Al Rabiy Ibn Zayad Al Haarithy Upanga Unaopambana na Maadui


MAISHA YA MASAHABA
 صور من حياة الصحابة
cha Mwandishi Dr. Abdurrahman Raafat Al-basha)

Kimefasiriwa na Ustaadh Talib Juma

Huu ni Mji wa Madina, bado unatuliza huzuni zake kwa kifo cha kipenzi  - Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam). Na pia unasikitishwa na kifo cha Khalifa Abubakr Assiddiyq, Alla amuwie radhi
 
Na hawa ni wawakilishi mbali mbali wanakuja toka miji mbali mbali kumfanyia bay-‘ah  Khalifa ‘Umar ibn Al Khattaab juu ya utiifu kwa kila hali.
Asubuhi moja ulimjia Amirul Muuminina ‘Umar, ujumbe wa Bahrain na kundi la wajumbe wengine. Alikuwa ‘Umar Al Farouq ni mwenye hima ya kusikiliza ujumbe wa wajumbe wote wanaomjia pengine, apate katika mazungumzo yao mawaidha na fikra zenye manufaa au nasaha kwa ajili ya Allah na kitabu chake na kwa waislamu wote. Lakini licha ya fursa waliyopewa hapakuwa na mazungumzo yenye kuingia akilini mno.
Akamtazama mmoja wa watu, alietarajia kwake kheri na akamwambia; "Sema ulichonacho". Yule mtu akamshukuru Allah Subhaanahu Wata’ala na akasema; "Hakika wewe ni Amirul Muuminina hujatawalishwa masuala ya umma huu ila ni mtihani wa Allah Subhaanahu Wataa’ala amekuletea kwako. Mche Allah kwa yale uliyotawalishwa na tambua akipotea kondoo mmoja pembezoni mwa mto Euphrate (Alfurat) utaulizwa siku ya kiyama"
Amirul Muuminiina alilia kwa sauti kubwa akasema; "Hakika hajapata mtu kuniambia maneno ya ukweli tangu nilipopata ukhalifa kama ulivyoniambia wewe".
Akauliza; “Wewe ni nani hasa?"
Akasema; “Al Rabiy ibn Zayad Al Haarithy"
Akasema;“Ndugu yake Al Muhajir ibn Zayad?"

Akasema; "Ndiyo."
Baada ya wageni kuondoka, Amirul Muuminiina alimwita Abu Mussa Al Ash’ary na akamwambia; “Hebu mfuatilie Al Rabiy ibn Zayad akiwa ni mkweli, basi atakuwa ni mtu wa kheri nyingi na atatusaidia katika kazi yetu. Hivyo mpe majukumu na uniandike habari zake".
Hazikupita siku nyingi mpaka Abu Mussa Al Ash’ary alipotayarisha jeshi kufungua mji wa Manadhir katika ardhi ya Al-Ahwazi. Kwa amri ya Khalifa akawachagulia katika kikosi Al Rabiy ibn Zayad na ndugu yake Al Muhajir. Abu Mussa Al-ash’ary aliuzunguka mji wa Manadhir na akaingia nao vitani, vita ambavyo  vilikuwa vikali havikuwa na mfano wake.
Washirikina waliingia vitani kwa nguvu zao zote na subira ambavyo haikutarajiwa na waislamu walikufa wengi bila ya matarajio. Waislamu walipigana siku hiyo wakiwa wamefunga ndani ya Ramadhaan.
Alipoona Al Muhajir vifo vimekuwa vingi ndani ya safu za waislamu, akaazimia kuiuza nafsi yake kupata radhi za Allah Subhaanahu Wata’ala na akajitayarisha kwa mauti na kumuusia ndugu yake.
Alitoka Al Rabiy kwenda kwa Abu Mussa akamwambia; “Hakika Al Muhajir ameazimia leo kuiuza nafsi yake kwa ajili ya Allah nae amefunga. Na waislamu wamo kwenye vita na wamefunga jambo lenye kupunguza azma na nguvu zao na hawataki kufungua, hebu fanya unaloliona (la kheri).”
Abu Mussa Al Ash’ary akasimama na kulihutubia jeshi: “Enyi waislamu, naapa kwa kila aliefunga kwamba afungue au aache kupigana”
Akachukua birika la maji akanywa ili watu wamfuate. Aliposikia Al Muhajir maneno hayo akapiga funda la maji na kusema; “ Wallahi sijapiga funda hili kwa sababu ya kiu lakini ni kuitikia kiapo cha Amiri wangu.”
Akachukua upanga wake akaanza kukata safu na kupambana bila ya khofu wala woga. Alipoingia ndani ya jeshi la maadui wakamzingira kila pembe na panga zikamzingira mbele na nyuma mpaka kufariki.
Wakakikata kichwa chake na kukitundika juu ya nguzo refu katikati ya uwanja wa vita. Al Rabiy akamtazama na kusema; “Umefanikiwa na marejeo mazuri. Wallahi nitalipiza kisasi kwa ajili yako na kwa ajili ya waislamu waliouawa..” Abu Mussa alipoona hali ile ya huzuni ya Al Rabiy juu ya ndugu yake na alidiriki kinachompitikia kifuani mwake dhidi ya adui, aliamua kumpa uongozi wa kikosi na akaelekea kufungua mji wa Al Suusi.
Al Rabiy na askari wake waliwashambulia washirikina mfano wa kimbunga na kuzivamia ngome zao mfano wa majabali yanayovamiwa na mafuriko. Wakavunjavunja safu zao na kuvunja nguvu zao na Allah akajaalia ufunguzi wa Manadhir katika mikono ya  Al Rabiy ibn Zayad kwa kujisalimisha watu wake. Wakauawa waliojaribu kupigana na wengine wakatekwa na waislamu kupata ngawira nyingi.
Nyota ya Al Rabiy ibn Zayad iling'ara baada ya vita vya Manadhir na jina lake kutajwa na kila ulimi. Akawa ni mmoja ya viongozi wakubwa wenye kupendwa na wanaotarajiwa amali bora. Waislamu walipoazimia kufungua mji wa Sajistani alikabidhiwa uongozi wa kikosi na kutarajiwa nusra.
Aliendelea Al Rabiy ibn Zayad na jeshi lake la ufunguzi katika njia ya Allah kuelekea Sajistan akikata pori lenye urefu meli sabini na tano zisizo rahisi hata kukatwa na wanyama.
Ikawa mji wa mwanzo kumkabili njiani ni Rostokzalik kwenye mipaka ya Sajistan. Hii  ni ngome kuu iliyokuwa na majengo na makasri ya fakhari yaliyo ndani ya ngome kubwa na ndani yake mna aina mbali mbali za miti.
Al Rabiy alituma wapelelezi kabla ya kuingia Rostokzalik. Wakapata habari ya kwamba maadui walikuwa wanajitayarisha kwa moja ya sherehe zao. Akangoja awashtukizie usiku wa sikukuu hiyo na aweze kuwateka na kuufungua mji bila ya vita.
Akawateka mateka wasiopungua ishirini elfu na kiongozi wa mji ule akawa ni jumla ya mateka wa vita. Mmoja ya waliotekwa alikuwa amekusanya mali ya kiongozi wake ifikayo elfu thelathini[i] amekusanya kumpelekea kiongozi wake.  Al Rabiy akamuuliza;
“Umepata wapi mali zote hizi?”
Akasema; “Kijiji cha karibu cha bwana wangu.”
Akasema “ Je watu wa kijiji kimoja wamemkusanyia na kumpa mali yote hii?”
Akasema; “Ndiyo”
Akasema; “Vipi?”
Akasema; “kwa majembe yetu, masururu yetu na jasho letu.
Vita viliposimama,  mkubwa wa mji Adahqaan akaja kwa Al Rabiy kwa ajili ya kutaka kutoa fidya ili aachiwe yeye na jamaa zake.
Akamwambia Al Rabiy; “Nitakuachia huru ikiwa utatoa fidya ya kutosha kwa waislamu".
Akasema; "Unataka kiasi gani?"
Akasema; "Chomeka mkuki huu ardhini halafu ujaze dhahabu na fedha".
Akasema; “Nimekubali”
Akaanza kutoa fedha na dhahabu katika hazina zake na kuanza kujaza mkuki hadi ukazama.
Liliingia jeshi la Al Rabiy ibn Zayad lenye kushinda ardhi ya Sajistan na zikawa ngome zake ni zenye kuanguka moja baada ya nyengine kama majani ya miti yanavyopukutika kwenye msimu wa baridi[ii].
Watu wa mji huo wakawa ni wenye kujisalimisha na kutafuta amani kabla ya panga usoni mwao mpaka Al Rabiy akafika mji wa Zaranji (mji Mkuu wa Sajistani)
Hapo walimkuta adui amejidhatiti vya kutosha na katayarisha vikosi vya kupambana. Na akatangulizia wasaidizi wa kumsaidia mapambano akiwa na azma ya kurejesha nyuma kikosi cha waislamu kutoka mji mkuu na kusimamisha usongaji mbele wa waislamu kutoka Sajistan kwa thamani yoyote ile.
Vita vikali vilitokea baina Al Rabiy na maadui wake ambavyo uzito wa mhanga wake ulielemea pande zote mbili. Alama za ushindi zilipoonekana kwa waislamu aliona Mirzabani[iii] aliyejulikana kwa jina la Perwaz aje kwa Al Rabiy kutafuta suluhu akiwa bado ana nguvu labda pengine atafanikiwa yeye na watu kwa jambo zuri.
Akatuma mjumbe wake kwa Al Rabiy kupeana miadi kwa ajili ya mazungumzo ya suluhu. Al Rabiy aliwaamrisha watu wake wapange kwenye majlis mabaki ya askari wa kifursi na njiani ambamo atapita Perwaz mtawanywe miili ya askari wake waliouawa.
Al Rabiy alikuwa ni mtu mrefu wa kimo mwenye hima kubwa sana.  Pia ni mwenye rangi iliyokoza wekundu, mpana wa maumbo mwenye, kuogopesha kwa anaemtazama. Perwaz alipoingia kwa Al Rabiy, mwili ulimsisimka na hofu kumjaa kwa miili ya maiti njiani akashindwa kumkaribia Al Rabiy na hata kumpa mkono kumsalimia.
Akasema nae kwa kigugumizi na kitetemeshi cha ulimi na akataka suluhu na kwamba atamletea vijana elfu kila mmoja amebeba sinia yenye dhahabu na Al Rabiy alikubali suluhu hiyo. Siku ya pili yake Al Rabiy aliingia mjini akiwa na vijana hao huku waislamu wakileta tahlili[iv] na takbir[v] ilikuwa ni siku kubwa katika siku za Allah.
Alibakia Al Rabiy ibn Zayad akiwa kama  upanga ndani ya mikono ya waislamu ukipambana na maadui. Na Allah akawafungulia miji na majimbo hadi pale uongozi ulipokuwa mikononi mwa Banu Umayyah na Mu’awiya ibn Abu Sufiyan.  Al Rabiy akapewa uliwali wa Khurasan lakini hakupendezwa na uongozi wa Banu Umayyah.
Akabaki na kutoridhika kwake hadi pale Zayad ibn Abeyh mmoja wa viongozi wakuu wa Banu Umayyah alipomwandikia na kumwambia:
“Amirul Muuminina Mu’awiyah ibn Abi Sufiyan anakutaka ubakishe fedha na dhahabu katika Baytul Maal na nyenginezo uzigawe kwa mujahidina.” Akamwandikia kumjibu; “Mimi nimekipitia kitabu cha Allah kinaamrisha kinyume na unavyoniamrisha wewe kupitia Amirul Muuminina.” Akawaita watu wake na kuwaambia chukueni ngawira zenu.Na khumsu (moja ya tano) iliyobaki akaipeleka makao makuu ya ukhalifa Damascus.
Ilipofika siku ya Ijumaa akisoma barua ile, alitoka Al Rabiy ibn Zayad kwa ajili ya  sala ya Ijumaa akiwa amevaa nguo nyeupe akawahutubia watu (hotuba ya Ijumaa) na akasema; “Enyi watu mimi nimeshachoshwa na uhai hivyo naomba du’aa na itikieni Amin.”
Akasema; “Ewe mola ikiwa ni mwenye kunitakia kheri basi nifishe haraka au kidogo kidogo”. Watu wakaitikia; “Amin" Jua halikumaliza kuzama siku ile, Al Rabiy akatangulia kwa Mola wake.

 

[i] Mwandishi hakutaja kama ni za dhahabu au za fedha
[ii] Katika nchi za baridi majani ya miti hupukutika wakati wa pupwe na kuanza upya baada ya baridi
[iii] Kiongozi wa mji
[iv] Laa ilaha illa Llah
[v] Takbir ina maana ya Allahu Akbar