Abu Musa Al Ashariy - Msomaji Mahiri wa Quraan

Jina lake halisi ni Abdullah ibn Qays bin Salim na umaarufu wake tokea enzi na enzi alikuwa akijulikana kama Abu Musa. Jina la Ash’ariy ni la kabila lake la Yemen.
Alitokea Yemen na kuhamia Makkah na kusilimu baada ya kusikia kuletwa kwa Mtume ambae alikuwa akiwalingania watu kumuabudu Mungu mmoja.Tetesi hizi zilizidi kuzagaa Yemen za huyu mtu anaedai kuwa ni Mtume katika mji wa Makkah mpaka kumfanya Abu Musa kufanya safari kwenda kuhakikisha kama ni kweli.Hakuhakikisha tu bali aliingia moja kwa moja katika dini ya Allah Subhaanahu Wata’ala.
Muda mwingi alikuwa pamoja na Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam akijifunza dini pamoja na kupata mafundisho ya Daawah.Baadae aliagizwa na Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kurudi Yemen kuwalingania watu wake dini kwani wakati huo bado uislamu ulikuwa ukipigwa vita Makkah.
Baada ya kusikia kwamba Waislamu wamehamia Madina na kuanzisha Dola ya kiislamu Abu Musa alikusanya watu wake na waliosilimu wote wakaongoza njia kuelekea Madina kwa njia ya bahari na kwa bahati mbaya upepo ukawavumia vibaya na wakaangukia Habashah. Huko walikutana na masahaba wengine ambao walikuwa wakijiandaa kuelekea Madina akiwemo Jaafar ibn Abi Talib .
Imam Ahmad bin Hanbal anasimulia kwenye Musnad wake kwamba kabla ya kundi hili kuwasili Madina, Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam aliwasimulia masahaba juu ya ujio wa ugeni huu adhimu kama alivyoteremshiwa wahy na Jibriyl ‘Alayhi Ssalaam.
Abu Musa alitokea kuwa msomaji mahiri wa Quraan tokea enzi za Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Inasemekana kitu alichokuwa akikipenda kukifanya katika wakati wake wa mapumziko ikiwa mchana au usiku basi ni kuisoma Quraan. Masahaba walikuwa wakisimulia hata wakiwa safarini na kuwa na machofu bado humsikia Abu Musa akisoma Quraan kwa sauti nzuri akiwaliwaza. Imethibitika kutoka kwa Hadithi sahihi ya Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam kwamba aliwahi kusema kuhusu Qiraa (kisomo) cha Abu Musa kwamba:
: لو رأيتني وأنا أستمع قراءتك البارحة لقد أوتيت مزمارًا من مزامير آل داود                                                         
 Laiti ungeliniona ninavyokisikiliza kisomo chako kizuri hakika umepewa (sauti ya) zumari kama waliyopewa watu wa Daaud (Alayhi Ssalaam)
Muda wake mwingi hakupenda utumike ovyo kwani hata wakiwa safarini na masahaba kuanza kuzungumzia mambo ya kidunia basi huwatanabahisha na kuwausia kuzungumzia imani, aqidah, pepo au moto na mambo mengine ya dini. Mara nyengine huonekana akisoma Quraan kama ilivyo kawaida yake. Na alikuwa mwalimu mzuri wa kuisomesha kwani hata baada ya kufariki kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam alikuwa akienda Msikitini huku akiwaita waislamu kwa kusema:
“Ndugu zangu subirini na bakieni nikusomesheni Quraan kama nilivyojifunza kutoka kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam”
Maisha yake yalikuwa Quraan na Quraan ilikuwa ndiyo maisha yake si kwa kuisoma tu bali hata kwa matendo mpaka kufikia kuwahi kuwausia waliohifadhi Quraan kwa kusema:
               إن هذا القرآن كائن لكم أجرًا وكائن عليكم وزرًا فاتبعوا القرآن ولا يتبعنكم القرآن، فإنه من اتبع القرآن هبط به على رياض الجنة، ومن تبعه القرآن زج في قفاه فقذفه في النار                                                                         
Hakika hii Quraan ina sehemu ambayo mtapata ujira na pia ina sehemu ambayo mtapata dhambi basi ifuateni Quraan na wala Quraan isiwafuate (kuwakimbilia huku nyinyi mnaikimbia) kwani mwenye kuifuata Quraan basi atateremka nayo ndani ya bustani za peponi. Na mwenye kufuatwa na Quraan ndiyo itakayombeba na kumvurumisha katika moto”                                                                          
 Abu Musa ni miongoni mwa masahaba waliokuwa wakiheshimika na kufikia kupewa heshima ya kuwa Kadhi. Masahaba walikuwa wakisema “Makadhi katika umma huu ni ‘Umar (bin Khattaab), ‘Ali (bin Abi Talib) Abu Musa (Al Ash ‘ariy) na Zaid ibn Thabit”
Alikuwa pia ni miongoni mwa wapokezi wa Hadithi kutoka kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam na mjuzi katika elimu ya dini. Na inasemekana aliwahi kukusanya msahafu mzima hata kabla ya amri ya kukusanywa Quraan ilipotolewa baada ya wengi wa waliohifadhi kufariki.
Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam alimteua pamoja na Mu’aadh bin Jabal kwenda Yemen kuwalingania watu na alikuwa akimuusia kuendelea kuwafundisha na kuwaelimisha watu Quraan.
Pia enzi za ukhalifa wa ‘Umar ibnul Khattaab, Allah amuwie radhi, aliteuliwa kuwa Amiri wa mji wa Basra. Khalifa ‘Umar katika uteuzi wake aliagiza katika wasia akifariki, maamiri wote aliowateua wabaki kwa mwaka mmoja tu kisha wabadilishwe isipokuwa Abu Musa pekee aliagiza kuendelea kuwa Amiri kwa miaka mine zaidi! Hii si sudfa bali ni ile thiqa aliyekuwa nayo Khalifa kwa Amiri wake huyu ambae alisifika kwa ukweli na uadilifu.Kwani khalifa hakutaka kubeba jukumu wakati amekwishaondoka duniani lakini alikuwa tayari kwa Abu Musa Al Ash’Ariy. Ni khalifa huyu huyu alikuwa kila akimuona Abu Musa humwambia:
                                 : ذكرنا ربنا تعالى، فيقرأ (أي القرآن).
“Tukumbushe mola wetu mtukufu” na (Abu Musa) alikuwa akiwasomea (Quraan)        
Moja katika riwaya zilizopokewa kutoka kwa Abu Musa zikiwa na ujumbe mzito ni kama alivyowahi kuhutubia waislamu na kusema :
  أيها الناس، ابكوا فإن لم تبكوا فتباكوا، فإن أهل النار يبكون الدموع حتى تنقطع، ثم يبكون الدماء حتى لو أرسلت فيه السفن لجرت.
رواه الإمام أحمد رحمه الله.
Enyi watu lieni machozi na kama hamlii basi lizaneni ili mtokwe na machozi kwani watu wa motoni watatokwa na machozi mpaka yatakatika kisha wataanza kutokwa na machozi ya damu mpaka ingeliletwa meli basi ingelielea (kwa wingi wake)         Ahmad.
Abu Musa alikuwa mwana jihadi shujaa na kupigana katika vingi na aliwahi kupewa sifa ya  mpanda farasi mahiri vitani . Aliwahi kuteuliwa kuwa kiongozi na amiri jeshi wa jeshi la waislamu waliopigana katika vita vya Sasania katika mji wa Tutsar huko Isfahan(Iran) Jeshi hili pia lilikuwa na masahaba maarufu kama ‘Ammaar bin Yaasir, Al Barraa bin Maalik pamoja na ndugu yake Anas na wengineo.
Na wakati ilipokuja fitna kubwa kati ya waislamu  kupigana wenyewe kwa wenyewe kwa ajili ya ukhalifa, msimamo wa Abu Musa ulikuwa kutojifunga na kundi lolote na ni wazo lake la hekima alilolitoa kujaribu kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe pale alipotoa rai kwamba wote waliokuwa wakidai ukhalifa waache kwanza na jambo la kuchagua khalifa mwengine liachiwe kwa waislamu wenyewe.
 Licha ya busara zake kutofanyiwa kazi ipasavyo aliendelea na msimamo wake wa kutojifunga na upande wowote huku akiomba du’aa maarufu akisema: “Allahumma anta Ssalaam waminka Ssalaam”.
Mwishoni mwa uhai wake inasemekana alihamia Makkah ambapo aliishi na kufariki katika mwaka  42 au 52 Hijriyah.