Safiyyah Bint Abdulmuttalib - Mwanamke wa Mwanzo Kumuua Mshirikina


Safiyyah Bint Abdulmuttalib

Mwanamke wa Mwanzo Kumuua Mshirikina


Ni nani huyu mama mtukufu mwenye hadhi aliyetamaniwa na kutarajiwa na maelfu ya wanaume. Ni nani Sahaba huyu shujaa aliyekuwa wa mwanzo katika wanawake kumuua mshirikina katika uislam?
Ni nani mwanamke huyu mwenye ushujaa na ushupavu alietoa shujaa wa mwanzo kunyanyua upanga katika njia ya Allah. Hakika si mwengine ila ni Safiyyah bint Abdulmuttalib al-Hashimiya Al Qurayshiya, shangazi yake Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) unatosheleza utukufu wake kwa kila upande
Baba yake, Abdulmuttalib ibn Hashim ni babu wa Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam)   na kiongozi wa makureshi na bwana mwenye kutiiwa. Mama yake Haalab bint Wahab ni dada wa bibi Amina bint Wahab mama yake Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam).
Mumewe wa mwanzo ni Alharith ibn Harb, ndugu wa Abu Sufiyan ibn Harb kiongozi wa Bani Umaiyyah. Na alimkalia kizuka mumewe wa pili ambae ni         Al-Awwaam ibn Khuwaylid ndugu wa Bibi Khadija bint Khuwaylid mama mtukufu wa waarabu kabla uislam na ni mama wa waislam wa mwanzo. Na mtoto wake Zubeir ibn Al-Awwaam ni mlinzi wa Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam). Je baada ya haya kuna zaidi ya utukufu ambao nafsi zingeliutamani zaidi ya utukufu wa imani?!.
Alifariki mumewe Al-Awwaam ibn Khuwaylid, akiwa amemwachia mtoto mmoja mdogo nae ni Zubeir, mtoto aliemlea katika maisha ya kishujaa na ukakamavu na akamlea kuwa ni mpanda farasi na mpiganaji shujaa.  Ikawa mchezo wake daima ni kutunga shabaha na kutengeneza pinde na akitamani atumie ushujaa huu kwa kila lenye kumtisha na kumzonga na kumhatarisha. Na alikuwa akimuona anazembea au kuogopa humpiga sana. Ikafika hadi ami zake wakamgomba na kumwambia; "Sivyo hivi mtoto anavyolelewa na kupigwa wewe unampiga na kumuumiza. -sivyo hivyo- mama anatakiwa kumpenda mwanawe". Akawajibu kwa kusema; “Ama anaesema kwamba namchukia basi amesema uongo bali nampiga apate akili na ashinde na aje na ngawira"
Mwenyezi Mungu alipomtuma Mtume wake na dini ya uongofu na haki na akamtuma kuwa ni muhadharishaji na mtoa bishara njema kwa watu, akamuamrisha aanze kulingania watu wake wa karibu akakusanya Bani Abdulmuttalib wakike kwa kiume, wakubwa kwa wadogo akawahutubia na kusema:
“Ewe Fatma bint Muhammad, ewe Safiyyah bint Abdulmuttalib enyi ukoo wa Bani Abdulmuttalib hakika mimi similiki chochote kwenu mbele ya Allah".
Akawalingania imani kuwasisitiza kuiamini risala yake wakaikubali nuru ya imani waliyoikubali na wakaitakataa nuru wale waliyoikataa. Akawa Safiyyah bint Abdulmuttalib miongoni mwa kizazi cha mwanzo miongoni mwa waislamu waumini hapo ndipo alipozidi kujikusanyia utukufu wa nasaba na utukufu mkuu wa Uislamu.
Akaingia Safiyyah katika msafara wa nuru ya (kiimani) yeye na mwanawe, na akapata shida mithili ya zile zilizowakaribia waislamu wa mwanzo kutokana na vishindo na mateso ya makureshi.
Mwenyezi Mungu alipomuamrisha Mtume kuhajiri kwenda Madina, aliacha Bibi huyu Mtukufu nyuma yake Makka kila kumbukumbu njema na njia zote za fakhari, na akaelekea Madina akiwa ni mwenye kuhajiri na dini yake kwa ajili ya Allah na Mtume wake.
Licha ya kwamba mama huyu mtukufu alikuwa anaingia miaka sitini ya umri wake, alikuwa na nafasi kubwa katika medani za jihadi. Tarekhe (historia) ingali inaitaja nafasi huyu kwa ulimi wa mshangao na shukrani. Inatosheleza hapa kutaja matukio mawili. La mwanzo (wake?) ni katika vita vya Uhud na la pili ni siku ya  vita vya Handaki.
Ama yanayomuhusu kutokana na vita vya Uhud ni kwamba alitoka pamoja na jeshi la waislamu akiwa na kundi la wanawake wa kiislamu akawa ni mwenye kuchota maji kunywesheza wenye kiu, na kukusanya na kuweka sawa pinde na mishale. Huku akiwa na lengo lake kuu nalo ni kushuhudia vita kwa kila hisia zake.
Hakuna ajabu kwa hilo kwa ndugu yake Hamza, Simba wa Mwenyezi Mungu na mwanawe Zubeir, mlinzi wa Mtume wamo (vitani). Vile vile juu ya yote haya vita hivi ni muhimu kwake kwani Uislamu alijiunga nao kwa mapenzi na akahajiri kwa ajili ya Allah akitarajia malipo. Na kupitia dini hiyo, ndiyo pepo ataipata.
Pale alipoona waislamu wanamkimbia Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) ila wachache na wakawa washirikina wamemkaribia Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam)  na kutaka kumuua; akatupa mtungi chini na kuchupa mithili ya simba jike  ambae watoto wake walioshambuliwa. Akachomoa mkuki kwa mmoja aliyekufa, akawa anakata safu akishambulia nyuso za (washirikina) huku akipaza sauti yake  kuwaambia waislamu:
“Acheni nyie! mnashindwa mbele ya Mtume wa Allah?” Mtume alipomuona anamsogelea alichelea asije akamuona ndugu yake amekufa na kukatwakatwa vibaya vibaya na akamuashiria mwanawe Al-Zubeir akasema Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam). kumwambia:
“Zubeir!, mwanamke! Mwanamke!"
Zubeir akageuka kumwangalia na kumwambia;
"Ewe mama yangu rudi! rudi!"
Akamwambia: "Huna mama leo hapa!"
Akasema Zubeir; “Mtume amekuamrisha kurudi".
Akasema “kwa nini?, Wakati nimesikia ndugu yangu amepasuliwa?”
Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) akamwambia Zubeir; “Mwachilie aende zake"
Baada ya vita kumalizika, Safiyyah alisimama mbele ya ndugu yake Hamza, akamkuta amepasuliwa tumbo na ini kutolewa na pua imekatwa na masikio pia. Uso umechorwachorwa kwa kuchinjwa, akamtakia msamaha kwa Allah na akasema; "hakika nimeridhia qadhaa ya Allah .Wallahi nitasubiri na kutarajia ujira Inshaallah.”
Hivi ndivyo ilivyokuwa hali yake siku ya Uhud.
Ama hali yake siku ya Handaki, ni kisa hichi cha ajabu chenye kushangaza hata wale wenye akili. Pokea habari hizi kama zinavyosimuliwa na vitabu vya kihistoria.
Ilikuwa ni kawaida ya Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) anapoazimia vita, kuwaweka wanawake pamoja na watoto kwenye ngome ili kuwalinda dhidi ya mashambulizi ya ghafla dhidi ya mji wa Madina wakati wapiganaji waislamu hawapo.
Hivyo ndivyo ilivyokuwa siku ya Handaki akawaweka wakeze na shangazi yake na kundi la wanawake wa kiislamu kwenye ngome ya Hassan ibn Thabit ambayo aliirithi toka kwa wazee wake. Ilikuwa ni ngome imara na haikuwa rahisi kufikiwa.
Wakati waislamu walipokuwa ulinzini pembeni mwa Handaki kukabiliana na Makureshi na washirika wao, wakawa wameacha wanawake na watoto na kumshughulikia adui, Ghafla, Safiyyahh bint Abdulmuttalib, alikiona kivuli kinakwenda kwenye kiza cha alfajiri. Akatega sikio kusikiliza na kukitolea jicho na kukifuatilia. Kumbe alikuwa ni myahudi akijisogeza kwenye ngome huku akijaribu kutafuta habari na kupeleleza  kiliomo ndani ya ngome ile.
Safiyyah alitambua kuwa yule alikuwa ni jasusi alietumwa kutafuta habari. Je baina ya kuta zake kuna wanaume ndani ya ngome au hamna  zaidi ya wanawake na watoto?. Akasema Safiyyah ndani ya nafsi yake; Mayahudi wa Banu Quraidha wamevunja ahadi yao na Mtume na wamewaunga mkono makureshi na washirika wao dhidi ya waislamu. Wala hapana baina yetu na (mayahudi) wa kutuhami na Mtume (Sallallahu ‘Alayhi Wasallam) na masahaba wapo mstari wa mbele dhidi ya adui.
Akiweza kuchukua habari za uhakika wa kilichomo ndani ya ngome hii atateka wanawake na kuwafanya watumwa watoto na huo utakuwa ni mkosi mkubwa. Hapo hapo alichukua ushungi wake (khimar) na kufunika kichwa na akajizonga nguo zake vizuri kiunoni na akachukua kipande cha kigongo akaweka begani mwake na akatoka mpaka kwenye mlango wa ngome. Akafungua kwa hadhari na kumuangalia adui wa Allah kwa hadhari kubwa. Alipohisi yupo kwenye shabaha nzuri na kumpata akamwachia kigongo kizuri cha kichwa na papo hapo akaanguka chini na kumuongeza cha pili na cha tatu, mpaka akahakikisha amekwisha kufa.
Akamwendea tena na kisu chake na kukitenga kichwa cha adui huyo na mwili wake, baada ya hapo akakirusha nje ya ngome, kikibiringika mpaka walipo mayahudi. Mayahudi walipokiona kichwa cha mwenzao kikibiringita walisema; “Tunajua wazi kwamba Muhammad asingeweza kuwaacha wanawake na watoto pasina ulinzi”
Wakarudi nyuma kwenda zao.
Mwenyezi Mungu awe radhi na Safiyyah bint Abdulmuttalib. Hakika alikuwa ni mfano wa pekee wa wanawake wa kiislamu.
Amemlea mtoto wake na akakamilisha vyema malezi. Mitihani ikamjaribu ikamkuta ni shujaa na mwenye akili. Tarekhe ikamuandika katika kurasa zake safi: “Hakika Safiyyah bint Abdulmuttalib ni mwanamke wa mwanzo kumuuwa mshirikina katika Uislamu.