Abdullah ibn Masoud- mtaalamu wa Quraan



Abdullah ibn Masoud- mtaalamu wa Quraan
 
Tokea utotoni kwake alikuwa ni mtu wa milimani akichunga wanyama wa mmoja wa watukufu wa kiquraysh Uqbah ibn Muayt.  Watu walikuwa wakimwita Ibn Umm Abd wakimaanisha mtoto wa kijakazi.
 
Mtoto huyu akasikia habari za Mtume (SAW) ila hakuzitilia maanani.   Habari hizi kwani alikuwa bado mdogo na mara nyingi kuwa mbali ya jamii ya Makka. Na kawaida yake ilikuwa kutoka mapema asubuhi na harudi ila pale kiza kimeingia.
 
Siku moja, huku akiendelea na kuchunga wanyama wake, akawaona watu wawili kwa mbali  wakija upande wake.  Walionekana kuwa watu wazima na wenye heshima zao na kuwa na kila dalili za uchofu wa safari. Walikuwa na kiu pia kwani koo zao na midomo ilikuwa imekauka. Walikuja na kumsalimia na kusema:
“Kijana, tukamie mmoja wa hawa kondoo tupate kuondosha kiu zetu na kurudisha nguvu mwilini.”
“Siwezi, kondoo si wangu mimi nimekabidhiwa niwachunge tu, aliwajibu.
 
Wale watu hawakubishana nao na licha ya kuwa na kiu, walionesha tabasamu kwa ukweli waliousikia.
 
Hawa watu wawili si wengine bali ni Mtume (SAW) na Sahiba wake Abubakar (RA).  Siku hiyo walikimbilia milimani kuepukana na mateso na madhila ya maquraysh wa Makka.  Kijana naye pia alivutiwa na Mtume (SAW) pamoja na sahiba wake na akawa karibu nao sana.
 
Haukupita muda Abdullah alisilimu na kuomba kumwambata na  kumhudumia Mtume (SAW).  Mtume akakubali na tokea siku hiyo akaachana na kuchunga na kuanza  kumwambata na kumhudumia Mtume (SAW).
 
Abdullah alikuwa karibu sana na Mtume Muhammad (SAW) na alimshughulikia kwa shida zake ndani na nje ya nyumba yake, alifuatana naye safari zake za kawaida na vita.  Humwamsha anapolala na kumtengenezea pazia akioga na kumbebea vitu vyake kama mswaki na kadhalika.
 
Kwa kuwa karibu sana na Mtume (SAW), Abdullah alibahatika kusoma na kuiga tabia zake Al-Habib na alizifuata zote mpaka kuambiwa, alikuwa karibu kumfikia Mtume Muhammad (SAW) kitabia.
 
Abdullah alifundishwa kutoka madrassah ya Mtume (SAW) mwenyewe alikuwa msomaji mahiri wa Quran miongoni mwa masahaba. Aliifahamu vizuri zaidi Quran.  Moja kwa moja akawa mtaalam wa sheria ya kiislam. Mfano mzuri ni pale mtu mmoja alipokuja kwa Khalifa Umar ibn Khattab (RA) huku amesimama kwenye uwanja wa Arafa na kusema:
“Ewe Amirul muuminiin, nimekuja kutoka Kuffah ambapo nimemuacha mtu anaandika Quran kutoka kwenye hifadhi za watu.”
 
Umar alikasirika sana na hapo hapo kuuliza kwa ghadhabu, “ni nani huyo?”
 
“Abdullah ibn Masoud” akajibu.
 
Ghafla hasira zote za Umar zikaondoka.
 
Akaendelea kusema, “wallahi, simjui mtu mwengine aliebaki mwenye sifa za kuifanya kazi hii zaidi yake.Ngojea nikuhadithie”, Umar aliendelea:
 
“Usiku mmoja Mtume Muhammad (SAW) alikuwa na mazungumzo na Abubakar (RA) kuhusu hali ya waislam, mimi nilikuwepo.  Mtume (SAW) alipoondoka tukafuatana naye na tulipokuwa tunapita msikitini, kulikuwa na mtu amesimama akiwa katika sala ambaye hatukumwona vizuri.  Mtume (SAW) alisimama na kumsikiliza kisha akatugeukia na kusema, “yoyote anayetaka kusoma Quran ikiwa safi kama ilivyoteremeshwa basi asome kwa kisomo cha Ibn Umm Abd.”
 
Abdullah alipomaliza sala na huku amekaa akiomba dua, Mtume anasema, “Omba na utapewa”, (akikusudia dua ya Abdullah.)
 
Umar aliendelea, “Nikajisemea kwenye nafsi yangu nitakwenda moja kwa moja kwa Abdullah na kumpa habari njema za kumhakikishia kukubaliwa kwa dua zake.  Nilipofika nikamkuta tayari Abubakar ameshaniwahi!. Wallahi sijawahi kumpiku Abubakar katika kufanya jambo lolote la kheri.”
 
Abdullah alijaaliwa elimu na Quran mpaka mwenyewe kusema, Nnaapa kwa yule ambao hakuna Mungu mwengine isipokuwa yeye, hakuna aya katika kitabu cha Mwenyezi Mungu (SW) iliyoteremka ila mimi kuijua wapi imeteremshwa na katika mazingira gani, Wallahi kama mnajua mtu mwengine anayekijua kitabu cha Allah (SW) zaidi yangu, ningelifanya kila lililo ndani ya uwezo wangu kuwa karibu naye”
 
Abdullah hakuwa akitia chumvi wala kujisifu kwa usemi wake huu, mara moja Umar alikutana na msafara na ilikuwa usiku na ule msafara haukuonekana vizuri kwa giza nene lililotanda. Umar akaamrisha mmoja wao kwenda kuwasalimia, Umar akauliza:
 
“Mnatoka wapi?
 
“Fajjun Amiiq, (bonde kuu),” akajibiwa.
 
“Mnaelekea wapi?”
 
“Baytul Atiq (nyumba ya kale),” akajibiwa.
 
“Lazima kuna alim -msomi- miongoni mwenu” Umar akasema.
 
Umar akamuagiza mmoja katika wale amuulize.
 
“Ipi  ni sehemu adhimu katika Quran?”
 
“Allah, hakuna mwengine isipokuwa yeye, aliyehai, na kujitosheleza, halali, wala kuchukuliwa na usingizi….” akajibiwa na hii ni aayatul kursiy.
 
“Ni sehemu ipi katika    Quran iliyo wazi kabisa kuhusu uadilifu?”
 
“Mwenyezi Mungu (SW) anakuamrisheni uadilifu na kufanya ihsan, na kuwalisha jamaa wa karibu……………..” ,akajibiwa.
 
“Ni maelezo gani katika Quran yaliyoelezwa kwa upambanuzi yakinifu?”
 “Yoyote atakayefanya jambo kiasi cha uzito wa chembe ya ngano, likiwa zuri  ataliona na yoyote atakayefanya jambo kiasi cha uzito wa chembe ya ngano, likiwa la shari ataliona.” 
“Sehemu gani ya Quran inaongeza ari ya kuwa  na matarajio makuu?”
 
“Sema ewe Muhammad, enyi waja wangu mliopoteza rasilmali zenu, msikate tamaa kwa rehma za Mwenyezi Mungu (SW). Hakika Allah (SW) anasemehe madhambi yote…………..”
 
Kufika hapo Umar akauliza:
 
“Mko na Abdullah ibn Masoud?”
 
“Wallahi, naam.”
 
Sifa za Abdullah ibn Masoud hazikuwa katika usomaji Quran bali alikuwa mchangamfu, pia mpiganaji hodari na shujaa hasa pale inapohitajika.
 
Siku moja, masahaba walikuwa pamoja Makka wakiwa bado wachache na kutokuwa na nguvu yoyote na wakaambizana, “maquraysh hawajawahi kuisikia Quran ikisomwa hadharani na kwa sauti kubwa, nani atathubutu kuwasomea?”
 
Abdullah akajitolea, “mimi nitawasomea”
“Tunakuhofia maisha yako” wakamwambia.
“Tunataka mtu mweye nasaba ya kuweza kumkinga na ghadhabu zao”
Abdullah bado akawa anasisitiza, “niacheni, Allah (SW) atanilinda na kuniepusha na yale yote maovu watakayoyakusudia”
Akaenda Al-Kaaba mpaka alipofikia ‘Maqaam Ibrahim’, Abdullah akaanza kusoma:
 
“Bismillahi Rrahmanir Rahiim, Ar Rahmaan, Allamal Quraan.  Khalaqal Insaan.  Allamahul bayaan………..”
 
(Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwenye kuneemesha neema kubwa kubwa na mwenye kuneemesha neema ndogo ndogo.  Nnaapa kwa mola mwenye kurehemu.  Ambaye amefundisha Quran.  Akamuumba Binadamu.  Akafundisha kuweza kubaini ‘haki na batil’ ……..
 
Aliendelea kusoma huku maquraysh wametulia wakimsikiliza mpaka baadhi yao kuuliza:
“Nini unasema Ibn Umm Abd?”
Walipokuja kugutuka, “du! anasoma baadhi ya maneno aliyokuja nayo Muhammad.”
 
Wakamvamia na kuanza kumpiga usoni huku akiendelea kusoma.   Aliporudi kwa wenzake na kuona jinsi uso wake ulivyoharibika na kuvuja damu wakamwambia, “haya ndio tuliyokuowa tukiyahofia.”
 
“Wallahi, maadui wa Mwenyezi Mungu, sasa hivi hawana raha hata kidogo tena zaidi yangu na kama mkitaka, kesho nitakwenda tena kuwasomea.” Abdullah aliwaambia.
“Uliyofanya yametosha, tayari umeshawafanya wasikilize yale wasiyoyapenda Abdullah,”
 
Abdullah ibn Masoud aliishi hadi enzi za ukhalifa wa Uthman (RA).  Alipougua na kuwa taabani kitandani alitembelewa na Khalifa:
 
“Unaumwa na nini?”
 
“Dhambi zangu,” Abdullah alijibu.
 
“Na nini unatamani?”
 
“Rehma za mola wangu”
 
“Hutaki nikupe ruzuku, ambayo umeikataa kwa miaka sasa hivi.” Aliulizwa Abdullah.
 
Abdullah alijibu, “sina haja nayo.”
 
“Itabaki na kuwasaidia mabinti zako baada yako”
 
“Hivi kweli unahofia umasikini wa wanangu, nimewaamrisha wasome Suratul Waqiah kila usiku kwani nilimsikia Mtume Muhammad (SAW) akisema, “atakae soma Suratul waqiah kila siku usiku, hatopatwa na balaa la umasikini maishani kwake.”
 
Usiku huo Abdullah, aliiaga dunia kuelekea kwa Mola wake, ulimi wake ukiwa bado na unyenyekevu kwa kumkumbuka Allah (SW) na kwa kukisoma kitabu chake Quraan.