Abdullah ibn Abbass- msomi wa umma huu



Abdul


Abdul                                Abdullah  ibn Abbass-   msomi wa umma huu


Abdullah ibn Abbas bin Abdul Muttalib ni mtoto wa ami yake Mtume (SAW). Alizaliwa miaka mitatu kabla ya Hijra.  Na Mtume alipofariki, Abdullah alikuwa na umri wa miaka kumi na mitatu.
 
Alipofika umri wa kutambua - miaka saba - alijifunga na kumwambata Mtume (SAW).  Alikuwa akimuandalia Mtume (SAW) maji ya kutawadhia.  Husimama nyumba ya Mtume Muhammad (SAW) anaposali na wanapokuwa safarini, hujaribu kuwa karibu na Mtume (SAW) mpaka kuambiwa alikuwa kama kivuli cha Mtume, kwani anapokuwepo Mtume na Abdullah anakuwa karibu naye.
 
Muda wote huo, Abdullah huwa mtulivu na kufuatilia kila ambalo Mtume (SAW) hufanya na kusema.  Moyo wake umejaa hamu ya kutaka kuelewa na akili yake kuwa bado changa na safi hivyo kuweza kuhifadhi maneno ya Mtume (SAW) kwa uhakika kama mfano wa chombo cha kurekodia.
 
Kwa njia hii pamoja na utafiti wake baadaye, Abdullah akawa mmoja katika wasomi wakubwa miongoni mwa masahaba na kuweza kuzihifadhi hadithi za Mtume (SAW) kwa ajili ya kizazi kijacho.  Inasemekana aliweza kuhifadhi hadithi elfu moja mia sita na sitini, ambazo zimeandikwa na kuhakikiwa katika Bukhari na Muslim.
 
Mara nyingi Mtume (SAW) alikuwa akimweka Abdullah karibu naye na kumpiga piga mabegani mwake na kuomba
 “Ewe Mola, mjaalie kupata elimu ya kina ya dini ya kiislam na umuongoze katika kufahamu na utaalam wa vitu.” 
Mtume Muhammad (SAW) pia alimuombea awe mtu wa hekima pia, mbali na elimu na ufahamu wa mambo Abdullah anasimulia:
“ Mara moja Mtume (SAW) alikuwa akijiandaa kutia udhu. Niliharakia kumwekea maji.  Akafurahishwa na nilivyofanya. Alipokuwa anataka kuanza kusali, aliashiria nisimame ubavuni mwake.  Hata hivyo, nikasimama  nyuma yake. sala ilipokwisha aligeuka na kusema,  ‘Nini kilichokuzuia kutosimama ubavuni mwangu eeh Abdullah?’ 
Abdullah akajibu, “wewe ni mwingi wa haiba na taadhima kubwa nisiyostahili kwa mimi kusimama ubavuni mwako.”
Mtume (SAW) akanyanyua mikono juu na kuomba, “ewe mola mjaalie hekima,” Dua hii ya Mtume Muhammad (SAW) ilikuja kuthibitika baadae kwani Abdullah alikuwa mwenye hekima na busara hata kupita umri wake.  Hekima na busara hizi zilikuja kwa ucha Mungu na kutafuta elimu alikojishughulisha Abdullah enzi za uhai wa Mtume (SAW) na hata baada ya kufariki kwake.
 
Enzi za uhai wa Mtume (SAW), Abdullah hakuwahi kukosa vikao vyote vya Mtume Muhammad (SAW) na kuhifadhi yale yote atakayoyasema na baada ya kufariki kwake, alijihimu kwenda kwa masahaba wengi kujifunza yale waliyofundishwa na Mtume (SAW).
 
Akisikia tu! Kuna mtu anajua hadithi fulani ambayo yeye haijui atakwenda kwake haraka na kuiandika.  Ataihakiki na kuilinganisha na hadithi nyengine na aliwahi kwenda kwa masahaba karibu thelathini kuhakiki jambo moja tu.
 
Abdullah anaeleza nini alichofanya baada ya kusikia hadithi ambayo hakuijua kabla:
 
“Nilikwenda kwake wakati wa Qaylula (baina ya adhuhuri na alasiri watu wanapojipumzisha kwa usingizi) nikatandika guo langu mbele ya mlango wake. Upepo ukawa unavuma na nikajawa na mavumbi.  Kama ningelitaka ningegonga mlango na kuomba rukhsa na nina hakika angelinifungulia.  Nikaona bora nisubiri ili atakapoamka atakuwa ameshapumzika.  Alipokuwa anatoka na kuniona katika hali yangu akasema, “ewe bin ami wa Mtume (SAW) una nini? Hata kama ungeagiza nije kwako ningelikuja.”  Abdullah akajibu, mimi ndie ninaepaswa kuja kwako kwani elimu hufuatwa, haiji. Nikamuuliza kuhusu ile hadithi na kujifunza kutoka kwake”
 
Katika njia hii, Abdullah aliendelea kuuliza na kuuliza na kuendelea kuuliza huku akihakiki na kuchunguza kila alichokusanya.  Abdullah hakuwa mtaalam wa hadithi pekee, alizama pia katika elimu nyenginezo.  Alikuwa akimhusudu sana Zayd ibn Thabit, mkusanyaji Quran mkuu na mshauri wa sheria Madina, mtaalam wa sheria ya mirathi na kusoma Quran.  Endapo Zayd amekusudia kwenda safari Abdullah humkamatia kipando chake kwa unyenyekevu kama vile mtumwa mbele ya bwana wake.  Zayd humwambia, “Usifanye hivyo, ewe bin ami wa Mtume (SAW).”
 
“Hivi ndivyo tulivyoamrishwa kuwatendea wasomi miongoni mwetu,” Abdullah akajibu.
Zayd naye humwambia, “hebu lete mkono wako niuone.”
 
Abdullah naye akiupeleka, Zayd huubusu na kusema, “Hivi ndivyo tulivyoamrishwa kuwatendea Ahlul bayt (watu wa nyumbani wa Mtume (SAW).”
 
Kila kiwango chake cha elimu kikikua basi na hadhi yake pia ikaongezeka. Masruq ibn al-Ajda anamzungumzia Abdullah, “Kila nikimuona Abdullah, husema ni kijana mzuri wa kuvutia.  Akiongea, husema ni mzungumzaji fasaha na akisimamia mazungumzo husema “ni msomi wao.”
 
Khalifa Umar ibn Khattab mara nyingi husikiliza ushauri wake katika mambo muhimu yanayolihusu dola la kiislam na kumweleza kama, “kijana aliyekomaa.”
Saad ibn Abi Waqas anamuelezea, “Sijawahi kumuona mtu anayefahamu kwa haraka, mwingi wa elimu na hekima zaidi ya Ibn Abbass.  Nilimuona Umar akimwita kushauriana naye kwenye mambo mazito tena mbele ya wakongwe wa Badr miongoni mwa Muhajiriin na Ansaar na akiongea, Umar hayadharau.”
 
Kutokana na sifa hizi ndio maana Abdullah ibn Abbas anafahamika zaidi “Msomi wa umma huu.”
 
Abdullah hakuwa mtafutaji tu wa elimu bali alielewa kwamba ana wajibu wa kufundisha umma wa kiislam na wale wanaotafuta elimu.  Akawa maalim na nyumba yake kuwa chuo kikuu.  Naam! Ni chuo kikuu kikitakhassas na elimu ila tu kulikuwa na maalim mmoja tu jinsi watu walivyomiminika kwenye darasa za Abdullah! Sahaba mmoja anasimulia:
 
“Niliwaona watu wengi wakielekea nyumbani kwake mpaka kukawa hakuna nafasi nje.  Niliingia ndani na kumfahamisha kwamba watu wanapigania kuingia ndani na wamejaa mlangoni, akasema, “nipatie maji nitie udhu.”  Alitia udhu na akakaa kitako cha kudarsisha na kusema, “nenda nje kawaambie, yoyote anaetaka kuuliza juu ya Quran na lafdhi (matamshi) yake na aingie ndani.  Nikafanya kama nilivyoagizwa, nyumba ikawa bado imejaa na akaelezea na kutoa maelezo ya ziada kuliko yale yaliyoulizwa.
 
Kisha akawaambia wanafunzi wake, “wapisheni wenzenu sasa.”
Akaniagiza tena, “nenda nje kawaambie, yoyote anayetaka kuuliza juu ya Quran na tafsiri yake na aingie ndani.”
Nyumba ikajaa tena na kama kawaida Abdullah akaeleza na kutoa maelezo ya ziada.  Ikaendelea hivyo huku makundi kwa makundi yanakuja kujadiliana na ‘Ustaadh’ kuhusu fiqh, halali, haramu, mirathi, lugha ya kiarabu na mashairi na kadhalika.
 
Kwa kutaka kuondoa msongamano, Abdullah akaweka siku moja kwa somo moja.  Kama leo kutasomeshwa fiqh basi kesho yake ni Quran na tafsiri. Vita vya Mtume, Mashairi, historia ya kiarabu kabla ya uislam hayo yote yalitengewa siku zao.
 
Njia yake ya kudarsisha ilikuwa ya uhakika kwani akisaidiwa na hifadhi yake timamu, hekima na busara, maelezo yake yalikuwa wadhihi,wazi na ya kimantiki.  Hoja zake zilikuwa za nguvu huku zikishindikizwa na dalili za kimaandiko na matukio ya kihistoria.
 
Katika tukio moja, nguvu za hoja zilihitajika kutumika enzi za ukhalifa wa Ali ibn Talib.  Kundi kubwa lililokuwa likimuunga mkono Ali dhidi ya Muawiya likaanza kumtenga.  Abdullah akaenda kwa Ali na kuomba rukhsa azungumze nao.
 
Kwanza Ali alisita akichelea kwamba Abdullah ataweza kufikwa na jambo lolote baya akiwaendea.  Abdullah akamhakikishia kwamba hakuna lolote baya litakalotokezea na hivyo kuruhusiwa.
 
Alikwenda, baadhi yao hawakuwa tayari kumsikiliza lakini wengine walikubali.  Abdullah akaanza:
“Niambieni mna malalamiko gani dhidi ya bin ami wa Mtume (SAW), mume wa mtoto wake na wa mwanzo kusilimu?
 
Wakaeleza matatizo yao matatu makuu;
 
Kwanza, ateue watu kuhukumu mas-ala ya dini ya Mwenyezi Mungu wakimaanisha Ali alikubali kusuluhishwa na Abu Musa al-Ash-ari na Amr ibn Aadh dhidi yake na Muawiya.
Pili, alipigana na wala hakuchukua ngawira wala mateka.
Tatu, hakusisitiza kwenye wa kikao cha usuluhishi kuitwa Amirul Muuminiin wakati tayari waislam walishaapa kiapo cha utii kwake na yeye kuwa Khalifa halali.”
 
Kwa wale waliomuasi Ali, hizi zote zilikuwa alama za udhaifu na kwamba Ali alikuwa tayari kuingiza alama za kuuliza katika cheo chake cha Amir.
Abdullah alipoanza kuwajibu akawaomba ataje aya za Quran na hadithi za Mtume Muhammad (SAW) ambazo hawana mashaka nazo na zinahusiana na malalamiko yao, iwapo watakuwa tayari kubadilisha msimamo wao.  Walikubali na Abdullah kuendelea:
 
“Kuhusu maelezo ya kuteua watu kutoa hukumu katika mas-ala ya dini ya Mwenyezi Mungu (SW).”  Mwenyezi Mungu (SW) anasema, “Enyi mlioamini wala msiuwe wanyama  wa kuwinda (kwa mchezo) wakati mpo ndani ya Hijja. Na mongoni mwenu atakaemuuwa basi malipo yake yatakuwa sawa na alichokiua, katika mifugo kama wanavyohukumu waadilifu wawili miongoni mwenu…………..”
 
“Nnakuombeni mhukumu, wallahi je! Hii hukumu ya watu hawa kuhusiana na kuenzi maisha yao na kufanya suluhu baina yao inahitaji kutazamwa zaidi kuliko ile suluhisho la sungura ambaye thamani yake ni robo dirham?
 
Bila ya shaka majibu yao yakawa suluhu ni muhimu zaidi kwa ajili ya kuyaenzi maisha ya watu na kuweka amani baina yao, kuliko mchezo wa vinyama kwenye baytul haraam:
Akawambia, “tumemalizana kwa hilo?”
Wakajibu, “Allahumma na’am”.
 
Abdullah akaendelea.  Kuhusiana na maelezo kwamba Ali alipigana na wala hukuchukua mateka wa kivita kama alivyofanya Mtume (SAW).  Hivi kweli mnataka kumchukua ‘mama’ Aisha kama mateka? Na kumtendea kama wanavyofanyiwa mateka? Ikiwa jibu lenu ni ndio basi mmeshaingia katika kufuru, na kama mkisema kwamba si ‘mama’ yenu vile vile mtaingia katika kufuru kwani Mwenyezi Mungu (SW) kasema:
 
“Mtume yu bora sana na waumini kuliko hata nafsi zao. Na wakeze ni mama zao.Na jamaa ni karibu wao kwa wao katika kitabu cha Mwenyezi Mungu kuliko waumini wengine na wahamiaji . Ila muwe munawafanyia wema marafiki zenu. Ahzaab/6
 
Abdullah akaendelea, “chagueni mtakalo, na akamalizia, tumemalizana na hili?”. Na jibu kurudi, “ Allahumma na’am.”
 
Na maelezo kwamba Ali amekubali kutoitwa Amirul Muuminiin (kumbukeni) Mtume (SAW) mwenyewe kwenye suluhu ya Hudaybiyah, aliwataka makafiri waandike kwenye mkataba “hivi ndivyo Mtume wa Mwenyezi Mungu mtukufu alivyokubali………”,  lakini wakadai “tungelikubali kama wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu (SW) tusingekuzuia kwenda Al kaaba na wala tusingepigana na wewe. Andika badala yake Muhammad ibn Abdullah.”  Mtume akakubaliana na madai yao huku akisema,
 “Wallahi mimi ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu hata kama wananikataa” 
Alipofika hapa akawauliza walioasi, “Je! Na hili tumemalizana nalo?”
Na jibu, “Allahumma na’am.”
 
Moja katika faida ya nguvu za hoja kwenye mjadala, sifa aliyeionesha Abdullah ibn Abbass na ile hiba aliyojaaliwa ya kuifahamu vyema Quran na sira ya Mtume (SAW) na hatimaye kiasi cha watu elfu ishirini waliokuwa tayari wamemuasi Ali wakarudi kwenye himaya yake.  Hata hivyo, kiasi cha watu elfu nne wakaendelea na msimamao wao wa uasi.  Baadaye wakajafahamika kama Khawarij.
 
Kwenye tukio hili Abdullah alionesha msimamo wake wa kupendelea amani kuliko vita na mantiki dhidi ya nguvu na fujo.
 
Abdullah alikuwa mtu mwenye kuwajali sana waislam wenzake na aliwahi kusikika akisema:
“Pale ninapoona umuhimu wa aya ya kitabu cha Mwenyezi Mungu hutamani watu wote wakajua lile linalolijua.”
 
“Pale ninaposikia kiongozi wa waislam anaongoza kwa haki na kutawala kwa uadilifu hufurahi na kumuombea dua…..”
 
“Pale ninaposikia mvua inanyesha kwenye ardhi ya waislam, basi na mimi hujawa na furaha.”
 
Abdullah alikuwa mcha mungu mwenye kufunga funga za sunna na kusimama usiku, hulia wakati akisoma Quran na akifika kwenye aya za mauti, kiama na akhera sauti yake huwa nzito na kujawa na kwikwi kwa khofu.
 
Alipofariki akiwa na umri wa miaka sabiini huko Taif.