Rumaysah bint Milhan-mahari yake ilikuwa Qur'aan

Rumaysah bint Milhan-mahari yake ilikuwa Qur'aan

 
Hata kabla kufika Uislam Yathrib, Bi Rumaysa alifahamika kwa uzuri wa tabia, akili na mwanamke mwenye msimamo.  Alijulikana kwa majina tofauti yakiwemo Rumaysa na Ghumaysah.  Yote haya inasemekana hayakuwa majina yake halisi. Jina lake lilikuwa Sahlah na baadaye kuwa maarufu kwa jina la Umm Sulaym.
 
Aliolewa chuo cha kwanza na Malik ibn an Nadr na kujaaliwa mtoto Anas ibn Malik, sahaba maarufu enzi za Mtume Muhammad (SAW).
 
Bi Umm Sulaym alikuwa miongoni mwa wanawake wa mwanzo kusilimu Yathrib. Daawa iliyotolewa na Mus-ab ibn Umayr alietumwa maalum na Mtume (SAW) kwa kazi hiyo ilimuingia vyema.  Ilikuwa ni baada ya kiapo cha utii ambapo watu kumi na mbili kutoka Yathrib walikwenda Aqaba kando kando ya mji wa Makka kwa ajili ya kiapo cha utii kwa Mtume (SAW).
 
Kitendo cha kusilimu Umm Sulaym kilifanyika bila ya ridhaa ya mumewe Malik.  Alikuwa nje ya Yathrib kipindi hicho na aliporudi aliona mabadiliko kwenye nyumba na kumuuliza mkewe:
“Vipi umepata mwamko nini?”
Akajibu Umm Sulaym, “hapana ila nimemuamini huyu mtu (akikusudia Mtume (SAW).”
 
Malik hakufurahishwa kabisa na kitendo cha mkewe kusilimu na alizidi kukasirika pale mkewe alipokwenda kuitangaza imani yake hadharani na pia kumfundisha mwanawe Anas mafunzo na mafundisho ya dini mpya:
Alimfundisha kutamka, “Laa ilaha illa Llahu  Muhammadun Rasuulu Llah.” 
Anas alikuwa akipenda kulirudia ‘kalima’ kila mara nyumbani kwao tena kwa ufasaha kabisa.  Malik akajawa na ghadhabu na kumkanya, “Usiniharibie mwanangu.”
Umm Sulaym akajibu, “Wala sijamuharibu.”
 
Mumewe aliamua kuondoka  kwenye nyumba na inasemekana baadhi ya maadui zake walimfanyia njama na kumuua.  Habari hizi zilimshitusha Umm Sulaym lakini hazikumhuzunisha.   Aliendelea kumlea mwanawe na kuhakikisha anapata malezi ya uhakika na aliwahi kusema kwamba hatokuwa tayari kuolewa tena mpaka mwanawe Anas akubali.
 
Taarifa za ujane wa Umm Sulaym zilipozagaa, mtu mmoja Zayd ibn Sahl maarufu Abu Talha aliazimia kwenda kumposa kabla ya watu wengine.  Alikuwa na uhakika wa kutokataliwa, kwani alikuwa tajiri na kuwa na jumba la fahari.  Alikuwa askari farasi na mrusha mishale stadi.  Juu ya yote hayo walikuwa wanatoka kabila moja, Banu Najjar.
 
Abu Talha akaelekea nyumbani kwa Umm Sulaym.  Alikumbuka njiani kwamba Daawa ya Mus-ab  ibn Umayr ndio iliyomfanya asilimu.
Akajisemea, “kwani kitu gani, mbona mumewe mpaka kufa kwake alikufa katika dini yake na alikuwa akimpinga Muhammad na ujumbe wake?”
 
Alifika nyumbani na kugonga, akafunguliwa na Anas naye alikuwepo.  Abu Talhah akajieleza lengo na madhumuni ya ujio ule ni kutaka kumwoa.
 
“Mtu kama wewe Abu Talha, si rahisi kukataliwa.  Lakini sitokubali kamwe kuolewa na wewe ukiwa kafiri.”Alijibu Umm Salaym.
 
Abu Talha akadhani labda ni tabia tu za mwanamke kutotoa jibu hapo hapo na kutaka kumzungusha au labda keshapata mtu tajiri zaidi kuliko yeye.
Hivyo akamwambia, “Nini hasa kinakuzuia kunikubali, Umm Salaym? Ni chuma cha manjano na cheupe? (dhahabu na fedha).
 
Dhahabu na fedha! Umm Sulaym alishtushwa kidogo.  Abu Talha akamwambia kwa sauti iliyojaa upole, “Naam”
 
Umm Sulaym akasema, “Nnakuapia, Abu Talha na nnaapa kwa Allah (SW)  ukikubali kuingia Uislam, nitakuwa radhi kukubali kama mume wangu bila ya hata dhahabu wala fedha.  Uislam wako ndio mahari yangu.”
 
Abu Talha alifahamu vyema athari za maneno yale, na ikawa nafasi muafaka kwa Umm Sulaym kufanya Daawa na kuonesha upofu wa kuabudu masanamu na kusema:
 
“Kwani huyu, Mungu unayemuabudu asiyekuwa Allah (SW) ametoka kwenye udongo, Abu Talha?”
 
Abu Talha akajibu, “ni kweli”
 
“Hujioni kama mpumbavu kuabudu sehemu ya mti halafu sehemu hiyo hiyo iliyobaki kuitumia kuoka mikate na kujipashia moto?  (ikiwa utaachana na itikadi hizo potofu) na ingia uislam, nitakuwa radhi kukubali kama mume wangu na wala sitodai sadaka (mahari) kutoka kwako mbali na uislam wako.”
 
“Nani ataniongoza (kuingia) katika uislam?
 
“mimi”
 
“vipi”
 
“Tamka tamko la haki na ushuhudie kwamba hapana mola anayestahiki kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah (SW) na Muhammad (SAW) na mjumbe wa Allah (SW)
Ukimaliza nenda zako nyumbani na uvunje masanamu yote na uyatupilie mbali.”
 
Umm Sulaym na Abu Talha wakaoana.  Anas, mwanawe alikuwa radhi na waislam walikuwa wakisema:
“Hatujawahi kusikia mahari yenye thamani na hadhi kubwa kuliko mahari Umm Sulaym kwani uislam ndio ulikuwa mahari yake.”
 
Umm Sulaym aliishi kwa furaha na mumewe na alizidi kupendezwa kwani zile fani zake zote sasa alizitumia kwa ajili ya uislam. Abu Talha ni miongoni mwa watu sabini na tatu walioapa kiapo cha pili cha utii kwa Mtume (SAW) hapo Aqaba.
 
Abu Talha alipendezwa sana na Mtume (SAW).  Alipenda kukaa na kumuangalia jinsi anavyoongea na jinsi maneno matamu yanavyotoka kinywani kwa Mtume (SAW).  Alishiriki vita vyote vikubwa na kujulikana zaidi kwa saumu kwani muda mwingi huwa yupo katika funga.  Inasemekana alikuwa na kikataa kimoja maridadi sana Madina kikiwa kimejaa mitende, mizabibu na kuzungukwa na chemchem za maji.
 
Siku moja alikuwa akisali chini ya mti na ndege mmoja mwenye rangi nzuri za kupendeza akaruka mbele yake.  Alishughulishwa na ndege yule mzuri mpaka kusahau rakaa ngapi amesali, mbili? au tatu?. Alipomaliza  akaenda moja kwa moja kwa Mtume (SAW) na kumweleza jinsi alivyoshughulishwa.   Mwisho akasema:
“Shuhudia ewe mjumbe wa Mwenyezi Mungu tokea leo nimekitoa sadaka kikataa hiki kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mtukufu”
 
Ilionekana kwamba Mtume (SAW) alikuwa na huruma sana kwa Umm Sulaym na alipoulizwa akajibu, “Kaka yake aliuwawa pembeni mwangu.”
 
Umm Sulaym alikuwa na dada yake maarufu – Umm Haram,mke wa ubaadah ibn Samit.  Alikufa kwenye jahazi akiwa safarini na kuzikwa Cyprus, mumewe Abu Talha alikufa kwenye jahazi enzi za Ukhalifa wa Uthman na kuzikwa baharini.
 Umm Sulaym alikuwa mwanamke shujaa, alikuwa akificha silaha kwenye mikunjo yake ya nguo zake vitani huku akiwashughulikia majeruhi.  Alijaribu pia kumhami Mtume (SAW) pale vita vya Uhud vilipowageukia waislam.  Na katika vita vya Khandaq, Mtume (SAW) alimuona Umm Sulaym kabeba silaha na kumuuliza ni ya nini.  Umm Sulaym akasema, “ni kwa ajili ya kupigana na hawa walioasi” Mtume (SAW) akamwambia, Mwenyezi Mungu akukinaishe kwa hilo.” 
Wakati wa majanga na mitihani, alikuwa mtu wa subira na uvumilivu wa hali ya juu. Mmoja kati ya watoto wake (Umayr) aliugua hadi kufa wakati mumewe yupo kwenye kikataa.  Alimuosha na kumkafini na kuwaambia waliokuwepo wasimpe habari mumewe kwani alitaka yeye mwenyewe kumtaarifu licha ya kuwa na huzuni na msiba wa mwanawe.
 Alikuwa na mtoto mwengine Abdullah, siku chache baada ya kuzaliwa alimpeleka kwa Mtume (SAW) pamoja na Anas.  Mtume (SAW) akamchukua Abdullah na kumuweka mapajani kwake kasha akasaga tende mdomoni mwake na kumrambisha kidogo Abdullah akawa anajiramba na Mtume (SAW) kusema, “Waansaar wao wanapenda tende tu.” 
Abdullah alipokuwa mkubwa alijaaliwa watoto saba  na wote walihifadhi Quran.
Umm Sulaym alikuwa muislam, mke na mama wa kupigiwa mfano.  Imani yake ilikuwa ya dhati na hakuwa tayari kuhatarisha imani yake na malezi ya watoto wake kwa ajili ya fedha na utajiri hata kama unavutia kiasi gani!
 
Mapenzi yake kwa Mtume (SAW) yalikuwa makubwa mpaka kumpatia kijana wake Anas awe mwambata wake.  Alichukua jukumu la kuwafundisha watoto wake na kushiriki kikamilifu katika shida na raha walizozipata waislam katika kujenga taifa la kiislam na kuishi maisha yake kwa kutaraji radhi za Mwenyezi Mungu.