016 - Hadiyth Ya 16: Athari ya Kuelekeza Kwenye Hidaayah Na Upotofu

016 - Hadiyth Ya 16: Athari ya Kuelekeza Kwenye Hidaayah Na Upotofu


عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه) أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ (صلى الله عليه و آله وسلم): ((مَنْ دَعَا إِلَى هُدًى كَانَ لَهُ مِنْ الأَجْرِ مِثْلُ أُجُورِ مَنْ تَبِعَهُ, لاَ يَنْقُصُ ذَلِكَ مِنْ أُجُورِهِمْ شَيْئًا, وَمَنْ دَعَا إِلَى ضَلاَلَةٍ كَانَ عَلَيْهِ مِنْ الإِثْمِ مِثْلُ آثَامِ مَنْ تَبِعَهُ لاَ يَنْقُصُ ذَلِكَ مِنْ آثَامِهِمْ شَيْئًا)) رواه مسلم
Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah (رضي الله عنه)  kwamba Mtume wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Atakayelingania katika uongofu, atapata ujira mfano wa aliyemfuata, bila ya kupunguziwa chochote katika ujira wao. Na atakayelingania katika upotofu, atapata dhambi mfano wa dhambi za waliomfuata bila ya kupunguziwa chochote katika dhambi zake)).[1]
 
Mafunzo Na Hidaaya:
 
  1. Fadhila za mlinganiyaji ni nyingi mno kwa kufuatwa anayoyalingania, na thawabu zake zinazidi hata baada ya kufariki kwake kwa kila atakayefuata. [Rejea Hadiyth namba 54, 78].
 
  1. Ulinganiaji Dini ni katika mema yatakayoendelea baada ya kufariki kwake. ((Na mema yenye kudumu ni bora katika malipo mbele ya Mola wako na yana mwisho mwema)).[2]
 
  1. Fadhila za elimu na da’wah, nazo hazipatikani ila kwa kuwa na elimu ya Dini, na si kwa kufuata watu au matamanio. [Yuwsuf: 12: 108].
 
  1. Umuhimu wa kujifunza elimu sahihi, la sivyo kuna hatari nyingine, nayo ni kujitayarishia makazi ya motoni. [Rejea Hadiyth namba 77].
 
  1. Mlinganiyaji mema au maovu na mtendaji wake, watapata malipo sawasawa, mazuri au mabaya.

  1. Mlinganiyaji atahadhari anayoyalingania, kwani akilinganiya maovu ataacha athari nyuma yake na atabeba dhambi zake na kila atakayemfuata. [Yaasiyn: 36: 12]. Na pia:
 
لِيَحْمِلُوا أَوْزَارَهُمْ كَامِلَةً يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۙ وَمِنْ أَوْزَارِ الَّذِينَ يُضِلُّونَهُم بِغَيْرِ عِلْمٍ ۗ أَلَا سَاءَ مَا يَزِرُونَ
 Ili wabebe mizigo (ya madhambi) yao kamili Siku ya Qiyaamah, na mizigo (ya madhambi) ya wale waliowapoteza bila ya elimu. Tanabahi!  Ubaya ulioje (mizigo ya dhambi) wanayoyabeba[3]
 
  1. Muislamu atahadhari kufuata mafunzo ya ubatili na ajiepushe na wabatilifu wanaopotosha watu katika Dini.
 
  1. Mitume walipowalinganiya watu wao wasimshirikishe Allaah (سبحانه وتعالى) jibu la wengi wao lilikuwa kwamba wamewafuata mababa zao. Na hali imekuwa ni hivihivi kwa walio wakaidi katika kufuata uzushi. [Al-Baqarah 2: 170, Al-Maaidah 5: 104, As-Swaaffaat 37: 69-70, Az-Zukhruf 43: 22-23].
 
 
 



[1]  Muslim.
[2]  Al-Kahf  (18: 46) Maryam  (19: 76).
[3]  An-Nahl (16: 25).