Suhayb Ar-Rumi-aliefadhili dini badala ya mali

Suhayb Ar-Rumi-aliefadhili dini badala ya mali

 
Kati kati ya karne ya tano milaadiya na kabla ya kuja utume, mji wa Al-Uballah ulioko kwenye kingo za mto Euphrates ulitawaliwa na Mwarabu anaeitwa Sinan Ibn Malik. Alipewa jukumu hilo na mtawala wa kiajemi.  Alikuwa na watoto wengi na kwa bahati nzuri alipendezwa sana na mmoja wa watoto wake ambaye wakati huo alikuwa umri wake hata hajatimia miaka mitano. Jina lake ni Suhayb na alikuwa mtoto mchangamfu na mara nyingi alikuwa akimfurahisha baba yake.
 
Siku moja mama yake Suhayb alimchukua pamoja na ndugu zake wengine kwenda matembezi katika kjiji cha Ath-thani.  Ilikusudiwa iwe siku ya mapunziko na furaha lakini yaliyotokea siku hiyo yalikuwa mambo makubwa na kubadilisha mwelekeo wa maisha ya Suhayb.
 
Siku hiyo, kijiji hicho kilivamiwa na majeshi wa kibizantini.  Walinzi walioambatana na msafara wao wote walizidiwa nguvu na kuuliwa. Vitu vyao vyote vilitekwa na kundi la watu (kutekwa nyara) akiwemo mtoto mdogo wa miaka mitano, Suhayb.
 
Suhayb akachukuliwa na kupelekwa soko la watumwa mji mkuu wa Constantinpole na kuuzwa.  Hapo tena akapita kwenye mikono tofauti ya wafanyabiashara ya utumwa. Khatma yake haikuwa tofauti na maelfu ya watumwa waliojaa kwenye nyumba za kasri na mavilla ya wabizantini.
 
Utoto na ujana wake wote aliupitisha akiwa mtumwa na  kwa muda wa miaka ishirini alikuwa kwenye ardhi ya wabizantini.   Hii ilimsaidia kuweza kufahamu na kuelewa mfumo mzima wa maisha na jamii ya wabizantini. Aliona ndani ya makasri vipi udhalimu na ubadhirifu ulivyotawala na kuichukia sana hali hii huku akijisemea, “jamii kama hii itaweza kusafishwa na gharika”
 
Alikulia na kuongea kigiriki lugha ya kibizantini na kusahau kabisa kiarabu.  Hata hivyo, hakusahau asili yake mtoto wa jangwani. Alikuwa akiota na kutamani siku ambayo ataachiwa huru na kuungana na watu wake. 
 
Ilipojitokeza nafasi tu alitoroka na kukimbilia moja kwa moja Makka, unzi hizo ilikuwa ndio makaazi ya wakimbizi.  Alipewa jina la Arrumi kutokana na lugha na umbile lake. Mmoja katika waheshimiwa wa Makka enzi hizo Abdullah ibn  Judan akamchukua na kukaa naye.  Suhayb akajiingiza katika biashara na kupata mafanikio sana mpaka kuwa tajiri.
 
Siku moja aliporudi Makka kutoka katika safari zake za kibiashara akapata habari kwamba Muhammad ibn Abdulla anawalingania watu kumuamini Mwenyezi Mungu na kuwaamrisha kufanya mambo mema na kuwakataza kufanya mambo mabaya.  Akauliza kuhusu mtu huyu (Muhammad) ni nani hasa na wapi anakaa, akafahamishwa.
“Yupo kwa Al-Arqam ibn Al-Arqam, jihadhari na maquraysh wasikuone.  Wakikuona watakufanyia na wewe ni mgeni mji huu na wala huna uhusiano wowote wa kikabila wa kukutetea wala ukoo wa kukusaidia”
 
Suhayb akaenda kwa kujifichaficha mpaka nyumba ya Al-Arqam.  Mlangoni akakutana na Ammar bin Yassir ambaye baba yake anajuana naye. Alisita kwanza kisha akasogea na kusema,
“Umekuja kufuata nini (hapa) Ammar?”
“Nikuulize wewe, nini umefuata?, akajibu Ammar.
“Ninataka kwenda kwa huyu mtu (Muhammad) na kumsikiliza mimi mwenyewe nini anasema”
“Na mimi hivyo hivyo,” basi na tuingie, wakaambizana.
 
Wakaingia na kusikiliza kwa kituo. Nuru ya imani ikawaingia  nyoyoni mwao na siku hiyo hiyo wakasilimu.  Wakaitumia siku hiyo nzima wakiwa pamoja na Mtume (SAW) na ilipofika usiku wakaondoka kwa kujificha, nyuso zao zimejaa tabasamu .
 
Kama yale yaliyowasibu waislam waliopo Makka, yakampata na Suhayb pia. Aliteswa na kuteswa kama walivyoshughulikiwa Bilal, Ammar na mama yake Sumayyah, Khabab na wengineo. Yalikuwa ni mafundisho ya Mtume (SAW) na kupewa moyo na masahaba ndio vitu pekee vilivyomsaidia kutoterereka katika imani yake.
 
Rukhsa ya kufanya hijra, kwenda Madina ilipotoka Suhayb aliazimia kuandamana na Mtume Muhammad (SAW) pamoja na Abubakar.  Hata hivyo, maquraysh wakagundua mpango wake huu na kuamua kumwekea ulinzi wa hali ya juu ili asiweze kuondoka yeye mwenyewe pamoja na mali zake alizozipata  alipokuwa akifanya biashara Makka .
 
Baada ya Mtume na Abubakar kuondoka, Suhayb aliendelea kubaki Makka na kuvuta muda huku akisubiri wakati muafaka wa kufanya hijra. Alijitahidi kutafuta mbinu za kuwakwepa walinzi bila ya mafanikio mpaka ikambidi atumie hila.
 
Usiku mmoja ilikuwa baridi kali na Suhayb akadai kuwa maumivu ya tumbo na alitoka kila mara kwenda nje akijidai ‘anajisaidia’.  Walinzi walipomuona katika hali ile wakaambizana, “tusiwe na wasi wasi Lata na Uzza wanamshughulikia tumbo lake”.
Hawakushtushwa sana na wakaendelea na lindo lao hadi usingizi ukawachukua.  Suhayb akatoka tena kama kwenda msalani na alipowaona wamelala akawavuka na kupanda ngamia akielekea Madina.Walinzi waliposhtuka na kugundua kwamba Suhayb tayari ametoroka, wakapanda farasi wao mbio kumfuata wakijua wapi alikoelekea na hatimaye kumkaribia.
 
Suhayb alipowaona akapanda kwenye mlima na kujiandaa kwa kuelekeza mshale wake kwa maquraysh huku akitoa sauti kubwa na ya kutisha, “enyi maquraysh, nnakuahidini mimi ni mmoja katika mastadi wa mishale na nikitunga sikosei, na yoyote atakayenikaribia kila mshale nilionao nitampiga nao na kisha nitapambana nanyi kwa upanga wangu.”
 
Msemaji wa kiquraysh akasema, “ na sisi tutahakikisha kwamba hatutokuruhusu ukimbie na mali. Ulipokuja Makka ulikuwa maskini hohehahe, na ukapata ulichokipata.”
Suhayb akawauliza, “Nikikupeni mali zangu mtafanya nini?, mtaniachia niendelee na safari yangu?.
Akajibiwa, “ndiyo”.
 
Suhayb akawafahamisha wapi alipoficha mali zake Makka na maquraysh wakamruhusu.
 
Akaendelea na safari yake huku akiwa na furaha kwamba baada ya muda atakuwa karibu na Mtume (SAW) na kupata uhuru wa kuabudu. Alipofika Quba nje kidogo ya Madina ambapo Mtume Muhammad (SAW) alipumzika wakati wa safari yake, Mtume (SAW) alimuona Suhayb anakuja na alijawa na furaha na kumpokea.
 
“Biashara yako imezaa ewe Abu Yahya, biashara yako imezaa,” alisema Mtume (SAW) mara tatu. Suhayb alifurahi sana kusikia kauli ya Mtume Muhammad (SAW) ingawa alishangaa kidogo na kusema, “Wallahi, hajawahi kuja mtu yoyote (kukuhadithia) kabla yangu.  Ni Jibril peke yake ndio aliyekwambia, na kuyathibitisha hayo.  Aya 207 Surati Baqarah ikateremka.
 
“Na katika watu yupo ambae huiuza nafsi kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu;na Mwenyezi Muingu na mpole kwa waja wake”
 
Nini fedha, nini mali ni dhahabu na dunia yote mbele ya imani sahihi?  Suhayb akapendwa sana na Mtume (SAW) na kumbashiria kuwa atakuwa ufunguo wa kuifungua Byzantin kuingia uislam.
 Suhayb pia alikuwa mtu wa kupenda utani, siku moja Mtume (SAW) alimuona akila tende, akamuona Suhayb ana uvimbe kwenye jicho lake moja na kumwambia huku akicheka, “unakula tende mbivu wakati jicho lako moja lina uvimbe?”
Suhayb akajibu, “Kwani kuna ubaya gani?”
 
“nnakula na jicho jengine”.
 
Suhayb alikuwa mkarimu kwani ruzuku aliyokuwa akipata kutoka Baytul Mal alikuwa anaitoa kuwapa maskini na wanaohitaji, alikuwa mfano wa Aya ya Quran, “ Na kuwalisha chakula juu ya kukipenda kwake,maskini ,mayatima na wafungwa” Al –insaan /8
 
  Ukarimu wake ulisifiwa na Umar ibn Khattab pale aliposema:
“Nimekuona ukitoa chakula kwa wingi mpaka inaonekana unafanya israaf (katika kutoa).
 Suhayb akajibu, “Nilimsikia mjumbe wa Mwenyezi Mungu akisema “Mbora wenu ni yule anaelisha (chakula)” 
Uchamungu wa Suhayb ulikuwa wa kupigiwa mfano kwani hata Umar ibn Khattab alimteua kuwaongoza waislam katika kile kipindi alichokufa mpaka pale kuchaguliwa Khalifa mwengine.
 
Umar aliwaita masahaba sita, Uthman, Ali, Talha, Zubeir, Abdulrahaman ibn Awl na Saad ibn Abi Waqas.  Hakumchagua yoyote miongoni mwao, kwani kama angelifanya hivyo, kwa mujibu wa riwaya “kungelikuwa na muda ambao makhalifa wawili wangelitazamana”
 
Aliwaagiza hawa sita washauriane pamoja na waislam kumchagua mrithi na kusema, “Waliyusalli binnas Suhayb, Suhayb asalishe watu”
 
Alikuwa imamu kwa kipindi chote alichoteuliwa na Umar mpaka alipofariki na hadi kuchaguliwa Khalifa mwengine.
 
Uteuzi wa Suhayb umeonesha pia jinsi uislam ulivyowathamini watu mbali mbali, miongoni mwa waarabu na hata wasiokuwa waaarabu, waliokuwa watumwa na hata mabwana na kudhalika.
 
Enzi za Mtume (SAW) mnafiki mmoja, Qaysib Mutatiyah aliwatukana baadhi ya waislam aliowakuta kwenye ‘halaqah’ wakisoma. Walikuwapo kina Salman Alfarsi, Suhayb Arrumi na Bilal Al habashi na wengineo na akasema,
 
“Ni Aws na Khazraj ndio waliomlinda huyu mtu (Muhammad) na nyinyi mnafanya nini hapa pamoja naye?”
Muadhi ibn Jabal aliposikia dharau hii alikasirika na kumtaarifu  Mtume (SW) yote aliyoyasema Qays.  Mtume (SW) naye akajawa na hasira na hapa hapo akaingia msikitini na kuamrisha kuadhiniwe. 
 
Hii ndio ilikuwa njia ya kuitana waislam kama jambo kubwa limetokea, akasimama na kumshukuru Allah (SW) na kusema:
“Mola wenu ni mmoja, Baba yenu ni mmoja, dini yenu ni moja, chukueni mwongozo.  Hamjaupata uarabu kupitia baba na mama, ni kwa kupitia ndimi, hivyo yoyote anayezungumza kiarabu basi ni mwarabu”