Mipaka ya Allah Inavyokiukwa: Kumtundika Mke



Abu Ammaar

Heshima ambayo Allah Subhaanahu Wata’ala amempa mume katika ndoa ni kumkabidhi haki ya talaka kuwa mikononi mwake pekee bila ya kumshirikisha mke ambae wameoana katika ndoa halali ambapo kila mmoja angekuwa na haki sawa.
Heshima hii ingawa amepewa mume pekee lakini na mke pia ana haki ya kuitekeleza endapo mume atakubali katika masharti ya ziada katika ndoa (prenuptials) kwamba na mke nae anayo haki ya kumuacha mumewe kwa kutumia talaka. Vyenginevyo mke hupaswa kutumia njia nyengine kama kuomba kuachwa, Khul’u au kupitia kwa Kadhi.
Sababu za kimsingi kupewa mume heshima hii ni kama zifuatazo:
1              Mke mara nyingi hukosa uvumilivu na subira kuliko mume na hivyo kuweza kuitumia haki hii pasi na sababu za kimsingi.
2              Athari za talaka humfunga zaidi mume kama kulipa mahari (ikiwa hayakukamilishwa) kumhudumia mke muda wote wa eda.
Heshima hii hakupewa mume tu kama ni silaha au kuitumia kwa jinsi atakavyo,aonavyo au apendavyo bali amewekewa mipaka na taratibu maalum zinazohusiana na suala zima la ndoa ikiwa ni mkataba wa pande mbili zenye haki sawa na huku akitakiwa kuchunga mipaka ya Allah Subhaanahu Wata’ala.
Allah Subhaanahu Wata’ala alipoifanya ndoa kuwa ni moja katika mipangilio ya muendelezo wa maisha ya binadamu katika ardhi anataka kuhakikisha kwamba malengo ya ndoa yanakuwepo na kutimizwa kama kuwepo mapenzi, kuoneana huruma, kuweza kuenziana na kuwepo maelewano ya hali ya juu kati ya mume na mke.
Endapo kutatokea moja katika misingi na mihimili ya ndoa kushindwa kufikiwa kwa kutokea mabadiliko ya tabia, mapenzi kuondoka na kushindikana kwa waliopewa jukumu la kuleta maelewano kati ya wanandoa basi hakuna busara yoyote kuendeleza maisha ya ndoa katika mazingira ambayo ni kinyume na malengo yaliyokusudiwa.
Jamii ya kiislamu imepoteza mweleko katika masuala ya ndoa kwa ujumla na hasa katika masuala ya talaka ndiyo kuna mtihani mkubwa. Bado kuna miongoni mwa waume waislamu mawazo yao makubwa wanapoingia katika chuo hiki muhimu ni kustarehe na mke na wengine kufikia kuwaita mabinti wa kike kama ni bidhaa mbovu na huku ni kuwadhalilisha akinamama kijinsia.
Mtazamo huu ndio unaowafanya baadhi ya waume wasifahamu ya kujifunza maana na makusudio halisi ya ndoa katika dini yetu ya kiislamu. Wengine hata hawafahamu hekima ya kuletwa na kuruhusiwa talaka na kuitumia kwa istihzai na inda kama ni silaha, kitisho na mkwala kumtishia mke wa ndoa. Mke aliekabidhiwa kwa neno lake Allah Subhaanahu Wata’ala na kwa Sunnah za Mtume wake Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam.
Hekima hii ambayo Allah Subhaanahu Wata’ala ameitolea ufafanuzi kwa kuwepo aya tofauti ndani ya Quraan zinazofafanua utaratibu wa kufuatwa mpaka kufikia kutumika. Kama anavyosema Annisaa/35
وَإِنْ خِفْتُمْ شِقَاقَ بَيْنِهِمَا فَابْعَثُواْ حَكَماً مِّنْ أَهْلِهِ وَحَكَماً مِّنْ أَهْلِهَا إِن يُرِيدَا إِصْلاَحاً يُوَفِّقِ اللّهُ بَيْنَهُمَا إِنَّ اللّهَ كَانَ عَلِيماً خَبِيراً).                                                                                
Na mkichelea kutakuwepo mfarakano (Kutokuelewana) baina ya mke na mume basi pelekeni muamuzi kutokana na jamaa za mume, na muamuzi kutokana na jamaa za mke. Wakitaka mapatano Allah atawawezesha. Hakika Allah ni Mjuzi Mwenye khabari
Kabla ya kufikiwa kutolewa hupitiwa na taratibu za kutafutwa suluhu baina ya Wanandoa kwa mawaidha, nasaha, miongozi hadi kupelekea wawakilishi wa kila upande kukutana kwani suluhu ina kheri kubwa kuliko talaka kama anavyothibitisha Allah katika Quraan Annisaa/128
وَإِنِ امْرَأَةٌ خَـفَتْ مِن بَعْلِهَا نُشُوزاً أَوْ إِعْرَاضاً فَلاَ جُنَاْحَ عَلَيْهِمَآ أَن يُصْلِحَا بَيْنَهُمَا صُلْحاً وَالصُّلْحُ خَيْر       
Na mwanamke akichelea kutupwa au kutojaliwa na mumewe, basi si vibaya kwao wakisikizana kwa suluhu. Na suluhu ni bora   
Hata hivyo ikifika hali ya kutoelewana kwa wanandoa kufikia sura ya kushindikana kupatika suluhisho licha ya jitihada zote kupita hakuna budi ila talaka kutumika ikiwa ni hatua ya mwisho na wala si ya mwanzo kama wengi wanavyoitumia kimakosa, kwa kutokujua au kwa kufanya inda. Suluhisho hili ni kwa dharura iliopo tu – malengo yaliyokusudiwa kuwepo ndoa kuondoka.
Allah Subhaanahu Wata’ala anafahamisha utaratibu wa kutengua mkataba wa ndoa kama ifuatavyo Suuratul Baqarah /229
(الطَّلاَقُ مَرَّتَانِ فَإِمْسَاكٌ بِمَعْرُوفٍ أَوْ تَسْرِيحٌ بِإِحْسَانٍ                             
Talaka ni mara mbili. Kisha ni kukaa kwa wema au kuachana kwa vizuri.
Na pia kusema katika Suuratu Talaaq/2
                   (فَإِذَا بَلَغْنَ أَجَلَهُنَّ فَأَمْسِكُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ أَوْ فَارِقُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ)
Basi wanapofikia muda wao, ima warejeeni mkae nao kwa wema, au farikianeni (achaneni) nao kwa wema.
Hapa zimetajwa hali mbili tu nazo ni:
1              Kukaa na mke kwa wema
2              Kuachana nao kwa vizuri   kwa daraja ya Ihsaani
Allah Subhaanahu Wata’ala ndiye aliyetuumba na kutujua hali zetu na undani wetu anaejua yaliyojificha na ya dhahiri. Ni yeye aliyetupa moja ya machaguo haya mawili aliyoyataja ndani ya kitabu chake Quraan – kitabu kisicho na shaka wala dosari na kilichokamilika.
Kumomonyoka maadili na misingi sahihi aliyetuachia Mtume wetu Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam pamoja na watangu wema kumewafanya baadhi ya waislamu kuongeza jambo la tatu nalo ni kumtundika mke kwa kumuacha katika hali ya kuwa hajaachika na wala haishi na mume maisha ya kindoa. Annisaa /129
وَلَن تَسْتَطِيعُواْ أَن تَعْدِلُواْ بَيْنَ النِّسَآءِ وَلَوْ حَرَصْتُمْ فَلاَ تَمِيلُواْ كُلَّ الْمَيْلِ فَتَذَرُوهَا كَالْمُعَلَّقَة
 Wala hamtaweza kufanya uadilifu baina ya wake, hata mkikakamia. Kwa hivyo msimili moja kwa moja mkamwacha (mmojawapo) kama aliyetundikwa.
Anasema Ibn ‘Abbaas, Allah awawie radhi yeye na baba yake, kwamba neno “Mu’allaqah” maana yake ni mwanamke ambae hana mume na wala hajaachika - ametundikwa.
Baya zaidi wanaowafanyia wake zao uovu huu, huwa hawajioni kama wanamuasi Allah Subhaanahu Wata’ala pamoja na Mtume wake Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam bali hujiona na kujilabu kwa kitendo chao hiki. Na kila wakimuona mke akiatilika huchekelea ndani ya nafsi zao huku wakiisahau kauli ya Allah Subhaanahu Wata’ala Al Baqarah/231
 وَلاَ تُمْسِكُوهُنَّ ضِرَاراً لَّتَعْتَدُواْ وَمَن يَفْعَلْ ذَلِكَ فَقَدْ ظَلَمَ نَفْسَهُ وَلاَ تَتَّخِذُوَاْ آيَاتِ اللّهِ هُزُواً
Wala msiwarejee kwa kuwadhuru mkafanya uadui. Na atakayefanya hivyo, amejidhulumu nafsi yake. Wala msizichukulie Aya za Allah kwa utani.
Aya hii, anasema Ibnu ‘Abbaas Allah awawie radhi yeye na baba yake, ilikuwa wanaume wakiwaacha wake zao na wakikaribia kumaliza eda zao huwarudia si kwa wema bali kuwa kuwazuia ili wasiweze kuolewa na watu wengine na baada ya muda huwaacha tena na kisha kusubiri mpaka karibu na kumalizika kwa eda na kisha kuwarudia. Allah Subhaanahu Wata’ala akateremsha aya hii kuwakataza kwa kitendo chao hiki.
Na pia katika tafsiri ya Ibn Kathiyr anaifafanua aya  hii kwa kusema:
"هذا أمر من الله عز وجل للرجال، إذا طلق أحدهم المرأة طلاقاً له عليها فيه رجعة أن يحسن في أمرها إذا انقضت عدتها ولم يبقى منها إلا مقدار ما يمكنه فيه رجعتها، فإما أن يمسكها، أي يرتجعها إلى عصمة نكاحه بمعروف، وهو أن يشهد على رجعتها وينوي عشرتها بالمعروف، أو يسرحها، أي يتركها حتى تنقضي عدتها ويخرجها من منزله بالتي هي أحسن، من غير شقاق، ولا مخاصمة، ولا تقابح"                                                                     
Hii ni amri ya Allah Subhaanahu Wata’ala kwa wanaume. Akiacha mmoja wenu mkewe talaka(moja) basi ana haki ya kumrudia na kumfanyia wema katika mambo yake ikikaribia kumalizika eda yake na haikubaki isipokuwa muda mchache ambao utamuwezesha kumrudia mke ima amrudie katika ndoa kwa wema nako ni kushuhudia kumrudia na kunuia kukaa nae kwa wema au amuache yaani mpaka amalize eda yake na kisha kumfahamisha kuondoka katika nyumba katika hali nzuri ya masikilizano bila ya kuwepo chuki, ugomvi au kufanyiana ubaya.
Mke anaweza kutundikwa katika hali kama zifuatazo kwa kupigia mifano:
1              Aliedai talaka akiwa na sababu zinazokubalika kisheria na mume kumkatalia na kugoma kuitoa kwa vikwazo na visingizio tofauti.
2              Mke mwenza ambae ametelekezwa na mumewe bila ya huduma ya aina yoyote wala kupata haki zake za kimsingi na akidai kuachwa hukataliwa na wala hatimiziwi majukumu yake.
3              Alie mbali na mumewe kwa sababu tofauti na kutokuwa na mawasiliano kwa muda mrefu kupita muda mrefu huku akiwa hapati huduma ya aina yoyote.
4              Aliefukuzwa katika nyumba ya mke(mfano huu kwa waliodanganya kama hawana waume huku wameolewa kihalali kama ilivyo baadhi ya familia Uingereza kwa ajili ya kupata unafuu wa kimaisha) kisha akagoma kutoa talaka akidai mpaka warudi kule waliopooana.
5              Mume anaekataa kutoa talaka akidai lazima apewe haki ya kuwa na watoto na kadhalika.
Wake nao kwa upande wao huchangia hali hizi kutokana na mazingira kuwa dhidi yao kama
1              Kuwa na khofu na woga ya kunyang’anywa watoto.
2              Kukosa mtu wa kuweza kumsaidia na kumsimamia kudai haki zake.
3              Kuwa dhaifu na kutoweza kukabiliana na waume kuweza kudai haki zao za kimsingi kwa kuogopa vitisho na mbinu za waume.
4              Kufungika na vikwazo vyengine kama waliooana katika nchi za Ulaya na kusajili ndoa  kwa msajili (registrar) na hivyo kuweza kuachana kiislamu na kujikuta bado ni wanandoa kiserikali na kadhalika.  
Inawezekana wake kwa upande wao wakadai talaka kwa sababu zisizokuwa za msingi na hapa ni vyema pakaeleweka maapizo ya Allah Subhaanahu Wata’ala kama hadithi ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam    
                          أيما امرأة سألت زوجها الطلاق من غير ما بأس فحرام عليها رائحة الجنة رواه أحمد  
Mwanamke yeyote atakaedai talaka kutoka kwa mumewe pasi na kuwa na sababu za kimsingi ni haramu kwake harufu ya peponi
                                                                                                       Ahmad
Hakuna kitu ambacho mume atafaidika kwa kumuacha mke katika hali ya kumtundika hajijui cheo chake kwa kuwepo tu si mke wa ndoa yenye kutambulika na wala si mtalaka bali ni kuasi na kukiuka mipaka ya Allah Subhaanahu Wata’ala. Mipaka ambayo Mtume wetu Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam anatuhadharisha nayo kwa makaripio makali kwa kusema: 
إِنَّ اللهَ حَدَّ حُدُودًا فَلَا تَعْتَدُوهَا، وفَرَضَ فَرَائِضَ فَلَا تُضَيِّعُوهَا، وحَرَّمَ مَحَارِمَ فَلَا تَنْتَهِكُوهَا،   
                                وَسَكَتَ عَنْ أَشْيَاءَ رَحْمَةً لَكُمْ مِنْ غَيْرِ نِسْيَانٍ فَلَا تَسْأَلُوا عَنْهَا     
Hakika Allah ameweka mipaka yake basi msiivuke na amefaridhisha fardhi zake na wala msizipuuze na ameharamisha maharamisho yake na wala msiyafanye na amenyamaza katika baadhi ya vitu ikiwa ni rehma kwenu bila ya kughafilika basi msiviulizie na kuvidadisi.
                                      Addaylamiy na wengineo
Kadhia hii haina budi kupigwa vita na waislamu hasa kwa waume waliojijengea tabia ya kuwatelekeza na kuwatundika wake bila ya kuzingatia taratibu za kimsingi na kisheria kama anavyosema Allah katika Suuratul Baqarah/231
وَاذْكُرُواْ نِعْمَتَ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَمَآ أَنزَلَ عَلَيْكُم مِّنَ الْكِتَـبِ وَالْحِكْمَةِ يَعِظُكُم بِهِ وَاتَّقُواْ اللَّهَ وَاعْلَمُواْ أَنَّ اللَّهَ بِكُلِّ شَىْءٍ عَلِيم                                                                                                                 
Na kumbukeni neema ya Allah juu yenu, na aliyo kuteremshieni katika Kitabu na hikima anacho kuonyeni kwacho. Na mcheni Allah, na jueni kwamba hakika Allah ni Mjuzi wa kila kitu
Juu ya yote haya kwanini turuhusu hali ifikie katika daraja hii ya chuki mpaka kufikia kukomoana wakati Allah Subhaanahu Wata’ala anatuusia kwa maneno yenye hekima  kwa kusema - Al Baqarah/237
                                   وَأَن تَعْفُواْ أَقْرَبُ لِلتَّقْوَى وَلاَ تَنسَوُاْ الْفَضْلَ بَيْنَكُمْ إِنَّ اللّهَ بِمَا تَعْمَلُونَ
Na kusameheana ndiko kulio karibu zaidi na uchamungu. Wala msisahau fadhila baina yenu. Hakika Allah anayaona mnayo yatenda.
Ukaribu huu kwa uchamungu anauonesha Allah kwa kutuweza kutuonesha njia kama anavyosema a Attalaaq /2
                                            وَمَن يَتَّقِ اللَّهَ يَجْعَل لَّهُ مَخْرَجًا         
    Na anaye mcha Allah humtengezea njia ya kutokea   
Tujitahidi kurudi kwa mola wetu na kuheshimu mipaka yake katika kila tulifanyalo. Tumuombe Rahmaani atuondoshee uovu katika nafsi zetu na kuzingatia pamoja na kuheshimu mipaka yake bila ya kuikiuka.
Wabillahi Ttawfiyq.