Rabiah ibn Ka'ab- mwambata wa Mtume Muhammad (SAW)



Rabiah ibn Ka'ab- mwambata wa Mtume Muhammad (SAW)

 
Hiki ni kisa cha Rabiah kama mwenyewe anavyosimulia.
 
“Nilikuwa bado ndogo pale nuru ya imani iliponimulika na moyo wangu kufunguka na mafundisho ya dini ya kiislam na pale macho yangu yalipomuona mjumbe wa Mwenyezi Mungu kwa mara ya kwanza.  Nilimpenda pendo lisilokuwa na mfano.  Nilimpenda kuliko mtu mwengine yoyote.   Siku moja nikajisemea mwenyewe moyoni:
 
“Ole wako Rabiah, kwanini hujitolei nafsi yako kumhudumia Mtume (SAW).  Nenda na mtake shauri kwa hili.  Ikiwa ataridhika na wewe, utaona raha kuwa karibu naye, utakuwa na mafanikio kupitia mapenzi yako kwake na utakuwa na bahati nzuri ya kupata mambo mema hapa duniani na mema huko akhera.”
 
Nikafanya kama nafsi yangu ilivyoniagiza.  Mtume (SAW) hakunivunja moyo na alifurahi sana.  Tokea siku hiyo nikaanza kuishi chini ya kivuli cha Al-Habib Mustafa.  Niliongozana naye kila anapokwenda na kila anapogeuza uso wake na kunitazama, basi huruka haraka na kuwa mbele yake.  Akitaja tu shida yake, hunikuta tayari nimeshaanza kuitimiza.
 
Nitamshughulikia mchana na usiku unapoingia, na Mtume (SAW) kumaliza kusali sala ya Isha na kurudi nyumbani kwake, hufikiria kuondoka, lakini papo hapo hujisema moyoni:
“Wapi utakwenda Rabiah? Labda utaweza kuhitajika kumfanyia jambo Mtume (SAW) usiku.  Hivyo hubakia mlangoni kwake.  Mtume (SAW) huutumia baadhi  ya usiku kwa kusali.  Humsikia akisoma suratul Fatiha na huendelea kusoma nusu ya thuluthi ya usiku.  Mimi huchoka na kuondoka au macho yangu kuchoka na kulala.
 
Ilikuwa ni tabia ya Mtume (SAW), ikiwa mtu atamtendea jambo loloate zuri basi na yeye humrudishia mara mbili yake.  Alitaka kunifanya na mimi pia kwa jinsi nilivyokuwa nikimhudumia.  Siku moja akanijia na kuniambia:
“Ewe Rabiah ibn Kaab! 
Nikamuitika, “Labbayka yaa Rasulullah.”
 “Niombe kitu chochote utakacho na nitakupa.” 
Nikafikiri kidogo kisha nikamwambia Mtume (SAW):
 
“Nipe muda kidogo, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu, kufikiria hicho ninachokitaka halafu nitakujulisha.”
 
Kipindi hicyo nilikuwa bado kijana na maskini.  Sikuwa na aila wala utajiri na hata sikuwa na pahala pangu mwenyewe.  Nilikuwa nikilala msikitini kama walivyokuwa waislam wengine maskini kama mimi.  Watu walikuwa wanatutania ‘wageni wa uislam’.  Endapo muislam yoyote akileta sadaqa kwa Mtume (SAW) hutuletea sisi yote.  Na kama akipewa zawadi huchukua kidogo na iliyobaki pia kutuletea sisi.
 
Ikamjia nimuombe Mtume (SAW) jambo zuri la kidunia ambalo lingeniepusha na ufukara na kuwa kama wale wenye utajiri, wake na watoto.  Hapo hapo nikajisuta:
“Angamia wee Rabiah, dunia hii ni ya muda tu, una rizki yako ambayo tayari Mwenyezi Mungu amekuandikia na utaipata.  Mtume (SAW) anayo sehemu maalum kwa mola wake na ombi lake halikataliwi.  Kwa hivyo muombe Mtume (SAW) amuombe Mwenyezi Mungu akupe jambo la kheri na wewe akhera!”
Nikajihisi kuwa na furaha na wao hili na nikaenda kwa Mtume (SAW) na akaniuliza:
 “Unasemaje Rabiah?” 
Nikamjibu, “ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu, ninakuomba uniombee kwa mola kwa niaba yangu niwe mwenzako peponi.”
 
Mtume akauniuliza,
 
“ni nani aliyekupa wazo hili?”
 
“Hakuna mtu yoyote aliyenipa wazo.  Lakini pale uliponiambia niombe chochote na nitakupa, nikafikiri kukuomba khayraat za kidunia.  Baada ya muda tu nikaongozwa kuchagua kitu cha kidunia na milele kuliko kitu cha kupita na kumalizika ndo maana nikaomba hilo.”
 
Mtume Muhammad (SAW) akanyamaza kwa muda kisha akasema:
 “Huna ombi jengine zaidi ya hilo Rabiah?” 
Nikamjibu, “sina, mjumbe wa Mwenyezi Mungu hakuna chengine kitakachoweza kufanana na nililoliomba.”
 
“Ikiwa ni hivyo, basi nisaidie kwa minajili yako kwa kuzidisha sijda kwa Mwenyezi Mungu (SW),” akasema Mtume (SAW).
 
Hivyo nikazidisha juhudi katika kufanya ibada ili kupata bahati ya kuwa pamoja na Mtume (SAW) peponi.  Nilivyopata bahati ya kuwa mtumishi na sahaba wake hapa duniani.
 
Haikupita muda Mtume (SAW) akaniita na kuniuliza:
 “Hutaki kuoa Rabiah?” 
“Sitaki kitu chochote kitakachonishughulisha katika kukuhudumia.” Nikamjibu.
“Halikadhalika sina chochote cha kutoa mahari na wala pahala pa kukaa na mke.”
Mtume (SAW) akatulia kimya hakusema kitu siku hiyo.  Aliponiona tena siku nyengine akaniuliza tena suala la kuoa na jibu likawa lile lile.
 
Nilipokuwa peke yangu na kufikiria zaidi nikajuta kauli yangu ile na kujilaumu mwenyewe;
“Ole wako Rabiah, Mtume (SAW) anafahamu zaidi yako kujua lipi zuri kwako hapa duniani na huko akhera na anajua zaidi yako nini ulichonacho.  Basi ikiwa Mtume (SAW) ataniuliza tena kuhusu kuoa, nitamjibu nipo tayari.
 
Haukupita muda, Mtume (SAW) akaniuliza tena:
 “Hutaki kuoa Rabiah?” 
“Ninataka, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu,” nikamjibu.  “Lakini nani atakuwa tayari kuolewa na mimi hasa katika hali hii ambayo unaijua? Nikamuuliza.
Mtume (SAW) akasema,
  “nenda kwa familia ya fulani na uwaambie: Mtume (SAW) ameagiza nije kuposa kwenu.” 
“Kwa unyonge nikaenda na kusema kama nilivyoambiwa na Mtume Muhammad (SAW).  Wakashangaa na kusema, “mtoto wetu! ?”
Nikawajibu, “ndio mtoto wenu.”
“Karibu Mtume wa Mwenyezi Mungu, karibu mjumbe wake, mjumbe wa Mtume wa Mwenyezi Mungu atarudi huku amefanikiwa lengo lake.  Wakatufungisha ndoa.  Nikarudi kwa Mtume (SAW) kumpa habari njema.
 
“Ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu, nimekuja kutoka nyumba iliyobora kabisa.  Waliniamini (maneno yangu), wakanikaribisha na kunifungisha ndoa na binti yao.  Lakini wapi nitapata mahari ya kumpa mke wangu?”
 Mtume (SAW) akaagiza kuitwa Buraydah ibn Al-Khasib mmoja katika wakubwa wa kabila langu Banu Asiam na kumwambia, “ewe Burayadah kusanya kiasi fulani cha dhahabu kwa ajili ya Rabiah.” 
Zikakusanywa na kuletwa kwa Mtume (SAW) na kuniambia:
 “Chukua hizi wapelekee na uwaambie hii ni mahari ya binti yenu.” 
Nikapeleka yakapokelewa kwa mikono miwili na walifurahi sana na kusema, ni nyingi na nzuri.  Nilirudi kwa Mtume Muhammad (SAW) na kumhadithia:
“Sijawahi kuona watu wakarimu kama wale.  Wamependezewa sana na kile nilichowapa ijapokuwa ni kichache……, sasa nitapata wapi chakula cha walima, ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu?”
Mtume (SAW) akamwambia Buraydah  “kusanya kiasi cha fedha thamani ya kondoo kwa ajili ya Rabiah!” 
Wakanunua kondoo aliyenona na kisha Mtume (SAW) akaniambia:
 “Nenda kwa Bi Aisha na umwambie akupe kiasi chochote cha ‘mawele’ alichonacho.” 
Bi Aisha akanipa pishi saba na kusema, “Wallahi hatuna tena chakula!:
 Nikatoka na kuelekea nyumban ya familia ya mke wangu na wakaniambia:
“Sisi tutayatengeneza haya mawele lakini tafuta marafiki zako mumtengeneze huyu kondoo.”
Tukamchinja, kumchuna ngozi na kumpika.  Hivyo tukala mkate na nyama na nikamualika Mtume (SAW) na akahudhuria.
 
Mtume Muhammad (SAW) akampa kipande cha ardhi jirani na Abubakar.  Kuanzia hapo tena nikaanza kujishughulisha na dunia.  Nikawa na ugomvi kati yangu na Abubakar juu ya mtende.
 
“Uko ndani ya mpaka wangu” nikadai.
 
“Uko kwangu” akajibu Abubakar.
 
Tukaanza kubishana, Abubakar akanitukana, lakini ghafla tu akajirudi nafsi yake na kuniomba msamaha na kuniambia, “Rabiah, tamka kama nilivyotamka mimi ili kihisabike kama kisasi.  “Hapana, sitofanya hivyo.” Nikamjibu.
“Ikiwa ni hivyo, nitakwenda kukushitakia kwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu kukataa kwako kulipiza kisasi.”
 
Alikwenda na nilimfuata.  Jamaa wa kabila langu pia likafuata:
 
“Yeye ndiye aliyeanza kwa kukutukana halafu anakwenda kwa Mtume (SAW) kukushtakia?”
Nikawageukia na kuwaambia, “Ole wenu, mnajua ni nani huyu?  Ni Assiddiq……. Na ni mtu mzima anaeheshimika miongoni mwa waislam.  Rudini kabla hajatizama nyuma na kukuoneni na kufikiria labda umekuja kunisaidia dhidi yake, kwani atazidi kukasirika na kwenda kwa Mtume (SAW) na ghadhabu.  Mtume naye atakasirika kasha Mwenyezi Mungu atakasirika wote na Rabiah kumalizika! Wakarudi.”
 
Abubakar akamhadithia Mtume (SAW) kama ilivyotokea na Mtume alipomaliza kumsikiliza akainua kichwa chake na kuniambia:
 “Ewe Rabiah, mna matatizo gani wewe na Assiddiq?” 
“Mjumbe wa Mwenyezi Mungu alinitaka niseme maneno yale yale kama alivyonitamkia na mini nikakataa.”
 “Ndio, usiseme maneno yale kama alivyokutamkia, badala yake sema, ‘Inshallah Mwenyezi Mungu amsamehe Abubakar.” 
Abubakar akaondoka huku akitokwa na machozi huku akisema, “Inshaallah Mwenyezi Mungu akulipe mema kwa sababu yangu ewe Rabiah ibn Kaab……..”