Mus-ab bin 'Umayr: Mwakilishi wa kwanza katika Uislam



Mus-ab bin 'Umayr: Mwakilishi wa kwanza katika Uislam   

Wanahistoria wa kiislam wanamsimulia Mus’ab kwamba alikuwa kijana mchangamfu mno na mtanashati.  Alizaliwa na kukulia katika utajiri, kudekezwa na wazazi na kuwa kizungumzaji chao mabinti wa kikuraish wa Makka kwani alikuwa kijana wa kuvutia na alijaaliwa kuwa na kila kitu ambacho mwanamke yeyote angelihitaji toka kwa mwanamme.
 
Kijana huyu katika pitapita zake mjini Makka alisikia habari za Muhammad alietumwa na Mwenyezi Mungu kuwabashiria bishara njema na kuwalingania watu kumwabudu Mungu mmoja.  Uvumi huu wa ujio wa Mtume uliukumba mji wa Makka na Mus’ab alikuwa akisikiliza sana habari zake na ingawa bado alikuwa mdogo lakini tayari alikuwa ni kijana mwenye hekima na busara.
 
Baada ya kuifuatilia vizuri habari hii alijiunga na wenzake usiku mmoja kwenda kwenye nyumba ya al- Arqam kusikiliza kulikoni hasa!  Alimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu akiwafundisha waislam Quran na kusali na kwa kuwa hekima na busara zilikuwa tayari sifa zake, alipozisikia aya za Quran zikisomwa moyo wake uliingiwa na utulivu ambao haujawahi kumfikia na hapo hapo kutamka “Laa Ilaha ill allah, Muhammad rasuulu llah”
 
Mama yake Mus’ab, Khunaas bint Maalik, alikuwa na haiba kubwa mbele ya Maquraysh wa Makka kufika hadi kuogopewa.  Mus’ab alijitahidi kuficha imani yake akichelea ukali wa mama yake, huku akiendelea kwenda kwa al-Arqam kujifunza zaidi kutoka kwa Mtume Muhammad (SAW).
 
Siri hii haikuchukua muda kwani baadhi ya watu waliokuwa wakimuona Mus’ab akienda nyumba ya al-Arqam walimwambia mama yake Khunaas ambaye alishtushwa sana kusikia kwamba mwanawe amesilimu.  Zilimshtusha sana habari hizi kwani alichelea ghadhabu zitakazomfikia yeye na familia yake kutoka kwa miungu yao ya masanamu waliyokuwa wakiabudu, pia aliangalia nafasi yake mbele ya Maquraish wa Makka kama mwanamke mweye heshima na haiba sasa itakuwaje na mwanawe tayari ameshamuasi na kuwa muislam.
 
Alichokifanya ni kumpiga mwanawe kipigo cha hasira huku akimtaka aachane kabisa na dini ya Muhammad na kurudi kwa Latta, Uzza na Manat (waungu waliokuwa wakiwaabudu Maquraysh).  Mus’ab hakutetereka na kipigo wala mateso aliyoyapata na alibaki katika msimamo wake wa haki.  Kilichomsaidia ni mama yake kumhurumia mwanawe kwa kumwona katika hali mbaya. Huruma hii ya mama, ilichomsaidia ni kuepukana na kipigo tu ila badala yake alifungwa kwa minyonyoro kwenye chumba kichafu ndani ya nyumba yao na kufungiwa humo.
 
Katika hali ya upweke, kifungo na adhabu aliyokuwa akiipata Mus’ab kwa kuamini kwamba hakuna Mola anayepaswa kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah na Muhammad kuwa ni mjumbe wake, alisikia habari za Hijra ya baadhi ya waislam kuelekea Habashah, Ethiopia. Kwa uwezo wake Sub-hana aliweza kupenya kwa kuwatoroka walinzi na kuungana na msafara ulioelekea Habashah katika hijra ya kwanza.  Na kwa ushauri wa Alhabib Mustafa (SAW) alifanya hijra ya mara ya pili kwenda Habashah pamoja na Waislam.
 
Hijra mbili hizi zilizidi kujenga imani ya Mus’ab ya kuwa tayari kuyatoa muhanga maisha yake aliyokuwa akiishi kwa ajili ya Allah (SW).  Siku moja alikuja kwa Bwana Mtume (SAW) na baadhi ya masahaba walikuwa wamekaa naye, jinsi walivyomuona hali yake dhaifu na matambara aliyokuwa amevaa, baadhi ya masahaba waliinamisha nyuso zao na kuanza kutokwa na machozi wakimkumbuka Mus’ab mtanashati mwenye kuvaa nguo za kifahari.  Mtume (SAW) alipomuona Mus’ab alimtazama kwa jicho la hekima huku akitabasamu na kusema, “Mus’ab hapa na hakuna kijana yeyote Makka aliekuwa akipendwa na kudekezwa na wazazi wake kushinda yeye, kisha aliachana nayo yote hayo kwa ajili ya mapenzi ya Allah na Mtume wake”.
 
Mama yake kuona mwanawe hajatetereka bali imani yake ilizidi kuimarika kila kukicha, aliamua kumkatia huduma zote na kumwacha hohe hahe.  Na pale alipokusudia kumfungia kwa mara ya pili aliporudi Habashah, Mus’ab alimwahidi mama yake kwamba akiwa atathubutu kufanya hivyo basi atamuua kila yule atakayemkaribia.  Mus’ab hakuwa akikaidi amri ya mzazi wake bali alikuwa akifuatia ile kauli,  “Hakuna kumtii muumbwa katika jambo litakalomuasi muumba” Mama yake alilia sana kuona Mus’ab mwanawe wa kumzaa anamuendea kinyume na kumuaibisha na kumwambia, “Nenda uendako kuanzia leo mimi si mama yako”. Alichofanya Mus’ab ni kumkaribia mama yake na kumtaka aingie katika Uislam na atamke shahada.   Mama yake alikasirika na kujibu, “Nnaapa kwa nyota kamwe sitoingia katika dini yako nisije nikadhalilisha heshima yangu na kukosa sehemu ya kuweka uso wangu”.
 
Tokea siku hiyo aliachana na mama yake na maisha yake kubadilika kwa kuwa katika hali ya ngumu hata kula yake ilikuwa ya taabu na nguo zake ni matambara ingawa hakuwa kipenzi tena wa Maquraish kwa hali yake hii lakini alikuwa kipenzi cha Mtume (SAW).
 
Katika hali yake hii ndipo pale Mtume (SAW) alipomkabidhi jukumu kubwa katika maisha yake pale alipomchagua kuwa mwanaharakati na balozi wa kwanza wa Mtume katika mji wa Madina.  Kazi aliyoagizwa kufanya ni kuulingania Uislam na kuwaita watu wengine kuja katika dini ya Allah (SW), na pia kuiandaa Madina kwa ajili ya Hijra kubwa itakayofuata.
 
Miongoni mwa waislamu waliokuwapo palikuwa na wakubwa wa umri, walio karibu zaidi kwa Mtume. Lakini Mtume (SAW) alimchagua Mus’ab.
 
Naam! , Mus’ab aliitekeleza kazi yake ipasavyo kwani alipofika Madina kulikuwa na waislam kumi na wawili tu lakini miezi michache baadaye, waislam wa Madina walituma ujumbe wa watu 70 kike na kiume kwenda kwa Mtume akiwemo Maalim wao Mus’ab .  Fikiria hali halisi ya daawah katika mazingira ya kijahiliya na kazi aliyoweza kuifanya Mus’ab Madina ilikuwa ni ya kupigiwa mfano na kuthibitisha kwamba uchaguzi wa Mtume (SAW) haukuwa wa kubahatisha.
 
Siku, miezi na miaka ikapita Mtume (SAW) na masahaba wakahamia Madina, Maquraysh bado walikuwa na hasira za kutisha kwa waislam na vita vya Badr kutokea ambapo makafiri walishindwa vibaya, na baada ya kushindwa wakapanga mipango yao ya kulipiza kisasi na hatimaye kupiganwa vita vya Uhud.  Katika vita hivi Mtume alimteua Mus’ab kuwa mshika bendera, Mus’ab alikubali jukumu hili kwa moyo mkunjufu na kwa heshima kubwa kwani kufikia hadi ya kukabidhiwa bendera imeonesha ni jinsi gani Mtume (SAW) alivyokuwa na imani naye.  Naam! Mus’ab aliongoza jeshi la waislamu kwa kuhakikisha kwamba bendera ya “Laa Ilaha Ill Allah” inasimama wakati wote.
 
Vita viliendelea na waislam kuwapiga na kuwazidi nguvu makafiri hadi ikabidi warudi nyuma na kuanza kukimbia.  Kuona hivyo wale waislam mastadi wa kurusha mishale waliowekwa na Mtume (SAW) milimani kuweka kinga kwa maadui wakaanza kuteremka wakidhani kwamba vita vimekwisha na waislam kushinda.
 
Tendo hili walilolifanya bila ya ushauri wa Amiri jeshi mkuu wa waislam, Mtume (SAW) ndilo lililogeuza ule ushindi uliokuwa ukinukia kwa waislam kuwa kipigo cha ghafla na kuuwawa kwa waislamu wengi.
 
Wakati mtafaruku na vurugu mechi hii inatokea lengo kubwa na makafiri lilikuwa kumuuwa Mtume wa Allah (SW).  Mus’ab aliliona hili na kujua njama yao na hapa alizidi kuisimamisha bendera juu na kusema “Allahu Akbar” na kama simba aliejeruhiwa, alinguruma na kuanza kupigana huku na kule, kubwa alilolikusudia Mus’ab ni kuwashughulisha Makafiri kumfuata yeye badala ya Mtume wa Allah (SW).  Naam! Mus’ab alikuwa peke yake lakini kama ni jeshi zima kwani akiwa na bendera mkono mmoja na upanga mkono mwengine aliendelea kupambana na makafiri ambayo tayari walianza kumzidi nguvu.
 
Mmoja katika Masahaba waliopigana vita vya Uhudi anasimulia jinsi shujaa Mus’ab alivyoweza kupambana na maadui wa uislam kwa dhati na nguvu zake zote.  Ibn Saad amesema; Ibrahim bin Muhammad alisimulia kutoka kwa baba yake ambaye alisema, “Mus’ab alibeba bendera siku ya vita vya Uhud pale ambapo waislamu walipoingiwa na kiwewe na mtafaruku akapigana mpaka alipokabiliana na kafiri Ibn Qum’uah, askari farasi na kukatwa mkono wa kulia .
 
Kuona hivyo Mus’ab  hakuitupa wala kumtoka ile bendera ya kiislam. Ilisimama huku akiibeba kwa mkono wake wa kushoto huku akisema kwa sauti kubwa kuwaambia makafiri “Hakuwa Muhammad ila ni Mtume wa Allah, na Mitume walikuja na kupita kabla yake”.  Ibn Qumuah akamkata Mus’ab mkono wake wa kushoto, Mus’ab akiwa tayari keshakatwa mikono yote miwili aliendelea kukamata bendera kwa ile sehemu tu ya mkono iliyobakia na kuigandanisha na kifua chake huku damu zikichuruzika na kuendelea na kauli yake, “Hakuwa Muhammad ila ni Mtume wa Allah, na Mitume walikuja na kupita kabla yake” . Akaja kafiri mwengine na kumchoma Mus’ab mkuki uliomwangusha chini akidondoka pamoja na bendera.
 Nyota ya mashujaa imeanguka. Mus’ab alipigana vita hivi kwa ajili ya Allah (SW), vita ambavyo alipigana vilikuwa mtihani mkubwa kwa waislam, mtihani wa kujitolea muhanga na mtihani wa imani.  Kilichokuwa moyoni mwa Mus’ab ni kwamba akianguka, basi makafiri watamfikia Mtume (SAW) na kumuuwa, kwani asingekuwa na kinga wala himaya, akapatwa na woga (kuuwawa kwa Mtume na mapenzi ya Mtume) na hadi anachomwa mkuki na kudondoka bado alikuwa akirudia ile kauli yake “Hakuwa Muhammad isipokuwa ni Mtume, na Mitume walikuja na kupita kabla yake”. 
Kwa heshima kauli hii baadaye ilikuja kuteremka kwa Quran kama ilivyo katika Surat Al Imraan/144
 “ Na Muhammad hakuwa ila ni Mtume tu wamekwisha kupita kabla yake mitume. Je akifa au kuuwawa ndiyo mtageuka mrudi nyuma ?……..” 
Baada ya kumalizika vita masahaba waliuona mwili wa Mus’ab uko kifudifudi labda kwa kuogopa kuona madhara yatakayompata Mtume wa Allah au kuona haya kufa shahidi kabla ya kuhakikisha usalama wa Mtume (SAW).  Mtume (SAW) pamoja na masahaba wake walikuwa wakipita kukagua majeruhi na kuwaaga mashahidi na alipofika ulipo kuwepo mwili wa Mus’ab alisita na kuanza kutokwa na machozi.
 Amesema Khabbab ibn Al-Aratt kwamba, “Tulifanya Hijra pamoja na Mtume kwa ajili ya Allah (SW).  Baadhi tu walifariki hata kabla ya kufaidi matunda ya Hijra na malipo yake, miongoni mwao ni Mus’ab hakuacha kitu chochote pale alipokufa shahidi isipokuwa tambara tu alilokuwa akivaa.  Wakati tunamkafini kwa tambara hili lilikuwa halimtoshi kwani tukimfunika kwenye miguu uso wake unakuwa wazi na tukimfunika usoni miguu inaonekana!  Mtume (SAW) akasema , “Mfunikeni kwenye uso na sehemu itakayobaki muwekeeni majani kwenye miguu”. 
Mtume (SAW) alisimama na kuuangalia mwili wa Mus’ab huku machozi yakimtoka na kusoma,
 
“Miongoni mwa waumini wapo watu ambao wametimiza yale waliyoahidiana na Allah (SW) juu yake . Baadhi yao wamekwisha kufa na baadhi yao wanangojea, wala hawakubadilisha (ahadi) hata kidogo”  Suuratul Ahzaab / 23
 Akiangalia tambara alilopambiwa Mus’ab, Mtume (SAW) alisikitika sana na kusema, “nilikuwa nikukuona Makka ulikuwa kipenzi na kivutio kuliko vijana wote leo hii uko hapa na tambara tu!” Kisha Mtume  (SAW) akautazama uwanja wa vita jinsi ulivyojaa mashahidi na kusema “Mtume wa Allah (SW) anashuhudia kwamba nyinyi ni mashahidi wa Allah siku ya kiama”