja na Aliy (RAnhum) mpaka Basra
ili wote wafungamane naye.
Al Qaa qaa akarudi kwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumpa
habari hizi njema zilizoingiza furaha isiyo na kifani ndani ya kifua chake, kwa
kuweza kuikinga damu ya Waislamu isimwagike.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akainuka na kuwahutubia watu na
kuwakumbusha wakati wa ujahilia (kabla ya Uislamu) na upotovu wake na matendo
yake, kisha akazungumza juu ya Uislamu na uongofu wake pamoja na kuongoka kwa
watu wake kwa kuweza kuwafanya wawe kitu kimoja.
Akasema;
"Mwenyezi Mungu ametujumuisha baada ya kufa kwa Mtume
wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam) chini ya uongozi wa Khalifa Abubakar,
kisha baada yake chini ya uongozi wa Khalifa Umar bin Khattab, kisha chini ya
Khalifa Uthmaan, kisha yakatokea haya yaliyotokea ndani ya mwili wa umma.
Watu wanaikimbilia dunia na kuwaonea husda wale Mwenyezi
Mungu aliowaneemesha na kuwapa fadhila alizowapa.Wakataka kuturudisha nyuma,
lakini Mwenyezi Mungu lazima atalifanikisha lile alitakalo".
Kisha akasema;
"Mimi kesho naondoka na sitaki anifuate yeyote kati ya
wale waliosaidia kuuwawa kwa Uthmaan".
Ilipoingia asubuhi, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaondoka
pamoja na maaskari wake kuelekea Basra
kwa ajili ya kukamilisha mazungumzo ya amani. Wakawasili wakati wa usiku, na
kila mtu alilala katika kambi yake kwa furaha wakiingoja siku ya pili yake kwa
hamu kubwa.
Tukio la ngamia
Kambi zote mbili, (kambi ya upande wa Aliy na upande wa
Twalha na Al Zubair wakiongozwa na Bibi Aisha (Radhiya Llahu anhum)) walilala
wakiwa na furaha kubwa sana
usiku huo. Lakini waovu wenye nia mbaya wakiongozwa na Abdillahi bin Sab-a
myahudi, wao hawakuweza kupata usingizi, na usiku kucha walikuwa wakipanga hila
za kuuvunja mkataba huo wa amani ambao ungekamilika wangepata hasara kubwa sana.
Abdillahi bin Saba-a akasema
kuwaambia wenzake walioshiriki katika mauaji ya Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Makubaliano gani haya? Wallahi Aliy anakijua vizuri
zaidi kitabu cha Mwenyezi Mungu kupita hawa wanaodai kuuliwa kwa wauwaji wa Uthmaan.
Keshasema mliyoyasikia, na kesho atakuja kuwajumuisha wote chini ya neno moja
na wote watakuwa dhidi yenu. Mkae mkijua kuwa watu wote hawataki jengine
isipokuwa wanakutakeni nyinyi. Mtakuwa katika hali gani wakati idadi yenu ni
ndogo sana mbele yao?"
Al Ashtar akasema;
"Tulikuwa tukiijua rai ya Twalha na Al Zubair juu yetu
tokea mwanzo. Kilichoaki ilikuwa ni kuijua rai ya Aliy juu yetu. Ama leo baada
ya kuijua rai yake juu yetu, tumehakikisha kuwa mapatano yote haya ni kwa ajili
ya kuimwaga damu yetu. Kwa vile mambo yenyewe yashakuwa hivyo, basi bora
tumsukumize Aliy kule kule tulikomsukumiza Uthmaan".
Abdillahi bin Saba-a
akasema;
"Maneno gani uyasemayo? Tukimuuwa Aliy nasi tutauliwa,
kwani sisi idadi yetu hapa tulipo ni watu elfu mbili na mia tano tu, wakati
watu wa Twalha na Al Zubair pamoja na wenzao, idadi yao ni watu elfu thelathini. Hamna uwezo wa kupambana nao".
Mmoja wao aitwae Ghulab al Haytham akasema;
"Bora tuachane nao na tuondoke twende tukajikalie katika
nchi yoyote ile na tujitowe katika balaa hili".
Abdillahi bin Saba-a myahudi
akasema;
"Maneno gani haya usemayo na wewe. Wallahi tukifanya
hivyo watu watatunyakuwa. Enyi watu! Tumaini letu la pekee ikiwa mnataka kuishi
ni katika kuwagombanisha watu hawa wenyewe kwa wenyewe. Watakapokusanyika usiku
wakati wa kulala, sisi tufanye kila hila ili tuanzishe vita baina yao na wala tusiwape fursa
ya kupatana".
Kabla ya kuingia alfajiri ya siku ile iliyopangiwa kufanya
sulhu, watu wapatao elfu moja kutoka katika kambi ya waasi waliomuuwa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wakiongozwa na Abdillahi bin Saba-a Myahudi wakazivamia kambi za
jeshi la Basra
iliyokuwa ikongozwa na Twalha na Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu), na wengine
wakaivamia kambi ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kuwauwa watu wakiwa wamelala.
Watu wa kambi mbili hizo wakaamka na kukimbilia panga zao na
kuingia vitani moja kwa moja baina yao
wenyewe kwa wenyewe. Kila mmoja akidhania kuwa mwenzake amefanya khiana na
kwamba yale mazungumzo ya kusuluhisha baina yao yalikuwa ni hadaa ya kuwaingilia na
kuwauwa wakiwa wamelala.
Na hivi ndivyo majeshi mawili yalivyokutana katika uwanja wa
vita katika mapambano yaliyokuja kujulikana kwa jina la Mapambano ya ngamia, au
Tukio la ngamia.
Vita vikali sana
vilipiganwa na maelfu ya watu walikufa siku hiyo.
Anasema Dr. Khalid;
"Kila kichwa kinapoanguka au kiungo cha mwili
kinapokatwa, bali kila tone ya damu inapomwagika, moyo wa Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) ulikuwa ukiungua na kuyeyuka. Ingawa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
shujaa na akipenda kupigana vita, hasa pale anapopambana na majeshi ya makafiri
na ya washirikina huku akirudi nyuma na kusonga mbele ndani ya zahma, timko la
vumbi na zogo la sauti za panga na mikuki huku vichwa vya makafiri na
washirikina vikikatwa na kupeperuka huku na kule. Llakini leo hii anayeuwa na
kuuliwa ni wana wa dini moja. Na yeye ndiye Khalifa wao kiongozi wao na mwenye
jukumu juu yao
pamoja na jukumu la damu yote inayomwagika na roho zao zinazotoka mahala hapo.
Nani atakayemliwaza kwa haya yanayotokea? Na nani atakayemsaidia?"
Mwisho wa maneno ya Dr. Khalid
Mapambano baina ya jeshi la upande wa Bibi Aisha (Radhiya
Llaahu ‘anha) lililokuwa na watu wasiopungua elfu thelathini, na jeshi la Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) lililokuwa na watu wasiopungua elfu ishirini, yaliendelea kwa
nguvu sana, na kwa kasi kubwa sana, na maelfu ya watu waliuliwa na kujeruhiwa
siku hiyo.
Sayiduna Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawa anapiga kelele;
"Basi jamani! Basi jamani! Inatosha!"
Lakini hapana aliyekuwa akimsikia.
Kadhi wa Basra
aitwaye Kaab bin Suwaar akasema kumwambia Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha);
"Ewe mama wa Waislamu wadiriki watu! Yaingilie mambo
haya. Huenda Mwenyezi Mungu akajaalia ikapatikana sulhu baina yao kupitia kwako".
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akainuka na kukaa juu ya
hema lililofungwa juu ya ngamia wake, na watu wake wakalizungushia hema hilo ngao. Kisha akainuka
na kutizama huku na kule ili ajaribu kutafuta njia ya kuvisimamisha vita.
Kwa mbali akamuona Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) akiwa
keshamuangusha chini Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu), na Al Zubair (Radhiya Llaahu
‘anhu) huku akiwa ameushika mkuki wake akimuelekezea Ammar (Radhiya Llaahu
‘anhu).
Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawa anamuuliza;
"Ndiyo kweli utaniuwa ewe "Aba Yaqadhan' (umaarufu
wa Al Zubair)?
Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
"La ewe Aba Abdullah (umaarufu wa Ammar),
sitokuuwa".
Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mpiganaji bora na
mwenye nguvu kuliko Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu), lakini alimuacha bila kumuuwa
kwa sababu siku hiyo mtu yeyote asiyekuwa na silaha wala kinga aliachwa bila
kuuliwa, na anayeondoka vitani bila kupigana, naye pia aliachwa aondoke.
Na sababu nyingine ya Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu)
kumuacha Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni kwa sababu Mtume (Swalla Llahu alayhi
wa sallam) aliwahi kusema kumwambia Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu);
"Utakuja kuuliwa na upande wenye makosa".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipoona watu wengi sana wanakufa akamshika mwanawe Al Hassan (Radhiya Llaahu
‘anhu) akamsogeza kifuani pake na akamkumbatia kwa nguvu sana huku akimwambia;
"Ewe mwanangu, laiti babako angekufa miaka ishirini
iliyopita, kabla hakuiona siku hii ya leo".
Al Hassan (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia babake;
"Ewe babangu, si nilikukataza mimi juu ya jambo
hili".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
"Ewe mwanangu, sikutegemea mimi kama
mambo yangefikia kiasi hiki".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipowaona Twalha na Al Zubair (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kwa mbali, akawaita kwa sauti kali sana, na walipomkaribia akawaambia;
"Nakuoneni mmejitayarisha kwa jeshi lenu kubwa sana na farasi wengi sana.
Jee mmekwishautayarisha udhuru wenu pia siku ya kiama? Muogopeni Mola
wenu"
Kisha Aliy akamgeukia Twalha na kumwambia;
"Ewe Twalha! umemuacha mkeo nyumbani kwako na umekuja na
mke wa Mtume wa Mwenyezi Mungu ili upigane pamoja naye?"
Kisha akamgeukia Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumwambia;
"Na wewe Al Zubair, unaikumbuka siku ile ulipopita wewe
na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na mimi nilikuwa
nimesimama katika mtaa wa Bani Saqifa, Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
akacheka na wewe ukacheka pamoja naye, kisha Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akakuuliza;
"Unampenda Aliy ewe Al Zubair?"
Na wewe ukamjibu;
"Bila shaka mimi nampenda".
Kisha Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akakwambia;
"Itakuwaje siku hiyo utakapopigana naye vita ukiwa
unamdhulumu ewe Zubair".
Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) akapiga ukelele huku
akisema;
"Kweli, lo! ndiyo kwanza hivi sasa nimeyakumbuka maneno
haya".
Akautupa upanga wake chini na kuondoka katika uwanja wa vita
huku akilia. Alipokuwa akiondoka huku amemshika farasi wake, alikutana na
mwanawe Abdillahi bin Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyemuuliza;
"Mbona unaondoka ewe babangu?"
Al Zubair akamwambia;
"Naondoka kwa sababu Aliy amenikumbusha maneno aliyowahi
kuniambia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa siku
moja nitakuja kupigana vita na Aliy huku nikiwa namdhulumu".
Mwanawe akamwambia;
"Lakini baba, wewe hukuja kwa nia ya kutaka kupigana
vita, bali umekuja kwa nia ya kupatanisha".
Akasema;
"Nishaapa kuwa sitapigana naye vita".
Twalha na Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakaondoka katika
uwanja wa vita baada ya kusikia waliyoyasikia kutoka kwa Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) na baada ya kujua kuwa Ammar (Radhiya Llaahu ‘anhu) anapigana upande
wake.
Anasema Ibni Kathiyr;
"Al Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliuliwa na mtu mmoja
aitwaye Amr bin Jarmouz aliyemnyemelea wakati wa usiku alipokuwa amelala katika
bonde liitwalo Wadi al Sibaa na kumuuwa. Ama Twalha aliuliwa kwa mshale
usiojulikana umerushwa na nani wakati alipokuwa akiondoka katika uwanja wa
vita. Ingawaje zipo baadhi ya riwaya zinazosema kuwa mshale huo ulirushwa na
Marwan bin Al Hakam (Wallahu aalam)".
Mwisho wa maneno ya Ibni Kathiyr.
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) alipoona vita vinazidi kuwa
vikali, na Al Zubair keshaondoka uwanjani na Twalha keshauliwa, akajikuta
amebaki na jeshi bila ya viongozi, akainuka akiwa juu ya ngamia wake na kumwita
Kaab bin Siwaar - kadhi wa mji wa Basra
na kumtaka abebe msahafu na kuwaita watu wakusanyike chini yake.
Lakini wale waliomuuwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu),
akiwemo Abdillahi bin Saba-a, ambao wengi wao walikuwa msitari wa mbele katika
jeshi la Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), walipomuona Kaab bin Siwaar ameunyanyua
msahafu wakaogopa watu wasije kukusanyika chini yake na hatimaye ikapatikana
sulhu kisha wote wawe dhidi yao.
Wakaanza kumrushia mishale wote kwa pamoja mpaka wakamuuwa.
Na hili si jambo la ajabu kwani tokea mwanzo waasi hawa
walikwisha kubaliana kuwa wasiwape watu fursa ya kupatana.
Baada ya kumuuwa Kaab, wakawa wanaendelea kuivurumisha
mishale yao mahali alipo yule ngamia aliyembeba Bibi Aisha (Radhiya Llaahu
‘anha) kwa matumaini kuwa ngamia akianguka, wao watawahi kupavamia mahali hapo
na kumteka Mama wa Waislamu na kwa njia hiyo vita vitamalizika kama wanavyotaka
wao.
Lakini Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimtaka mwanawe Mohammad
bin Al Hanafiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa amebeba bendera, asonge mbele
kwa nguvu na kutangulia ili awahi kumfikia mama wa Waislamu kabla ya waovu hao
kumfikia. Naye akaichukua bendera hiyo ya babake na kutangulia nayo mbele huku
akitoa amri kwa watu wake kuwa mara watakapomuona ngamia huyo ameanguka wawahi
wao kulifikia hema hilo
na kumhami Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) kabla ya waasi kumfikia na
kumsibu.
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akawa ananyanyua sauti yake
juu huku akiomba dua na kuwalani wauwaji wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
watu wake walikuwa wakiitikia – 'Aamin', huku wauwaji wa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wakiwa wanaendelea kumtupia mishale ngamia wake.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliposikia kelele akauliza;
"Nini hicho?"
Akaambiwa;
"Huyo ni Bibi Aisha anawalani wauaji wa Uthmaan na watu
wake wanaitikia - Amin".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye akanyanyua sauti yake juu
huku akisema;
"Allahuma walaani wauwaji wa Uthmaan ardhini na
baharini".
Vita vikaendela kwa ukali sana, mara kundi hili linatangulia na mara
nyengine linatangulia kundi la pili. Watu wengi wakauliwa, hasa pale penye
ngamia, mpaka majeshi ya upande wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) yalipofanikiwa
kumfikia ngamia huyo ndipo vita vilipomalizikia.
Baada ya kumalizika kwa vita vya Ngamia
Baada ya vita kumalizika, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaomba
ruhusa ya kumuona Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha), akamwendea na kumsalimia,
kisha akamwambia;
"Mwenyezi Mungu akughufirie".
Kisha akamtaka ndugu yake Bibi Aisha, Muhammed bin Abubakar (Radhiya
Llaahu ‘anhu) aliyekuwa upande wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) afuatane naye
mpaka mjini Basra
na kumweka katika nyumba maalum iliyotayarishwa kwa ajili yake.
Kisha Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawageukia watu na
kuwahutubia akiwaambia;
"Atakayekimbia msimfuate, aliyejeruhiwa msimuuwe, mali
zao msizifanye kuwa ngawira, atakayeweka silaha yake chini yu katika amani na
atakayeufunga mlango wake kesha pata amani."
Huyu ndiye Jemadari muungwana wa hali ya juu na mwalimu
anayewafunza watu khulqa njema zinazopasa kuwa baina ya Waislamu katika nyakati
za vita na pia katika nyakati za amani.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliwasili Basra siku ya Jumatatu tarehe kumi mwezi wa
Rajab, mwaka wa Thelathini na sita. Siku hiyo hiyo watu wote wa mji huo wa Basra wakafungamana naye.
Siku ya pili Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akataka ruhusa ya
kuonana tena na Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha), akaomba ruhusa ya kuingia na
baada ya kuingia akamsalimia, kisha Bibi Aisha akasema;
"Hakika juu ya yote haya yaliyotokea, lakini hapakuwa na
chochote na wala hapana chochote baina yangu na baina ya mwanangu huyu Ali, au
sivyo?'
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajibu;
"Ndivyo ewe mama yetu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) kuwa anaweza kuondoka
na kurudi nyumbani kwake Madina wakati wowote apendapo, na akamtaka ndugu yake
Mohammad bin Abubakar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa upande wa Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) afuatane naye mpaka Madina.
Kilichomridhisha Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni kuwa viongozi
wote wa kambi ya pili walikiri kuwa yeye Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ndiye
aliyekuwa upande wa haki.
Twalha, Al Zubair na hata Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha),
wote walikubali kuwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ndiye aliyekuwa upande wa
haki. Na hili ndilo jambo analolipenda Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), kwani yeye
daima alikuwa akipenda awe upande wa haki. Na kauli hii aliitamka pia Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) siku
ile alipomuambia Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu):
"Utakuja kutokea mgogoro baina yako na baina ya
Aisha ".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akauliza;
“Mimi?”
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
akamwambia;
“Ndiyo wewe”.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
“Kwa hivyo mimi ndiye mwenye makosa.”
Mtume (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akamwambia;
“Sivyo, lakini yatakapotokea hayo, basi umrudishe kwake
kwa amani”.
Ahmed na Al Bazzar na Al Tabarani
Ama wewe uliyemuuwa mwana wa Safia, nakubashiria Moto
Baada ya vita kumalizika, Amr bin Jarmouz, yule aliyemuuwa Al
Zubair (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokuwa amelala, alitaka ruhusa ya kuonana na
Aliy bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu), na alipoingia akamkabidhi upanga wa
Al Zubeir kwa kutafakhari akidhani kuwa Khalifa huyo wa Waislamu atampokea
mapokezi ya heshima kama wanavyopokewa
wapiganaji mahodari.
Lakini mara baada ya kuingia, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akamuuliza kwa sauti kali kabisa;
"Huu upanga ulioubeba ni upanga wa Al Zubair?"
Amr akajibu;
"Ndiwo, nimeuteka baada ya kumuuwa".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) akauchukuwa upanga kwa mkono wake
wa kulia, kisha akaushika kwa mikono yake yote miwili, akaunyanyua kwa khushuu
mpaka akufikisha mdomoni pake, akaubusu kwa huzuni nyingi sana huku machozi yakimtiririka, akasema;
"Upanga huu Wallahi mara ngapi mwenyewe ameutumia katika
kumuondolea dhiki Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)."
Kisha akasema kumwambia Amr;
"Ama wewe, ewe uliyemuuwa mwana wa Safia (Al Zubeir),
nakubashiria Moto".
Amr bin Jarmouz akatoka akiwa amekasirika huku akisema;
"Ama nyinyi ni watu wa ajabu kabisa. Namuuwa adui yenu,
kisha mnanibashiria Moto?"
Huo ndio utukufu na uadilifu wa yule aliyelelewa katika
nyumba ya Wahyi, haikubali dhulma hata kama
imetendwa na mtu aliyesimama pamoja naye katika vita.
Vita vya Siffiyn
Vita vya Siffiyn vilivyopiganwa baina ya watu wa Iraqi
wakiongozwa na Sayiduna Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), na upande mwingine watu wa
Sham (Syria) chini ya
uongozi wa Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu) vilikuwa vita vikali sana.. Waislamu waliuwana
wenyewe kwa wenyewe, na athari yake inaendelea mpaka hii leo.
Anasema Ibni Kathiyr katika Al Bidaya wal Nihaaya;
"Hadithi sahihi iliyopokelewa kutoka kwa Imam Ahmed bin
Hanbal inasema kuwa; Ingawaje maelfu kwa maelfu ya Masahaba (Radhiya Llaahu
‘anhu) walikuwa bado wahai wakati vita hivyo vilivyopiganwa, lakini wengi wao
walikataa kushiriki isipokuwa wachache sana na
idadi yao
haizidi watu thelathini.
Hawakushriki katika vita hivi wale Masahaba waliopigana
katika vita vya Badr isipokuwa wawili tu, nao ni Khuzayma bin Thabit na Sahal
bin Hanif (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Hata hivyo wengi wa Masahaba juu ya kutoshiriki kwao lakini
walikiri kuwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ndiye aliyekuwa upande wa haki.
Wakamwendea na kumjulisha hayo, lakini walimtaka msamaha kuwa wao hawatoweza
kushiriki katika vita hivyo vya baina ya Waislamu wenyewe kwa wenyewe.
Ingawaje zipo baadhi ya riwaya zinazoelezea juu ya mamia ya
Masahaba walioshiriki katika vita hivyo, lakini kutokana na tahakiki
niliyoifanya nimegundua kuwa nyingi ya hadithi hizo si sahihi".
(Mwisho wa maneno ya Ibni Kathiyr).
Kanzu ya Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Baada ya kuuliwa kwa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), na ile
kanzu yake iliyojaa damu pamoja na kiganja na vidole vya mkewe Bibi Naila (Radhiya
Llaahu ‘anha) vilivyokatwa na wauwaji hao kuchukuliwa kutoka Madina na
kupelekwa Sham aliko Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu), na Muawiya (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kuviingiza ndani ya msikiti mkuu wa Damascus na kuvitundika juu
ya membari ya msikiti huo na kuwahutubia watu akiwaelezea juu ya ubaya wa
kitendo hicho cha kumuua Khalifa wa Waislamu, huku akilia na watu wakilizana
kwa kwikwi na kuwalani wauaji wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), watu wakawa
wanamiminika kwa maelfu kila siku msikitini hapo huku wakilizana na kudai
kisasi kilipwe kwa haraka sana.
Kwa njia hiyo Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliweza
kukusanya watu wapatao elfu hamsini waliokuwa tayari wakati wowote kuingia
vitani.
Tusisahau kuwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuwa akiwaunga
mkono wauaji hao na alikuwa akiwalani, isipokuwa yeye alikuwa na rai nyingine
juu ya jambo hilo,
na huko nyuma Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliwatuma wanawe wawili pamoja na
baadhi ya Masahaba (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwenda kumlinda Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wakati nyumba yake ilipozungukwa na waasi hao.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) pia hakuwa na nia ya kuwahami
wauaji hao, bali yeye sawa na Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa na nia ya
kuwakamata waasi hao na kuwahukumu kwa uovu wao huo, kwani kuachwa waasi hao
huru bila ya kuhukumiwa ni kwenda kinyume na mafundisho ya Mwenyezi Mungu na ya
Mtume wake (Swalla Llahu alayhi wa sallam). Kutokuchukuliwa hatua sahihi
kutapunguza heba ya dola ya kiislamu ikiongozwa na Khalifa huyo mpya. Lakini
yeye aliiona kuwa wakati mzuri bado haujafika wa kuweza kupambana na waasi hao,
na kwamba ni bora asubiri mpaka wakati huo utakapowadia.
Moja katika sababu kubwa ya kutochukuwa mapema hatua ya
kuwakamata, ni ile idadi kubwa ya waasi hao iliyopindukia elfu sita, na wengi
wao walikuwa wamejipenyeza ndani ya jeshi lake.
Hata wakati mmoja, pale ulipokuja ujumbe kutoka kwa Muawiya
kwa ajili ya kukutana na Aliy kuzungumzia namna ya kulitatua tatizo hilo kwa amani na namna ya kuwakamata waasi hao, watu
wapatao elfu sita na katika riwaya nyingine, idadi yao ilifika watu elfu kumi, walikusanyika nje
ya nyumba ambayo ndani yake mkutano huo ulikuwa ukifanyika, huku wakipiga
kelele wakisema;
"Sisi sote ni wauaji wa Uthmaan, kama
mnaweza basi tuuweni sote !!!".
Isitoshe, Khalifa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuuliwa
kwa njia ya kuviziwa, bali aliuliwa na watu waliouteka mji wa Madina na
kuizunguka nyumba yake kwa muda unaokaribia miezi minne, na wauaji hao hata
wakati huo walikuwa bado wakitamba na kubeba silaha zao.
Ali na Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu), kila mmoja kati yao aliliona tatizo hilo
kwa jicho lake, na alikuwa na fikra zake katika kulitata tatizo hilo.
Wakati Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokuwa akitayarisha
jeshi kubwa kwa ajili ya kupambana na wauaji wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu),
watu wengi walikuwa wakiwasili mji wa Al Kufa kwa ajili ya kufungamana na Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu).
Watu wa Makka na Madina, Misri, Basra na Al Kufa, watu wa Al
Hijaz, Yemen, Oman na watu wa Bahrain na Yamama, wote hao walifungamana na Aliy
(Radhiya Llaahu ‘anhu) isipokuwa Muawiya aliyekuwa Gavana wa Sham (Syria) ndiye
aliyebaki nje ya mfungamano huo akidai kuwa lazima wauaji wa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ambao wengi wao wamo ndani ya jeshi la Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) wakamatwe kwanza na kuhukumiwa, kabla ya kukubali kufungamana naye.
Ikumbukwe kuwa wakati wa uhai wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu),
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakupata kudai haki ya kuwa Khalifa na wala
hakutamka hata mara moja kuwa yeye ndiye anayeustahiki ukhalifa kuliko Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu), bali tatizo lao lilikuwa ni namna ya 'Kulipa kisasi cha wauaji
wa Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)'.
Barua ya Aliy kwa Muawiya
Ili kuepukana na vita vyengine, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alimtuma mjumbe wake aitwaye Jariyr bin Abdullah (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumpa barua aipeleke kwa Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu), na
kusudi la barua hiyo ni kumtaka Muawiya aingie katika kufungamana na Khalifa wa
Waislamu kama walivyofanya magavana wenzake wote, na kuirudisha dola ya
Kiislamu kuwa dola moja kubwa na pia kuuepusha umma na vita vyengine vya
wenyewe kwa wenyewe.
Zipo hadithi nyingi za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) zinazokataza mtu kujitoa nje ya mwili wa umma wa Kiislamu.
Hii ni kwa sababu katika umoja umma unakuwa na nguvu, na kwa mfarakano unakuwa
dhaifu unaomegeka kwa urahisi, na kugeuka kuwa tonge jepesi kwa adui.
Alipowasili Sham, Jariyr alikutana na Muawiya bin Abu Sufyan
na kumkabidhi barua hiyo iliyoandikwa yafuatayo;
"Bisimillahi Rahmani Rahiym,
Amma baad, kwa vile watu wote wamefungamana nami katika mji
wa Madina, basi nawe pia uliyeko huko Sham unalazimika kufungamana nami. Na hii
ni kwa sababu watu waliofungamana nami ni wale wale waliofungamana na Abubakar
na Umar na Uthmaan, kwa hivyo aliyehudhuria fungamanao hilo hana haki ya
kulikataa na asiyehudhuria hana haki ya kulipinga. Kwani kwa hakika Ushauri ni
wa Muhajirin na Ansar (Watu wa Makka na wa Madina), wakikubaliana wote juu ya
mtu na kumchagua kuwa ni Imamu wao. Na Mwenyezi Mungu anaridhika na uchaguzi
huo.
Na yeyote atakayejitenga kwa ajili ya maslahi yake ya
kibinafsi, basi watu watamrudisha kule alikotoka na kumweka juu ya njia iliyo
sawa. Na kama akikataa, basi watu watampiga
vita kwa sababu ya kufuata kwake njia nyengine isiyokuwa ya wenzake.
Twalha na Zubair, hapo mwanzo wote walifungamana nami, kisha
wakajitoa, na kwa ajili hiyo ikanibidi nipambane nao mpaka haki iliporudi na
amri ya Mwenyezi Mungu ikadhihiri. Kwa hivyo nawe ingia na uwe pamoja na
Waislamu, kwani mimi nakupendelea zaidi usalimike, ila kama
wewe mwenyewe unataka upambane na mitihani. Na ikiwa hivyo ndivyo utakavyo,
basi itanibidi nipambane nawe na kumuomba Mwenyezi Mungu anipe ushindi juu
yako.
Umepindukia mipaka katika kuwataka wauaji wa Uthmaan
wakamatwe. Kwa hivyo ingia katika yale waliyoingia Waislamu wenzako ndani yake,
kisha nitakupa wewe jukumu la kuwahukumu wauaji hao kwa kitabu cha Mwenyezi
Mungu.
Ama hayo unayoyataka wewe ni mfano wa kumhadaa mtoto mdogo
ili akubali kunywa maziwa. Wallahi kama utachunguza kwa akili yako utaona kuwa
mimi niko mbali kabisa na damu ya Uthmaan.
Jua kuwa wewe ni katika Tulaqaa, (Tulaqaa ni wale walioinga
katika Uislamu baada ya kutekwa mji wa Makka na Mtume (Swalla Llahu alayhi wa
sallam) akawaacha huru, kisha wao wenyewe wakaingia katika Uislamu), na kwa
ajili hiyo huna haki ya kudai ukhalifa, na wala huna haki ya kutakiwa ushauri
wowote.
Nimemtuma kwako Jariyr, naye ni katika watu wa Imani na watu
waliohajir, kwa hivyo fungamana nami - Walaa quwwata illa billaah!!".
Hii ndiyo barua aliyoituma Aliy kwa Muawiya (Radhiya Llaahu
‘anhu) akimtaka afungamane naye na wakati huo huo akimpa Muawiya fursa ya kuwa
Mwanasheria mkuu na kuisimamia kesi hiyo ya waasi waliomuuwa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ikiwa anataka.
Baada ya kuisoma barua hiyo, Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alimwita Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) pamoja na viongozi wa watu wa
Sham na kuwataka ushauri juu ya jambo hilo,
na wote wakakataa na kusema;
"Sisi hatufungamani na Aliy mpaka kwanza awauwe wauaji
wa Uthmaan au awakamate au atupe sisi tuwauwe wauaji hao. Ama sivyo, sisi tuko
tayari kupambana naye mpaka tutakapowauwa wauaji hao".
Mapambano
Baada ya majibu hayo makali, Muawiya bin Abu Sufiyan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akatoka na jeshi lake kubwa na kuelekea nalo mahali panapoitwa
Siffiyn katika nchi ya Syria, akipitia kando kando ya mto wa Euphrates, kwa
sababu alielewa kuwa hapakuwa na njia nyingine ambayo Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) angeweza kuitumia ili kumfikia isipokuwa hiyo. Na hapo ndipo mahali
mapambano makali yalipotokea baina yao.
Kwa upande mwingine Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye akatoka
na jeshi lake kubwa kutoka mji wa Al Kufa - Iraq, na kuelekea nalo nchi ya Sham
- Syria, lakini yeye alirudi nyuma na
kulitaka jeshi lake litangulie, na akawa anawaambia watu wake;
"Msianzishe vita mpaka waanze wao, na msiwakaribie sana ili kujiepusha na
mapambano. Wakati huo huo msiwe mbali nao sana
hata wakadhani kuwa mnawaogopa, na hata kama
vita vitapiganwa basi kila mara muwaite katika kufungamana".
Jeshi la Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) liliwahi kupafikia
mahali penye chemchem ya maji na kupazunguka, na Majeshi ya Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) yalipowasili na Aliy mwenyewe akiwa bado hajafika, yakajaribu
kuyasogelea maji hayo lakini watu wa Muawiya hawakuwaruhusu kuyakaribia.
Watu wa upande wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakasema;
"Vipi nyinyi, mnatunyima maji na sisi Waislamu
wenzenu?"
Wakajibu;
"Tunakunyimeni ili mupate na nyinyi kuonja utamu wake kama mlivyomnyima Uthmaan maji na kuizunguka nyumba yake
kwa muda wa siku arubaini".
Baada ya majadiliano marefu na mapambano makali kidogo baina yao, wakakubaliana kuwa
majeshi yote yaondoke mahali hapo na yapige kambi mbali na maji hayo na kwamba
kila upande uruhusiwe kuyachota".
Ali bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliwasili mahali
hapo asubuhi ya siku ya tatu baada ya tukio hilo, na mara baada ya kuwasili alisimama
katika msitari wa mbele wa jeshi lake, na Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipomuona, naye pia akasogea na kusimama mbele ya jeshi lake.
Kwa muda mrefu walikabiliana, kisha wakakumbushana kuwa huo
ulikuwa ni mwezi wa Dhul Hijjah, mwezi ambao umeharamishwa kupiganwa vita ndani
yake, na Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akarudisha jeshi lake na
kungoja mwezi mzima.
Baada ya mwezi kumalizika, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
alimtuma tena Bashir (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu)
ili azungumze naye na kujaribu kumfanya akubali sulhu na afungamane naye, na
alipokabiliana naye, Bashir akasema kumwambia Muawiya;
"Ewe Muawiya, dunia inakwenda zake hii, na akhera
inakuja, na Mwenyezi Mungu atakuhesabia amali zako, atakulipa jaza njema kwa
yale mema utakayojitangulizia kwa mikono yako. Mimi nakuomba usimamishe
umwagaji wa damu katika umma huu".
Muawiya akasema;
"Na huyo sahibu yenu umempa usia huu pia?"
Bashir akajibu;
"Sahibu yangu ni kiumbe aliye na haki kupita wote katika
jambo hili. Na hii inatokana na fadhila zake, uchamungu wake, na pia kutokana
na kutangulia kwake kuingia katika dini hii, na kutokana na kuhusiana kwake na
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam), na yeye anakuita
katika kufungamana naye ili upate usalama katika dini yako".
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Na damu ya Uthmaan iwe imemwagika bure? La wallahi
sikubali kamwe".
Mmoja kati ya watu wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajaribu
kumtolea ujeuri Muawiya, na Muawiya akawafukuza wote na kuwataka waondoke na
kurudi walikotoka.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipoona kuwa milango yote ya
amani imekwishafungika na kwamba kwa wakati huu hapana tamaa ya kupatikana
masikilizano. Akaanza kuyapanga majeshi yake na kuwagawa watu wake makundi
mbali mbali na kumweka kiongozi katika kila kundi.
Vita vikaanza kama kawaida kwa mapambano ya mtu mmoja mmoja
na mara nyingine vita vikali vilipiganwa baina yao kisha vikasita na mara nyingine
vilipiganwa vita mara mbili kwa siku kisha vikanyamaza.
Watu wa Sham wanyanyua misahafu
Kabla ya vita hivyo vikali kuanza, Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) kama kawaida yake alitoa amri ifuatayo
kwa watu wake;
"Mnapopigana nao mkawashinda msije mkamuuwa yeyote
anayerudi nyuma wala aliyejeruhiwa. Msimkashifu aliyekufa wala msiwakatekate
maiti, na mtakapoingia mjini msije mkaingia nyumba ya mtu bila ya idhini ya
mwenye nyumba wala msichukuwe chochote katika mali yake".
Majeshi hayo yakakutana mahali hapo panapoitwa Siffiyn, na
kuingia katika mapambano makali na marefu sana,
na damu nyingi sana
ilimwagika hata ardhi yake ikawa haionekani kwa wingi wa maiti na majeruhi.
Anasema Ibni Kathiyr katika Al Bidaya wal Nihaya;
"Ingawaje wanahistoria wamehitalifiana juu ya siku ngapi
vita hivyo vilipiganwa, lakini katika tahakiki yangu, nimeona kuwa siku zote za
Siffiyn ni sabini na saba, Wallahu aalam".
(Ibni Kathiyr hapa anazungumza juu ya siku zote za Siffiyn –
yaani tokea majeshi yalipoanza kujikusanya kabla ya mapambano kuanza hadi
kumalizika kwa mapambano na hatimaye kuanza mazungumzo ya kupatanisha mpaka
kumalizika kwa mazungumzo na majeshi kuanza kutawanyika na kurudi makwao.)
Zipo riwaya zinazosema kuwa vita hivyo vilipiganwa muda wa
siku tatu – mchana na usiku.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akitazama na kuona namna
gani watu walivyokuwa wakianguka baina ya wanaokufa na majeruhi, na mara kasi
ya vita ikiongezeka na mara nyingine kupungua, mpaka alipoamua kumuanidikia
tena barua Muawiya aliyoandika ndani yake maneno yafuatayo;
"Ewe Muawiya, kwa nini unasababisha kuuliwa kwa watu
wote hawa kwa ajili yangu mimi na wewe? Toka tupambane sisi wawili tu! na
atakayeshinda ndiye atakayetawala".
Lakini Muawiya baada ya kushauriana na sahibu yake Amr bin Al
Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa.
Vita vilipokuwa vinapamba moto na watu wa Sham (upande wa
jeshi la Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu)) walipoona namna maelfu ya watu
wanavyopukutika baina ya wanaokufa na wanaojeruhiwa wakakubaliana kuinyanyua
misahafu na kuitundika juu ya panga zao ikiwa ni ishara kuwa vita visimamishwe
na wahukumiane kwa Qurani.
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipoona hivyo akasema kuwaambia
watu wake;
"Enyi waja wa Mwenyezi Mungu, endeleeni kupigana mpaka
haki ipatikane, na wala msihadaike, maana mimi nawajua vizuri Muawiya na Amr
bin al Aaas. Wao hawakufanya hivi isipokuwa baada ya kuhisi kuwa majeshi yao yanakaribia kushindwa.
Hii ni mojawapo ya hadaa zao na mbinu zao za kivita tu. Kwani mimi napigana nao
kwa ajili gani nyingine gheri ya kuwa wao wamekwenda kinyume na kitabu cha
Mwenyezi Mungu?".
Lakini baadhi ya watu wake hawakuwa tayari kumtii,
wakamwambia;
"Ewe Ali, unapoitwa katika kitabu cha Mwenyezi Mungu
itikia, ama sivyo tutakufanyia yale yale tuliyomfanyia Uthmaan bin Affan, kwa
sababu yeye pia alikataa kuitikia alipotakiwa ahukumu kwa kitabu cha Mwenyezi
Mungu na sisi tukamuuwa".
Kisa cha kuhukumu
Vita vikasimamishwa na makubaliano yakafikiwa kuwa
wachaguliwe watu watakaohukumu baina yao, na kwamba kila upande umchague mtu
mmoja atakayeuwakilisha upande wake, na pande zote mbili utalazimika kuukubali
uamuzi utakaofikiwa, na kwamba mazungumzo hayo yahudhuriwe na wakubwa wa
Masahaba waliokuwepo wakati huo.
Upande wa Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakamchagua Amr bin
Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) na upande wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
walimchagua Abu Musa Al Ash ary (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliyejitoa katika vita
hivyo tokea mwanzo baada ya kuwakataza sana
watu wasiingie katika mapambano hayo ya wenyewe kwa wenyewe ambayo mwisho wake
utaleta mtengano baina ya Waislamu. Kwa vile hawakutaka kumsikiliza, akajiuzulu
hata ugavana waliompa na kuuhama mji.
Ali bin Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuridhika
kuchaguliwa kwa Abu Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwani yeye alipendekeza Ibni
Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) auwakilishe upande wake, na hii si kwa sababu Aliy
(Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuwa akimuamini, bali alikuwa akielewa vizuri kuwa Abu
Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni mtu mwema na mchaMungu sana, na alikuwa akijua
kuwa alikuwa akimpenda sana Ali, isipokuwa kwa vile upande wa Muawiya (Radhiya
Llaahu ‘anhu) unawakilishwa na Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu)
anayejulikana sana kwa umahiri wake katika kujadiliana, na uhodari wake wa
kupanga maneno na wepesi wake wa kufikiri na kutoa uamuzi unaosibu. Kwa hivyo
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye akataka upande wake pia uwakilishwe na mtu wa
kadiri yake. Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akijulikana kuwa ni kufu
yake Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu).
Lakini Al Ash'ath bin Qais aliyekuwa upande wa Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alipinga sana jambo hilo na kushikilia kuwa
lazima upande wao uwakilishwe na Abu Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu), ama sivyo
watajitenga naye, na Sayiduna Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kwa ajili ya kuogopa mfarakano akakubali ushauri huo.
Kisa kisichokuwa sahihi
Kuna kisa maarufu ambacho kimezushwa na wasimulizi waongo wa
historia. Uongo huo ni kuhusu mazungumzo yaliyokuwa baina ya Amr bin Al Aas na
Abu Musa Al Ash ary (R.Anhuma).
Kwa sababu mbali mbali kisa hiki kimeweza kupenya na
kuandikwa katika vitabu maarufu vya wanavyuoni wanaojulikana kwa uchaMungu wao kama vile Ibni Kathiyr na wengineo, lakini wamefanya
hivyo bila kukifanyia tahakiki.
Kisa chenyewe kinasema hivi;
"Baada ya Masahaba wawili hao kukubaliana kuwaondoa wote
wawili Aliy na Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) katika ukhalifa, Amr alifanya
khiana aliposimama na kumthibitisha mtu wake ambaye ni Muawiya (Radhiya Llaahu
‘anhu)."
Kisa kinaendelea kusema kuwa:
"Baada ya majadilianao marefu, Amr bin Al Aas na Abu
Musa al Ash'ary walikubaliana wawaondoe Aliy na Muawiya katika uongozi kisha
Waislamu washauriwe na wamchaguwe kiongozi mwingine. Baada ya kukubaliana, watu
wakakusanywa wapate kujulishwa juu ya makubaliano hayo, na Amr akamtaka Abu
Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu) aanze yeye kusema na Abu Musa (Radhiya Llaahu
‘anhu) akaanza kwa kusema;
"Mimi namvua Aliy Ukhalifa kama
ninavyoivua pete yangu hii". Kisha akaivua pete yake, na baada ya hapo Amr
bin al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akainuka na kusema;
"Na mimi pia namvua Aliy ukhalifa kama alivyomvua Abu
Musa na kama ninavyoivua pete yangu hii, lakini mimi namthibitisha Muawiya kuwa
ni Amiri wa Waislamu kama ninavyoithibitisha pete yangu hii".
Kwa vile Amr alikwenda kinyume na makubaliano - kisa hicho
cha uongo kinasema kuwa Abu Musa akaondoka hapo akiwa ameghadhibika na kurudi
Makka badala ya kwenda Al Kufa kwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), na Amr akarudi
Sham."
Tarekh ya Al Tabari 4/51, Al
Bidaya wal Nihaya Juz.7 mlango 'Ulipoingia mwaka wa 37 na Al Kamil fil
Tarikh3/168
Ukweli
Kwanza kabisa lazima ieleweke kuwa sehemu kubwa ya historia ya
Kiislamu imeandikwa mara baada ya kuanguka kwa dola ya Bani Umayya. Na kwa vile
wakati huo yalikuwepo makundi mbali mbali yanayowaunga mkono na mengine
yanayowachukia, pamoja na kundi lengine lililojihusisha na kuandika Historia
bila ya kuchukua jukumu ya kuifanyia tahakiki.
Kwa hivyo, vitabu vya historia ya kiislamu vikajaa
mchanganyiko wa hadithi sahihi na zisizokuwa sahihi, ikawa vigumu sana kuweza kuupata ukweli
mtupu juu ya yale yaliyotokea wakati wa misukosuko hiyo iliyoukumba umma huu.
Hata hivyo baadhi ya maulamaa wameweza kufanya jitihada kubwa
sana na
kufanikiwa kiasi kikubwa katika kuzichambua hadithi hizo na kuzibainisha zile
za kweli na kuziweka mbali na hadithi zisizo za kweli.
Katika kuzifanyia tahakiki riwaya zinazohusiana na kisa hiki
'Kisa cha kuhukumu', maulamaa wa elimu ya hadithi wamegundua kuwa asili yake
kinatokana na mtu anayejulikana kwa jina la Abu Makhnaf na jina lake hasa ni
Luut bin Yahya ambaye riwaya zake za uongo mia tano na themanini na saba
zimenukuliwa na Al Tabari katika kitabu chake cha Tarikh, na riwaya hizi
zinazungumzia juu ya ule wakati mgumu sana kwa Waislamu, kuanzia siku ile
alipofariki Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na
kumalizikia wakati wa ukhalifa wa Yazid bin Muawiya, na huu ndio wakati mgogoro
wa Saqifat Bani Saaida ulipoanza, kisha mgogoro wa Shuura, kisha sababu
zilizowafanya Khawarij wasimame msimamo wao dhidi ya Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) na hatimaye kuuliwa kwake. Hadithi hizo zinazungumzia pia juu ya
ukhalifa wa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), vita vya ‘Al Jamal’, vita vya
‘Siffin’, kisa hiki cha kuhukumu, (Tahkiym), vita vya Naharawan, ukhalifa wa
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu), na kuuliwa kwa Al Hussein (Radhiya Llaahu
‘anhu). Kote huko utazikuta riwaya zilizosimuliwa na Abi Makhnaf huyu, na
wazushi wanazishikilia sana riwaya hizi na
wanazitegemea sana katika kuineza batili yao.
Bila shaka khiyana kama hii haiwezi kutendwa na mtu kama Amr
bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye ni sahibu yake Mtume wa Mwenyezi Mungu
(Swalla Llahu alayhi wa sallam), na vitendo kama
hivi havitendeki isipokuwa katika vikao vya watu waongo na wenye kupenda
kuhadaa watu.
Pili, inajulikana kuwa Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) hakuwa
akipigania ukhalifa wala hakupata kuudai ukhalifa, na wakati huo yeye hakuwa
khalifa wa Waislamu hata aondoshwe au kuthibitishwa kama inavyothibitishwa pete
kidoleni, kama ilivyoelezwa katika riwaya
hiyo. Bali tokea mwanzo matakwa yake yalikuwa
wazi kabisa, nayo ni kulipa kisasi cha kuuwawa kwa Khalifa wa Waislamu Uthmaan
bin Affan (Radhiya Llaahu ‘anhu), na kwamba hatofungamana na Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) mpaka pale atakapochukua hatua ya kuwakamata waasi hao na
kuwafikisha mbele ya mahakama na kuhukumiwa kwa uovu wao huo.
Katika hadithi sahihi iliyosimuliwa na Addaraqutni pamoja na
Khalifa bin Khayyat (huyu ni mwalimu wa Imam Bukhari) juu ya kisa hiki,
wanasema;
"Katika mkutano ule Abu Musa alipendekeza Aliy na
Muawiya wasimamishwe na achaguliwe Abdillahi bin Umar bin Khattab (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kuwa Khalifa wa Waislamu kwa ajili ya heshima aliyonayo mbele ya
Waislamu, pamoja na elimu yake na ucha Mungu wake, na hasa kwa vile tokea
mwanzo alikataa kujiingiza katika mgogoro huu.
Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Kwa nini hatumchaguwi Muawiya?".
Baada ya kukataliwa pendekezo lake
hilo, Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu
‘anhu) akampendekeza Abdillahi bin Amr (mwanawe) aliyekuwa mcha Mungu na
akiheshimiwa sana
na Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) pamoja
na Waislamu wengine.
Abu Musa akamwambia;
"Mwanao ni mwanamume kweli kweli na mcha Mungu, lakini
kwa vile wewe umo ndani ya mgogoro huu, haitawezekana kumchagua yeye
akakubalika. Sikiliza ewe Amr! Waislamu wametubebesha sisi jukumu hili baada ya
kushindwa kulimaliza kwa panga zao na mikuki, kwa hivyo usizidi kuwaingiza
katika mitihani mingine".
Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Sasa wewe unaonaje?"
Abu Musa akasema;
'Mimi naona bora tuwaondoe wote wawili na tuwaachie uamuzi
Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) wamchaguwe
wanayemuona kuwa anafaa katika jambo hili".
Amr (Radhiya Llaahu ‘anhu) akauliza;
'Mimi na Muawiya tutakuwa na msimamo gani?'
Abu Musa akasema;
"Mkihitajiwa mtaitwa, la ikiwa hamkuhitajiwa nyinyi
hamtakuwa watu wa mwanzo wasiohitajiwa".
Wakakubaliana kuwaachia uamuzi Masahaba wakubwa kulitatua
tatizo hili kwa kumchagua yule wanayemuona kuwa ndiye anayefaa.
Walikubaliana pia kuwa, kwa wakati ule mambo yabaki kama
yalivyo, Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye alichaguliwa kuwa Khalifa baada ya
watu wote kufungamana naye abaki katika utawala wake, na Muawiya (Radhiya
Llaahu ‘anhu) abaki na ugavana wake huko Sham mpaka pale Masahaba
waliochaguliwa na wajumbe hao wawili watakapofikia uamuzi juu ya Khalifa mpya
wa Waislamu.
Abu Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa mtu mwenye hekima
kubwa sana,
kwani aliona kuwa mambo yamekwishapindukia mpaka, na kwamba maelfu ya Waislamu
wanakufa kila siku katika vita hivi. Alikuwa akielewa kuwa si sawa kuiangusha
haki iliyochaguliwa kisheria kwa ajili ya kuwaridhisha watu wanaopigana, lakini
wakati huo huo aliona kuwa hitilafu baina ya Aliy na Muawiya (Radhiya Llaahu
‘anhu) na mapambano baina ya watu wa Iraq na watu wa Sham yalifikia
daraja mbaya kiasi ambacho hapana budi watu wabadilishe fikra zao katika
kulitatua tatizo hili.
Abu Musa (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliona pia kuwa madai ya
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) hayakuwa madai ya kawaida, na hitilafu iliyopo
baina ya Waislamu haikuwa hitilafu ya kawaida, bali yote yaligeuka kuwa ni vita
vikali sana vya
wenyewe kwa wenyewe vilivyopoteza maelfu ya roho za Waislamu na wakati huo huo
hatari ya kuweza kupotea kwa maelfu ya roho nyengine za Wasilam ingalipo.
Akaona kuwa njia ya pekee inayoweza kusimamisha vita hivyo
kwa wakati huo ni kuwaondoa wale waliohusika na mgogoro huo katika mamlaka yao ikiwa kama ni chanzo
bora cha kusimamisha vita hivyo.
Ikiwa uamuzi wake wa pili wa kuwataka Masahaba (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wamchaguwe yule wanayemwona kuwa atafaa kuwaongoza Waislamu
katika wakati huo mgumu haukutimizwa, na hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya
haraka sana
yaliyotokea, basi wa kulaumiwa si Amr wala si Abu Musa (Radhiya Llahu anhum).
Walihudhuria mazungumzo hayo pia Masahaba wakubwa kama vile, Abdillahi bin Omar, Abdillahi bin Abbas,
Abdillahi bin Zubair, Al Mughiyra bin Shuuba na wengineo (RAnhum).
Kisa kama hiki pia kimeelezwa
katika Tarikh ya Bukhari kama alivyoelezea Sheikh Uthmaan Al Khamis katika
'Huqbah mina Tariykh – uk.84'.
Baada ya makubaliano
Haujapita muda mrefu baada ya makubaliano hayo baina ya Abu
Musa na Amr (Radhiya Llaahu ‘anhu), zikasikika sauti kutoka kwenye kambi ya
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) zikisema;
"Tulikosea tulipokubali kuhukumiwa na watu, na sasa
tunarudia tena makosa yetu yale yale. Hatukubali kuhukumiwa isipokuwa kwa
kitabu cha Mwenyezi Mungu".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye tokea mwanzo
alikwishawaonya watu wake kuwa madai ya upande wa Muawiya (Radhiya Llaahu
‘anhu) ya kutaka kuhukumu kwa Qurani yalikuwa ni katika hadaa na mbinu za
kivita akawajibu watu wake kwa kuwaambia;
"Sasa hivi tena baada ya kutoa ahadi zetu na baada ya
makubaliano ndiyo mnasema maneno haya?".
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliondoka hapo akiwa pamoja na
watu wachache aliobaki nao na kuelekea mje wa Al Kufa.
Wengi kati ya wafuasi wake walijitenga naye kwa hoja kuwa eti
alikubali kuhukumiwa na watu badala ya kuhukumiwa na kitabu cha Mwenyezi Mungu,
na wengine waliamua kujitenga kwa kuchoshwa tu na vita virefu visivyokwisha
Inasemekana kuwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alijikuta
amebakiwa na watu wasiozidi elfu kumi na sita, na riwaya nyingine zinasema kuwa
alibakiwa na watu wapatao elfu kumi na mbili na nyengine zinasema kuwa
waliobaki walikuwa wachache zaidi kuliko idadi hiyo.
Kuanzia hapo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawa anakabiliwa na
makundi mawili - Moja lipo Sham likidai kisasi cha kuuliwa kwa Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu), na kundi la pili lipo Iraq,
limepiga kambi katika mji unaoitwa Naharawan, ulio kando kando ya mto Tigris. Kundi hili lilipewa jina la Khawarij, na kundi hilo lilikuwa likimlaumu
Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa kukubali kwake kuhukumiwa na watu badala ya
kuhukumiwa kwa sheria ya Mwenyezi Mungu
Walikuwa wakisema;
"Hapana hukmu isipokuwa ile ya Mwenyezi Mungu".
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alimuomba Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) amkubalie ende kujadiliana na watu hao, Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu) akasema;
"Mimi nakuogopea."
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Hapana hofu yoyote Inshaallah".
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipowaendea akawakuta kuwa
ni watu wenye kufanya ibada sana,
na walipomuona wakamwambia;
"Karibu ewe Ibni Abbas, kipi kilichokuleta?"
Akasema;
"Nimekuja kuzungumza nanyi".
Wengine kati yao
wakasema;
"Msizungumze naye".
Wengine wakamwambia;
"Sema tutakusikiliza".
Akasema;
"Hebu niambieni, mnamlaumu kwa makosa gani Aliy bin Ammi
yake Mtume wa Mwenyezi Mungu, mume wa mwanawe na wa mwanzo kumuamini?"
Wakasema;
"Mambo matatu".
"Yepi hayo?"
Wakasema;
"La mwanzo ni kukubali kwake kufuata hukmu ya wanadamu
katika dini ya Mwenyezi Mungu. La pili, amepigana vita na Aisha na Muawiya bila
kuchukuwa ngawira wala kuwateka, na la tatu amekubali kujiondolea mwenyewe cheo
chake cha Ukhalifa juu ya kuwa Waislamu wamefungamana naye na kumkubali kuwa
yeye ni Khalifa wao".
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawauliza;
"Mnaonaje nikikupeni dalili kutoka katika kitabu cha
Mwenyezi Mungu na kutoka katika mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llahu alayhi wa sallam) juu ya haya mnayomlaumu, mtarudi kwake na kuyaacha haya
mliyo ndani yake?"
Wakasema;
"Ndiyo".
Akasema;
"Ama ile kauli yenu katika kumlaumu kukubali kwake
kuhukumiwa na watu katika dini ya Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu anasema;
"Enyi mlioamini! Msiuwe mawindo na hali mumo katika Hija
au Umra. Na miongoni mwenu atakayemuua kwa kusudi, basi malipo yake yatakuwa
kwa (kuchinja) kilicho sawa na alichokiuwa katika wanyama wanaofugwa, kama watakavyohukumu waadilifu wawili miongoni
mwenu."
Al Maidah - 95
Semeni ukweli wenu, hivyo kuhukumiwa na wanadamu katika
kusimamisha umwagaji wa damu na kupoteza nafsi zenu na kupatanisha baina yenu
ni bora au kuhukumiwa na wanadamu juu ya sungura (aliyeuliwa na mtu anayehiji)
ambaye thamani yake ni sawa na robo dirham?"
Wakasema;
"Bali katika
kusimamisha umwagaji wa damu na kupatanisha baina ya watu".
Akasema;
"Hilo
tushalimaliza?'
Wakasema;
"Ndiyo".
Akasema;
"Ama ile kauli yenu kuwa Aliy alipigana vita na
hakuwateka ngawira wanawake kama vile Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alivyofanya. Kweni nyinyi
mlikuwa mkitaka amteke ngawira Mama yenu Bibi Aisha na awe halali kwenu kama wanavyohalalishwa wanawake wanaotekwa katika vita?
Mkijibu 'ndiyo', mtakuwa mumekufuru, na mkisema kuwa yeye si mama yenu, pia
mtakuwa mumekufuru, kwa sababu Mwenyezi Mungu anasema;
"Na wakeze ni mama zao"
Ahzab - 6
Kwa hivyo jichagulieni mnachotaka".
Wakasema;
"Na hili pia tushalimaliza".
Ibni Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Ama kauli yenu kuwa Aliy alijifutia mwenyewe cheo chake
cha Ukhalifa, hata Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
alifanya hivyo siku ya mapatano ya Hudaibia, pale washirikina walipomtaka
aandike mkataba, na yeye akaandika; "Haya ni makubaliano baina ya Muhammad
Mtume wa Mwenyezi Mungu." Na makafiri wakasema; "Tungelikuwa
tunaamini kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, tusingelikuzuwia kwenda kutufu
Al Kaaba, na wala tusingekupiga vita, lakini andika;
"Muhammd bin Abdillah". Na Mtume (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) akalikubali sharti lao huku akisema;
"Wallahi mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu hata
mkinikadhibisha".
Wakasema;
"Na hili pia nalo tushalimaliza.
Ikawa katika matunda ya majadiliano hayo yenye hoja zilizo
wazi, watu wapatao elfu tano walirudi katika kambi ya Aliy bin Abu Talib (Radhiya
Llaahu ‘anhu) na riwaya nyingine zinasema kuwa idadi kubwa kuliko hiyo
walirudi.
Vita vya Nahrawan
Baada ya wengi kati ya wale waliojitenga na jeshi la Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kutambua makosa yao na kurudi
katika kambi ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu), waliobaki katika kundi la Khawarij
wakaondoka na kupiga kambi mahali panapoitwa Nahrawan, mji uliopo kando kando
ya mto Tigris, na huko wakawa wanafanya zogo
na kuingia misikitini huku wakipiga kelele wakisema; "Hatukubali
kuhukumiwa isipokuwa na Mwenyezi Mungu."
Aliposikia kauli hiyo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alisema;
"Ni kauli ya haki hiyo lakini (wanaitamka) kwa ajili ya kutaka kuipitisha
batili yao."
Anasema Imam Ahmed bin Hanbal:
Nimehadithiwa na Is'haq bin Issa al Taba'a aliyehadithiwa na
Yahya bin Suleyam kutoka kwa Abdullah bin Uthmaan bin Khaytham kutoka kwa
Ubeidullah bin Iyadh bin Amr al Qariy kuwa amesema; "Abdullahi bin Shaddad
alikuja kwa Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) wakati sisi tupo kwake tumekaa na
wakati huo alikuwa anarudi kutoka Iraq katika siku za kuuliwa kwa Ali, na bibi
Aisha akamwambia; "Ewe Abdullah bin Shaddad utanielezea ukweli kwa
nitakayokuuliza? Nihadithie juu ya hawa waliomuua Ali" Abdulah akasema;
"Na kwa nini nisikuelezee ukweli." Akasema; "Haya nihadithie juu
ya kisa chao."
Akasema; "Hakika Aliy alipokubali mkataba na Muawiya na
waamuzi wawili walipotoa uamuzi wao, wakajitoa kutoka katika jeshi lake watu
elfu nane miongoni mwa wasomi na kuelekea mahali panapoitwa Hururaa pembezoni
mwa mji wa Al Kufa huku wakimwambia; "Umejivua nguo aliyokuvisha Mwenyezi
Mungu na (umelikataa) jina alilokupa Mwenyezi Mungu kisha ukakubali hukmu ya watu katika dini ya
Mwenyezi Mungu wakati hapana hukmu isipokuwa ya Mwenyezi Mungu."
Zilipomfikia habari hizo Aliy akaamrisha patangazwe kuwa kila
mtu aje kwake akiwa amebeba msahafu. Na nyumba ilipojaa watu
wenye elimu zao Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akataka aletewe msahafu. Akauweka
mbele yake na kuushika huku akiuambia; "Ew msahafu! Zungumza na
watu!"
Watu wakamwambia; "Ewe Amiri wa Waislamu unazungumza na
nani? Hizi ni karatasi na uwino tu, sisi ndio tunaozungumza kama
kitabu kinavyotutaka, unataka nini?"
Akasema; "Sahibu zenu hawa waliojitenga, baina yangu na
wao kitabu cha Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu katika kitabu chake anasema;
"Na kama mkijua
kuwa kuna ugomvi baina ya mke na mume basi pelekeni mwamuzi mmoja katika jamaa
za mwanamume na mmoja katika jamaa za mwanamke. Kama
wakitaka mapatano Mwenyezi Mungu atawawezesha."
Annisaa 35
Na damu ya umati wa Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam)
ni adhimu zaidi na tukufu zaidi kupita ugomvi baina ya mume na mke. Kisha
wananilaumu kuwa nimekubali kama alivyotaka Muawiya kuliandika jina langu Aliy bin
Abu Talib (bila kuandika kuwa mimi ni Khalifa wa Waislamu), wakati Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikubali katika sulhu ya
Hudaibia kuliandika jina lake
Muhammad bin Abdillah
bila ya kuandika Muhammad Rasulullah kwa ajili ya kutaka sulhu."
Na hapo ndipo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipokubali Ibni
Abbas (Radhiya Llaahu ‘anhu) awaendee waliojitenga naye na wakatubu waliotubu
na kurudi katika jeshi la Ali."
Bibi Aisha (Radhiya Llaahu ‘anha) akaendelea kumuuliza
Abdulla bin Shaddad; "Kisha Aliy akapigana vita nao?"
Akasema;"Ndiyo wallahi, na Aliy akawashinda, na ndani ya
kundi hilo alikuwemo Dhu Thadiy, na ikawa kama alivyosema Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kuwa; wakati Waislamu watakapokhitalifiana
(wakawa makundi mawili) litatokea kundi la tatu litakalopigwa vita na kundi la
haki baina ya mawili hayo, na ndani ya kundi hilo (la tatu) atakuwemo Dhu
Thadiy. Na vita vilipomalizika Aliy akawa anatafuta baina ya waliouliwa mpaka
alipomuona Thu Thadiy ndipo aliposujudu kumshukuru Mwenyezi Mungu maana
alielewa kuwa yupo upande wa haki."
Muslim
- mlango wa Zaka juu ya kundi hilo. Imam Ahmed -
katika Musnad ya Aliy bin Abu Talib, na hadithi hii imefanyiwa tahakiki
na Ahmed Shakir na akasema kuwa ni hadithi sahihi.
Vita vilianza baada ya habari nyingi kumfikia Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) juu ya mauaji ya kila siku yanayofanywa na watu hao na Aliy bin
Abu Talib (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaamua kuwafuata huko na kuwapiga vita.
Walimuuwa sahaba mcha Mungu aitwaye Abdullahi bin Khubab (Radhiya
Llaahu ‘anhu), kisha wakamuua mkewe na kumkatakata tumbo lake na
wakati huo alikuwa na mimba, na Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipotuma ujumbe
kutaka kujua nani aliyemuuwa wakajibu;
"Sote tumemuua!"
Hapo ndipo Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipoamua kupeleka
majeshi yake na kuwashambulia watu hao na kuwashinda katika vita hivyo
vilivyokuja kujulikana kwa jina la 'Vita vya Naharawan'.
Hata hivyo uasi na mapambano marefu ya chini kwa chini baina yao yaliendelea muda mrefu sana na hatimaye Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
akauliwa.
Kuuliwa kwa Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Ali (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliuliwa wakati wa alfajiri baada
ya kupita kiasi cha miaka miwili tokea vita vya Nahrawan kumalizika alipokuwa
katika jukumu lake la kila siku la kuwaamsha watu Sala ya alfajiri. Akastukia
akishambuliwa na mtu aliyekuwa katika kundi la Khawarij aitwaye Abdurahman bin
Muljim al Muradiy huku akimchoma kwa panga na visu vilivyojazwa sumu.
Aliuliwa alipokuwa akisema kwa sauti kubwa;
"Assalaatu enyi watu, amkeni Mungu akurehemuni".
Muuaji huyo alikuwa keshapangana na wenzake wawili, Breik bin
Abdullah Al Tamimi na Amr bin Bakar Al Tamimi. Mmoja aende Sham na kumuuwa
Muawiya na mwengine aende Misri na kumuuwa Amr bin Al Aas (RAnhum) kwa mpigo
mmoja katika siku moja na wakati mmoja waliokubaliana baina yao,
ili wawapumzishe watu na matatizo yao.
Wakakubaliana wote kuwa watimize ukatili wao huo siku ya
Ijumaa, Ramadhani ya kumi na saba, mwaka wa arubaini baada ya Hijra
Sayiduna Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa na kawaida ya
kutoka peke yake bila ya ulinzi kabla ya Sala ya alfajiri kwa ajili ya kuwaamsha watu, na kwa ajili hiyo ilikuwa
rahisi kwa muuaji wake kumshambulia kwa upanga wake alioulaza ndani ya sumu kwa
muda wa mwezi mzima.
Ama Breik, aliyekwenda kumuuwa Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu),
alimkosea na kumjeruhi pajani, na watu wa Muawiya waliwahi kumkamata mtu huyo,
na alipokamatwa alisema;
"Usuniuwe ewe Muawiya, maana nataka kukupa habari
njema".
Muawiya akamuuliza;
"Habari gani hizo?"
Akasema;
"Mwenzangu tuliyepangana naye keshamuuwa Aliy bin Abu
Talib siku hii ya leo".
Muawiya akamuuliza;
"Unajuaje pengine naye pia hakufanikiwa?"
Akasema;
"Lazima atafanikiwa kwa sababu Aliy hatoki na walinzi kama wewe".
Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaamrisha auliwe, akauliwa.
Amr bin Al Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) naye siku hiyo kwa
bahati alishikwa na tumbo la kuharisha akachelewa kutoka, na badala yake
akatoka mmoja katika majemadari wa jeshi lake aitwaye Kharija bin Abi Hubaibah,
na yule aliyepewa jukumu la kumuuwa Amr ambaye jina lake pia ni Amr bin Bakar
alimshambulia Kharija na kumuuwa akidhania kuwa ndiye aliyemkusudia.
Maziko yake
Alipokuwa akianguka baada ya kupigwa panga na visu, Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alisema;
"Mkamateni na msimuache. Nikifa naye auliwe bila ya
kukatwa katwa, ama nikiishi basi mimi mwenyewe nitaamuwa ikiwa nimuuwe au
nimsamehe".
Baada ya kufariki dunia, watoto wake wakamuuwa Abdurahman bin
Muljim.
Maiti ya Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) ilisaliwa na mwanawe mkubwa
Al Hassan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kisha akazikwa katika nyumba iitwayo Dar al
Imara katika mji huo huo wa Al Kufa.
Ama ile hadithi mashuhuri isemayo kuwa eti maiti yake
ilipakiwa juu ya mnyama na kuachwa iende isikojulikana, hadithi hiyo si sahihi,
na jambo hilo
haliwezekani kufanywa na Masahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu
alayhi wa sallam) waliofundishwa na Mtume wao
namna ya kuzika maiti wao.