Uthmaan bin
‘Affaan (Radhiya Llahu ‘anhu)
Khalifa
wa tatu wa tatu aliyeongoka
‘Uthmaan na vita
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alikuwa mtu asiyependa vita wala umwagaji wa damu wa aina yoyote
ile. Hata hivyo pale inapobidi alikuwa msitari wa mbele kuitikia mwito wa
jihadi dhidi ya maadui wa Mwenyezi Mungu kwa hali na mali.
Hakupigana vita vya
Badr ingawaje alikuwa miongoni mwa wachache waliotoka kwenda kushiriki, na hii
ni kwa sababu walipokuwa wakielekea Badr, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llaahu ‘alayhi wa sallam) alimtaka ‘Uthmaan arudi nyumbani kwake Madiynah kwa
ajili ya kumuuguza mkewe Bibi Ruqayyah (Radhiya Llaahu ‘anha) ambaye hali yake
ilikuwa mbaya sana, na hatimaye akafariki dunia siku ile zilipowafikia habari
za ushindi wa Waislamu katika vita hivyo.
Katika vita vya Uhud,
‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alishiriki, akapigana, lakini alirudi nyuma
pamoja na wenzake pale majeshi ya makafiri yalipofanikiwa kuwazunguka na
kuupanda mlima Uhud na kuanza kuwarushia mishale na kusababisha kuuliwa kwa
Waislamu wengi.
Katika vita hivyo
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) aliwaweka juu ya
jabali Uhud watu hamsini waliokuwa mahodari wa kutupa mishale wapate kuwalinda
wenzao wanaopigana chini, akawataka wasiondoke hapo iwe itakavyokuwa ili baada
ya kumalizika vita hivyo majeshi ya washirikina yasiweze kuwazunguka na
kuwashambulia kwa nyuma .
Lakini watupa mishale
hao walikwenda kinyume na amri hiyo mara baada ya kuwaona wenzao walioshinda
wakianza kuwaendesha mbio washirikina huku wakikusanya ngawira. Baadhi yao
isipokuwa watu kumi na nne tu walikhalifu amri hii, wakateremka na kwenda
kuwasaidia wenzao katika kuwateka washirikina na katika kukusanya ngawira.
Baadhi ya majemadari
wa jeshi la washirikina waliokuwa wakirudi nyuma, walipowaona Waislamu
wakiliteremka jabali, wakageuza njia na kulizunguka kwa nyuma, wakalipanda na
kuanza kuwashambulia Waislamu kwa kuwamiminia mishale.
Waislamu wengi
walikufa na wengine kujeruhiwa, na wengi wengine akiwemo ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) wakarudi nyuma kwa msituko wa walipoona wenzao wanapukutika, na
Mwenyezi Mungu akateremsha kauli yake ya kuwasamehe wale waliorudi nyuma siku
hiyo akasema;
"…..Naye sasa
amekusameheni. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye ihsani nyingi juu ya
wanaoamini."
Aali Imran - 152
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alishiriki katika vita vyote vilivyobaki walivyopigana Waislamu.
Alishiriki katika vita vya Khaybar, vita vya kuuteka mji wa Makkah, vita vya
Taif, Howazin, Tabuk na vingi vinginevyo.
Siku ya Hudaybiyah
kama tulivyoona hapo mwanzo kuwa yeye ndiye aliyepewa jukumu la hatari, pale
alipochaguliwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)
kwenda Makkah akajadiliane na washirikina, naye akalikubali jukumu hilo kwa
ushujaa mkubwa, yakatokea yaliyotokea, na kwa ajili yake Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) aliwataka Waislamu wafungamane naye
chini ya mti, na kwa ajili yake siku hiyo Mwenyezi Mungu aliteremsha aya ya
kuridhika na Maswahaba wake watukufu (Radhiya Llaahu ‘anhum) waliofungamana na
Mtume wake mtukufu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Khalifa wa tatu
Alipokuwa akivuta
pumzi zake za mwisho, ‘Umar bin Al-Khattwwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa
kumchagua Khalifa atakayeongoza baada yake juu ya kuwa Maswahaba (Radhiya
Llaahu ‘anhum) walimshikilia afanye hivyo; ‘Umar aliwaambia;
"Mzigo wenu
nimeubeba nikiwa hai, na baada ya kufa kwangu mnanitaka nikubebeeni pia? Ikiwa
kuchagua basi amekwisha chagua aliyekuwa bora kuliko mimi - Abu Bakr , na ikiwa
ni kuacha basi aliacha kuchagua aliyekuwa bora kuliko mimi - Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na Mwenyezi Mungu ataihifadhi dini
yake".
Lakini ‘Umar (Radhiya
Llaahu ‘anhu) aliwaita Maswahaba sita; Ali, ‘Uthmaan, Twalha, Al Zubayr, Saad
na ‘Abdur-Rahmaan bin Al-’Awf (Radhiya Llaahu ‘anhum) na kuwaambia;
"Nimetazama na
nikakuoneni kuwa nyinyi ndio mnaostahiki kuwa viongozi, na Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipofariki dunia alikuwa radhi nanyi
nyote. Mimi sikuogopeeni watu iwapo mtasimama katika njia ya haki, basi
nitakapokufa mushauriane muda wa siku tatu, na siku ya nne ikiingia muwe
mumekwishamchagua kiongozi kati yenu. Na ahudhurie pamoja nanyi ‘Abdullaah bin
‘Umar akiwa kama ni mshauri tu, lakini yeye hana haki yoyote ya kuchaguliwa
kuwa kiongozi".
Twalha hakuwepo
Madiynah siku walipokutana, na ‘Abdur-Rahmaan bin Al-’Awf(Radhiya Llaahu ‘anhu)
aliwashauri Maswahaba waliohudhuria kuwa itakuwa bora iwapo mmoja wao atajitoa
ili pawezekane kuchaguliwa Khalifa kwa urahisi. Kisha yeye mwenyewe akajitoa,
kisha Al Zubeir (Radhiya Llaahu ‘anhu) akajitoa na Sa’ad bin Abi Waqaas
(Radhiya Llaahu ‘anhu) pia akajitoa. Wakabaki wawili, nao ni ‘Uthmaan na Ali
(Radhiya Llaahu ‘anhumaa), na ‘Abdur-Rahmaan bin Al-’Awf akapewa jukumu la
kumchaguwa mmoja kati yao.
Ibni Al-’Awf (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alikuwa na kazi kubwa ya kuwashauri Maswahaba wote waliopo
Madiynah kwa muda wa siku tatu tu ili aweze kutoa uamuzi wake muhimu.
Anasema Ibni Kathir
katika kitabu cha 'Al Bidaya wa Nnihaya';
"‘Abdur-Rahmaan
alikuwa na kazi kubwa katika siku tatu hizo ya kuupitia mji wote wa Madiynah na
kuwagongea milango watu akiwashauri na kusikiliza rai zao.
Aliwauliza Maswahaba
waliokuwa maarufu, watu wa kawaida, wanawake, na ilimbidi wakati mweingine
awaulize hata watoto wadogo na wasafiri waliokuwa wakiwasili Madiynah katika
siku hizo."
Ibni Kathir
anaendelea kusema;
"Kisha
‘Abdur-Rahmaan bin Al-’Awf akawaita ‘Uthmaan na Ali, wakamjia, na yeye
akawakabili na kuwaambia;
"Nimewauliza
watu wote juu yenu na sikumpata hata mmoja anayekufadhilisheni baina yenu
wawili, kwani wote wanataka mmoja wenu awe Khalifa wao."
Kisha ‘Abdur-Rahmaan
akawataka watoe ahadi kuwa yeyote kati yao atakayechaguliwa kuwa Khalifa
atahukumu kwa uadilifu na yule asiyechaguliwa atatii.
Kisha akatoka pamoja
nao na kuelekea msikitini, ‘Abdur-Rahmaan akiwa amevaa kilemba alichopewa na
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) huku akiwa ameufunga
upanga wake kiunoni, na alipowasili msikitini akawataka watu wote wakusanyike.
Kisha pakanadiwa; "Assalaatu Jaamia", watu wakamiminika msikitini
mpaka msikiti ukajaa na kufurika hata ‘Uthmaan hakupata mahali pa kukaa
isipokuwa mwisho wa safu, na alikuwa mtu mwenye kuona haya sana.
Kisha ‘Abdur-Rahmaan
akapanda juu ya membari ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa
sallam) na kuomba dua ndefu sana, kisha akasema;
"Enyi watu! Mimi
nilikuulizeni kwa siri na kwa dhahiri na sikumpata hata mmoja katika yenu
anayemtaka mwengine isipokuwa Ali au ‘Uthmaan. Inuka njoo kwangu ewe Ali".
Ali akainuka na
kumwendea, na ‘Abdur-Rahmaan akaushika mkono wake na kumuuliza;
"Je! Upo tayari
kufungamana nami kufuatana na kitabu cha Mwenyezi Mungu na mafundisho ya Mtume
wake na matendo ya Abu Bakr na
‘Umar?"
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akasema;
"Kufuatana na
kitabu cha Mwenyezi Mungu na mafundisho ya Mtume wake na Ijtihadi kwa rai yangu".
Kisha akasema;
"Inuka njoo
kwangu ewe ‘Uthmaan".
‘Uthmaan akainuka na
kumwendea, na ‘Abdur-Rahmaan akaushika mkono wake na kumuuliza;
"Je! Upo tayari
kufungamana nami kufuatana na kitabu cha Mwenyezi Mungu na mafundisho ya Mtume
wake na matendo ya Abu Bakr na
‘Umar?"
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akasema;
"Allahumma
Ndiyo, nimekubali".
‘Abdur-Rahmaan
(Radhiya Llaahu ‘anhu) akaunyanyua uso wake juu na kutizama juu ya sakafu ya
msikiti huku mkono wake ukiwa ndani ya mkono wa ‘Uthmaan kisha akasema;
"Ewe Mola wangu
sikia na ushuhudie, mimi nimeitua amana iliyokuwa juu ya shingo yangu na
kuiweka juu ya shingo ya ‘Uthmaan".
Watu wakaanza
kumkimbilia ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) ili wafungamane naye, na mkono wa
mwanzo uliofungamana naye ulikuwa mkono wa ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya
Llaahu ‘anhu), kisha Waislamu wote waliobaki wakafungamana naye.
Na hivi ndivyo
‘Uthmaan alivyopewa Ukhalifa akiwa na umri unaokaribia miaka sabini".
Hotuba yake ya mwanzo
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alikuwa msemaji hodari, lakini siku ile alipopanda juu ya membari
kutoa hotuba yake ya mwanzo, alishindwa kusema maneno mengi, na badala yake
alitamka maneno machache yafuatayo;
"Hakika dunia
imejaa ghururi, basi yasikudanganyeni maisha ya dunia wala asikudanganyeni yule
mdanganyi mkubwa (Iblisi) katika (mambo ya) Mwenyezi Mungu. Dunia itupeni mbali
kama vile Mwenyezi Mungu alivyoitupa na itafuteni akhera yenu, kwani Mwenyezi
Mungu ameipigia mfano dunia Akasema;
"Na wapigie
mfano wa maisha ya dunia ni kama maji tunayoyateremsha kutoka mawinguni; kisha
huchanganyika nayo mimea ya ardhi kisha ikawa majani makavu yaliyokatikakatika
ambayo upepo huyarusha huku na huko. Na Mwenyezi Mungu Ana uweza juu ya kila
kitu.
"Mali na watoto
ni pambo la maisha ya dunia. Na vitendo vizuri vibakiavyo ndivyo bora mbele ya
Mola wako kwa malipo na tumaini bora (kuliko hayo mali na watoto)".
Al Kahf - 45 - 46
Anasema Ibni Kathir
katika Al Bidaya wal Nihaya;
"‘Uthmaan
ameianza kazi yake ya ukhalifa kwa kuwaandikia wakuu wa mikoa mbali mbali,
washika hazina pamoja na majemadari wake akiwanasihi pamoja na kuwaamrisha mema
na kuwakataza maovu na akawataka wafuate mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu
(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na kuacha kuzusha mambo mepya katika dini.
Katika utawala wake nyumba
ya Hazina ya Waislamu (Baytul Mal), ilijaa mali nyingi, akawaongezea watu
mishahara na kuhusisha kiwango maalum cha mali kwa ajili ya kuwalipa na
kuwalisha wanaokesha wakifanya ibada na kutafuta elimu misikitini ".
Uasi
Mara baada ya
‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kukamata hatamu za kuongoza umma, Warumi na
baadhi ya Wafursi wakaanza kuvunja mikataba iliyokuwa baina yao na dola ya
Kiislamu. Uasi ulianza katika nchi za Azarbeijan na Armenia, na Warumi
wakajaribu kuuvamia mji wa Alexandria na Palestine, na moto wa uasi ukaendelea
kuwaka mpaka ukafika sehemu za Khurasan na Karman na kwengineko.
Waasi hawakuwa watu
wa kawaida wa miji ile, kwani watu wa miji hiyo baada ya kukombolewa na
Waislamu kutokana na utawala wa Kirumi na wa Kifursi waliridhika na utawala wa
viongozi waadilifu wa Kiislamu. Lakini uasi huo ulitokana na nguvu iliyokuwa
ikitawala kabla ya Uislamu, nguvu iliyopoteza ufalme na utawala wake, nguvu
iliyokula hasara ya kila kitu baada ya kushindwa na Majeshi ya Kiislamu.
Nguvu hiyo ilipoona
kuwa Khalifa mwenye nguvu ‘Umar bin Al-Khattwwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu)
ameuliwa na kafiri mwenzao, na kwamba Khalifa mzee mwenye umri unaokaribia
miaka sabini ndiye aliyetawala, tamaa ikawaingia, wakaona hii ndiyo fursa nzuri
ya kuurudisha utawala wao.
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) hakuwa akijulikana kama ni mtu wa vita kama vile Khalid bin Walid
au Sa’ad bin Abi Waqaasau ‘Aliy bin Abi Twaalib(Radhiya Llaahu ‘anhum) na
wengineo, bali umaarufu wake ulikuwa juu ya ukarimu na wingi wa kuona haya, na
kwa ajili hiyo tamaa ikaingia katika nafsi za waasi, wakadhani kuwa fursa
imewadia ya kuurudisha utawala wao.
Lakini mzee huyu
anayekaribia umri wa miaka sabini akaona ni vizuri awaoneshe makafiri hawa kuwa
Maswahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)
hawapimwi kwa umri wao wala hawakisiwi kwa miili yao, bali vipimo vyao ni Imani
iliyojaa nyoyoni mwao, imani yao juu ya Dini yao, juu ya Mola wao na juu ya
Mtume wao mtukufu Muhammad (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
‘Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) akatoa amri ya kuuzima moto huo wa uasi kwa haraka sana kama ulivyoanza.
Si hivyo tu, bali aliyapa majeshi yake amri ya kusonga mbele na kuiteka miji
mingine ya Warumi ili wasiipate kwa wepesi fursa nyengine ya kuanzisha uasi
kama huo karibu na dola ya Kiislamu.
‘Uthmaan mwenyewe
(Radhiya Llaahu ‘anhu) ndiye aliyewachagua wakuu wa majeshi yatakayoifanya kazi
hiyo. Jambo la ajabu ni kuwa hapana hata jeshi moja katika majeshi ya ‘Uthmaan
yaliyoshindwa katika mapambano hayo isipokuwa katika pambano moja tu.
‘Uthmaan alikuwa
akipanga, akifikiri, akikisia kama kwamba amerejeshewa tena ujana wake
Radhiyallahu anhu. Na alipoona kuwa ipo haja ya kuunda jeshi la baharia,
akaliunda. ‘Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu), juu ya ushujaa wake hakujaribu
kuchukua hatua kama hiyo ambayo ni ngeni na ingehatarisha usalama wa majeshi ya
Kiislamu.
Waislamu walipomuona
Khalifa wao akiwa na hamasa, imani pamoja na moyo ule wa kishujaa, wao pia
imani yao ikaongezeka nguvu. Wakawa wajasiri zaidi na wenye moyo thabiti.
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akaanza kwa kutoa amri ya kuushambulia mji wa Azerbeijan, kisha
Armenia, ile miji iliyovunja ahadi. Akamchagua Al Walid bin ‘Uqbah (Radhiya
Llaahu ‘anhu) kuwa mkuu wa majeshi yatakayokwenda huko, na baada ya kuwashinda
akafanikiwa kuwafanya waasi hao watie saini (sahihi) mkataba mwingine kama ule
waliouvunja.
Walipokuwa wakirudi
mji wa Al Kuufa baada ya kuwashinda waasi hao, Al Walid na majeshi yake
wakapata habari kuwa majeshi ya Warumi yameanza uchokozi katika miji ya Sham. Ikamfikia
amri kutoka kwa Khalifa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa atayarishe jeshi
la watu elfu kumi sharti liongozwe na mtu mwaminifu tena mkarimu.
Al Walid (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akamchagua mtu mmoja aitwae Habib bin Maslamah al Fahariy
(Radhiya Llaahu ‘anhu) kuliongoza jeshi hilo. Habib akaondoka na jeshi lake
lisilozidi watu elfu kumi na kupambana na majeshi ya Warumi pamoja na Waturki
yasiyopungua watu elfu themanini.
Mke wa Habib alikuwa
miongoni mwa wanajeshi hao, na alipomuuliza mumewe kabla ya kuanza vita;
"Tutaonana wapi
ikiwa vita vitapamba moto na majeshi kutawanyika?"
Akamjibu;
"Katika hema la
mkuu wa majeshi ya Kirumi au Peponi".
Majeshi mawili hayo
yakakutana katika mapambano makali, na Habib aliyashinda majeshi ya Warumi na
Waturuki kwa pamoja, kisha hakusimama hapo, bali alisonga mbele kuelekea nchi
za Warumi huku akizivunja ngome zao moja baada ya moja.
Habari nyengine
zikamfikia Khalifa wa Waislamu kuwa majeshi ya baharia ya Warumi yanauvamia mji
wa Alexandria huko Misri na kwamba majeshi mengine zaidi yanakuja kutoka Roma
kuelekea huko.
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akamuamrisha ‘Amr bin Al-‘Aas (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa
Gavana wa nchi ya Misri apeleke jeshi lake Alexandria na ayaangamize majeshi ya
Kirumi. Wakati huo huo Muawiya bin Abu Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa
akiuteka mji wa Qansarin, na Majemadari wengine walikuwa wakizima moto ya uasi
katika sehemu mbali mbali.
Khalifa ‘Uthmaan
(Radhiya Llaahu ‘anhu) akayaamrisha majeshi yake kwenda Afrika ya Kaskazini
chini ya uongozi wa Abdullah bin Saad pamoja na Abdullaah bin ‘Amr na Abdullaah
bin Zubayr (Radhiya Llaahu ‘anhu), na baada ya mapambano makali majeshi hayo
yakawashinda majeshi ya wabarbari ya Afrika ya Kaskazini.
Jeshi la baharia la
Warumi lilokuwepo Cyprus, lilikuwa katika hali ambayo lingeweza kusababisha
hatari kwa nchi za Kiislamu, na ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaona ni bora
ahatarishe na kupeleka jeshi la baharia la Waislamu kupambana nalo.
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akamchagua Muawiya bin Abi Sufyan (Radhiya Llaahu ‘anhu), kuwa
kiongozi wa jeshi la kuiteka nchi ya Cyprus na akampelekea jeshi lingine
likongozwa na Saeed bin Abu Sarh (Radhiya Llaahu ‘anhu) ili washirikiane katika
jukumu hilo. Majeshi mawili hayo makubwa yakapambana na hatimaye jeshi la
Warumi likasalimu amri na kutia saini (sahihi) mkataba wa sulhu uliowekewa
masharti na Waislamu.
Vita hivyo
vikafuatiliwa na vita vya Sawariy. Vita ambavyo Constantine, mfalme wa Roma
alitayarisha jeshi kubwa sana lisilopata kutayarishwa mfano wake kwa ajili ya
kupambana na majeshi ya Kiislamu. Akalipeleka jeshi hilo Morocco pamoja na
merikebu mia tano za kivita, na mapambano makali yakatokea huko na hatimaye
majeshi ya Kiislamu yakawashinda Warumi katika vita hivi ambavyo watu wengi
sana kutoka pande zote mbili walikufa.
Hivi ndivyo
ilivyokuwa, mara baada ya kutawala ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu). Majeshi ya
Kiislamu yalisonga mbele kila upande na kuyashinda majeshi ya Warumi na ya
Wafursi na kufanikiwa kuiteka miji mbali mbali kama vile Constantinople, Karman
na kwengineko, na hatimaye kufanikiwa kuuzima moto huo wa uasi.
Yule waliyemdhania
kuwa ni mzee na wangeweza kumchezea, aligeuka kuwa simba mshambuliaji.
Msahafu Mmoja
Inajulikana kuwa
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akiteremshiwa
Qur-aan kidogo kidogo kutokana na sababu na matukio mbali mbali, na wakati
mwingine bila hata sababu wala matukio, wala hakuteremshiwa yote kwa pamoja.
Tunaelewa pia kuwa
Qur-aan tukufu imeteremshwa kwa lugha (lahja) ya Ki-Quraysh, na kwamba pale
Madiynah yalikuwepo makabila mengine yasiyokuwa ya Ki-Quraysh, na kwa ajili ya
kuwarahisishia usomaji wa Qur-aan, Mtume wa mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu
‘alayhi wa sallam) alimuomba Mola wake awaruhusu kuisoma na kuiandika kwa lahja
zao mbali mbali. Idadi ya lahja hizo zilikuwa saba, na inaeleweka pia kuwa
baadhi ya wale walioandika Qur-aan kwa lahja zao hizo waliieneza kila pembe ya
nchi za Kiislamu.
Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa kila anapoteremshiwa Wahyi
akiwaamrisha waandishi wake kuandika Wahyi huo mbele yake. Kwa hivyo Qur-aan
iliandikwa wakati wa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na mbele yake
ndani ya sehemu mbali mbali za kuandikia za wakati huo kama vile magamba ya
miti, mbao, makozi nk. Na baada ya kuandikwa ikawa inawekwa nyumbani kwa Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Maswahaba (Radhiya
Llaahu ‘anhum) nao pia waliihifadhi Qur-aan kwa moyo na kuisoma majumbani mwao
na katika sala zao, na waliokuwa wakijua kuandika waliiandika katika sehemu
mbali mbali na kuzihifadhi majumbani mwao pia.
Kwa hivyo Qur-aan
iliandikwa tokea wakati wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa
sallam) na kuhifadhiwa na Maswahaba wengi (Radhiya Llaahu ‘anhum), lakini
haikuwa katika kitabu kimoja, bali iliandikwa katika sehemu mbali mbali
zilizowarahisikia kuandika.
Alipotawala Abu
Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu), alishauriwa
na ‘Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) aikusanye ile Qur-aan iliyoandikwa mbele ya
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na kuilinganisha na
ile iliyoandikwa na Maswahaba wengine na ile iliyohifadhiwa vifuani mwa
waandishi wa wahyi pamoja na Maswahaba wengine wengi (Radhiya Llaahu ‘anhum),
na kuijumuisha katika kitabu kimoja.
Abu Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu) hapo mwanzo
hakupendelea kufanya jambo kama hilo ambalo Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llaahu ‘alayhi wa sallam) hakulifanya, lakini hatimaye alilikubali pendekezo
hilo la ‘Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumpa Zayd bin Thabit (Radhiya Llaahu ‘anhu)
jukumu la kuisimamia kazi hiyo akishirikiana na Maswahaba wenzake kama vile
Saeed bin ‘Aas, ‘Abdullaah bin Zubayr, ‘Abdur-Rahmaan bin Al-Haarith na
wengineo waliokuwa wakiuandika wahyi huo mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu
(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) pale ulipokuwa ukiteremshwa.
Alimpa jukumu hilo
Zayd (Radhiya Llaahu ‘anhu) kwa sababu yeye ndiye aliyeandika wahyi zaidi
kuliko Maswahaba wengine, na alikuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llaahu ‘alayhi wa sallam) kwa muda mrefu zaidi kuliko waandishi wa wahyi
wenzake.
Baada ya juhudi kubwa
sana, Zayd pamoja na wenzake (Radhiya Llaahu ‘anhum) wakafanikiwa kuikusanya
Qur-aan na kuiandika yote katika msahafu mmoja, na kuanzia siku hiyo ile
Qur-aan iliyoandikwa mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa
sallam) katika sehemu mbali mbali na kuhifadhiwa vifuani mwa Maswahaba (Radhiya
Llaahu ‘anhum) ikawa imekusanywa na kuandikwa katika msahafu mmoja tu
uliopangwa sura zake na aya zake kama alivyowapangia Mtume wao (Swalla Llaahu ‘alayhi
wa sallam). Kisha msahafu huo ukawekwa na kuhifadhiwa nyumbani kwa Abu
Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu), na baada ya
kufa kwake ukawa nyumbani kwa ‘Umar (Radhiya Llaahu ‘anhu) ambaye kabla ya kufa
kwake alimkabidhi binti yake Hafswa (Radhiya Llaahu ‘anha), mke wa Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Wakati huo huo ile
misahafu ya mwanzo iliyoandikwa kwa lahja zile saba ilienea na kusomwa na watu
katika nchi mbali mbali za Kiislamu, na inajulikana kuwa alipotawala ‘Uthmaan
(Radhiya Llaahu ‘anhu) dini ya Kiislamu ilipata nguvu zaidi, na majeshi yao
yaliweza kuzishinda nchi mbali mbali na kusonga mbele hadi kufikia Azarbeijan
na Armenia na Cyprus, na kuweza pia kuziteka nchi mbali mbali za Asia na za
Ulaya na Afrika.
Baadhi ya Maswahaba
kama vile ‘Hudhaiyfa (Radhiya Llaahu ‘anhu) walikuwa wakiona mambo ya kiajabu
kila wanaposonga mbele kuziteka nchi hizo. Katika nchi ya Syria na Misri kwa
mfano, Waislamu walikuwa wakigombana na kushindana kwa kutamba katika usomaji
wao wa Qur-aan kila mmoja kwa lahaja yake, kila mmoja akisema kuwa usomaji wake
wa Qur-aan ni bora kuliko wa mwenzake na kufikia hadi kukufurishana.
Zilizpomfikia habari
hizo, ‘Uthmaan akashauriana na Maswahaba wenzake (Radhiya Llaahu ‘anhum) na
wote wakaona kuwa ipo haja kubwa ya kuwaunganisha Waislamu wote wawe wanaisoma
Qur-aan kwa msomo mmoja tu na kwa kutumia Lahaja moja tu.
Wakakubaliana
wauchukue ule Msahafu uliokusanywa na kuandikwa wakati wa Abu Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kuunukuu kwa
kuuandika tena katika misahafu mingine mingi, na wakakubaliana kuwa itumike
lugha ya ki Quraysh iliyoteremshiwa Qur-aan, kisha waisambaze misahafu hiyo
katika nchi za Kiislamu na kuichoma moto misahafu yote iliyobaki iliyoandikwa
kwa misomo na lahaja tofauti ili kuukata mizizi ya fitna kuanzia chanzo chake,
mizizi ambayo kama ingeachwa basi mwisho wake usingekuwa mwema.
Ikachaguliwa tume ya
waliohifadhi Qur-aan pamoja na wajuzi wa lugha ya kiarabu, wote wakiwa ni wale
waandishi wa wahyi wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa
sallam), pamoja na wale walioihifadhi mbele yake, na ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) akawaambia;
‘Itakapotokea
khitilafu yoyote kati yenu katika usomaji basi andikeni kwa lahja ya ki
Quraysh’.
Baada ya kukamilika
kazi hiyo, akaurudisha ule msahafu wa Abu Bakr
(Radhiya Llaahu ‘anhu) nyumbani kwa Bi Hafswa (Radhiya Llaahu ‘anha), na
Waislamu wakaanza kunukuu kutoka katika msahafu huo ulioandikwa mbele ya
Maswahaba wote (Radhiya Llaahu ‘anhum) na kuisambaza duniani kote. Haya
yalifanywa baada ya kupatikana makubaliano baina ya Maswahaba wote (Radhiya
Llaahu ‘anhum) ya kuwepo haja kubwa ya kuifanya kazi hiyo.
Sayyidna ‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alipowasikia baadhi ya
watu wakimlaumu ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa ameichoma moto misahafu,
aliwaambia;
“Mcheni Mola wenu
enyi watu! Msipindukie mipaka katika kumlaumu ‘Uthmaan na kusema kuwa eti yeye
ni mchomaji wa misahafu, kwani Wallahi misahafu imechomwa mbele ya Maswahaba
wote na baada ya sote kukubaliana. Na mimi ningelikuwa Khalifa basi ningefanya
kama alivyofanya”.
Kwa hivyo Abu
Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu) akihofia
Qur-aan isije ikapotea baada ya kufa kwa waliohifadhi aliikusanya na kuiandika
mahala pamoja, na ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliiandika katika kitabu
kimoja na kuichoma iliyobaki kwa kuogopa mtafaruko.
Lakini Qur-aan
aliyoiandika ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) ni ile ile aliyoiandika Abu
Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu), aliyoinukuu
kutoka katika ile iliyoandikwa mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu
‘alayhi wa sallam) na kuhifadhiwa nyumbani kwake.
Katika hadithi
iliyosimuliwa na Imam Ahmad, Ibni Majah, At-Tirmidhiy na kwa njia nyingi,
anasema Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam);
"Yule kati yenu
atakayeishi (miaka mingi), atakuja kuona hitilafu nyingi sana, basi (mtakapoona
hitilafu hizo) mzifuate (msiziache) Sunnah zangu na Sunnah za Makhalifa
waongofu watakaokuja baada yangu. Zikamateni kwa magego yenu".
Na ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) ni katika hao Makhalifa waongofu (Radhiya Llaahu ‘anhum) ambao
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) anatutaka tufuate
mafundisho yao na mwenendo wao.
Miaka Migumu
Baada ya kushindwa
katika mapambano ya uso kwa uso, ile nguvu ya shari ya kikafiri ikiongozwa na
wafalme wa Fursi pamoja na Warumi ikaingia katika mapambano ya siri na ya hila
dhidi ya Khalifa wa Waislamu.
Mayahudi nao
hawakutaka kubaki wawe washangiliaji tu, kwani wao pia walitolewa na kufukuzwa
nje ya Madiynah na kupoteza vyote walivyomiliki baada ya kufanya hiana yao
katika vita vya Khandaq.
Wote hawa walikuwa
wakiungulika kila wanapoona na kusikia juu ya kusonga mbele kwa majeshi ya
Kiislamu, na namna Waislamu walivyokuwa wakiteka nchi baada ya nchi huku
wakiwatoa watu kutoka katika kiza cha kufru na kuwaingiza katika nuru ya Uislamu.
Warumi na Wafursi
walifanya mbinu zao kwa nje, na Mayahudi wakafanya mbinu zao na hila zao kwa
ndani, na halikuwa jambo la sudfa pale alipokuja kutoka nchi ya Yemen myahudi
aitwaye ‘Abdullaah bin Saba-a na kudai kuwa eti amesoma juu ya dini ya Kiislamu
na akaipenda, na kwamba anataka kuingia katika dini hii na kuchukua nafasi yake
anayostahiki katika kuuongoza umma huo.
Myahudi huyo
aliyekuwa akijifanya mcha Mungu sana alikuwa mwingi wa hila, na akafanikiwa
kiasi kikubwa katika kuwagombanisha Waislamu.
Alianza kuingiza
fitna zake kidogo kidogo kwa kumtuhumu Khalifa wa Waislamu ‘Uthmaan bin ‘Affaan
(Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa amejichukulia uongozi kwa nguvu na kwamba
amemdhulumu ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Llaahu ‘anhu). Na katika tuhuma zake
hizo alikuwa akizitumilia hadithi za Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu
‘alayhi wa sallam) zinazozungumza juu ya sifa mbali mbali za Sayiduna
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) kama vile;
"Anayenipenda
mimi ampende Ali ".
na;
"Mola wangu
mnusuru atakayemnusuru na uwe dhidi ya atakayekuwa dhidi yake".
Alizitumilia hadithi
kama hizi ili kuonesha kuwa wote waliokuwa Makhalifa kabla yake walikuwa maadui
wa ‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kwamba hawakuwa wakimpenda, bali hawakuwa wakifuata hata maamrisho ya Mwenyezi Mungu
na ya Mtume wake (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikuwa akichukizwa na
maneno hayo ya ‘Abdullaah bin Saba-a na mara nyingi alimjulisha juu ya
kuchukizwa kwake huko na kuwatahadharisha Waislamu juu ya ubaya wake, lakini juu
ya yote hayo Ibni Saba-a huyu alifanikiwa kuieneza chuki yake hiyo katika nyoyo
za baadhi ya Waislamu.
Alikuwa akisafiri
nchi mbali mbali kuanzia mji wa Al-Kuufah (Iraq), kisha nchi ya Sham, kisha
akaelekea Misri na kukaa huko muda mrefu akijifanya kama ni mtu anayependa
kuamrisha mema na kukataza maovu huku akiieneza sumu yake hiyo na kuwataka watu
wainuke na kupigana kwa ajili ya kuirudisha haki hiyo kwa wanaoistahiki, na
kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) ameusia juu ya
Ukhalifa wa ‘Aliy (Radhiya Llaahu
‘anhu).
‘Abdullaah bin Saba-a
alifanikiwa kuyatumilia baadhi ya makosa yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya
magavana wa Kiislamu wakati ule kwa ajili ya kuifanikisha fitna yake hiyo.
Bora damu yangu imwagike
Habari za njama hizo
pamoja na matayarisho ya uasi yaliyokuwa yakifanyika huko Misri, Basra na
Al-Kuufah zilimfikia ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), lakini kila anaposhauriwa
kutumia nguvu kuzivunja njama hizo, alikuwa akikataa huku akisema;
"Iwapo damu
lazima imwagike, basi bora imwagike damu yangu badala ya kumwagika damu ya
Waislamu.".
Alikuwa akisema pia;
"Sipendi
nikutane na Allah na juu ya shingo yangu ipo hata tone ya damu ya
Mwislamu".
Wafuasi wa ‘Abdullaah
bin Saba-a walifanikiwa kujipenyeza na kuingia Madiynah kwa makundi na wakati
mwengine mmoja mmoja bila ya kuonesha nia yao hiyo ovu, wakidai kwamba wamekuja
kwa ajili ya kujitayarisha kwenda Makkah kwa ajili ya Hija. Wengine walidai
kuwa wamekuja Madiynah kutafuta elimu.
Wakafanikiwa kuingiza
hofu pale Madiynah baada ya kutambua kuwa wengi kati ya Maswahaba wa Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) hawakuwepo Madiynah wakati
huo, kwani wengi wao walikuwa nje kwa ajili ya kupigana Jihadi na wengine
walikuwa Makkah kwa ajili ya Hija.
Haukupita muda waasi
hao wakataka kukutana na Khalifa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) wapate
kumjulisha juu ya nia yao ya kutaka kusahihisha baadhi ya makosa yaliyokuwa
yakitendwa na baadhi ya magavana wake, na ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Llaahu
‘anhu) alifanikiwa kuleta makubaliano kuwa maombi yao yaangaliwe sharti wao
warudi katika nchi zao kwanza.
Hali ya mambo ilizidi
kuwa mbaya, na waasi hao ambao wengi wao walitoka nchi ya Misri walitishia
kufanya uasi mkubwa na kumuuwa Khalifa wa Waislamu, na Muawiya (Radhiya Llaahu
‘anhu) akamwandikia ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) akimtaka ende Sham mahali
alipo yeye Muawiya (Radhiya Llaahu ‘anhu) mpaka mambo yatakapotulia, lakini
‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa akamwambia;
"Mimi sikubali
kuhamia mahali pengine nikawa mbali na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu
‘alayhi wa sallam)".
Muawiya (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akashauri kumpelekea jeshi kubwa liuzunguke mji wa Madiynah na
kumlinda na waasi hao, lakini ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamjibu;
"Naogopa wasije
wakafanya zahma katika mji wa Madiynah na kuwadhiki Maswahaba wa Mtume katika
Muhajirin na Ansar".
Muawiya akamuandikia
kuwa;
"Waasi hao
wanaweza kukuuwa"
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akajibu;
"Hasbiya Llahu
wa neema l wakiyl"
(Mwenyezi Mungu
ananitosha Naye ni mlinzi bora kabisa).
Asubuhi moja watu wa
Madiynah walipoamka walistukia mji wao umezungukwa na maelfu ya watu wenye
silaha waliotanda barabarani na kuanza kufanya zogo na kutaka kukutana na
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu).
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawaambia;
"Rudini katika
nchi zenu".
Wakakataa halafu
wakaanza kumuamrisha ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) awaachishe kazi baadhi ya
magavana na wakataka wapewe Marwan bin Al Hakam wamhukumu, jambo lisilowezekana
kwani ikiwa leo wamemtaka huyu na kesho watamtaka mwengine. ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akamtaka ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Llaahu ‘anhu) amsaidie
kulitatua tatizo hili na kumuomba ende kuzungumza na waasi hao na kuwataka
warudishe silaha ndani ya ala zake na kurudi katika nchi zao, na akatoa ahadi
kuwa iwapo watafanya hivyo atamuondoa Al Hakam katika kazi yake na pia baadhi
ya magavana wanaotuhumiwa.
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akatoka kwenda kwenye
kambi ya waasi akifuatana na Muhammad bin Maslamah pamoja na Sa’ad bin Abi
Waqaas (Radhiya Llaahu ‘anhumaa), na baada ya majadiliano marefu waasi hao
wakakubali kurudi makwao iwapo masharti yao yatatimizwa, na ‘Aliy (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akawapa ahadi kuwa masharti yatatimizwa.
Waasi warudi tena
Hazikupita siku
chache waasi wakarudi tena mjini, wakatanda barabarani na vichochoroni na
kuizunguka nyumba ya Khalifa wa Waislamu. ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Llaahu
‘anhu) akatoka na kuwaendea kwanza wale waasi waliotoka Misri na kuwauliza ni
jambo gani lililowafanya wavunje ahadi na kurudi baada ya makubaliano?
Wakamwambia;
"Tumemkamata mtu
aliyebeba barua iliyopigwa mhuri wa Khalifa, inayomtaka gavana wa Misri
atukamate na kutuuwa mara baada ya kuwasili kwetu huko. Na tulipomuuliza nani
aliyempa barua hiyo, akasema kuwa amepewa na Marwan".
Kisha ‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawaendea waasi
waliotoka mji wa Al-Kuufah na kuwauliza suali hilo hilo;
"Nini kilichokurudisheni
wakati tumeshakubaliana?"
Wakamjibu kuwa wao
wamekuja kuwasaidia wenzao wa Misri.
Kisha akawaendea watu
wa Basra na kuwauliza;
"Na nyinyi kipi
kilichokurudisheni baada ya makubaliano kumalizika?"
Akapata jibu lile
lile kuwa wao wamekuja kuwasaidia wenzao waliotoka Misri.
‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) akawauliza;
"Lakini nyinyi
mlipoondoka hapa, kila mmoja alipita njia yake. Mlipita njia mbali mbali,
mmezipataje nyote habari za barua hii?"
Hawakuwa na jawabu,
na ndipo ilipojulikana kuwa tokea mwanzo nia yao hasa ilikuwa ni kutaka
kumuondoa Khalifa, na kwamba hawakuwa na nia ya kuondoka na kurudi makwao, na
kwamba sababu iliyowafanya warudi tena Madiynah ni kile walichokijia hapo
mwanzo nayo ni kutaka kumuangusha au kumuuwa Khalifa wa Waislamu.
Ukweli juu ya barua
Anasema Dr. Khalid
Mohammed Khalid;
"‘Uthmaan
(Radhiya Llaahu ‘anhu) alikula kiapo kuwa yeye hakuiandika barua hiyo wala
hakutoa amri ya kuandikwa. Na bila shaka yoyote ile ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) hasemi uongo, kwani yeye ni mkweli anayejulikana kwa kupenda ukweli.
Kisha vipi atoe amri ya kuuliwa jeshi zima la waasi wakati alikwisha kataa ombi
la Muawiya la kumpelekea jeshi kubwa kwa ajili ya kumlinda akahiari imwagike
damu yake kuliko kumwagika damu ya Waislamu katika vita vya wenyewe kwa
wenyewe?
Ama Marwan naye pia
haiwezekani afanye hivyo, kwani alikuwa akijulikana kuwa ni mtu anayemuogopa
Mwenyezi Mungu na mwenye kumpenda Khalifa wake, na alikuwa mtu mwenye hekima
sana, na kwa hivyo anajua kuwa jambo kama hilo lingeharibu sifa ya Khalifa huyo
mkarimu anayempenda.
Kwa hivyo hapana
aliyebaki wa kuweza kutuhumiwa kwa jambo kama hilo isipokuwa viongozi wa waasi
hao. Na hii ndiyo sababu baada ya uasi huo kusababisha vita vikubwa baina ya
Waislamu na hatimaye kuuliwa kwa ‘Uthmaan na Ali (Radhiya Llaahu ‘anhumaa).
Viongozi wa waasi hao
walikamatwa na barua nyengine za uongo walizoziandika wenyewe, zilizojulikana
baadaye kuwa ni 'barua za fitna' iliyosababisha vita hivyo, na waasi hao kama
kawaida yao walikanusha tena na kudai kuwa si wao walioziandika, na kuwatuhumu
Mama wa Waislamu ‘Aaishah na Talha na Az-Zubayr (Radhiya Llaahu ‘anhum) kuwa
eti wao ndio walioziandika.
Nia ya waasi hao
ikajulikana vizuri pale walipotoa masharti yao ya mwisho waliposema kuwa;
"Ama Khalifa
ajiuzulu, au tutamuuwa".
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) alikataa kujiuzulu, na hii ni kwa sababu angekubali kufanya hivyo
atakuwa amewakubalia waasi hao matamanio yao, na kwa ajili hiyo heshima pamoja
na haiba ya dola ya Kiislamu itaondoka kwa sababu siku za mbele kila
asiyeridhika na Khalifa atakusanya makundi ya watu na kulazimisha matakwa yake.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) aliwahi kumwambia
‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu):
"Ewe ‘Uthmaan!
Mwenyezi Mungu atakapokuvalisha joho kisha wakaja wanafiki kukutaka ulivue,
usikubali kulivua".
Imam Ahmad bin Hanbal
– Al-Haakim na Sunan za Abu Daawuud
Na joho alilokusudia
Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) ni ukhalifa.
Baadhi ya watu
walidhania kuwa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) alikataa kujiuzulu kwa sababu
ya kupenda ukubwa. Lakini ukweli ni kwamba alikataa kwa sababu alikuwa akiona
mbali, alikuwa akiona yale wenzake hawakuwa wakiyaona, na hii ndio sababu ya
kutowachukulia hatua kali waasi hao, pamoja na kustahamili adha zao na kuhiari
kufa iwapo hapana budi, badala ya kusababisha vita baina ya Waislamu.
Siku moja aliposimama
juu ya membari ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)
akiwahutubia Waislamu, alisema;
"Baadhi ya watu
wamefanya pupa kuukimbilia uasi na kutamani nife haraka. Lakini wallahi
wakiniuwa watatamani ningeishi zaidi kila siku moja mfano wa mwaka, na hii ni
pale watakapoiona damu ikimwagika kwa wingi.
Enyi watu! Wallahi
mimi nia yangu ni kutengeneza, iwapo nitakosea au nitasibu. Na nikiuliwa basi
mjuwe kuwa hamtopendana tena na wala hamtosali pamoja tena na hamtoweza kuteka
miji mingine tena baada yangu".
"Kuona kwake
mbali huko", anaendelea kusema Dr. Khalid Mohammed Khalid;
"Kulionekana baada ya kufa kwake, kwani maana mara baada ya Khalifa huyo
mtukufu kuuliwa, chuki ikaenea na umma ukatawanyika na kugawanyika, na wala
hawakuweza kukubaliana juu ya Khalifa mmoja tena mpaka siku ya leo".
Ananyimwa hata maji ya kunywa
Waasi wakaizunguka
nyumba ya Khalifa kwa muda wa siku nyingi na hawakumruhusu kutoka nje. Hata
maji ya kunywa yalipomalizika, hawakumruhusu kwenda kuchota, wakasahau kuwa
siku ile Waislamu walipokuwa hawana maji ya kunywa, ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) ndiye aliyekinunua kisima cha Roma kwa pesa zake binafsi na kuwaacha
Waislamu wachote bila malipo yoyote, na mpaka siku hiyo walikuwa bado
wanaendelea kuchota kutoka kisima hicho, lakini leo wanakataa kumruhusu yeye na
ahli yake waliokuwa nyumbani kwenda kuchota.
Hapana aliyetegemea
kuwa waovu hao watafikia daraja hii ya ukatili hasa kutokana na sababu
zifuatazo;
Kwanza - ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) wakati huo
alikuwa na umri upatao miaka themanini.
Pili - Alikuwa
miongoni mwa watu wa mwanzo kuingia katika dini ya Kiislamu.
Tatu – ‘Uthmaan ameoa
mabinti wawili wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).
Nne - Alikuwa Khalifa
wa Waislamu.
Tano – Amebashiriwa
mara nyingi na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)
kuingia Peponi.
Tano - Yeye ndiye
aliyetayarisha kwa pesa zake jeshi la wakati wa dhiki lililotoka kwenda
kupambana na Warumi.
Sita - Na yeye ndiye
aliyekuwa akitoa mali yake bila hesabu kwa ajili ya kuwasaidia Waislamu na kwa
ajili ya kuinusuru dini ya Mwenyezi Mungu.
Yote haya na mengi
mengineyo hayakutiwa maanani hata kidogo na waasi hao.
‘Aliy bin Abi Twaalib
(Radhiya Llaahu ‘anhu) akawataka baadhi ya vijana waende kuizunguka nyumba ya
Khalifa kwa ajili ya kumlinda. Akawachagua Al-Hasan, Al-Husayn, (wanawe),
Abdullaah bin Zubayr, Abdullaah bin ‘Umar bin Al-Khattwwaab na Maswahaba
wachache (Radhiya Llaahu ‘anhum) waliokuwepo Madiynah wakati ule na kuwapa
jukumu hilo.
Anasema Ibni Taimiya
katika kitabu chake kiitwacho 'Minhaji Sunnah' kuwa;
"Hapana hata
mmoja katika Maswahaba watukufu (Radhiya Llaahu ‘anhum) aliyesimama pamoja na
waasi hao, isipokuwa Muhammad bin Abu Bakr aliyethubutu kuingia ndani ya nyumba
ya ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumshika ndevu zake na kuzivuta kwa
nguvu, na ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) akamwambia;
"Baba yako
alikuwa akiziheshimu ndevu hizi na laiti angekuona katika hali hii basi angeona
haya kwa haya unayoyatenda".
Baada ya kuambiwa
maneno hayo Muhammad akatoka mbio nje ya nyumba huku akiwa analia na mikono
yake ikimtetemeka".
(Mwisho wa maneno ya
Ibn Taymiyyah).
Waasi wanajaribu ndani ya nyumba ya Khalifa
Waasi, wengi wao
wakiwa watu waliotoka nchi ya Misri walijaribu kuuvamia mlango wa nyumba ya
Khalifa na kuingia kwa nguvu, lakini Maswahaba wachache waliokuwepo nje ya
nyumba h iyo kwa ajili ya kuilinda walifanikiwa kuwazuwia na kuwarudisha nyuma.
‘Abdullaah bin Salaam
(Radhiya Llaahu ‘anhu)[1] alikuja pia na akajaribu kuwazuwia
huku akiwaambia;
"Msizisalitishe
panga za Mwenyezi Mungu baina yenu, kwani Wallahi mkizisalitisha hamtoweza tena
kuuzima moto wake, na mji wenu huu umezungukwa na Malaika, Wallahi mkimuuwa
basi Malaika wataondoka na
kukuacheni."
Wakamwambia;
"Ondoka ewe
mwana wa kiyahudi".
Imepokelewa kutoka
kwa ‘Abdullaah bin Omair (Radhiya Llaahu ‘anhu) kuwa; ‘Abdullaah bin Salaam
aliingia nyumbani kwa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu), lakini ‘Uthmaan ambaye
hakuwa akitaka kulindwa na mtu yeyote akamwambia:
"Kwangu mimi
bora uwe nje kuliko ndani humu".
‘Abdullaah akatoka na
kuwahutubia tena waasi hao akawaambia;
"Enyi watu! Jina
langu wakati wa Ujahilia lilikuwa fulani, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla
Llaahu ‘alayhi wa sallam) akanipa jina la ‘Abdullaah, na kwa ajili yangu
ikateremshwa aya ya kumi katika Suratul Ah-qaf isemayo;
"Sema;
"Mnaonaje kikiwa (kitabu hiki) kimetoka kwa Mwenyezi Mungu; nanyi
mumekikanusha na mashahidi MIONGONI MWA WANA WA ISRAILI, (Mayahudi waliosilimu)
walishuhudia juu ya mfano wa haya na wakaamini haya na nyinyi mnafanya kiburi.
Kwa yakini Mwenyezi Mungu hawaokoi watu madhalimu".
Na pia imeteremshwa
juu yangu aya ya 43 ya Suratul Raad isemayo;
"Na wanasema
waliokufuru "Wewe si Mtume", sema; "Mwenyezi Mungu anatosha kuwa
shahidi baina yangu na baina yenu (kuwa mimi ni Mtume) na (pia) yule MWENYE
ILIMU YA KITABU.[2]"
Nakuusieni msije
mkazisalitisha panga zenu baina yenu kwani mji huu umejaa Malaika na mtakapomuuwa
Khalifa wa Waislamu basi Malaika watakuhameni".
Waasi wote kwa pamoj
wakasema; "Muuweni Myahudi huyu"
Anasema Ibni Kathiyr
(Rahimahu Allaahu);
"Tizameni
tofauti kubwa iliyopo baina ya ‘Abdullaah bin Salaam (Radhiya Llaahu ‘anhu)
aliyesilimu mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam)
na ambaye aya nyingi zimeteremka juu yake zikimsifia, vipi alivyokuwa akimtetea
Khalifa wa Waislamu, na ‘Abdullaah bin Saba-a Myahudi aliyesilimu kwa unafiki
aliyekuwa akiwachochea watu wamuuwe Khalifa huyo".
Kuuliwa kwa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
Wakati nje ya nyumba
waasi wanajibizana na Maswahaba, huko ndani ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
aliuchukua msahafu wake na kuanza kusoma mpaka usingizi ulipomchukua, na
alipokuwa amelala akamuota Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa
sallam) akimwambia;
"Njoo ule futari
pamoja nasi leo". Na ‘Uthmaan siku hiyo alikuwa amefunga. Alipozindukana
alifurahi sana, akawa akijisemesha moyoni mwake; 'Nimemuota Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na amenialika nile futari pamoja naye!
Subhanallah!", Akainuka na kwenda kuwaeleza watu wa nyumba yake juu ya
ndoto ile, kisha akaingia chumbani kwake na kuendelea kusoma Qur-aan.
Waasi baada ya
kushindwa kuingia kupitia mlangoni kutokana na ulinzi mkali uliopo nje,
wakaamua baadhi yao waondoke kwa siri na kujaribu kuingia kwa njia ya uwani.
Wakafanikiwa kuubomoa
ukuta wa uwa na kuingia bila ya walinzi walioko mbele ya nyumba kuwa na habari,
wakenda moja kwa moja mpaka chumbani kwa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumsimamia mbele yake huku yeye akiwa anaendelea kusoma Qur-aan bila kuwajali,
na wakati huo alikuwa ameifikia aya 173 ya Suratul Imran, pale Mwenyezi Mungu
Anaposema;
"Wale ambao watu waliwaambia;
"Watu wamekukusanyikieni. Kwa hivyo waogopeni". Lakini (maneno hayo)
yakawazidisha imani wakasema; "Mwenyezi Mungu anatutosha. Naye Mlinzi bora
".
Mmoja wa waasi hao
aitwaye Saudan bin Hamran alinyanyua chuma alichokuwa amekibeba na kumpiga
nacho ‘Uthmaan mkononi kwa nguvu zake zote, na ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu)
hakupiga kelele wala kujitetea, bali alistahamili huku akiwaambia;
"Huu ni mkono wa
mwanzo ulioandika Qur-aan".[3]
‘Uthmaan akataka
kuukumbatia msahafu, na khabithi yule akaupiga teke ili asiweze kuukumbatia,
lakini msahafu ulikataa kutengana na yule aliyefanya juhudi ya kuuandika katika
kitabu kimoja, ukazunguka na kubaki mikononi mwake.
‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) akaufunga msahafu akihofia asije akauchafua kwa damu iliyokuwa
ikimtoka kwa wingi, lakini mnafiki yule aliendelea kumpiga kwa chuma tumboni na
kila sehemu aliyoweza kuifikia huku akitumia nguvu zake zote na alikuwa
akisaidiwa na mnafiki mwengine aitwae Al Ghafiqiy aliyeunyanyua upanga wake juu
na kuuteremsha kwa nguvu zake zote ili ampige nao ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu
‘anhu) na kumuuwa, lakini mke wa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliupeleka
mkono wake kumkinga mumemwe, na upanga wa khabithi yule ukaangukia mkononi
mwake na kukikata kiganja pamoja na vidole vya mkono wake, kisha akaunyayua tena
upanga wake juu na kumchoma ‘Uthmaan kwenye tumbo mara tisa mpaka akamuuwa, na
baada ya kumuuwa akasema kwa kujisifu;
"Nimemchoma mara
tisa, tatu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na mara sita kwa ajili ya yaliyokuwa
moyoni mwangu".
Amesema uongo mnafiki
yule, kwani angelisema;
"Nimemchoma mara
tisa kwa ajili ya yaliyomo moyoni mwangu", hapo angekuwa amesema kweli.
Kisha wanafiki hao
wakasema;
"Kwa vile damu
yake ni halali kwetu, kwa hivyo hata mali yake ni halali kwetu pia".
Wakaanza kuchukua
kila kilichokuwemo ndani ya nyumba, na mwisho wakamvua mke wa ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) hata kitambaa alichokuwa amejifunikia, na baada ya kufanya dhulma
yao hiyo wakaondoka na kumuacha Khalifa wa Waislamu akiwa keshafariki dunia na
mkewe waliyemkata mkono akiwa taabani huku damu ikimtoka kwa wingi.
Maziko Yake
Ulipita muda kidogo
kabla ya watu waliopo nje kutanabahi juu ya yaliyotendeka ndani ya nyumba ya
Khalifa ‘Uthmaan (Radhiya Llaahu ‘anhu). Walipoingia walimkuta akiwa
keshairudisha roho yake kwa Mola wake. Wakaichukua maiti yake na kuikosha,
wakamsalia, kisha wakaenda nayo Al Baqiy-i kwa ajili ya kumzika. Lakini waasi
wakafanya zogo kubwa sana na kuzuwia asizikwe humo, na badala yake akazikwa nje
ya ukuta wa makaburi ya Al Baqiy-i, mahala panapoitwa 'Hishil kaukab', lakini
wakati wa utawala wa Muawiya bin Abi Sufyan Radhiyallahu anhu, akaamrisha ukuta
wa Al Baqiy-i uvunjwe na eneo lake kuongezwa ili kaburi la ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) liwemo ndani ya eneo la Al Baqiy-i.
"Wewe Ndiye Rafiki Yangu Peponi ewe ‘Uthmaan"
Katika Mujamma al
Zawaida kitabu cha Manaqib, anasema Al Haythamiy;
"Siku moja Mtume
wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alisema kuwaambia Maswahaba
wake (Radhiya Llaahu ‘anhu):
"Leo nimeoneshwa
daraja zenu Peponi", kisha akamsogelea Abu Bakr (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumwambia;
"Pana mtu
ninayemjua jina lake na jina la baba yake na la mama yake. Mtu huyu mlango
wowote wa Peponi atakaoupitia atakuwa akiambiwa;
'Marhaban Marhaban
(karibu karibu)".
Salman (Radhiya Llaahu
‘anhu) akauliza;
"Bila shaka mtu
huyu shani yake ni kubwa sana?"
Mtume wa Mwenyezi
Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akasema;
"Mtu huyo ni Abu
Bakr bin Abi Quhafa" (Jina halisi
la Abu Bakr Asw-Swiddiyq)
Kisha akamuelekea
‘Umar bin Al-Khattwwaab (Radhiya Llaahu ‘anhu) na kumwambia;
"Ewe ‘Umar,
nimeoneshwa kasri iliyojengwa kwa lulu nyeupe na kupambwa kwa Yakuti,
nikauliza:
'Kasri ya nani hii?'
Nikaambiwa kuwa ni ya
kijana wa Ki-Quraysh. Nikadhania ni yangu, na nilipotaka kuingia ndani,
nikaambiwa; 'Muhammad, hii ni kasri ya ‘Umar, na hakuna kilichonizuwia
nisiingie isipokuwa nilipokumbuka wivu wako".
‘Umar (Radhiya Llaahu
‘anhu) akalia sana, kisha akamwambia;
"Nakufidia kwa
baba na mama yangu. Nikuonee wivu wewe ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?"
Kisha Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwendea ‘Uthmaan (Radhiya
Llaahu ‘anhu) na kumwambia;
"Kila Mtume ana
rafiki yake Peponi na wewe ndiye rafiki yangu Peponi (Ewe
‘Uthmaan)",
Kisha akauchukua
mkono wa ‘Aliy (Radhiya Llaahu ‘anhu) na
kumwambia;
"Ewe ‘Aliy!
hutoridhika ikiwa nyumba yako Peponi imekabiliana na nyumba yangu?"
Ali Akamwambia;
"Nakufidia kwa
baba yangu na mama yangu ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu".
Kisha Mtume wa
Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia;
"Basi nyumba
yako imeelekezana na nyumba yangu Peponi…"
[1] Huyu alikuwa Myahudi aliyesilimu
mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na aya nyingi katika Qurani
ziliteremshwa kumsifia
[2] Ambaye
ni Abdullahi bin Salaam (Radhiya Llahu anhu)
[3]
‘Uthmaan (Radhiya Llahu ‘anhu) ndiye aliyeiandika Sura za
mwanzo za Qurani, Suratul Fatiha,
Suratul Naas na Suratul Falaq.