Tukijifunza, Tutekeleze



Waliwahi kusema wema waliotutangulia – Salafun Saalih – kwamba: “Ikiwa Allah Subhaanahu Wata’ala anamtakia kheri mja wake basi humfungulia mlango wa vitendo na humfungia mlango wa mijadala na mabishano. Hivyo kila ukimuona muislamu anaeitekeleza dini yake kivitendo na kutekeleza sunnah za Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam basi ujue hiyo ni moja katika alama za kheri”.

Tatizo la umma wetu wa leo kubwa ni utekelezaji. Tunaweza kubahatika kupata maarifa ya dini yetu lakini yakabaki kwenye bongo zetu kama nadharia tu – theory lakini hakuna vitendo au kuyatekeleza hata yale kidogo tuliyojaaliwa kuyapata.

Tuangalie mfano mizuri walituachia masahaba katika kutekeleza kwa vitendo yale waliyobahatika kujifunza kutoka kwa mwalimu wetu, kigezo chetu na ruwaza njema, al habib Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kama ilivyopokelewa kwamba:

  أُمّ حبيبة رضي الله عنها أنها قالت: قال النبي صلى الله عليه وسلم : ((من صلّى لله في يوم وليلة ثنتي عشر ركعة تطوّعاً غير الفريضة إلا بُني له بهنّ بيتٌ في الجنة))
         أخرجه أحمد وابن ماجة   
Ummul Muuminiyn, Ummu Habibah, Allah amuwie radhi, alisema: Amesema Mtume: Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam:

“Mwenye kusali katika siku moja na usiku wake rakaa kumi na mbili za sunnah zisizokuwa za fardhi basi hujengewa kwa ajili yake nyumba peponi”.
                                                                              Ahmad na ibnu Majah
Anasema Ummu Habibah, Allah amuwie radhi, ambae alikuwa mke wa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam: “Sikuziwacha tena tokea siku nilipomsikia Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Anasema Anbasa ambae aliipokea hadithi hii kutoka kwa Ummu Habibah: “Nami sikuziwacha hata siku moja tokea siku nilipomsikia Ummu Habibah”. Anasema Annu’umaan bin Salim, ambae aliipokea hadithi hii kutoka kwa Anbasa: “Hata na mimi sikuziwacha tena tokea siku nilipomsikia Anbasa.”

Huu ndio mfano unaoonesha utekelezaji baada ya kujifunza jambo lolote la dini.

Tusitosheke nalo tu kwamba tayari tumeshalijua bali likiwa jambo hilo linahitaji utekelezaji basi tokea wakati huo tutakuwa na dhimma la kulifanyia kazi na kulitenda kama walivyotuwekea kigezo masahaba, taabiina na wema waliotutangulia inshaAllah.

Aliwahi kunukuliwa Abdullah ibn Mas’ud, Allah amuwie radhi, akisema:

“Elimu ya kweli si ile iliyohifadhiwa kisha kunukuliwa tu bali elimu ya kweli ni ile itakayodhihirishwa kwa kuwepo taqwa (kumuogopa Allah). Jifunze na kisha tekeleza kwa vitendo yale uliyobahatika kujifunza”