Abdulrahman ibn Awf-alitoa mali yake kwa ajili ya Allah (SW)



Abdulrahman ibn Awf-alitoa mali yake kwa ajili ya Allah (SW)
 
Ni mmoja kati ya watu wanane wa mwanzo kusilimu.  Pia ni miongoni mwa watu kumi walibashiriwa pepo na Mtume (SAW).  Alikuwa mmoja kati ya watu sita waliochaguliwa na Umar kuunda baraza la ‘Shura’ kumchagua Khalifa baada ya kifo chake.
 
Jina lake enzi za ujahiliya lilikuwa Abu Amr.  Aliposilimu Mtume (SAW) akamwita Abdulrahman (mja wa mwenye kurehemu).  Alisilimu hata kabla Mtume (SAW) hajaanza kwenda kwa Al-Arqam na inasemekana alisilimu siku mbili tu baada ya kusilimu Abubakar Siddiq.
 
Abdulrahman hakukimbia mateso na adhabu za Maquraysh.  Alivumilia madhila na mateso na kubaki na imani yake thabiti.  Pale walipolazimika waislam kufanya Hijira kwenda Habashah, Abdulrahman naye pia alikwenda.  Alirudi Makka baada ya kusikia uvumi kwamba hali za waislam zimekuwa nzuri na baada ya kuthibitika kwama zilikuwa ni uzushi tu, alifanya tena Hijra kuelekea Habashah na alihitimisha kwa hijra ya Madina.
 
Punde tu, alipowasili Madina.  Mtume (SAW) aliwaunganisha Muhajirin na Ansaar. Lengo la udugu huu lilikuwa kuweza kuwa na maelewano ya kijamii na pia kuwapunguzia ukiwa muhajiruun.   Abdulrahman akakutanishwa na Saad ibn Ar-Rabiah.  Baada ya kuatambulishwa rasmi, Saad akamwambia Abdulrahman:
“Ndugu yangu, mimi ndiye mwenye utajiri mkubwa hapa Madina, nina vikataa viwili na wake wawili.  Angalia ni kipi kati ya vikataa hivi viwili utakipenda na nitakuachia na angalia yupi kati ya wake zangu amekupendeza na nitampa talaka kwa ajili yako”
 
Abdulrahman hakutarajia yote haya kwani alionekana kidogo kuingiwa na aibu na kujibu:
“Inshaallah Mwenyezi Mungu akurehemu katika familia yako na utajiri wako.  Tafadhali kwa hisani yako nioneshe soko tu liko wapi?”
 
Abdulrahman alioneshwa soko na kuanza biashara kwa kile kichache alichokuwa nacho.  Akafanya biashara na kupata faida haraka.  Muda mchache tu hali yake ikawa nzuri sana kibiashara akajitafutia mke na kuoa.
 
Siku moja, alikwenda kwa Mtume (SAW) huku akinukia uturi na manukato:
 “Maliyam!, ewe Abdulrahman! Akasema Mtume Muhammad (SAW) kwa mshangao. (maliyam ni neno la asili ya kiyemen linaainisha mshangao).” 
“Nimeoa,” akajibu Abdulrahman.
 “Na mkeo ulimpa kitu gani kama mahari yake?”
“Uzito wa ‘uwat’ wa dhahabu”
 
“Lazima ulishe walima hata kama ni kondoo mmoja na Mwenyezi Mungu (SW) akubariki katika utajiri wako,” akamalizia Mtume (SAW) huku akitabasamu.
 
Abdulraham alipigana vita vya Badr na Uhud kwenye vita vya Uhud alisimama imara licha ya kuwa na majeraha karibu ishirini mwilini mwake na mengine ya kutisha.  Jitihada yake ya nafsi ilikwenda sambamba na jihadi yake ya mali.
 
Kuna siku moja, Mtume (SAW) alikuwa akijiandaa kutuma jeshi vitani na akalihutubia kwa kusema:
 “Toeni sadaka kwani ninataka kulituma jeshi.” 
Haraka haraka Abdulrahman alikwenda nyumbani kwake na kurudi, “ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu; akasema, nina (dinar) elfu nne.  Ninatoa elfu mbili kama mkopo kwa mola wangu na kuiachia familia yangu zilizobaki.”
 
Mtume (SAW) alipoamua kutuma jeshi Tabuk ambapo kulikuwa mbali sana.  Haja ya msaada wa fedha ilikuwa kubwa kama ilivyokuwa haja ya wana jihadi.  Kwani majeshi yao yalikuwa yameandamana vyema na kuwa na zana nzito za kivita. 
 
Mwaka huo Madina kulikuwa na njaa na ukame.  Safari ya Tabuk ilikuwa ndefu na zaidi ya kilomita elfu moja.   Chakula hakikutosha na usafiri ulikuwa mchache mno mpaka Mtume (SAW) kuwarudisha kundi la waislam waliokuwa tayari kwa vita kwa kukosekana usafiri.
 
Waislam walioachwa nyuma walisikitika sana na wakajaeleweka kama ‘Bakkaa-in’ waliokuwa wakilia.  Na jeshi hili likaitwa jeshi la Usrah- ‘taabu’.  Hapo Mtume (SAW) akawahimiza masahaba watoe walichonacho kwa moyo mmoja kulisaidia jeshi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kuwahakikishia malipo makubwa kwa Mwenyezi Mungu.
 
Naam! Wito ukaitikiwa na waislam wakajitolea kwa wingi na miongoni mwao ni Abdulrahman.  Alitoa wakia mia mbili za dhahabu na hapo Umar ibn Khattab alisema:
“Sasa nimemuona Abdulrahman anafanya kosa, hukuiachia chochote familia yake.”
“Umeiachia chochote familia yako, Abdulrahman?”  Mtume (SAW) alimuuliza.
“Ndio, nilichowaachia ni kingi kuliko nilichotoa na ni bora,” akajibu Abdulrahman.
Mtume akauliza, “kiasi gani?”
“Kile ambacho Mwenyezi Mungu na Mtume wake ameahidi navyo ni rizki, mambo mema na malipo.”
 
Jeshi la waislam likaanza safari kuelekea Tabuk. Abdulrahman akabahatika kupata heshima ambayo kabla yake hajawahi kupewa mtu yoyote.  Ulipofika wakati wa sala na Mtume (SAW) hakuwepo wakamchagua Abdulrahman kuwa Imam.  Mtume (SAW) alipodiriki sala, tayari rakaa ya kwanza ilikwisha malizika na akasali maamuma.  Je! Kuna hadhi imam wa Al-habib Mustafa (SAW), kiumbe kilicho bora zaidi kwa Mwenyezi Mungu, imam wa Mitume yote Muhammad alayhi ssalaatu wassalam!
 
Mtume Muhammad (SAW) alipofariki, Abdulrahman alichukua jukumu la kuihudumia familia yake, Ummahatul Muuminiin.  Aliwashughulikia kwa mahitaji yao na kwenda nao Hija pamoja ili kuhakikisha mahitaji yao yametimizwa.  Huu ni uaminifu ambao alipata katika familia ya Mtume (SAW).
 
Aliwahi kuuza sehemu ya ardhi kwa dinar elfu arubaini na kuzigawa zote kwa Banu Zahrah jamaa wa mama yake Mtume (SAW), wakeze Mtume (SAW) waliokuwa masikini.  Na Bi Aisha (RA) alipopata mgao wake aliuliza:
 
“Ni nani aliyeleta fedha hizi?
Akaambiwa ni, “Abdulrahman.”
Mtume amesema, “hakuna mtu yoyote atakayewaonea huruma nyinyi baada ya kufa kwangu isipokuwa wale walio na subira.” 
Dua za Mtume (SAW) zilikubalika kwani Abdulrahman Ibn Awl alikuja kuwa tajiri mkubwa miongoni mwa masahaba wa Mtume (SAW), makundi yake ya misafara toka na kuja Madina yalizidi kukua siku hadi siku.  Aliwaletea watu wa Madina unga, ngano, samli, nguo, vyombo vya kupikia, manukato na chochote kitakachohitajika na kuuza nje bidhaa zilikuwa zikizalishwa.
 
Siku moja, sauti kubwa ikasikika ikitokea nje ya mipaka ya mji wa Madina, mji ambao kwa kawaida ni tulivu sauti ilizidi kuongezeka huku mawingu ya vumbi na michanga yakirushwa juu angani.  Wakagundua kwamba ni kundi kubwa la ngamia takriban mia saba huku limesheheni mizigo linaingia Madina.  Watu wakawa wanaitana kuja kushuhudia ni bidhaa gani msafara huu wa ngamia wote hawa umeleta:
 
Bi Aishah, akasikia zogo lile na akauliza, “nini tena hiki kinachotokea Madina?
Akaambiwa, “ni msafara wa Abdulrahman ibn Awl unatoka Syria na bidhaa”
“Msafara tu ndio unaofanya zogo lote hili?” Akauliza huku haamini.
“Naam, Yaa Ummul Muuminiin, wapo ngamia mia saba”
 
Bi Aisha akatikisa kichwa chake na akashika tamaa kama aliyepigwa na butwaa kama kwamba anajaribu kukumbuka tukio au jambo lililopita kasha akasema:
“Nimemsikia mjumbe wa Mwenyezi Mungu akisema, nimemuona Abdulrahman Ibn Awl anaingia peponi, huku akitambaa.” 
Kwa nini atambae? Kwa nini haingii mara moja kwa kuruka pamoja na masahaba wa mwanzo wa Mtume (SAW).
 
Baadhi ya masahaba wake wakamhadithia Abdulrahamn riwaya hii.  Akakumbuka alishawahi kuisikia hadithi hii zaidi ya mara moja kutoka kwa Al-habib Mustafa (SAW) na akaharakiza kuelekea kwa Bi Aisha na akamwambia: “Yaa Ammah! Ewe mama yangu! Umeyasikia haya kutoka kwa Mtume (SAW).
“Ndio,” akajibu.
Abdulrahman akafurahi sana na akaongezea:
“Kama ningeliweza ningeliingia peponi huku nimesimama.  Nnakuapia yaa Ammah, msafara wote huu na bidhaa zake zote ninautoa fi Sabiili Llah!
 
Hilo alilitekeleza kwa ukarimu huu aliounesha na uadilifu na kuwagawia watu wa Madina na vitongoji vyake.
Hili ni tukio moja tu linalomuonesha Abdulrahman kuwa ni mtu wa aina gani?  Alipata utajiri mkubwa lakini haukumvaa wala hakuuvaa.
 
Aliendelea kutoa kwa mikono yuke yote miwili kwa siri na kwa dhahiri.  Na baadhi ya misaada aliyoitoa, dirham elfu arubaini, dinar elfu arubaini.  Wakia mia mbili za dhahabu, farasi mia tano kwa mujahidina, dinar mia nne kwa waliopona vita vya Badr na sehemu kubwa aliyoitoa kwa wake za Mtume (SAW) na bado listi inaendelea……
 
Na kwa ukarimu wake Bi Aisha alisema:
 
“Inshallah Mwenyezi Mungu (SW) amnywishe kwenye chemchem ya Salsabil.”
 
Utajiri wote huu haukumtia jeuri wala kiburi na haukumbadilisha chochote.  Alipokuwa na wafanyakazi na wasaidizi wake hawezi kumtofautisha kabisa.   Siku moja aliletewa chakula kufutari, alikitazama kasha akasema;
“Musab ibn Umayr aliuwawa, yeye alikuwa bora kuliko mimi.  Hatukuwa na hata guo la kumsitiri tukimfunika kichwani miguu huwa wazi, kisha Mwenyezi Mungu (SW) akatujaalia rizki hizi za kidunia………nina wasi wasi kwamba malipo yetu tayari tumeshalipwa mapema duniani.”  Akaanza kulia na kushindwa kula.
 
Na Inshallah Mwenyezi Mungu amuweke Abdulrahman katika kundi la wale…… Suratul Baqarah 262.