Nuaim Ibn Masoud - Vita ni Hadaa





Nuaim Ibn Masoud - Vita ni Hadaa



Nu’aim ibn Masoud ni kijana alie na moyo mpana na akili nyingi na mbinu za kutosha na asieshindwa na jambo bali huwa na hila na njia za kutoka. Ni mfano bora wa kijana wa jangwani kwa kila maana, kutokana na sifa aliyopewa na Allah Subhaanahu Wata’ala ya kufikiria.
Lakini alikuwa ni mwenye kupenda raha na urafiki ambao aliudhihirisha kwa marafiki zake wa kiyahudi wa Madina. Alikuwa kila anapotaka starehe ya waimbaji wa kike na masikio yakitamani nyuzi za ala (Muziki na nyimbo), hufanya safari kutoka kwao Najd na kuelekea Madina ambapo hupoteza mali nyingi kwa mwanamke wa kiyahudi ili apate starehe kwa wingi.
Hili lilimfanya mara kwa mara aende na kurudi Madina jambo lililopelekea awe na urafiki mkubwa na mayahudi hasa wa kabila la Bani Quraidhah.
Mwenyezi Mungu aliukarimu ubinadamu kwa kuwateremshia Mtume wa uongofu na haki na vichochoro vya Madina kung’ara kwa nuru ya Uislamu. Alikuwa Nu’aim bado ni mwenye kuzama nafsi yake katika dimbwi la matamanio, akaupinga uislam kwa nguvu zake zote, akiogopea usijemzuia na matamanio yake na raha zake.  Akajikuta nafsi yake ni mwenye kujiunga na mahasimu wa Uislamu wakubwa akiwa tayari kutoa upanga dhidi yake.
Lakini Nu’aim ibn Masoud alifungua ukurasa mpya siku ya vita ya Al - Ahzaab katika tarehe ya da’awah ya kiislamu na akajiweka katika kurasa hizo za kitabu cha mbinu na hadaa za kivita. Kisa ambacho kingali kinasimuliwa na tarehe kwa mshangao kwa milango yake madhubuti na kwa mshangao wa ushujaa wake na umahiri wa akili yake. Ili usimame katika kisa hiki cha Nu’aim ni lazima urejee kwanza nyuma kidogo.
Kabla ya vita vya Al - Ahzaab kwa muda mdogo, mayahudi walikutana Madina na viongozi wao wakawa wanakusanya makundi kwa ajili ya kumpiga vita Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) na kuivunja dini yake.
Wakawaendea Makureshi, Makkah na kuwashawishi kupambana dhidi ya waislamu na wakawaahidi kuwaunga mkono watakapowasili Madina na wakapeana ahadi bila ya kuivunja na wakawapa wakati maalum.
Makureshi walitoka Makkah kwa jumla yao, walio juu ya vipando na waendao kwa miguu wakiongozwa na Abu Sufiyan wakielekea Madina. Wakatoka Ghatfan kutoka Najd na kila kitu chao na watu wao wakiongozwa na kiongozi wao Uyeynah ibn Hisnu Al -Ghatfany na miongoni mwao ni shujaa wa kisa hichi Nu’aim ibn Masoud.
Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) alipopata habari ya kutoka kwao, aliwakusanya masahaba wake na kuwashauri juu ya hali hii na hatua ya kuchimba Khandak ikapitishwa kuuzunguka mji wa Madina, ili kuzuia uvamizi huu na Khandak kuwa ni kizuizi kikuu dhidi ya jeshi hilo.
Kabla ya kukaribia vikosi vya Makkah na Najd milangoni mwa Madina, viongozi wa Mayahudi Banu Nadhir waliwaendea viongozi wa mayahudi wa Bani Quraidhah na kuaanza kuwashawishi kuingia vitani pamoja nao dhidi ya Muhammad na kuwataka kuyaunga mkono majeshi ya Makkah na Najd. Lakini viongozi wa Banu Quraidhah wakawajibu; “Hakika mumetuambia jambo tunalolipenda na kulitaka lakini mnajua kuwa sisi na Muhammad tuna mikataba ili tuweze kuishi Madina kwa salama na amani, na hata wino wa mikataba hiyo bado haujakauka.”
“Nasi tunaogopa atakaposhinda Muhammad vita, atatushambulia kwa nguvu zote, na kututoa Madina ikiwa ni malipo ya khiyana yetu.”
Lakini viongozi wa Banu Nadhir wakazidi kuwaghururi  Banu Quraidhah kuvunja mkataba na kuwahakikishia ushindi na hilo halina muhali.
Wakawatia tamaa kwa sababu ya vikosi viwili vikubwa ambavyo vinashiriki. Banu Quraidhah wakalainika na kuvunja mkataba wao na Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam). Wakachanachana waraka wa mkataba na wakatangaza kujiunga na washirika wa Al - Ahzaab katika vita. Waislam waliipokea habari hii kama vile radi. Majeshi ya Al - Ahzaab yaliuzunguka mji wa Madina na kukata njia za misaada na vyakula. Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) akahisi hakika sasa yumo ndani ya midomo ya makulabu ya adui.
Makureshi na Ghatfan wamepiga kambi uso na macho na waislam nje ya mji wa Madina. Na Banu Quraidhah wanaangaza ndani na kujitayarisha nyuma ya waislamu. Vilevile  ndani ya Madina wanafiki na wale madhaifu wenye maradhi nyoyoni wameanza kufichua siri zao na kusema; “Muhammad alikuwa daima akituahidi kumiliki hazina za mfalme Kisra na Kaizari na sisi leo hakuna hata mmoja alie na dhamana ya usalama wa nafsi yake au kwenda hata chooni kufanya haja yake".
Wakaanza kutawanyika toka kwa Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) kundi baada ya kundi, kwa hoja ya woga na hofu kwa wake zao, watoto wao na nyumba zao dhidi ya shambulizi linalotarajiwa toka Banu Quraidhah vita vitakapoanza. Na hawakubakia pamoja na Mtume ila mamia machache ya waislam walio wakweli.
Katika usiku mmoja wa mzunguko uliodumu siku ishirini, Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) alielekeza uso kwa Mola wake na kumuomba du’aa ya mwenye shida na kusema; “Ewe Mola nakuomba ile ahadi yako, ewe Mola nakuomba ile ahadi yako".
Usiku ule Nu’aim ibn Masoud alikuwa akihangaika mchagoni (kitandani) pake kama vile mtu aliegongomelewa misumari. Macho kayafumbua usingizi umeruka. Akawa ni mwenye kukodolea nyota zilizotanda kwenye mbingu zilizo safi kabisa huku amezama ndani ya tafakuri. Ghafla akajikuta ni mwenye kujiuliza;
 “Una nini ewe Nu’aim?! Ni kitu gani kilichokuleta toka mbali huko Najd kuja kumpiga vita mtu huyo na wenzake".
 “Wewe humpigi vita kwa kunusuru haki aliyoiiba au kulinda heshima iliyovunjwa bali umekuja pasina sababu ijulikanayo".
"Inasihi kwa mtu mwenye akili mithili yako kupigana ukauawa au kuuwa pasina sababu?"
"Ewe Nu’aim ni jambo gani linakupelekea kunyanyua upanga wako mbele ya uso wa mtu huyu mwema, mwenye kuamrisha wafuasi wake uadilifu, na ihsani na kutendea wema walio karibu?".
"Ni kitu gani kinakufanya uchomoe mkuki wako ndani ya ala dhidi ya wafuasi wake ambao amewalingania haki na uongofu?".
Hakumaliza mazungumzo haya mazito na nafsi yake ila ni uamuzi wa mwisho kabisa aliyoutekeleza hapo hapo.
Nu’aim akanyemelea kutoka katika kambi yake chini ya kiza kizito, na kupiga hatua kuelekea kwa Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam). Mtume alipomuona mbele yake alimwita;
 “Nu’aim ibn Masoud?”. Akasema;
 “Ndio ewe Mtume wa Allah”
"Kitu gani kimekuleta saa hizi?”
 “ Nimekuja kutamka shahada. Na wewe ni mja na mjumbe wa Allah na uliyokuja nayo ni haki" Akaendelea: “Mimi nimesilimu ewe Mtume wa Allah na watu wangu hawajui kusilimu kwangu. Niamrishe utakalo"
Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) akasema;
 “Wewe ni mmoja wetu. Hebu nenda kwa watu wako na ufanye hila utuepushe nao. Hakika vita ni hadaa".
Akasema; “Naam ewe Mtume wa Allah utaona yale yenye kukupendeza InshaAllah"
Akatoka Nu’aim hapo hapo na kuelekea kwa Banu Quraidhah, kwani kabla alikuwa ni marafiki na vipenzi wake. Akawaambia. “Enyi Banu Quraidhah, mnajuwa mapenzi na urafiki wangu kwenu hivyo nimekuja kuwapa nasaha" Wakasema;
“Ndio wewe kwetu siye mwenye tuhuma”.
Akasema; "Hakika Makureshi na Ghatfan ni wenye nafasi kubwa kwenye vita hivi, kinyume nanyi"
Wakasema; “vipi”?
Akasema; “Nyinyi hii ni nchi yenu mna mali zenu, watoto wenu na wake zenu. Hamna nafasi ya kuhama kwenda kwengine. Ama Makureshi na Ghatfan, nchi yao, mali zao, watoto wao na wake zao wako nje ya mji huu. Wamekuja kupigana na Muhammad na wamekutakeni mvunje mikataba na muwaunge mkono mkakubali”.
“Wakifanikiwa basi mmefanikiwa ama wakishindwa kumpiga vita wakirudi kwao, kwa salama watakuacheni nyinyi na Muhammad nae atakulipizieni kisasi kibaya kabisa".
 “Na mnajua hamna uwezo kwake peke yenu".
Wakasema; “ Umesema kweli sasa nini ushauri wako”?
Akasema; “Ushauri wangu, ni kwamba msipigane nae mpaka, kundi la watu bora wao muwe nalo kama rehani mikononi mwenu. Kwa hilo mtafanya wapigane na Muhammad mpaka kushinda, au watu wote nyinyi nao mmalizike"
Wakasema; “Umeelekeza na kutoa nasaha"
Nu’aim akatoka na kumuelekea Abu Sufiyani ibn Harb, mkuu wa Makureshi akamwambia yeye na walio nae;
“Enyi makundi! Mnajua tosha mapenzi yangu kwenu na mnajua uadui wangu kwa Muhammad. Lakini nimepata habari nimeona ni vyema na haki nikujuilisheni kama ni nasaha, mzifiche na wala msizitangaze kuwa ni mimi niliekwambieni"
Wakasema; "Umepata ahadi hiyo"
Akasema; “Banu Quraidhah wanajutia juu ya uadui wao kwa Muhammad, na wamemtuma mjumbe kumwambia. ‘Hakika sisi tunajuta juu ya matendo yetu na tumedhamiria kurudi kwenye mkataba wetu na amani yetu’. ‘Je utaridhika tukikukabidhi watu bora na wengi baina ya Makureshi na Ghatfan ili uwauwe, kisha tutajiunga nawe kuwapiga vita?".
Akaendelea kuwaambia; “Basi watakujieni Mayahudi wanataka kwenu rehani ya watu wenu msiwape hata mtu mmoja".
Akasema Abu Sufiyan; “Wewe ni rafiki mwema utalipwa kheri”
 Kisha akatoka Nu’aim kuelekea watu wake wa Ghatfan akawaambia kama yale aliyomwambia Abu Sufiyan na akawahadharisha  aliyomtahadharisha.
Abu Sufiyan alitaka kuwajaribu Banu Quraidhah. Akamtuma mwanawe akasema; "Abu Sufiyan anakusalimieni na anasema ‘muda umekuwa mwingi wa kumzunguka Muhammad na watu wake na tushachoka. Nasi tumeazimia kupigana nae tumalizane nae’.
"Hivyo baba yangu amenituma nikwambieni kwamba kesho tupambane".
Wakasema; “Kesho ni Jumamosi na sisi hatufanyi kazi. Halafu sisi hatutapigana pamoja nanyi hadi mtupatie watu wenu bora sabini pamoja na Ghatfan wawe ni rehani. Sisi tuna wasiwasi vita vikipamba moto mtakimbilia kwenu haraka na kutuacha peke yetu na Muhammad na mnajua sisi hatumuwezi Muhammad".
Aliporudi mtoto wa Abu Sufiyan kwa jamaa zake akawapa habari kwa aliyoyasikia toka Banu Quraidhah, wakasema kwa pamoja; “Waovu gani hawa wajukuu wa manyani na nguruwe, Wallahi wangelitaka kondoo tu awe ni rehani tusingaliwapa”
Amefanikiwa Nu’aim ibn Masoud kuvunja safu za Al-Ahzaab na kuuvunja umoja wao.
Allah akawapelekea makureshi na washirika wao upepo mkali uliong'oa mahema na kuangusha vyungu  kwenye mafya. Moto ukazimika, nyuso zikamiminiwa mavumbi hawakuwa na hila ila kuvunja kambi na kurudi makwao ndani ya kiza kizito.
Asubuhi kuchomoza waislamu wanakuta maadui wameshaondoka. Wakawa wanasema; “Alhamdulillahi alienusuru waja wake, akatukuza jeshi lake, akayashinda makundi peke yake".
Akabakia Nu’aim tangu siku ile  ni mwenye kuaminiwa na Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) akampa majukumu mbali mbali na akabeba mikononi mwake bendera (ya jihadi). Ilipofika siku ya Fat-h (kuikomboa) Makkah, Abu Sufiyan alisimama na kuangalia vikosi vya waislamu, alimuona Nu’aim akibeba bendera ya Ghatfan.
Akawauliza walio nae; "Nani yule?”
Wakajibu; “Nu’aim ibn Masoud”
Akasema; “Ametutendea uovu huyo siku ya Khandak. Wallahi alikuwa ni mtu adui mkubwa wa Muhammad na huyu sasa anabeba bendera ya Qaumu yake na anakuja kwa kutupiga vita chini ya bendera yake!?”.